-
Mimweko ya Nuru Katika Nyakati za KimitumeMnara wa Mlinzi—1995 | Mei 15
-
-
Mimweko ya Nuru Katika Nyakati za Kimitume
“Nuru imemzukia [“imemmwekea,” “NW”] mwenye haki, na furaha wanyofu wa moyo.”—ZABURI 97:11.
1. Mashahidi wa Yehova leo hufananaje na Wakristo wa mapema?
TUKIWA Wakristo wa kweli, twathamini kama nini maneno ya Zaburi 97:11! ‘Nuru imetumwekea’ mara nyingi. Kwa kweli, baadhi yetu tumeona mmweko wa nuru ya Yehova kwa miongo kadhaa. Yote hayo yatukumbusha juu ya Mithali 4:18, lisemalo hivi: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” Kwa kuwa twathamini Maandiko badala ya mapokeo, sisi Mashahidi wa Yehova twafanana na Wakristo wa mapema. Mtazamo wao waweza kuonwa wazi katika vitabu vya kihistoria vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na kutoka kwa barua zayo, zilizoandikwa chini ya upulizio wa kimungu.
2. Ni mambo yapi yaliyokuwa miongoni mwa mimweko ya kwanza ya nuru ambayo wafuasi wa Yesu walipokea?
2 Miongoni mwa mimweko ya kwanza ya nuru ambayo wafuasi wa mapema wa Yesu Kristo walipokea ni ile iliyohusu Mesiya. Andrea alimwambia ndugu yake Simoni Petro: “Tumemwona Masihi.” (Yohana 1:41) Wakati fulani baadaye, Baba aliye mbinguni alimwezesha mtume Petro kutoa ushuhuda wa jambo hilo alipomwambia Yesu Kristo hivi: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mathayo 16:16, 17; Yohana 6:68, 69.
Nuru Kuhusu Utume wao wa Kuhubiri
3, 4. Baada ya ufufuo wake, Yesu aliwapa wafuasi wake nuru gani kuhusu utendaji wao wa wakati ujao?
3 Baada ya ufufuo wake, Yesu Kristo alitoa mimweko ya nuru kuhusu wajibu ambao wafuasi wake wote walipaswa kutimiza. Yaelekea kwamba ni kwa wale wanafunzi 500 waliokusanyika Galilaya aliowaambia: ‘Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na roho takatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.’ (Mathayo 28:19, 20; 1 Wakorintho 15:6) Baada ya hapo, wafuasi wote wa Kristo walipaswa kuwa wahubiri, na utume wao wa kuhubiri haukuhusu “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli” pekee. (Mathayo 10:6) Wala hawakupaswa kufanya ubatizo wa Yohana katika kuonyesha toba kwa ajili ya msamaha wa dhambi. Badala ya hivyo, wao walikuwa wabatize watu ‘kwa jina la Baba, na Mwana, na roho takatifu.’
4 Punde tu kabla ya Yesu kupaa mbinguni, mitume wake waaminifu 11 waliuliza: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” Badala ya kujibu swali hilo, Yesu alitoa maagizo zaidi kuhusu utume wao wa kuhubiri, akisema: ‘Mtapokea nguvu, ikiisha kuwajilia juu yenu roho takatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.’ Kufikia wakati huo, wao walikuwa wamekuwa mashahidi wa Yehova pekee, lakini sasa wangekuwa mashahidi wa Kristo pia.—Matendo 1:6-8.
5, 6. Wanafunzi wa Yesu walipokea mimweko gani ya nuru katika Pentekoste?
5 Siku kumi tu baadaye, wafuasi wa Yesu walipokea mimweko miangavu kama nini ya nuru! Katika siku ya Pentekoste 33 W.K., kwa mara ya kwanza, walielewa kabisa umaana wa Yoeli 2:28, 29: “[Mimi Yehova] nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono; tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu.” Wanafunzi wa Yesu waliona roho takatifu, ikiwa kwa namna ya miale ya moto, ikiwa imekaa juu yao wote—wanaume na wanawake wapatao 120—waliokusanyika Yerusalemu.—Matendo 1:12-15; 2:1-4.
6 Pia katika siku ya Pentekoste, wanafunzi walielewa kwa mara ya kwanza kwamba maneno ya Zaburi 16:10, NW, yalitumika kwa Yesu Kristo aliyefufuliwa. Mtunga-zaburi alikuwa amesema: “Wewe [Yehova Mungu] hutaacha nafsi yangu katika Sheoli. Wala hutaruhusu mwaminifu-mshikamanifu wako aone shimo.” Wanafunzi walitambua kwamba maneno hayo hayangehusu Mfalme Daudi, kwa kuwa kaburi lake lilikuwapo pale mpaka wakati huo. Si ajabu kwamba wapatao 3,000 kati ya wale waliosikia nuru hii mpya ikifafanuliwa walisadiki kabisa wakabatizwa siku iyo hiyo!—Matendo 2:14-41.
