Uadilifu Hutukuza Taifa
BAADA ya siku za mvua, inapendeza kama nini kuamka na kuona jua likiangaza katika anga isiyo na mawingu! Dunia imeburudishwa, na sasa mimea yaweza kukua kwa wingi. Wakati mmoja Yehova Mungu alitumia kielezi cha jinsi hiyo ili kuonyesha baraka za utawala mwadilifu. Alimwambia Mfalme Daudi hivi: “Atawalaye wanadamu kwa haki [“uadilifu,” NW], akitawala katika kicho cha Mungu, atakuwa kama nuru ya asubuhi jua lichapo [“liangazapo,” NW], asubuhi isiyo na mawingu. Lachipuza majani mabichi juu ya nchi, kwa mwangaza baada ya mvua.”—2 Samweli 23:3, 4.
Maneno ya Mungu yalithibitika kuwa ya kweli wakati wa utawala mwadilifu wa Mfalme Sulemani, mwana wa Daudi. Biblia huripoti hivi: “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.”—1 Wafalme 4:25.
Israeli la kale lilikuwa taifa teule la Mungu. Yeye alilipa sheria zake akaliambia kwamba ikiwa lingetii sauti yake, yeye angeliweka “juu ya mataifa yote ya duniani.” (Kumbukumbu la Torati 28:1) Haukuwa uadilifu wa Israeli wenyewe bali ni uadilifu wa Yehova uliowatukuza. Amri ambazo Mungu aliwapa zilikuwa bora zaidi ya sheria za mataifa yaliyowazunguka. Wao wakiwa kikundi cha watu, walikuwa wasio wakamilifu sawa na mataifa yote hayo. Kwa hiyo, sifa ya kuinuliwa kwao juu ya mataifa yaendea Sheria ya Yehova iliyo bora zaidi na kushikamana kwao sana nayo. Walipotii sheria za Yehova, walifurahia upendeleo wake na baraka yake. Mfalme Sulemani alijionea hilo wakati wa utawala wake. Yeye aliweza kusema hivi: “Uadilifu ndio hutukuza taifa, bali,” akaonya, “dhambi ni jambo lenye kufedhehesha kwa vikundi vya kitaifa.”—Mithali 14:34, NW.
Kwa kuhuzunisha, kupitia matendo ya kutokutii ya mara nyingi, taifa la Israeli lilishushwa cheo. Lilipatwa na fedheha ya kitaifa. Hilo hatimaye likaongoza kwenye kukataliwa kwalo daima na upendeleo kupewa taifa jipya la kiroho.—Mathayo 21:43.
Israeli wa Kiroho
Kwenye mkutano wa baraza lililoongoza la Kikristo katika Yerusalemu, Yakobo, aliyezaliwa Myahudi, alisema akiwa chini ya upulizio kwamba Mungu alikuwa ‘amewaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.’ (Matendo 15:14) Mtume Paulo aliliita taifa hili jipya la Kikristo “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Kwa habari ya kusudi la kuitwa kwao, Petro aliandika hivi: “Ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.” (1 Petro 2:9) Wakiwa watu wateule wa Mungu, walipaswa wang’ae wakiwa wamulikaji ulimwenguni. Uadilifu wa Yehova ungewainua juu.—Wafilipi 2:15.
Uteuzi wa Waisraeli hawa wa kiroho waweza kufananishwa na uchimbaji wa almasi. Wakati udongo wenye kujaa almasi unapotolewa nje ya mgodi, waweza kutokeza karati 1 (miligramu 200) ya almasi katika kila tani 3 za udongo. Njia iliyotumiwa wakati mmoja ya kutenganisha almasi ilihusisha kuchanganya udongo wenye almasi pamoja na maji na kuutiririsha mchanganyiko huo juu ya meza zenye mafuta. Almasi hazivutani na maji, nazo zilishikana na mafuta huku vitu visivyotakiwa vikipita na maji. Katika hatua hii almasi hazikuwa laini. Hata hivyo, zilipokatwa na kung’arishwa, zilirudisha nuru pande zote.
