Har-magedoni Lini?
“SISI twasimama kwenye Har–Magedoni na twapigana kwa ajili ya Bwana.” Kwa maneno hayo, Theodore Roosevelt aliyekuwa hapo kwanza rais wa United States alitumia mtajo “Har–Magedoni” kuhusu pigano la kisiasa ambamo alihusika. Kwa hiyo, je! tutafute Har–Magedoni katika uwanja wa kisiasa?
Miaka michache iliyopita, gazeti la Kikanada Business Life lilikuwa na makala yenye kichwa “Har–Magedoni ya Kiuchumi.” Kichwa kidogo kiliuliza hivi: “Je! kulemewa na madeni kwa Ulimwengu wa Tatu kungeweza kutokeza angamio letu la kiuchumi?” Lakini je! twapasa kufikiria Har–Magedoni kuwa msiba wa kiuchumi?
Kulingana na jarida Newsweek, mwisho wa ulimwengu ulipata kuwa suala la kufanyia kampeni wakati wa mjadala mmoja wa 1984 wa kugombea urais. Pindi hiyo, Ronald Reagan aliyekuwa rais wa United States wakati huo “aliulizwa kama kweli yeye huamini kwamba ulimwengu waelekea kwenye ‘Har–Magedoni ya kinyukilia.’ Reagan alikiri kulikuwako ‘mazungumzo yasiyohangaisha’ juu ya usadifiano (ulingano) uliopo kati ya matukio ya sasa na ishara za Kibiblia zilizo dalili ya siku za mwisho, lakini amiri-mkuu akasisitiza kwamba yeye hajasema kamwe kwamba ‘ni lazima tupange mambo kulingana na Har–Magedoni.’” Hata hivyo, je! utafutaji wetu kuhusu maana ya Har–Magedoni wapasa kukaza fikira juu ya kitendo cha kijeshi chenye kutisha kutokeza teketezo la kinyukilia?
Wanadini wengi husema kwamba Har–Magedoni ni pigano. Lakini mapema katika karne ya 19, Adam Clarke mwanachuo wa Biblia aliandika hivi: “Dhana za wanadamu kuhusu jambo hili zimekuwa za kipuuzi sana! Mnamo miaka ishirini iliyopita pigano hili limepiganwa mahali mbalimbali, kulingana na waonaji wetu walio nusu-vipofu na manabii wenye kujivuvia wenyewe! Wakati mmoja lilifanyika Austerlitz, wakati mwingine Moscow, wakati mwingine Leipsic, na sasa Waterloo! Na hivyo ndivyo wameendelea kusema-sema, tena wataendelea kusema-sema, wakivuruga na kujivuruga.”
Ni wazi kwamba kutafuta maana ya Har–Magedoni hutokeza maswali fulani muhimu. Har–Magedoni ni nini? Ikiwa ni pigano, washiriki watakuwa nani? Kwa nini litapiganwa? Litafanyi-ka wapi? Na Har–Magedoni itatukia wakati gani?
Har–Magedoni Ni Nini?
Mtajo “Har–Magedoni” umetolewa katika neno lipatikanalo katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, ambacho chajulikana kwa lugha ya mfano. Humo mtume Yohana aliandika hivi: “Na mimi nikaona semi chafu tatu zilizovuviwa ambazo zilionekana kama vyura zikitoka katika kinywa cha drakoni na katika kinywa cha hayawani-mwitu na katika kinywa cha nabii bandia. Kwa hakika, hizo ni semi zilizovuviwa na roho waovu na hufanya ishara, nazo hutoka kwenda kwa wafalme wa dunia nzima inayokaliwa, kukusanya wao pamoja kwenye vita ya ile siku kubwa ya Mungu Mweza Yote. . . . Na zikakusanya wao pamoja mahali ambapo huitwa kwa Kiebrania Har–Magedoni.”—Ufunuo 16:13-16, NW.
