-
Yehova Mungu Awarehemu MabakiUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
‘Chipukizi la Yehova’
5, 6. (a) Isaya aufafanuaje wakati wenye amani baada ya tufani inayokuja? (b) Ni nini maana ya neno “chipukizi,” nalo laonyesha nini juu ya nchi ya Yuda?
5 Sauti ya Isaya yachangamka atazamapo mbele kwenye kipindi cha amani baada ya tufani inayokuja. Aandika: “Siku hiyo chipukizi la BWANA [“Yehova,” “NW”] litakuwa zuri, lenye utukufu, na matunda ya nchi yatakuwa mema sana, na kupendeza, kwa ajili ya Waisraeli wale waliookoka.”—Isaya 4:2.
6 Hapo Isaya azungumza juu ya urudisho. Neno la Kiebrania linalofasiriwa “chipukizi” larejezea ‘kile kinachoanza kuchipuka, mche, tawi.’ Hilo huhusianishwa na ufanisi, ongezeko, na baraka kutoka kwa Yehova. Kwa hiyo Isaya atoa wazo la tumaini—ukiwa unaokuja hautadumu milele. Kwa baraka ya Yehova, nchi ya Yuda iliyokuwa imesitawi hapo awali itazaa tena matunda mengi.a—Mambo ya Walawi 26:3-5.
7. Chipukizi la Yehova litakuwaje “zuri, lenye utukufu”?
7 Isaya atumia maneno dhahiri kufafanua utukufu wa mabadiliko yaliyo mbele. Chipukizi la Yehova “litakuwa zuri, lenye utukufu.” Neno “zuri” latukumbusha juu ya uzuri wa Bara Lililoahidiwa wakati ambapo Yehova aliwapa Israeli bara hilo karne kadhaa mapema. Lilikuwa zuri sana hivi kwamba lilionwa kuwa “utukufu [“kito,” New American Bible] wa nchi zote.” (Ezekieli 20:6) Hivyo, maneno ya Isaya yawahakikishia watu hao kuwa nchi ya Yuda itarudishwa kwenye utukufu na uzuri wake wa hapo awali. Kwa kweli, itakuwa kama kito kitukufu duniani.
8. Ni nani watakaokuwapo ili kufurahia uzuri uliorudishwa wa nchi, na Isaya aelezaje hisia zao?
8 Japo hivyo, ni nani watakaokuwapo ili kufurahia uzuri uliorudishwa wa nchi hiyo? “Waisraeli wale waliookoka,” aandika Isaya. Naam, baadhi ya watu wataokoka uharibifu wenye kufedhehesha uliotabiriwa hapo awali. (Isaya 3:25, 26) Mabaki ya wenye kuokoka watarudi Yuda nao watashiriki kuirudisha. Kwa hao waliorudishwa—“walioponyoka”—mazao mengi ya nchi yao iliyorudishwa “yatakuwa mema sana, na kupendeza.” (Isaya 4:2; NW, kielezi-chini) Fedheha iliyoletwa na ukiwa itabadilika na kuwa hali mpya ya kujionea fahari.
9. (a) Maneno ya Isaya yalitimizwaje mwaka wa 537 K.W.K.? (b) Kwa nini yaweza kusemwa kuwa “walioponyoka” hutia ndani baadhi ya wale waliozaliwa uhamishoni? (Ona kielezi-chini.)
9 Kupatana na maneno ya Isaya, dhoruba ya hukumu ilifika mwaka wa 607 K.W.K. Wababiloni walipoharibu Yerusalemu na Waisraeli wengi wakaangamia. Baadhi yao waliokoka na kupelekwa uhamishoni huko Babiloni, lakini isingekuwa kwa sababu ya rehema ya Mungu, hakuna yeyote ambaye angeokoka. (Nehemia 9:31) Hatimaye, Yuda iliachwa ukiwa kabisa. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-21) Ndipo, mwaka wa 537 K.W.K., Mungu wa rehema akawaruhusu “walioponyoka” warejee Yuda ili kuirudisha ibada ya kweli.b (Ezra 1:1-4; 2:1) Toba ya dhati ya wahamishwa hao waliokuwa wakirudi yasimuliwa vema katika Zaburi 137, ambayo labda iliandikiwa utekwani au muda mfupi baadaye. Waliporudi Yuda, walilima na kupanda mbegu nchini humo. Hebu wazia jinsi ambavyo hapana budi walihisi walipoona kwamba Mungu anabariki juhudi zao, akiifanya nchi kuchipuka kama “bustani ya Edeni” yenye kuzaa sana!— Ezekieli 36:34-36, BHN.