Kama vile almasi zisizovutana na maji ambazo si sehemu ya vile vitu vingine vinavyozizunguka, watu wa Yehova wametenganishwa na ulimwengu. (Yohana 17:16) Walipovutwa kwenye nuru mara ya kwanza, huenda hawakuwa na uangavu. Lakini Neno na roho ya Yehova inatokeza utu mpya ndani yao, nao wanang’aa kama wamulikaji katika ulimwengu huu. Ni kwa sababu ya uadilifu wa Yehova kwamba wao wanainuliwa juu na wanarudisha pande zote ile nuru tukufu ya kweli ya Ufalme, si kwa sababu ya uadilifu wao wenyewe.
Hata hivyo, tangu sehemu ya pili ya karne ya kwanza W.K., uasi-imani ulipenya ndani ya makutaniko ukaathiri wengi. Wale walioitwa Wakristo isivyofaa wakaunganika na mataifa ya ulimwengu na hawakuweza kuonwa kuwa tofauti na ulimwengu uliowazunguka.
Leo mabaki waaminifu wa Israeli wa kiroho wamerudishwa kwenye upendeleo wa Yehova. Wamejitenga na ulimwengu na wamejisafisha “na uchafu wote wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Wakiwa safi na wanyoofu mbele ya Yehova, wao huunga mkono uadilifu wake. Hilo limewainua kwenye mahali pa juu pa upendeleo juu ya mataifa ya ulimwengu. Kupitia kuhubiri kwao kwa bidii habari njema ya Ufalme, umati mkubwa wa kimataifa umevutwa kwa Yehova na umekuwa sehemu ya watu wake.—Ufunuo 7:9, 10.
Ulimwengu Waweza Kuona Tofauti
Nyakati nyingine wenye mamlaka za kilimwengu husifu mwenendo wa watumishi wa Mungu. Wakati fulani uliopita, ofisa mkuu wa usalama wa Uwanja wa Maonyesho wa Pretoria, Afrika Kusini, alitoa maelezo juu ya mwenendo wa Mashahidi wa Yehova, kutoka jamii zote, wanaotumia uwanja huo kwa mikusanyiko yao ya kila mwaka. Miongoni mwa mambo mengine, yeye aliandika hivi: “Kila mtu alikuwa [na adabu] na ni mwenye adabu, watu wanaosemezana vizuri, mtazamo ulioonyeshwa katika hizi siku chache ambazo zimepita—[mambo hayo] yote yathibitisha kadiri ya ubora wa washiriki wa jamii yenu, na kwamba wote huishi pamoja kama familia moja yenye furaha.”
Watu wa Yehova waweza kuchangia uadilifu wa taifa lake si kwenye makusanyiko hayo makubwa pekee bali pia katika maisha zao za faragha. Kwa kielelezo, tawi la Afrika Kusini la Watch Tower Society lilipokea barua kutoka kwa mwanamke fulani katika Johannesburg, ikisema hivi: “Juma lililopita niliendesha gari langu nikiwa na kibeti changu juu yalo. Kilianguka katika [barabara iitwayo] Jan Smuts Avenue nacho kikaokotwa pamoja na vitu vyote vilivyokuwa ndani yacho na mshiriki wa kutaniko lenu, Bw. R—, aliyenipigia simu na kukirudisha kwangu. . . . Nathamini sana unyoofu huu ambao umekuwa sifa haba katika nyakati za sasa na ninapongeza kutaniko lenu kwa kuweka kanuni ambazo washiriki wenu hushikamana nazo.”
