Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi—1993 | Septemba 15
    • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo

      “Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW].”—2 PETRO 1:5, 6.

      1, 2. Kwa nini ni lazima sisi sote tuvumilie hadi mwisho?

      MWANGALIZI mmoja asafiriye pamoja na mke wake walikuwa wakimtembelea Mkristo mwenzao aliyekuwa katika miaka yake ya 90. Alikuwa ametumia miongo kadhaa katika huduma ya wakati wote. Walipokuwa wakiongea, ndugu huyo mwenye umri mkubwa zaidi aliyakumbuka baadhi ya mapendeleo aliyokuwa amefurahia katika miaka iliyopita. “Lakini,” akaomboleza huku machozi yakianza kutiririka usoni pake, “sasa siwezi kufanya mengi.” Mwangalizi huyo asafiriye alifungua Biblia yake, akasoma Mathayo 24:13, ambapo Yesu Kristo ananukuliwa akisema: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” Kisha mwangalizi huyo akamtazama ndugu huyo mpendwa na kusema: “Mgawo wa mwisho ambao sisi sote tunao, haidhuru tunaweza kufanya mengi kadiri gani au machache kadiri gani, ni kuvumilia hadi mwisho.”

      2 Naam, tukiwa Wakristo ni lazima sisi sote tuvumilie hadi mwisho wa mfumo huu wa mambo au hadi mwisho wa maisha zetu. Hakuna njia nyingine ya kupokea kibali cha Yehova ili kupata wokovu. Tumo katika shindano la mbio la kupata uhai, na ni lazima “tupige mbio kwa saburi [uvumilivu, NW]” mpaka tufike mwisho. (Waebrania 12:1) Mtume Petro alikazia umaana wa sifa hiyo alipowahimiza Wakristo wenzake hivi: “Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW].” (2 Petro 1:5, 6) Lakini uvumilivu ni nini hasa?

      Uvumilivu—Maana Yao

      3, 4. Kuvumilia kunamaanisha nini?

      3 Kuvumilia kunamaanisha nini? Kitenzi cha Kigiriki kwa neno “-vumilia” (hy·po·meʹno) humaanisha kihalisi “kuendelea au kufululiza kuwa chini.” Hilo hutokea mara 17 katika Biblia. Kulingana na watunga-kamusi W. Bauer, F. W. Gingrich, na F. Danker, hilo humaanisha “kuendelea kusimama badala ya kutoroka . . . , kusimama imara, kukabiliana na hali.” Nomino ya Kigiriki kwa neno “uvumilivu” (hy·po·mo·neʹ) hutokea zaidi ya mara 30. Kuhusu neno hilo, A New Testament Wordbook, cha William Barclay, chasema: “[Uvumilivu] ni nia inayoweza kustahimili mambo, si kwa sababu tu ya kukata tamaa, bali kwa [sababu ya kuwa na] tumaini jangavu . . . Ni ile sifa inayomfanya mtu aendelee kusimama akikabili magumu. Ni ile sifa iwezayo kugeuza jaribu lililo gumu zaidi liwe utukufu kwa sababu inatazama ng’ambo ya maumivu hadi kwenye mradi.”

      4 Basi, uvumilivu hutuwezesha tusimame imara na tusikose kuwa na tumaini tunapokabili vizuizi au magumu. (Warumi 5:3-5) Hutazama ng’ambo ya maumivu yaliyopo hadi kwenye mradi—ile tuzo, au zawadi, ya uhai wa milele, iwe ni mbinguni au duniani.—Yakobo 1:12.

      Uvumilivu—Kwa Nini?

      5. (a) Kwa nini Wakristo wote ‘wanahitaji kuwa na uvumilivu’? (b) Majaribu yetu yanaweza kugawanywa katika vikundi gani viwili?

      5 Tukiwa Wakristo, sisi sote ‘tunahitaji kuwa na uvumilivu.’ (Waebrania 10:36, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa nini? Kwa msingi ni kwa sababu ‘tunaangukia katika majaribu mbalimbali.’ Maandishi ya Kigiriki hapa kwenye Yakobo 1:2 hudokeza kabiliano lisilotazamiwa au lisilopendeza, kama vile wakati mtu anapokabiliwa na mnyang’anyi. (Linganisha Luka 10:30.) Tunaangukia majaribu yanayoweza kugawanywa katika vikundi viwili: yale yaliyo ya kawaida kwa wanadamu kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa, na yale yanayotokea kwa sababu ya ujitoaji kimungu wetu. (1 Wakorintho 10:13; 2 Timotheo 3:12) Baadhi ya majaribu hayo ni gani?