7. Mtume Petro alipokea nuru gani nyangavu alipotembelea Kornelio aliyekuwa ofisa wa Jeshi la Roma?
7 Kwa karne nyingi, Waisraeli walijua yale Mungu alikuwa amesema kuwahusu: “Ni ninyi tu niliowajua katika jamaa zote zilizo duniani.” (Amosi 3:2) Kwa hiyo ulikuwa mmweko mwangavu sana wa nuru uliopokewa na mtume Petro pamoja na wale walioandamana naye kwenye nyumba ya Kornelio aliyekuwa ofisa wa jeshi la Roma wakati roho takatifu ilishuka kwa mara ya kwanza kwa waamini Wasio Wayahudi ambao hawakutahiriwa. Ni muhimu kuona kwamba hii ndiyo pindi ya pekee ambayo roho takatifu ilitolewa kabla ya ubatizo. Lakini ilikuwa ni lazima iwe hivyo. Kama sivyo, Petro hangejua kama hawa Wasio Wayahudi walistahili ubatizo. Akitambua kabisa umaana wa tukio hilo la ajabu, Petro aliuliza: ‘Ni nani awezaye kukataza maji, hawa Wasio Wayahudi wasibatizwe, watu waliopokea roho takatifu vile vile kama sisi?’ Bila shaka hakuna mtu aliyekuwapo ambaye angekuwa na haki ya kupinga hilo, na hao Wasio Wayahudi wakabatizwa.—Matendo 10:44-48; linganisha Matendo 8:14-17.
Hakuna Tohara Tena
8. Kwa nini baadhi ya Wakristo wa mapema waliona ugumu wa kuachilia fundisho la tohara?
8 Mmweko mwingine mwangavu wa kweli ulihusu swali la tohara. Zoea la tohara lilianza katika 1919 K.W.K. Yehova alipofanya agano pamoja na Abrahamu. Kisha Mungu akaamuru Abrahamu kwamba yeye pamoja na watu wote wa kiume katika nyumba yake watahiriwe. (Mwanzo 17:9-14, 23-27) Basi tohara ikawa ishara ya kutambulisha wazao wa Abrahamu. Nao walijivunia zoea hilo kama nini! Matokeo yakawa kwamba neno “asiyetahiriwa” likaja kuwa mtajo wa dhihaka. (Isaya 52:1; 1 Samweli 17:26, 27) Ni rahisi kuona sababu iliyofanya Wakristo fulani wa mapema walio Wayahudi kutaka kudumisha ishara hiyo. Baadhi yao wakawa na mazungumzo sana pamoja na Paulo na Barnaba juu ya jambo hilo. Ili kulisuluhisha, Paulo na wengine walienda Yerusalemu kutafuta mashauri kutoka kwa baraza linaloongoza la Kikristo.—Matendo 15:1, 2.
9. Ni mimweko gani ya nuru iliyofunuliwa kwa baraza linaloongoza la mapema, kama ilivyorekodiwa katika Matendo sura 15?
9 Wakati huu, haikuwa kwa njia ya muujiza wa wazi kwamba wale Wakristo wa mapema walipokea nuru kwamba tohara haikuwa tena takwa kwa watumishi wa Yehova. Badala ya hivyo, walipata nuru hiyo iliyoongezeka kwa kutafuta katika Maandiko, wakitegemea roho takatifu kwa ajili ya mwongozo, na kusikia maono ya Petro na Paulo kuhusu kugeuzwa kwa watu Wasio Wayahudi. (Matendo 15:6-21) Uamuzi huo ulitolewa katika barua iliyosema hivi kwa sehemu: ‘Ilipendeza roho takatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima, yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati.’ (Matendo 15:28, 29) Hivyo Wakristo wa mapema waliwekwa huru kutoka kwa amri ya kufanya tohara na kwa matakwa mengine ya Sheria ya Kimusa. Kwa hiyo, Paulo, angeweza kuwaambia Wakristo Wagalatia hivi: “Kwa ajili ya uhuru wa namna hiyo Kristo alituweka huru.”—Wagalatia 5:1, NW.
Nuru Katika Gospeli
10. Ni ipi baadhi ya mimweko ya nuru iliyofunuliwa katika Gospeli ya Mathayo?
10 Hakuna shaka kwamba Gospeli ya Mathayo, iliyoandikwa karibu 41 W.K., ina mimweko mingi ya nuru kwa manufaa ya wasomaji wayo. Ni wachache wa Wakristo wa karne ya kwanza kwa kulinganisha waliokuwa wamemsikia binafsi Yesu akifafanua mafundisho yake. Hasa Gospeli ya Mathayo ilikazia kwamba kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu kilikuwa Ufalme. Naye Yesu alikazia kama nini umuhimu wa kuwa na nia ifaayo! Kulikuwa na mimweko ya nuru kama nini katika Mahubiri yake ya Mlimani, katika mifano yake (kama ile iliyorekodiwa katika sura ya 13), na katika unabii wake mkubwa katika sura za 24 na 25! Yote hayo yalitajwa kwa Wakristo wa mapema katika Gospeli ya Mathayo, iliyoandikwa kama miaka minane tu baada ya Pentekoste ya 33 W.K.
11. Ni nini yaweza kusemwa kuhusu yaliyomo katika Gospeli za Luka na Marko?
11 Karibu miaka 15 baadaye, Luka aliandika Gospeli yake. Ingawa sehemu kubwa inafanana na simulizi la Mathayo, asilimia 59 ni nyongeza. Luka alirekodi miujiza sita ya Yesu na zaidi ya maradufu ya hesabu hiyo ya vielezi Vyake havitajwi na waandikaji wengine wa Gospeli. Kwa wazi miaka michache tu baadaye, Marko aliandika Gospeli yake, akiweka mkazo kwa Yesu Kristo akiwa mtu wa matendo, mfanya miujiza. Ingawa Marko alisimulia matukio yaliyorekodiwa awali na Mathayo na Luka, yeye alirekodi mfano mmoja ambao wale wengine hawakurekodi. Katika kielezi hicho, Yesu alifananisha Ufalme wa Mungu na mbegu iotayo, inayokuwa ndefu, na polepole kuanza kuzaa matunda.a—Marko 4:26-29.