10, 11. (a) Wanafunzi wa Biblia walikuwaje katika utekwa kwa “Babiloni Mkubwa” mapema katika karne ya 20? (b) Yehova alibarikije mabaki ya Waisraeli wa kiroho?
10 Kurudishwa kama huko kumetukia katika siku yetu. Mapema katika karne ya 20, Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo, waliingia katika utekwa wa kiroho kwa “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 17:5) Ingawa walikuwa wameyakataa mafundisho mengi ya kidini yasiyo ya kweli, Wanafunzi wa Biblia walikuwa bado wana doa la mawazo na mazoea fulani ya Kibabiloni. Upinzani uliochochewa na makasisi ulifanya baadhi yao watiwe gerezani kihalisi. Nchi yao ya kiroho—eneo lao la kidini, au la kiroho—iliachwa ukiwa.
11 Lakini katika masika ya mwaka wa 1919, Yehova aliwarehemu mabaki hao wa Waisraeli wa kiroho. (Wagalatia 6:16) Aliona toba yao na tamaa yao ya kumwabudu katika roho na kweli, kwa hiyo akaelekeza kuachiliwa kwao kutoka katika kifungo halisi gerezani na, la muhimu zaidi, kutoka katika utekwa wa kiroho. “Walioponyoka” hao walirudishwa kwenye eneo lao la kiroho, alilowapa Mungu na kulifanya lichipuke kwa wingi. Eneo hilo la kiroho limedhihirisha sura nzuri na yenye kuvutia ambayo imewachochea mamilioni ya watu wengine wenye kumhofu Mungu wajiunge na mabaki katika ibada ya kweli.
12. Maneno ya Isaya yatukuzaje rehema ya Yehova kwa watu wake?
12 Hapo maneno ya Isaya yatukuza rehema ya Mungu juu ya watu wake. Ingawa Waisraeli wakiwa taifa walimwasi Yehova, yeye aliwarehemu mabaki wenye toba. Twaweza kufarijika kwa kufahamu kuwa hata wale wanaotenda makosa mazito wanaweza kumrudia Yehova wakiwa na tumaini. Wenye kutubu hawapaswi kuhisi kuwa hawawezi kupata rehema ya Yehova, kwa sababu yeye haukatai moyo wenye huzuni. (Zaburi 51:17) Biblia yatuhakikishia: “BWANA amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA [“Yehova,” NW] anavyowahurumia wamchao.” (Zaburi 103:8, 13) Kwa hakika, Mungu huyo mwenye rehema astahili sifa zetu zote!
-
-
Yehova Mungu Awarehemu MabakiUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
a Wasomi fulani hudokeza kuwa usemi ‘chipukizi la Yehova’ humrejezea kwa njia isiyo ya moja kwa moja, Mesiya ambaye hangetokea kabla ya kurudishwa kwa Yerusalemu. Katika Targum za Kiaramu, fungu hilo lasimuliwa hivi kwa maneno mengine: “Mesiya [Kristo] wa Yehova.” Kwa kupendeza, baadaye Yeremia alitumia neno hilohilo la Kiebrania (tseʹmach) anapozungumza juu ya Mesiya akiwa kama “chipukizi la haki” analochipushiwa Daudi.—Yeremia 23:5; 33:15.
b “Walioponyoka” walitia ndani baadhi ya wale waliozaliwa uhamishoni. Hao wangeonwa kuwa ‘wameponyoka,’ kwa maana hawangalizaliwa kamwe ikiwa babu zao hawangaliokoka uharibifu.—Ezra 9:13-15; linganisha Waebrania 7:9, 10.
-