      6. Shahidi mmoja alivumiliaje alipokabiliwa na ugonjwa wenye maumivu?

      6 Ugonjwa mahututi. Kama vile Timotheo, ni lazima Wakristo fulani wavumilie ‘magonjwa ya mara kwa mara.’ (1 Timotheo 5:23) Hasa tunapokabili ugonjwa wenye kuendelea, labda wenye maumivu mengi, ndipo tunahitaji kuvumilia, kusimama imara, kwa msaada wa Mungu na tusikose kuwa na tumaini letu la Kikristo. Fikiria kielelezo cha Shahidi mmoja katika miaka yake ya mapema ya 50 aliyeshindana vikali na kwa muda mrefu, dhidi ya tezi lenye kudhuru na lenye kukua upesi. Kupitia upasuaji wa visa viwili aliendelea kuwa thabiti katika azimio lake la kutokubali kutiwa damu mishipani. (Matendo 15:28, 29) Lakini tezi hilo lilitokea tena tumboni mwake, likaendelea kukua karibu na uti wa mgongo wake. Lilipoendelea kukua, alipatwa na maumivu makali ya kimwili yasiyowazika ambayo hayakuweza kupunguzwa na kiasi chochote cha dawa. Lakini, alitazama ng’ambo ya maumivu yaliyopo hadi kwenye zawadi ya uhai katika ulimwengu mpya. Aliendelea kushiriki tumaini lake jangavu pamoja na madaktari, wauguzi, na wageni. Alivumilia hadi mwisho kabisa—mwisho wa uhai wake. Huenda ikawa tatizo lako la afya si lenye kutisha uhai au lenye maumivu kama lile lililompata ndugu huyo mpendwa, lakini huenda bado likawa mtihani mkubwa wa uvumilivu.

      7. Uvumilivu hutia ndani maumivu ya aina gani kwa baadhi ya ndugu na dada zetu wa kiroho?

      7 Maumivu ya kihisiamoyo. Mara kwa mara, baadhi ya watu wa Yehova hukabili “huzuni ya moyo” inayosababisha ‘roho iliyopondeka.’ (Mithali 15:13) Mshuko mkubwa wa moyo ni jambo la kawaida katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, NW) Science News la Desemba 5, 1992, liliripoti hivi: “Viwango vya mshuko mkubwa wa moyo, ambao mara nyingi ni wenye kulemaza vimeongezeka katika kila kizazi kinachofuata ambacho kimezaliwa tangu 1915.” Kuna visababishi tofauti-tofauti vya mshuko huo wa moyo, kuanzia sababu zinazohusu viungo vya mwili hadi maono yasiyopendeza yanayoumiza sana. Kwa Wakristo fulani, uvumilivu unahusisha shindano la kila siku la kusimama imara wanapokabili maumivu ya kihisiamoyo. Lakini, hawakati tamaa. Wanaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova yajapokuwa machozi.—Linganisha Zaburi 126:5, 6.

      8. Twaweza kukabili jaribu jipi la kifedha?

      8 Majaribu mbalimbali tunayokabili yaweza kutia ndani matatizo makubwa ya kiuchumi. Wakati ndugu mmoja katika New Jersey, U.S.A., alipopoteza kazi yake kwa ghafula, kwa kueleweka alikuwa na wasiwasi juu ya namna ya kulisha familia yake na kutopoteza nyumba yake. Hata hivyo, hakukosa kuwa na tumaini la Ufalme. Alipokuwa akitafuta kazi nyingine, alitumia fursa hiyo kwa faida yake akitumikia akiwa painia-msaidizi. Hatimaye, alipata kazi.—Mathayo 6:25-34.

      9. (a) Kumpoteza mpendwa katika kifo kunaweza kutakaje uvumilivu? (b) Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba si vibaya kulia machozi ya huzuni?

      9 Ikiwa umempoteza mpendwa katika kifo, unahitaji uvumilivu unaodumu muda mrefu baada ya wale walio karibu na wewe kurudia utaratibu wao wa kawaida. Huenda hata ukaona kwamba inakuwa vigumu kwako hasa kila mwaka karibu na wakati mpendwa wako alipokufa. Kuvumilia hali hiyo ya kupoteza mpendwa hakumaanishi kwamba ni vibaya kulia machozi ya huzuni. Ni jambo la asili kuomboleza kifo cha mtu tuliyempenda, na hilo halionyeshi hata kidogo ukosefu wa imani katika tumaini la ufufuo. (Mwanzo 23:2; linganisha Waebrania 11:19.) Yesu ‘alilia machozi’ baada ya Lazaro kufa, ingawa Yeye alikuwa amemwambia Martha hivi kwa hakika: “Ndugu yako atafufuka [atainuka, NW].” Na Lazaro aliinuka!—Yohana 11:23, 32-35, 41-44.