Ndiyo, kwa kushikamana na kanuni za Yehova zenye uadilifu, watu wake wanafanywa watokeze kuwa tofauti na ulimwengu. Kwa sababu wao huonyesha uadilifu wa Yehova, wale wenye mioyo minyoofu wanavutwa kwenye kutaniko la Kikristo. Ni jambo la asili kuvutiwa na kitu kilicho safi na ambacho kimetakata. Kwa kielelezo, wakati mmoja mgeni alikuja kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova katika Zurich, Uswisi, akasema kwamba alitaka kuwa mshiriki wa kutaniko. Yeye alieleza kwamba dadake alikuwa ametengwa na ushirika kwa sababu ya ukosefu wa adili akaongeza kwamba alitaka kujiunga na tengenezo ambalo “halivumilii mwenendo mbaya.” Hata New Catholic Encyclopedia yakiri kwamba Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa “kimojapo vikundi vyenye mwenendo bora zaidi ulimwenguni.”
Ingawa uadilifu huinua, dhambi huleta fedheha juu ya jina zuri la mtu, hasa ikiwa kosa zito limepata kujulikana katika jumuiya. Nyakati nyingine kutaniko la Kikristo linalazimika kuchukua aibu ambayo limewekewa wakati washiriki mmoja-mmoja wanapofanya dhambi nzito. Kwa kueleweka, washiriki waaminifu wa kutaniko waweza kutetea jina zuri la kutaniko kwa kuonyesha kwamba mkosaji ametiwa nidhamu katika njia yenye rehema, yaani, kwa kupatana na kanuni za Kimaandiko. Mtu akizoea dhambi naye hatatubu, yeye ataondoshwa kutanikoni—atatengwa na ushirika.—1 Wakorintho 5:9-13.
Sababu kwa Nini Wengine Wanatengwa na Ushirika
Ingawa maelfu ya watu wanatengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo kila mwaka, hao ni asilimia ndogo tu ya Mashahidi karibu milioni tano ulimwenguni. Kwa nini hatua hiyo kali sana ichukuliwe dhidi ya yeyote katika kutaniko la Kikristo? Namna ya kosa ni mojapo mambo yanayoamua. Lakini jambo la maana zaidi ni kama mkosaji ni mwenye kutubu kikweli kosa zito lililofanywa. Ikiwa amechomwa moyo kikweli, amemwendea Yehova katika sala ya kuhisiwa moyoni, akiomba msamaha wa dhambi iliyofanywa dhidi Yake, naye ametafuta msaada wa wanaume wenye daraka kutanikoni, yeye aweza kusaidiwa kupata tena upendeleo wa Mungu na kuendelea kuwa sehemu ya kutaniko.—Mithali 28:13; Yakobo 5:14, 15.
Wakati mtoto aliye na uhusiano mzuri, wenye nguvu pamoja na babake afanya jambo linalomhuzunisha baba, wote wawili wapaswa kufanya haraka ili kurudisha uhusiano huo wenye thamani. Vivyo hivyo, tunapoweka wakfu maisha zetu kwa Yehova, sisi twaingia katika uhusiano naye ulio na thamani zaidi. Kwa hiyo, tufanyapo jambo linalomhuzunisha, twapaswa kutenda haraka katika kujaribu kurudisha uhusiano huo na Baba yetu wa Kimbingu.
Kwa furaha, wengine waliokuwa katika hali ya kutengwa na ushirika wamezingatia moyoni kielezi cha mwana mpotevu. Humo Yehova anafananishwa na Baba mwenye upendo aliye tayari kupokea mtenda-dhambi mwenye kutubu ikiwa huyo ageuka na kutafuta msamaha wa Mungu. (Luka 15:11-24) Toba ya kweli, yenye kuhisiwa moyoni na kugeuka mbali na lililo baya kumekuwa njia ya kurudi kwenye upendeleo wa Yehova na kwenye kutaniko la Kikristo. Wakosaji wengine wenye kutubu ambao wamehisi kupondeka chini ya mzigo wenye kulemea wa hatia yao wamesukumwa kutubu na kuchukua hatua za kurudi kwenye mazingira yenye upendo ya kutaniko la Kikristo. Hivyo wamekuja kuthamini maneno ya Yehova kwenye Isaya 57:15.