Har–Magedoni, au Armagedoni, ni neno lililotoholewa kutokana na neno-mlingano la Kigiriki la usemi wa Kiebrania Har Meghid·dohnʹ unaomaanisha “Mlima wa Megido,” au “Mlima wa Kusanyiko la Vikosi.” Wahusianishwa na “vita ya ile siku kubwa ya Mungu Mweza Yote.” Kwa hiyo Har–Magedoni si mzozo wa kisiasa, msiba wa kiuchumi, teketezo la kinyukilia, wala pambano la kibinadamu. Bali, Har–Magedoni ni vita ya Mungu.
Washiriki Watakuwa Nani?
Zile semi chafu tatu zilizovuviwa zilizo kama vyura hutoka katika vinywa vya drakoni (Shetani Ibilisi), hayawani-mwitu (muundo wake wa kisiasa wa kidunia), na nabii bandia aliye muungano wa Waingereza na Waamerika. Semi hizi zilizovuviwa na roho waovu, au malaika waovu, zakusanya wafalme, au watawala wa kidunia kwenye Har–Magedoni.—Ona sura 32 ya kitabu Revelation—Its Grand Climax At Hand! kilichochapishwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti.
Upande wa Yehova katika vita ya Har–Magedoni lipo jeshi kubwa la vikosi vya roho wasioonekana wenye kuongozwa na Mfalme Yesu Kristo. Mtume Yohana aliripoti hivi: “Mimi nikaona mbingu zimefunguka, na, tazama! farasi mweupe. Na mmoja aketiye juu yake anaitwa Mwaminifu na Wa-kweli, na yeye anahukumu na kuendeleza vita katika uadilifu. . . . Pia, majeshi ambayo yalikuwa katika mbingu yalikuwa yakifuata yeye . . . Na katika kinywa chake unatokeza upa-nga mkali mrefu, kwamba yeye apate kupiga mataifa kwa huo, na yeye atayachunga kwa ufito wa chuma. Yeye hukanyaga vilevile shinikizo la divai ya kasirani ya hasira-kisasi ya Mungu Mweza Yote. Na juu ya vazi lake la nje, hata juu ya paja lake, yeye ana jina lililoandikwa, Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana.” (Ufunuo 19:11-16, NW) Huo upanga mkali mrefu huwakilisha mamlaka ya Kristo kuua wote ambao wakataa kuunga mkono Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 1:16; 2:16) Majeshi makubwa sana yasiyoonekana yapatikana kwa ajili ya vita ya Har–Magedoni.
Upande wa upinzani kuna Shetani, vikosi vyake vya roho waovu, na wafalme wa dunia nzima inayokaliwa. Lakini haitupasi kufikiria watawala wa ulimwengu tu katika makao yaonekanayo, kwa maana watu ambao wao huwasimamia wanahusika pia. Ilitabiriwa hivi: “Maana BWANA [Yehova, NW] ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote.”—Isaya 34:2.
Kwa Nini Itapiganwa?
Har–Magedoni itapiganwa kwa sababu Mungu ni mwadilifu na hatavumilia tena uovu. (Zaburi 11:7) Tengenezo la Shetani Ibilisi, linalojumlisha roho waovu na pia wanadamu waasi, ambalo kwa mileani kadhaa ndilo limekuwa na daraka la kuleta uovu na ole, ni lazima basi liharibiwe. (Linganisha Mwanzo 3:15.) Enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova itathibitishwa kwenye Har–Magedoni, na vita hiyo itaondolea jina lake suto lililorundikwa juu yalo kwa karne nyingi. Kama vile Mungu alivyojulisha rasmi kupitia Ezekieli nabii wake: “Wala sitaliacha jina langu takatifu kutiwa unajisi tena; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].”—Ezekieli 39:7.
Kwa kweli vita ya Mungu ya Har–Magedoni itazuia kuharibiwa kwa ainabinadamu yote. Yehova aliumba dunia ikaliwe, si iharibiwe katika vita yenye moto wa kinyukilia miongoni mwa wanadamu au kwa njia nyingineyo iharibiwe isifae kwa uhai. (Isaya 45:18) Yeye ‘atawaangamiza wale wanaoangamiza dunia.’ (Ufunuo 11:18, HNWW) Lakini mtunga zaburi alijulisha rasmi hivi: “Yehova mwenyewe amekuwa mfalme. Bara lenye kuzaa [Kiebrania, te·velʹ; dunia, ikiwa na rutuba na yenye kukaliwa, tufe lenye kukalika] huwa pia thibitifu hivi kwamba haliwezi kutikiswa.”—Zaburi 96:10, NW.
