Je, Tunaishi Katika Siku za Mwisho?
FUNGU la maneno “nyakati mbaya zilizo ngumu kushughulika nazo” latafsiriwa kutoka maneno ya Kigiriki kai·roiʹ. kha·le·poiʹ. (2 Timotheo 3:1, NW) Neno kha·le·poiʹ ni wingi wa neno ambalo kihalisi humaanisha “kali” na huwasilisha wazo la tisho na hatari. Mfafanuzi mmoja wa Biblia asema neno hilo hurejezea “shambulio lenye kutisha la uovu.” Kwa hivyo, ingawa mihula iliyopita ilipatwa na msukosuko, “siku za mwisho” zingekuwa katili zaidi ya ilivyo kawaida. Kama vile 2 Timotheo 3:13 inavyosema, “watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu.”
Je, hili lafafanua siku yetu? Acheni tuchanganue baadhi ya uthibitisho hususa uliorekodiwa kwenye 2 Timotheo 3:2-5 ili tuone ikiwa huo waashiria kwamba tunaishi katika siku za mwisho.
“Watu watakuwa . . . wenye kupenda fedha.”—2 Timotheo 3:2.
Ulaghai umekuja kuwa, kama U.S.News & World Report inavyouita, “upitaji kiasi wa uhalifu wa kiuchumi.” Katika Marekani, kiwango cha ulaghai wa utunzi wa afya pekee chabaki kati ya dola bilioni 50 na bilioni 80 kwa mwaka. Kwa kusikitisha, ukosefu huo wa uaminifu ni wa kawaida. Kama vile Gary Edwards, rais wa Kitovu cha Utafiti wa Maadili, aoneleavyo tuna “utamaduni ambao nyakati nyingine husherehekea ukosefu wa ufuatiaji wa haki.” Yeye aeleza hivi: “Sisi huona walaghai kuwa ndio mashujaa, watu ambao ni wanasiasa, wanabiashara wanaodanganya serikali na kuepuka adhabu.”
“Wenye kiburi.”—2 Timotheo 3:2.
Mtu mwenye kiburi huwadharau wengine. Jinsi hili lionekanavyo katika ubaguzi wa kijamii na wa kitaifa leo! “Watu wote walio wachache ndio shabaha,” lasema The Globe and Mail la Toronto, Kanada. “Jeuri ya kijamii yazidi kupanda katika Ujerumani, kikundi kinachotetea ukuu wa weupe ni chenye kutenda katika Marekani na alama za swastika zinaharibu vijia vya kando ya barabara na masinagogi ya Toronto.” Irving Abella, rais wa Kongamano la Kiyahudi la Kanada, asema: “Twauona kila mahali: katika Sweden, Italia, Uholanzi na Ubelgiji na vilevile Ujerumani.”
“Wasiotii wazazi wao.”—2 Timotheo 3:2.
“Vijana wenye kujisitawisha sana wanalaumiwa na wengi kwa ajili ya kizazi cha watoto watundu walio na midomo mirefu, wenye nia ya kukorofishana, wasio na heshima,” lasema The Toronto Star. Uasi unaoanza nyumbani mara nyingi huenea shuleni. Mwalimu mmoja aonelea kwamba watoto wadogo kiasi cha umri wa miaka minne hurudisha majibu kwa ukavu wa macho. “Walimu wanatumia wakati mwingi zaidi katika kushughulikia tabia kuliko wanaotumia kufundisha,” yeye asema. Bila shaka, si vijana wote walio waasi. Hata hivyo, “kama kitabia,” aonelea mwalimu mmoja wa siku nyingi wa shule ya sekondari Bruce MacGregor, “wao huonekana wakiwa na heshima kidogo sana kwa kitu chochote.”
“Wasio na shauku ya asili.”—2 Timotheo 3:3, NW.
Siku za mwisho zingeona uzorotaji mkubwa katika familia—ambapo, zaidi ya mahali penginepo pote, shauku ya asili yapaswa kuwepo. The New York Times laripoti kwamba “jeuri ya nyumbani ndio kisababishi kinachoongoza cha umizo na kifo kwa wanawake Wamarekani, ikisababisha dhara zaidi ya aksidenti za magari, kulalwa kinguvu, na kuporwa yakiunganishwa.” Kwingi kwa kutendwa vibaya kwa watoto hufanywa na washirika wa familia wanaotumainika. Kiwango cha juu cha talaka, kutenda vibaya wazee-wazee, na utoaji-mimba pia hutoa uthibitisho kwamba wengi “wanakosa kabisa . . . shauku ya kawaida ya kibinadamu.”—Phillips.
“Wakali, wasiopenda mema.”—2 Timotheo 3:3.
“Wauaji wachanga hawahitaji nia ili kuua mtu,” aandika mwanasafu fulani wa gazeti Bob Herbert. “Idadi kubwa za watoto walishika kwa idili ile dhana ya kulipua binadamu mwengine ‘bila sababu hususa.’” Hata wazazi wengine yaonekana hawana hisi ya kiadili. Wakati kikundi cha vijana matineja kilishtakiwa kwa kupokea pointi kimashindano ili kuona ni nani angepata pointi nyingi zaidi kwa kufanya ngono na wasichana wengi iwezekanavyo, baba mmoja alieleza hivi: “Hakuna chochote mvulana wangu alichofanya hakingefanywa na kijana yeyote Mmarekani mwenye utendaji katika umri wake.”
“Wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:4.