12. Gospeli ya Yohana iliandaa nuru zaidi kwa kadiri gani?
12 Kisha kulikuwa na Gospeli ya Yohana, iliyoandikwa zaidi ya miaka 30 baada ya Marko kuandika simulizi lake. Yohana alitokeza mmweko mkubwa kama nini wa nuru kwa huduma ya Yesu, hasa kupitia marejezo mengi kuhusu uhai Wake wa kabla ya kuwa mwanadamu! Ni Yohana pekee anayeandaa simulizi la ufufuo wa Lazaro, na ni yeye pekee anayetupa mengi ya maelezo mazuri ya Yesu kwa mitume wake waaminifu na vilevile sala yake ya kuchangamsha moyo katika usiku wa kusalitiwa kwake, kama ilivyorekodiwa katika sura 13 hadi 17. Hakika, yasemwa kwamba asilimia 92 ya Gospeli ya Yohana ni ya kipekee.
Mimweko ya Nuru Katika Barua za Paulo
13. Kwa nini wengine wameona barua ya Paulo kwa Warumi kana kwamba ni Gospeli?
13 Mtume Paulo hasa alitumiwa kuleta mimweko ya nuru ya kweli kwa Wakristo walioishi katika nyakati za kimitume. Mathalani, kuna barua ya Paulo kwa Warumi, iliyoandikwa karibu 56 W.K.—karibu na wakati ambapo Luka aliandika Gospeli yake. Katika barua hiyo Paulo akazia kwamba uadilifu hupatikana kupitia fadhili zisizostahiliwa za Mungu na kupitia imani katika Yesu Kristo. Mkazo wa Paulo kwa sehemu hiyo ya habari njema umefanya wengine waone barua hiyo kwa Warumi kana kwamba ni Gospeli ya tano.
14-16. (a) Katika barua yake ya kwanza kwa Wakristo walio Korintho, Paulo alitoa nuru gani juu ya uhitaji wa muungamano? (b) Wakorintho wa Kwanza ina nuru gani zaidi kuhusu mwenendo?
14 Paulo aliandika kuhusu mambo fulani yaliyokuwa yakisumbua Wakristo katika Korintho. Barua yake kwa Wakorintho yatia ndani shauri lililopuliziwa ambalo limenufaisha Wakristo kufikia leo hii. Kwanza, ilikuwa ni lazima awape Wakorintho nuru juu ya kosa walilokuwa wakifanya la kuwa wafuasi wa watu fulani. Mtume aliwanyoosha, akiwaeleza kwa ujasiri: “Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.”—1 Wakorintho 1:10-15.
15 Ukosefu mbaya sana wa adili ulikuwa umeachiliwa katika kutaniko la Kikristo katika Korintho. Mtu mmoja huko alikuwa amemchukua mke wa baba yake, hivyo akifanya “zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa.” Bila kuficha, Paulo aliandika: “Mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.” (1 Wakorintho 5:1, 11-13) Hilo lilikuwa jambo jipya kwa kutaniko la Kikristo—kutenga na ushirika. Jambo jingine ambalo kutaniko la Korintho lilihitaji nuru kulihusu lilikuwa kwamba baadhi ya washiriki walo walikuwa wakipeleka ndugu zao wa kiroho katika mahakama za kilimwengu ili kusuluhisha matatizo yao. Paulo aliwakemea kwa nguvu kwa kufanya jambo hilo.—1 Wakorintho 6:5-8.
16 Jambo jingine lililotatiza kutaniko la Korintho lilihusu mahusiano ya kingono. Katika 1 Wakorintho sura ya 7, Paulo alionyesha kwamba kwa sababu ya kuenea kwa ukosefu wa adili kingono, ingekuwa vema kwa kila mtu kuwa na mke wake mwenyewe na kila mwanamke kuwa na mume wake mwenyewe. Paulo alionyesha pia kwamba ingawa waseja wanaweza kumtumikia Yehova bila vikengeushi vingi, si wote walikuwa na zawadi ya useja. Na iwapo mume wa mwanamke afe, yeye angekuwa huru kuolewa tena lakini “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.
17. Paulo alitoa nuru gani kuhusu fundisho la ufufuo?
17 Ni mimweko kama nini ya nuru ambayo Bwana alitumia Paulo kuangaza juu ya ufufuo! Wakristo watiwa-mafuta watainuliwa wakiwa na miili ya aina gani? “Hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho,” akaandika Paulo. Hakuna miili ya mnofu itakayopelekwa mbinguni, kwa kuwa “nyama na damu haziwezi kuurithi Ufalme wa Mungu.” Paulo aliongezea kwamba si watiwa-mafuta wote watalala usingizi katika kifo bali kwamba wakati wa kuwapo kwa Yesu wengine watainuliwa kupata uhai usioweza kufa mara hiyo wakati wa kifo.—1 Wakorintho 15:43-53.
18. Barua ya kwanza ya Paulo kwa Wathesalonike ilikuwa na nuru gani kuhusu wakati ujao?
18 Katika barua yake kwa Wakristo walio Thesalonike, Paulo alikuwa akitokeza nuru juu ya wakati ujao. Siku ya Yehova ingekuja kama vile mwizi ajavyo usiku. Paulo alieleza pia hivi: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.”—1 Wathesalonike 5:2, 3.
19, 20. Ni mimweko gani ya nuru ambayo Wakristo katika Yerusalemu na Yudea walipokea katika barua ya Paulo kwa Waebrania?