Ili kuzuia watu mmoja-mmoja wasirudi kwenye utunzaji wenye upendo wa Yehova, Shetani angetaka watu waamini kwamba hakuna msamaha kwa dhambi ambazo zimefanywa. Lakini dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu inatosha ili kufunika dhambi za wowote wanaotubu—ndiyo, hata hali yenye dhambi iliyorithiwa ya “ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Dhambi moja isiyofunikwa na fidia ni dhambi dhidi ya roho takatifu ya Mungu, ambayo ni kuasi kimakusudi dhidi ya utendaji wa roho ya Mungu, kama zile dhambi nzito za Yuda Iskariote na waandishi na Mafarisayo wengi.—Mathayo 12:24, 31, 32; 23:13, 33; Yohana 17:12.
Kuunga Mkono Uadilifu wa Yehova
Tangu mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliporudishwa kwenye upendeleo wa Yehova katika 1919, wamezidi kuinuliwa juu ya ulimwengu unaowazunguka. Hilo si kwa sababu ya wema wowote kwa upande wao bali ni kwa sababu ya utayari wao wa kujinyenyekeza chini ya sheria na viwango vya Yehova. Likiwa tokeo, mamilioni ya “kondoo wengine” wa Kristo yamevutwa kushirikiana na Israeli wa kiroho yakiwa waandamani waaminifu-washikamanifu. (Yohana 10:16) Watu hawa humletea Yehova utukufu na heshima katika ulimwengu ambao umetengwa mbali na viwango vyenye uadilifu vya Mungu. Ni kama vile gazeti la Afrika Kusini Personality lilivyoonelea wakati mmoja: “Mashahidi wa Yehova waonekana kama wanabubujika sifa zilizo nzuri na ni kama hawana [zile sifa] mbaya.”
Ili kudumisha hali hii ya kuinuliwa juu katika ulimwengu usiomwogopa Mungu, kila mshiriki mmoja-mmoja wa kutaniko la Kikristo ahitaji kuishi maisha safi, yaliyo manyoofu mbele ya Yehova. Katika Biblia, tengenezo la Yehova la kimbingu linaonyeshwa kwa vitu safi. Linaonwa likiwa mwanamke mwenye kupendeza aliyevikwa jua na akiwa na mwezi chini ya miguu yake. (Ufunuo 12:1) Yerusalemu Jipya, linafafanuliwa kuwa jiji takatifu, lenye sura ya kupendeza. (Ufunuo 21:2) Washiriki waaminifu wa bibi-arusi wa Kristo wanapewa “kitani nzuri, ing’arayo, [na] safi.” (Ufunuo 19:8) Wale wa umati mkubwa wanaonwa wakiwa “wamevikwa mavazi meupe.” (Ufunuo 7:9) Watu wanaoelekea kwenye uadilifu wanavutwa kwenye tengenezo lililo safi. Kinyume cha hilo, tengenezo la Shetani si safi. Mfumo wake wa kidini unaonyeshwa kuwa kahaba, na wale walio nje ya jiji takatifu wanafafanuliwa kuwa wachafu, wasio safi.—Ufunuo 17:1; 22:15.
Uhai udumuo milele unaahidiwa kwa walio waadilifu. Watu waliokusanyika wanaounga mkono uadilifu wa Yehova wana taraja la kuokoka mwisho wa mfumo huu mwovu. “Kila anisikilizaye atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya,” Mungu aahidi kwenye Mithali 1:33.
Itachangamsha kama nini wakati Sulemani Mkubwa Zaidi, Kristo Yesu, atawalapo juu ya ule ulimwengu mpya katika uadilifu, katika hofu ya Yehova! (2 Petro 3:13) Itakuwa kama vile nuru ya asubuhi jua liangazapo, asubuhi isiyo na mawingu. Wakaaji wote wa dunia wataishi katika usalama, kana kwamba kila mmoja akiketi chini ya mzabibu na mtini wake mwenyewe. Jamii ya kibinadamu yenye uadilifu itairembesha dunia na kukaa katika mahali payo pafaapo katika ulimwengu wote mzima kwa sifa idumuyo milele ya Mungu wetu, Yehova.—Mika 4:3, 4; ona pia Isaya 65:17-19, 25.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Garo Nalbandian