Kulingana na kadirio moja, matineja hutumia saa 15 na vyombo vya habari vya kielektroni katika kila saa inayotumiwa na kikundi cha kidini. “Leo,” laripoti Altoona Mirror, “utamaduni unaoendeshwa na vyombo vya habari unaositawi madukani na kwenye kumbi za shule hutawala maisha ya utineja. Halafu yaja familia. Na mwishoni mwa orodha ni kanisa.” Mirror laonelea pia, “ikiwa wazazi hawapo, na makanisa yako kimya, basi vyombo vya habari vyawa sauti kubwa zaidi katika maisha ya vijana.”
“Wakiwa na namna ya ujitoaji kimungu lakini wakithibitika kutokuwa kweli kwa nguvu ya huo.”—2 Timotheo 3:5, NW.
Kweli ya Biblia ina nguvu za kubadili maisha. (Waefeso 4:22-24) Lakini baadhi ya matendo yasiyo ya kimungu kabisa hutendeka chini ya shela ya dini. Kielelezo chenye kuogofya ni kutendwa vibaya kingono kwa watoto na makasisi. Kulingana na The New York Times, mwanasheria fulani katika Marekani “asema ana kesi 200 zinazongoja katika majimbo 27 kwa niaba ya wateja wake ambao wasema walitendwa vibaya na makasisi.” Kwa kweli, aina yoyote au kujidai ujitoaji kimungu wanakoonyesha makasisi hawa unafunuliwa kuwa unafiki mtupu kupitia kwa kazi zao za uovu.
UTHIBITISHO ZAIDI WA SIKU ZA MWISHO
2 TIMOTHEO 3:2-4, NW, HUTAARIFU PIA KWAMBA WATU WATAKUWA . . .
□ “Wenye kujitanguliza.”
□ “Wakufuru.”
□ “Wasio na shukrani.”
□ “Wasio waaminifu-washikamanifu.”
□ “Wasiotaka kufanya upatano wowote.”
□ “Wachongezi.”
□ “Bila ujidhibiti.”
□ “Wasaliti.”
□ “Wenye vichwa vigumu.”
□ “Wenye kututumuka kwa majivuno.”
“ISHARA YA KUWAPO KWAKO”
Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliulizwa: “Itakuwa ni nini ishara ya kuwapo kwako na umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Yesu alitaja kihususa hali na matukio ambayo yangeonyesha siku za mwisho. Acheni tuchunguze baadhi yazo.
“Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.”—Mathayo 24:7.
“Karne ya ishirini—ingawa kwa ujumla ni ya ujamii ulioboreshwa na ufikirio uliokaziwa wa kiserikali kwa maisha ya maskini—imemilikiwa na bunduki-mimina, kifaru, ndege za kivita za B-52, bomu ya kinyukilia na, mwishowe kombora la masafa marefu. Imetiwa alama na vita vyenye umwagaji damu na vyenye uharibifu zaidi ya vile vya muhula wowote ule.”—Milestones of History.
“Matetemeko ya nchi mahali mahali.”—Mathayo 24:7.
Katika karne hii, matetemeko yafikayo 7.5 hadi 8.3 kwenye kipimio cha Ritcher yamepata kuonekana katika Chile, China, India, Iran, Italia, Japani, Peru, na Uturuki.
“Kutakuwa . . .na mambo ya kutisha.”—Luka 21:11.
Kwa sababu ya matukio yenye kuhofisha katika miaka ya majuzi, labda hofu ndiyo hisia-moyo pekee iliyo kubwa zaidi ya zote katika maisha ya watu. Watu wanahofu vita, uhalifu, uchafuzi, maradhi, infleshoni, na mambo mengine mengi ambayo yanatisha usalama wao na maisha yao yenyewe.
“Upungufu wa chakula.”—Mathayo 24:7, NW.
“Njaa Yatisha Huku Vikundi vya Msaada Vikizozana,” chatangaza kichwa kikuu katika gazeti New Scientist. Kulingana na aliyekuwa rais fulani wa Marekani, njaa yatisha kuangamiza sayari katika kipindi cha miongo miwili. “Licha ya matabiri hayo yenye kutisha,” makala hiyo yaeleza, “kiwango cha msaada ambacho nchi tajiri hupatia nchi zinazositawi kwa ajili ya usitawishaji wa kilimo kinapungua kwa kutazamisha.”
“Mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kuambukiza.”—Luka 21:11, NW.
Kulingana na jopo fulani la wastadi, pigano la serikali ya Marekani dhidi ya UKIMWI—likigharimu zaidi ya dola milioni 500 kila mwaka—limeitwa kushindwa kwenye kuhuzunisha. “Tunapoteza kizazi kizima cha utokezaji mazao kwa sababu ya UKIMWI,” aonya Dakt. Donna Sweet, anayefanya kazi na wagonjwa wapatao 200 hadi 300. Katika Marekani, UKIMWI sasa ndio kisababishi kinachoongoza cha kifo miongoni mwa wanaume kati ya umri wa miaka 25 hadi 44.
“Kuongezeka kwa maasi.”—Mathayo 24:12.
Uchunguzi fulani wa Marekani wa vijana 2,500 ulifunua kwamba asilimia 15 walikuwa wamebeba bunduki wakati fulani katika siku 30 zilizokuwa zimepita, asilimia 9 walikuwa wamefyatulia mtu mwingine, na asilimia 11 walikuwa wamepigwa risasi katika mwaka uliopita.
NI NINI KILICHO MBELE?
Kama vile tumekwisha kuona, wanadamu wako mbali sana na mkondo ufaao, mbali sana na ulimwengu wenye amani. Kuhusiana na ukuu, hali zilizotajwa juu haziwezi kulinganishwa na chochote. Kwa kweli, familia ya kibinadamu inajikuta katika eneo isilolifahamu. Inapitia katika muhula unaoitwa siku za mwisho.
Ni nini kitakachokuja baada ya kipindi hiki?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
Michael Lewis/Sipa Press