19 Kwa kuandika barua yake kwa Waebrania, Paulo aliwasilisha mimweko ya nuru kwa Wakristo wa mapema katika Yerusalemu na Yudea. Alionyesha kwa nguvu kama nini ukuu wa mfumo wa ibada ya Kikristo kuliko mfumo wa ibada ya Kimusa! Badala ya kufuata Sheria iliyopitishwa na malaika, Wakristo wana imani katika wokovu uliotajwa kwa mara ya kwanza na Mwana wa Mungu, ambaye ni mkubwa zaidi kuliko watumishi hao wa kimalaika. (Waebrania 2:2-4) Musa alikuwa mhudumu tu katika nyumba ya Mungu. Lakini, Yesu Kristo asimamia nyumba yote. Kristo ni kuhani wa cheo cha juu kwa namna ya Melkizedeki, akiwa na cheo kikubwa sana kuliko ukuhani wa Kiharuni. Paulo pia alitaja kwamba Waisraeli walishindwa kuingia katika pumziko la Mungu kwa sababu ya kukosa imani na utii, lakini Wakristo waliingia katika pumziko hilo kwa sababu ya uaminifu na utii wao.—Waebrania 3:1–4:11.
20 Kisha, pia, agano jipya ni kuu zaidi kuliko agano la Sheria. Kama unabii ulivyotolewa miaka 600 mapema kwenye Yeremia 31:31-34, wale walio katika agano jipya wameandikiwa sheria ya Mungu katika mioyo yao na kufurahia msamaha wa kweli wa dhambi. Badala ya kuwa na kuhani wa cheo cha juu aliyewajibika kutoa dhabihu kila mwaka kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe na zile za watu, Wakristo wana Kuhani wa Cheo cha Juu Yesu Kristo, asiye na dhambi na ambaye mara moja pekee alitoa dhabihu kwa ajili ya dhambi. Badala ya kuingia patakatifu palipofanyizwa kwa mikono kutoa toleo lake, yeye aliingia mbinguni penyewe, huko akatokea mbele ya Yehova mwenyewe. Na zaidi, dhabihu za wanyama chini ya agano la Sheria ya Kimusa hazingeweza kuondoa dhambi kabisa, kama sivyo hazingekuwa zikitolewa kila mwaka. Lakini dhabihu ya Kristo, iliyotolewa mara moja pekee, yaondolea mbali dhambi. Yote haya yaangaza nuru juu ya hekalu kubwa la kiroho, ambalo katika ua walo mabaki watiwa-mafuta na “kondoo wengine” hutumika leo.—Yohana 10:16; Waebrania 9:24-28.
21. Mazungumzo haya yameonyesha nini kuhusu utimizo wa Zaburi 97:11 na Mithali 4:18 katika nyakati za kimitume?
21 Nafasi haitoshi kutaja mifano mingine zaidi, kama vile mimweko ya nuru ipatikanayo katika barua za Petro na zile za wanafunzi Yakobo na Yuda. Lakini hayo yaliyotajwa yatosha kuonyesha kwamba Zaburi 97:11 na Mithali 4:18 yalikuwa na utimizo wenye kutokeza katika nyakati za kimitume. Kweli ilianza kuendelea kutoka kwa mifano na vivuli hadi utimizo na mambo halisi.—Wagalatia 3:23-25; 4:21-26.
22. Ni nini kilichotendeka baada ya kifo cha mitume, na makala ifuatayo itaonyesha nini?
22 Baada ya kifo cha mitume wa Yesu na mwanzo wa uasi-imani uliotabiriwa, nuru ya kweli ilikuwa imefifia sana. (2 Wathesalonike 2:1-11) Hata hivyo, kwa kupatana na ahadi ya Yesu, baada ya karne nyingi Bwana-Mkubwa alirudi na kupata “mtumwa mwaminifu mwenye akili” akiwapa ‘watumishi wa nyumbani’ chakula chao kwa wakati ufaao. Matokeo ni kwamba Yesu Kristo alimweka rasmi mtumwa huyo “juu ya vitu vyake vyote.” (Mathayo 24:45-47) Ni mimweko gani ya nuru iliyofuata? Hii itazungumzwa katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Hapo udongo unarejezea mazingira ambamo Mkristo achagua kusitawisha sifa za utu.—Ona Mnara wa Mlinzi, Desemba 15, 1980, kurasa 18-19.
-
-
Mimweko ya Nuru—Mikubwa na Midogo (Sehemu ya Kwanza)Mnara wa Mlinzi—1995 | Mei 15
-
-
Mimweko ya Nuru—Mikubwa na Midogo (Sehemu ya Kwanza)
“Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—MITHALI 4:18.
1. Kwa nini kweli imefunuliwa hatua kwa hatua?
NI UTHIBITISHO wa hekima ya kimungu kwamba, kwa kupatana na Mithali 4:18, kufunuliwa kwa kweli za kiroho kumetokea hatua kwa hatua kupitia mimweko ya nuru. Katika makala inayotangulia, tuliona jinsi andiko hili lilivyotimizwa katika nyakati za kimitume. Ikiwa kweli zote za Kimaandiko zingefunuliwa mara moja, zingeangaza mno na kutatanisha—kama lile tokeo la kutoka katika pango lenye giza na kuingia katika jua jangavu. Isitoshe, kweli ifunuliwayo hatua kwa hatua huimarisha imani ya Wakristo kwa njia ya kuendelea. Hiyo hufanya tumaini lao kuwa jangavu zaidi na kufanya njia wanayopasa kutembea kuwa wazi zaidi.
“Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”
2. Yesu alionyesha kwamba angetumia nani kuleta nuru ya kiroho kwa wafuasi wake, na chombo hicho chajumuisha nani?
2 Katika nyakati za kimitume Yesu Kristo aliona kuwa jambo la kufaa kutumia njia zenye nguvu zipitazo za kibinadamu kuwapa wafuasi wake mimweko ya mapema zaidi ya nuru. Tuna vielelezo viwili juu ya jambo hili: Pentekoste 33 W.K., na kugeuzwa kwa Kornelio katika 36 W.K. Baadaye, Kristo ameona ikifaa kutumia chombo cha kibinadamu, kama alivyotabiri: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake [“watumishi wake wa nyumbani,” NW], awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.” (Mathayo 24:45-47) Mtumwa huyo hawezi kuwa mtu mmoja tu kwa sababu alipaswa kuandaa chakula cha kiroho tangu kutaniko la Kikristo lilipoanza katika Pentekoste mpaka Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo, alipokuja kutoza hesabu. Mambo ya hakika yaonyesha kwamba jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili yajumuisha Wakristo wote watiwa-mafuta wakiwa kikundi duniani wakati wowote ule.
3. Ni nani waliotiwa ndani ya washiriki wa kwanza wa jamii ya mtumwa?
3 Ni nani waliokuwa miongoni mwa washiriki wa kwanza wa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili? Mmoja alikuwa mtume Petro, aliyetii amri hii ya Yesu: “Lisha kondoo zangu.” (Yohana 21:17) Washiriki wengine wa jamii ya mtumwa walitia ndani Mathayo, aliyeandika Gospeli inayoitwa kwa jina lake, na Paulo, Yakobo, na Yuda, walioandika barua zilizopuliziwa. Mtume Yohana, aliyerekodi kitabu cha Ufunuo, Gospeli yake, na barua zake, pia alikuwa mshiriki wa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili. Wanaume hawa waliandika kwa kutii utume wa Yesu.
4. ‘Watumishi wa nyumbani’ ni akina nani?
4 Ikiwa watiwa-mafuta wote wakiwa kikundi, hata wawe wanaishi wapi duniani, ni washiriki wa jamii ya mtumwa, basi wale ‘watumishi wa nyumbani’ ni nani? Ni haohao watiwa-mafuta lakini wakionwa kutoka kwa mtazamo mwingine—wakiwa mtu mmoja-mmoja. Ndiyo, wakiwa mtu mmoja-mmoja wao wangekuwa wa “mtumwa” au wangekuwa wa ‘watumishi wa nyumbani,’ ikitegemea ikiwa wanaandaa chakula cha kiroho au kushiriki kukila. Kwa kielezi: Kama ilivyorekodiwa kwenye 2 Petro 3:15, 16, mtume Petro arejezea barua za Paulo. Anapozisoma, Petro angekuwa mmoja wa watumishi wa nyumbani wanaojilisha chakula cha kiroho kinachoandaliwa na Paulo akiwa mwakilishi wa jamii ya mtumwa.
5. (a) Ni nini lililopata mtumwa huyo katika karne za baada ya mitume? (b) Ni maendeleo gani yaliyotokea katika sehemu ya mwisho ya karne ya 19?
5 Kwa habari hii, kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached kilisema hivi: “Kwa habari ya jinsi jamii ya ‘mtumwa mwaminifu mwenye akili’ imekuwapo na kutumika katika karne zilizopita baada ya kifo cha mitume wa Bwana-Mkubwa Yesu Kristo, hatuna rekodi hususa ya kihistoria. Kwa wazi kizazi kimoja cha jamii ya ‘mtumwa’ kililisha kizazi kilichofuata baadaye. (2 Timotheo 2:2) Lakini katika sehemu ya mwisho ya karne ya kumi na tisa kulikuwa na watu wenye kumhofu Mungu waliopenda chakula cha kiroho cha Biblia Takatifu na ambao walitamani kujilisha chakula hicho . . . Madarasa ya funzo la Biblia . . . yalianzishwa nayo yakafanya maendeleo katika kufahamu kweli za msingi za Maandiko Matakatifu. Wale wenye mioyo myeupe na wasio na ubinafsi miongoni mwa hawa wanafunzi wa Biblia walitamani kushiriki sehemu hizo muhimu za chakula cha kiroho pamoja na wengine. Wao walikuwa na roho ya uaminifu ya ‘mtumwa’ aliyewekwa rasmi kuwapa ‘watumishi wa nyumbani chakula cha kiroho kilichohitajiwa kwa wakati wake.’ Wao walikuwa wenye ‘akili’ katika kutambua kwamba ulikuwa wakati mzuri na ufaao na ni zipi njia bora za kukipakua chakula hicho. Walijitahidi kukipakua.”—Kurasa 344-345.a
Mimweko ya Mapema ya Nuru Katika Nyakati za Kisasa
6. Ni jambo gani hakika linalojitokeza sana kuhusu kufunuliwa kwa kweli hatua kwa hatua?
6 Jambo moja linalotokeza sana kuhusu wale ambao Yehova alitumia kuleta nuru hii ya kiroho yenye kuongezeka hatua kwa hatua ni kwamba wao hawakujisifu. Mtazamo wa C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, ulikuwa kwamba Bwana alifurahi kutumia vipawa vyao vya kawaida. Kuhusu maneno ya kukejeli ambayo maadui wake walipenda kutumia, Ndugu Russell alisisitiza sana kwamba hajapata kamwe kukutana na “Mruseli” na kwamba hakukuwa na “Uruseli” wowote. Sifa zote zilimwendea Mungu.
7. Ndugu Russell na wafanyakazi wenzake walitoa uthibitisho gani kwamba kwa kweli wao walishirikiana na mtumwa mwaminifu mwenye akili?