Yale ambayo Mungu atafanya kwenye Har–Magedoni yatapatana kabisa na sifa zake kuu za haki, hekima, nguvu, na upendo. (Kumbukumbu 32:4; Ayubu 12:13; Isaya 40:26; 1 Yohana 4:8) Atachukua hatua dhidi ya “wenye dhambi wasiomcha Mungu,” si dhidi ya wanyoofu. (Yuda 14, 15) Ni ‘waovu tu watatolewa wauawe kwa upanga.’ (Yeremia 25:31, NW) Hiyo itaandaa njia ya kurudishwa kwa Paradiso, ikitimiza kusudi la kimungu kwa dunia na ainabinadamu.—Luka 23:43, ZSB.
Itatukia Wapi?
Kwa kuwa mtajo “Har–Magedoni” watokana na usemi wa Kiebrania unaomaanisha “Mlima wa Megido,” huenda watu fulani wakakata shauri kwamba vita hii itapiganwa juu ya mwinuko mkubwa wenye jina hilo. Hata hivyo, hakujapata kamwe kuwako mlima wenye jina Megido. Zapata kilometa 100 kaskazini-magharibi ya Yerusalemu kulikuwako mji, au jiji la kilimani lililoitwa Megido, lakini sasa kilichopo mahali hapo ni kichuguu tu chenye kimo cha karibu meta 20.—Yoshua 17:11,
Jiji hilo la kale lilitazamana na “uwanda wa bonde la Megido.” (2 Nyakati 35:22, NW) Kushirikisha Har–Magedoni (au Armagedoni) na ujirani huo kwafaa kwa sababu hapo palikuwa mahali pa mapigano ya kukata maneno. Mathalani, hapo Mungu aliwezesha Mwamuzi Baraka kuwapiga kumbo la kuwafutilia mbali Yabini mfalme Mkanaani na majeshi yake yenye kuamrishwa na Sisera. (Waamuzi 4:12-24; 5:19, 20) Katika ujirani huo Gideoni na kikosi chake kidogo waliwakimbiza Wamidiani. (Waamuzi 7:1–8:35) Hapo pia ndipo Wafalme Ahazia na Yosia waliuawa.—2 Wafalme 9:27; 23:29, 30.
Hata hivyo, yastahili kuangaliwa kwamba huu uwanda wa bonde, ambao pia huitwa Uwanda wa Esdraeloni, una urefu wa kilometa 32 na upana wa kilometa 29 tu kwenye ncha yao ya mashariki. Wafalme wa dunia nzima inayokaliwa wakiwa na majeshi yao hawangeweza kamwe kutosha katika eneo dogo hivyo. Isitoshe, kichuguu (chungu cha Megido) wala uwanda si mlima. Basi, kwa wazi Har–Magedoni haitakuwa kwenye kituo fulani cha mlimani katika Mashariki ya Kati. Bali, Har–Magedoni (au Armagedoni) hufananisha hali fulani ya ulimwenguni pote, ingawa neno hilo hupata kadiri fulani ya maana yalo kutokana na Megido na yaliyofanyika katika eneo hilo.
Har–Magedoni Itatukia Lini?
Kwa kuwa Megido ilikuwa katika bara la watu wa kale wa Mungu, yenye kutendeka kwenye Har–Magedoni yawahusu Mashahidi wa Yehova katika huu “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Har–Magedoni hutumika kuhusu “mahali” ambapo watawala wa kisiasa wa dunia wakusanywa katika kupinga Yehova na Ufalme wake ulio mikononi mwa Yesu Kristo. (Ufunuo 16:14, 16) Lakini “mahali” hapo (Kigiriki, toʹpos) huonyesha hali fulani ya ulimwengu. Har–Magedoni itatukia wakati hali fulani itakapositawi iathiri Mashahidi wa Yehova kuzunguka dunia.