7 Kwa kutazama matokeo, hakuna shaka kwamba roho takatifu ya Yehova ilikuwa ikielekeza jitihada za Ndugu Russell na wale walioshirikiana naye. Walionyesha uthibitisho wa kushirikishwa na mtumwa mwaminifu mwenye akili. Ingawa makasisi wengi wa wakati huo walidai waliamini kwamba Biblia ilikuwa Neno la Mungu iliyopuliziwa na kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, wao walikubali mafundisho bandia ya Kibabiloni, kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya binadamu, na mateso ya milele. Kwa kupatana na ahadi ya Yesu, kwa kweli ni kupitia roho takatifu kwamba jitihada za unyenyekevu za Ndugu Russell na washiriki wake zilisababisha kweli kuangaza kuliko wakati mwingine wowote. (Yohana 16:13) Hawa Wanafunzi wa Biblia watiwa-mafuta walithibitisha kwamba kwa kweli wao walikuwa sehemu ya jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambayo utume wayo ni kuandaa chakula cha kiroho kwa watumishi wa nyumbani wa Bwana-Mkubwa. Jitihada zao zilikuwa msaada mkubwa katika kukusanya watiwa-mafuta.
8. Ni mambo gani ya hakika yaliyo ya msingi kuhusu Yehova, Biblia, Yesu Kristo, na roho takatifu ambayo Wanafunzi wa Biblia walielewa wazi?
8 Ni jambo la kutokeza sana kuona jinsi Yehova, kwa kupitia roho takatifu, aliwapendelea sana hawa Wanafunzi wa Biblia wa mapema kwa kuwapa mimweko ya nuru. Kwanza, walithibitisha kabisa kwamba Muumba yupo na kwamba yeye ana jina la kipekee Yehova. (Zaburi 83:18; Warumi 1:20) Walitambua kwamba Yehova ana sifa kubwa nne—uwezo, haki, hekima, na upendo. (Mwanzo 17:1; Kumbukumbu la Torati 32:4; Warumi 11:33; 1 Yohana 4:8) Wakristo hawa watiwa-mafuta walithibitisha wazi kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa na ndiyo kweli. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17) Zaidi, wao walisisitiza kwamba Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliumbwa na kwamba alitoa uhai wake ukiwa fidia kwa ajili ya wanadamu wote. (Mathayo 20:28; Wakolosai 1:15) Roho takatifu, mbali na kuwa mtu wa tatu wa ule Utatu, ilionwa kuwa kani ya utendaji ya Mungu.—Matendo 2:17.
9. (a) Ni kweli zipi ambazo Wanafunzi wa Biblia walielewa kabisa kuhusu asili ya mwanadamu na hali za wakati ujao zinazotajwa katika Biblia? (b) Ni kweli zipi nyingine ambazo watumishi wa Yehova waliona wazi?
9 Wanafunzi wa Biblia walitambua wazi kwamba mwanadamu hana nafsi isiyoweza kufa bali yeye ni nafsi iwezayo kufa. Wao walitambua kwamba “mshahara wa dhambi ni mauti,” bali si mateso ya milele, huku kukiwa hakuna kabisa helo yenye kuwaka moto. (Warumi 5:12; 6:23; Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4) Isitoshe, wao walitambua wazi kwamba nadharia ya mageuzi si ya kimaandiko na pia haina msingi wowote wa mambo ya hakika. (Mwanzo, sura 1 na 2) Walitambua pia kwamba Biblia inataja mahali pawili—mbinguni kwa wale watiwa-mafuta 144,000 wafuatao hatua za Kristo na dunia paradiso kwa “umati mkubwa” usiohesabika wa “kondoo wengine.” (Ufunuo 7:9, NW; 14:1; Yohana 10:16) Hao Wanafunzi wa Biblia wa mapema walitambua kwamba dunia hudumu milele nayo haitachomwa, kama vile dini nyingi hufundisha. (Mhubiri 1:4; Luka 23:43) Walijifunza pia kwamba kurudi kwa Kristo kungekuwa kusikoonekana na kwamba angetekeleza hukumu kwa mataifa na kuleta paradiso ya kidunia.—Matendo 10:42; Warumi 8:19-21; 1 Petro 3:18.
10. Ni kweli ipi Wanafunzi wa Biblia walijifunza kuhusu ubatizo, mgawanyo wa makasisi na watu wa kawaida, na Ukumbusho wa kifo cha Kristo?
10 Wanafunzi wa Biblia walijifunza kwamba ubatizo wa Kimaandiko si kunyunyizia vitoto vichanga maji bali kwamba kwa kufuata amri ya Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20, ni kuzamisha waamini ambao wamefundishwa. Walikuja kutambua kwamba hakuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kuunga mkono mgawanyo kati ya makasisi na watu wa kawaida. (Mathayo 23:8-10) Kinyume cha hilo, Wakristo wote wanapaswa kuwa wahubiri wa habari njema. (Matendo 1:8) Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba Ukumbusho wa kifo cha Kristo wapaswa kuadhimishwa mara moja tu kila mwaka, katika Nisani 14. Na zaidi, wao walitambua kwamba Ista ni sikukuu ya kipagani. Kwa kuongezea, wale watiwa-mafuta walikuwa na hakika sana kwamba Mungu alikuwa akiunga mkono kazi yao hata hawakuwa wakikusanya michango. (Mathayo 10:8) Kutoka nyakati za mapema zaidi, wao walielewa kwamba ni lazima Wakristo waishi kwa kupatana na kanuni za Biblia, jambo linalotia ndani kusitawisha matunda ya roho takatifu ya Mungu.—Wagalatia 5:22, 23.
Mimweko Yenye Kuongezeka ya Nuru
11. Ni nuru gani iliyoangaza kwenye utume wa Wakristo na kwenye mfano wa Yesu juu ya kondoo na mbuzi?
11 Hasa tangu 1919 watumishi wa Yehova wamebarikiwa na mimweko yenye kuongezeka ya nuru. Ni mmweko mwangavu kama nini wa nuru ulioangaza katika mkusanyiko wa Cedar Point wa 1922 wakati J. F. Rutherford, msimamizi wa pili wa Watch Tower Society, alipokazia kwamba wajibu mkubwa wa watumishi wa Yehova ni ‘kutangaza, kutangaza, kutangaza, Mfalme na ufalme wake’! Mwaka uliofuata tu, nuru nyangavu iliangaza kwenye mfano wa kondoo na mbuzi. Ilitambuliwa kwamba unabii huu ulikuwa utimizwe katika siku ya Bwana ya wakati huu, si wakati ujao katika Mileani kama ilivyofikiriwa awali. Katika kipindi cha Mileani, ndugu wa Kristo hawangekuwa wagonjwa, wala hawangefungwa gerezani. Na zaidi ya hayo, mwishoni mwa Mileani, ni Yehova Mungu, na si Yesu Kristo, atakayehukumu.—Mathayo 25:31-46.
12. Ni mmweko gani wa nuru uliotokea kuhusu Har–Magedoni?
12 Katika 1926 mmweko mwingine mwangavu wa nuru ulifunua kwamba vita ya Har–Magedoni haingekuwa mapinduzi ya kijamii, kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyodhani wakati fulani. Badala ya hivyo, ingekuwa vita ambayo Yehova ataonyesha uwezo wake kwa njia ya wazi sana hivi kwamba watu wote watasadiki kwamba yeye ni Mungu.—Ufunuo 16:14-16; 19:17-21.
Krismasi—Sikukuu ya Kipagani
13. (a) Ni nuru gani iliyoangazwa juu ya sherehe za Krismasi? (b) Kwa nini siku za kuzaliwa zilikoma kusherehekewa? (Tia ndani kielezi-chini.)
13 Muda mfupi baadaye, mmweko wa nuru ulifanya Wanafunzi wa Biblia waache kusherehekea Krismasi. Kabla ya wakati huo Krismasi ilikuwa imesherehekewa sikuzote na Wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote, na sherehe yayo katika makao makuu ya Brooklyn ilikuwa pindi yenye furaha sana. Lakini ikaja kutambuliwa kwamba mwadhimisho wa Desemba 25 ulikuwa hasa wa kipagani nao ulichaguliwa na Jumuiya ya Wakristo yenye uasi-imani ili kufanya iwe rahisi kugeuza wapagani. Isitoshe, ilipatikana kwamba Yesu hangeweza kuzaliwa katika majira ya kipupwe, kwa kuwa wakati wa kuzaliwa kwake, wachungaji walikuwa wakilisha makundi yao ya kondoo mashambani—jambo ambalo hawangefanya wakati wa usiku katika mwishoni-mwishoni mwa Desemba. (Luka 2:8) Badala ya hivyo, Maandiko yaonyesha kwamba Yesu alizaliwa karibu Oktoba 1. Wanafunzi wa Biblia pia walitambua kwamba wale waitwao eti wanaume wenye hekima waliomtembelea Yesu karibu miaka miwili baada ya kuzaliwa kwake walikuwa wanajimu wa kipagani.b
Jina Jipya
14. Kwa nini jina Wanafunzi wa Biblia halikuwakilisha vizuri watu wa Yehova?
14 Katika 1931 mmweko mwangavu wa kweli ulifunulia hao Wanafunzi wa Biblia jina la Kimaandiko lenye kufaa. Watu wa Yehova walikuwa wameelewa kwamba hawangekubali lolote kati ya majina waliobandikwa na wengine, kama vile Waruseli, Millennial Dawnists, na “wapinga-helo.”c Lakini wao pia walianza kutambua kwamba jina ambalo wao wenyewe walikuwa wamechukua—Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa—halikuwawakilisha vizuri. Wao walikuwa zaidi ya wanafunzi wa Biblia tu. Zaidi ya hayo, kulikuwa na wengine wengi waliokuwa wanafunzi wa Biblia lakini ambao hawakuhusika hata kidogo na Wanafunzi wa Biblia.
15. Wanafunzi wa Biblia walichukua jina jipi katika 1931, na kwa nini lafaa?
15 Wanafunzi wa Biblia walikuja kupataje jina jipya? Kwa miaka mingi The Watch Tower imekuwa ikitokeza sana jina la Yehova. Kwa hiyo, ilifaa sana kwamba Wanafunzi wa Biblia wachukue jina lipatikanalo kwenye Isaya 43:10: “Ninyi ni Mashahidi wangu, asema BWANA, na mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine.”
Utetezi na “Umati Mkubwa”
16. Kwa nini unabii mbalimbali wa urudisho haukuhusu kurudi kwa Wayahudi wa asili Palestina, bali unahusu nani?
16 Katika buku la pili la Vindication, lililotangazwa na Watch Tower Society katika 1932, mmweko wa nuru ulifunua kwamba unabii mbalimbali wa urudisho uliorekodiwa na Isaya, Yeremia, Ezekieli, na manabii wengine haukuhusu (kama ilivyofikiriwa wakati fulani) Wayahudi wa asili, ambao walikuwa wakirudi Palestina wakiwa hawana imani na wakiwa na madhumuni ya kisiasa. Badala ya hivyo, unabii mbalimbali wa urudisho, ambao ulikuwa na utimizo mdogo wakati Wayahudi walirudi kutoka utekwa wa Babiloni katika 537 K.W.K., ulikuwa na utimizo mkubwa katika kuokolewa na kurudishwa kwa Israeli la kiroho kuanzia 1919 na ule ufanisi uliofuata katika paradiso ya kiroho inayofurahiwa na watumishi wa kweli wa Yehova leo.