Ufanisi wa kiroho wa Mashahidi wa Yehova humtia kiruu Shetani Ibilisi, ambaye karibuni atafyatusha shambulio la kufa na kupona dhidi ya Wakristo hawa wenye kuonekana kana kwamba hawana kinga. Shambulio hili la ulimwenguni pote lenye kufanywa na Shetani, au Gogu, lasimuliwa katika Ezekieli sura za 38 na 39. Chini ya uvutano wa Ibilisi, mataifa yatasonga mbele dhidi ya watu wa Yehova wanaopenda amani waliokusanywa kutoka mataifa yote. Ndiyo, upinzani wa kishetani utadhihirishwa kwa kitendo cha tufe lote dhidi ya watumishi wa kidunia wa Yehova, wale wawakilishi na wapiga mbiu waonekanao wa Ufalme wa Mungu.
Mara nyingi pigano hujulikana kwa mahali ambapo lapiganwa. Hivyo, kinga hodari ya Mungu kwa watu wake yaweza kuitwa pigano au vita ya Har–Magedoni. Yehova ainukapo ili akinge watumishi wake dhidi ya shambulio la Gogu, Har–Magedoni itakuwa yaendelea! Serikali za kibinadamu zitaangamia. Mawingu yenye kububujisha mafuriko, mawe-barafu yenye kuharibu sana, moto wenye kumweka, magonjwa ya kipuku yenye kuenea sana—hivyo vikiwa ni vitendo vya Mungu kweli kweli—vitasababisha bumbuazi la ulimwengu nje ya safu za Mashahidi wa Yehova. Adui zao wa kibinadamu watageuziana silaha zao. Na wale ambao hawatauawa na vita hii ya kujiua wenyewe kwa wenyewe, Yehova atawatokomeza.—Ezekieli 38:18-23; Danieli 2:44.
Kwa ogofyo kuu, mkono wa kila mwanadamu utageuzwa dhidi ya jirani yake katika harakati yenye kichaa ya kuokoka lakini wapi. (Zekaria 14:12, 13) “Waliouawa na BWANA [Yehova, NW] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.” (Yeremia 25:33) Jaribio lolote kubaki bila kuunga mkono upande wowote katika pigano la Mungu litakugharimu uhai wako kwenye Har–Magedoni! Na kama vile imethibitishwa mara nyingi sana Kimaandi-ko katika jarida hili, kizazi kilichopo hakitapitilia mbali kabla Har–Magedoni haijatukia!—Mathayo 24:21, 34.
Yale Ambayo Har–Magedoni Itatimiza
Har–Magedoni itaondoa salio la mwisho la tengenezo la kidunia la Shetani. Zaidi ya hilo, Ibilisi na roho wake waovu watatiwa katika abiso. (Ufunuo 20:1-3, NW) Lo, ni mibaraka iliyoje ambayo wakati huo itatiririkia watu wa Yehova, wale waokokaji wenye shangwe wa vita yake kubwa ya Har–Magedoni! Wao watasonga mbele kwa furaha na kazi ya kujenga upya ambayo itageuza dunia nzima iwe paradiso, isiyo na uchafuzi, maumivu, maombolezo, machozi, na kifo. (Ufunuo 11:15, 18; 21:3, 4) Nawe waweza kuwapo ukiyazingatia moyoni maneno haya ya mtunga zaburi: “Wewe umngoje BWANA [umtumainie Yehova, NW], uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.” (Zaburi 37:34) Kwa kweli, wewe waweza kuishi uone vita ya ile siku kubwa ya Mungu Mweza Yote na uwe mwokokaji mwenye furaha wakati Har–Magedoni ipigapo kumbo!
“Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, nyinyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya ujitoaji kimungu, mkingojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.”—2 Petro 3:11, 12, NW
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Har-Magedoni si mzozo wa kisiasa, msiba wa kiuchumi, teketezo la kinyukilia, wala pambano la kibinadamu. Har–Magedoni ni vita ya Mungu
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Vita ya Mungu ya Har–Magedoni itazuia kuharibiwa kwa ainabinadamu yote
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Jaribio lolote kubaki bila kuunga mkono upande wowote katika vita ya Mungu litakugharimu uhai wako kwenye Har–Magedoni!