17, 18. (a) Baada ya muda, kupitia mmweko wa nuru, nini lilionyeshwa kuwa kusudi kubwa la Yehova? (b) Ni mmweko gani wa nuru kuhusu Ufunuo 7:9-17 uliotokea katika 1935?
17 Baada ya muda, mimweko ya nuru ilifunua kwamba kusudi kubwa la Yehova halikuwa wokovu wa viumbe vyake, bali kutetewa kwa enzi yake kuu. Kichwa kikubwa cha Biblia kilicho muhimu zaidi kilionwa kuwa, si ile fidia, bali ule Ufalme, kwa kuwa huo ungetetea enzi kuu ya Yehova. Huo ulikuwa mmweko wa nuru ulioje! Wakristo waliojiweka wakfu sasa hawakuhangaikia hasa kwenda kwao mbinguni.
18 Katika 1935 mmweko mwangavu wa nuru ulifunua kwamba umati mkubwa uliotajwa kwenye Ufunuo 7:9-17 haukuwa jamii ya pili ya kimbingu. Ilikuwa imefikiriwa kwamba wale wanaotajwa katika mistari hiyo walikuwa baadhi ya watiwa-mafuta ambao hawakuwa wamekuwa waaminifu vya kutosha na kwa hiyo walikuwa wamesimama mbele ya kiti cha enzi badala ya kuketi katika viti vya enzi wakitawala wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Yesu Kristo. Lakini hakuna jambo lolote kamwe la kuwa nusu mwaminifu. Ama mtu ni mwaminifu ama yeye si mwaminifu. Kwa hiyo ilionwa kwamba unabii ulirejezea umati mkubwa usioweza kuhesabika kutoka kwa mataifa yote unaokusanywa sasa na ambao tumaini lao ni la kidunia. Wao ni “kondoo” wa Mathayo 25:31-46 na “kondoo wengine” wa Yohana 10:16.
Msalaba—Si Ishara ya Kikristo
19, 20. Kwa nini msalaba hauwezi kuwa ishara ya Ukristo wa kweli?
19 Kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walifanya msalaba utokeze sana ukiwa ishara ya Ukristo. Hata walikuwa na “pini zenye msalaba na taji.” Kulingana na King James Version, Yesu aliwaomba wafuasi wake kuchukua “msalaba,” na wengi wakaja kuamini kwamba aliuawa kwenye msalaba. (Mathayo 16:24; 27:32) Kwa miongo mingi ishara hiyo ilikuwa ikitokea pia katika jalada la gazeti la Watch Tower.
20 Kitabu Riches, kilichotangazwa na Sosaiti katika 1936, kilielewesha wazi kwamba Yesu Kristo hakuuawa kwenye msalaba bali kwenye mti uliosimama wima. Kulingana na mamlaka moja, neno la Kigiriki (stau·rosʹ) lililotafsiriwa “msalaba” katika King James Version “laonyesha, hasa, mti uliosimama wima. [Wa]tofautiana na msalaba wa kidini wenye boriti mbili. . . . [Msalaba] huu ulianzia Kaldayo ya kale, nao ulitumiwa ukiwa ishara ya mungu Tamuzi.” Badala ya kufanywa kiabudiwa, kitu ambacho Yesu alitundikiwa chapasa kuchukiwa.
21. Ni nini litakalozungumzwa katika makala ifuatayo?
21 Kuna vielelezo vingine zaidi vya mimweko mikubwa na ile iwezayo kuonwa kuwa midogo. Kwa mazungumzo ya hayo, tafadhali ona makala ifuatayo.
[Maelezo ya chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Baada ya muda, ilionwa kwamba ikiwa uzaliwa wenye umaana zaidi uliopata kutokea haungesherehekewa, hatupaswi kusherehekea siku yoyote ya kuzaliwa. Zaidi ya hayo, wala Waisraeli wala Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku za kuzaliwa. Biblia yataja siku mbili tu za kuzaliwa, moja ya Farao na nyingine ya Herode Antipa. Kila sherehe ilikuwa na uuaji. Mashahidi wa Yehova hawasherehekei siku za kuzaliwa kwa sababu miadhimisho hiyo ina vyanzo vya kipagani nayo huelekea kukweza wenye kusherehekea siku ya kuzaliwa.—Mwanzo 40:20-22; Marko 6:21-28.
c Hilo ni kosa lililofanywa na madhehebu kadhaa ya Jumuiya ya Wakristo. Lutheri lilikuwa jina ambalo maadui wa Martin Luther walibandika wafuasi wake, ambao nao walilikubali. Vivyo hivyo, Wabaptisti walikubali jina walilokuwa wamebandikwa na watu wa nje kwa sababu walihubiri ubatizo wa kuzamisha. Kwa njia ambayo karibu ifanane na hiyo, Wamethodisti walikubali jina walilobandikwa na mtu wa nje. Kuhusu jinsi Society of Friends ilivyokuja kuitwa Quakers (watetemeshaji), The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Neno Quaker awali lilikusudiwa kudhihaki Fox [mwanzilishi], aliyemwambia hakimu mmoja Mwingereza ‘atetemekee Neno la Bwana.’ Hakimu huyo akamwita Fox ‘quaker.’”
-