      10. Kwa nini watu wa Yehova wana uhitaji wa pekee wa uvumilivu?

      10 Kuongezea kuvumilia majaribu yaliyo ya kawaida kwa wanadamu wote, watu wa Yehova wana uhitaji wa pekee wa uvumilivu. “Mtakuwa watu wa kuchukiwa na watu wa mataifa yote kwa ajili ya jina langu,” Yesu akaonya. (Mathayo 24:9) Alisema hivi pia: “Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi.” (Yohana 15:20) Kwa nini kuwe chuki na mnyanyaso huo wote? Kwa sababu haidhuru kule tunakoishi kwenye dunia hii tukiwa watumishi wa Mungu, Shetani anajaribu kuvunja uaminifu-maadili wetu kwa Yehova. (1 Petro 5:8; linganisha Ufunuo 12:17.) Hivyo mara nyingi Shetani amesababisha mnyanyaso mwingi, akitahini sana uvumilivu wetu.

      11, 12. (a) Mashahidi wa Yehova na watoto wao walikabili mtihani gani wa uvumilivu katika miaka ya 1930 na miaka ya mapema ya 1940? (b) Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawasalimu mfano wa kitaifa?

      11 Kwa kielelezo, katika miaka ya 1930 na miaka ya mapema ya 1940, Mashahidi wa Yehova pamoja na watoto wao katika United States na Kanada walinyanyaswa kwa sababu hawakusalimu mfano wa kitaifa kwa sababu za dhamiri. Mashahidi hustahi mfano wa kitaifa wanamoishi, lakini wanaitii ile kanuni iliyoandikwa katika Sheria ya Mungu kwenye Kutoka 20:4, 5: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunai. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.” Wakati watoto wengine wa shule walio Mashahidi walipofukuzwa shuleni kwa sababu walitamani kuelekeza ibada yao kwa Yehova Mungu pekee, Mashahidi walianzisha Shule za Ufalme ili kuwafunza. Wanafunzi hao walirudia shule za umma wakati Mahakama Kuu Zaidi ya United States ilipotambua msimamo wao wa kidini, kama vile mataifa yaliyonurishwa yanavyofanya leo. Hata hivyo, uvumilivu wenye moyo mkuu wa vijana hao unatumika ukiwa kielelezo chema hasa kwa vijana Wakristo ambao huenda wakakabili dhihaka sasa kwa sababu wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya Biblia.—1 Yohana 5:21.

      12 Majaribu mbalimbali tunayokabili—yale yaliyo ya kawaida kwa wanadamu na pia yale tunayokabili kwa sababu ya imani yetu ya Kikristo—huonyesha sababu kwa nini tunahitaji uvumilivu. Lakini tunaweza kuvumiliaje?

      Vumilia Hadi Mwisho—Jinsi Gani?

      13. Yehova hutoaje uvumilivu?

      13 Watu wa Mungu wana manufaa dhahiri kuliko wale wasiomwabudu Yehova. Ili kupata msaada, tunaweza kumwendea “yule Mungu ambaye hutoa uvumilivu.” (Warumi 15:5, NW) Lakini, Yehova hutoaje uvumilivu? Njia moja ambayo anafanya hivyo ni kupitia vielelezo vya uvumilivu ambavyo vimeandikwa katika Neno lake, Biblia. (Warumi 15:4) Tunapotafakari vielelezo hivyo, tunatiwa moyo kuvumilia na pia tunajifunza mengi juu ya jinsi ya kuvumilia. Fikiria vielelezo viwili vyenye kutokeza—ule uvumilivu wenye moyo mkuu wa Ayubu na ule uvumilivu wa Yesu Kristo usio na dosari.—Waebrania 12:1-3; Yakobo 5:11.

      14, 15. (a) Ayubu alivumilia majaribu gani? (b) Ayubu aliwezaje kuvumilia majaribu aliyokabili?

      14 Ni hali zipi zilizotahini uvumilivu wa Ayubu? Alipatwa na magumu ya kiuchumi wakati alipopoteza mali zake nyingi. (Ayubu 1:14-17; linganisha Ayubu 1:3.) Ayubu alihisi maumivu ya kupoteza wapendwa wakati watoto wake wote kumi walipouawa katika dhoruba. (Ayubu 1:18-21) Alipatwa na ugonjwa mahututi, wenye maumivu mengi. (Ayubu 2:7, 8; 7:4, 5) Mke wake mwenyewe alimsonga ampe Mungu kisogo. (Ayubu 2:9) Mashirika wa karibu walisema mambo yenye kuumiza, yasiyo na fadhili, na yasiyo kweli. (Linganisha Ayubu 16:1-3 na Ayubu 42:7.) Hata hivyo, katika hayo yote, Ayubu alisimama imara, akidumisha uaminifu-maadili. (Ayubu 27:5) Mambo aliyovumilia yanafanana na majaribu ambayo watu wa Yehova hukabili leo.

      15 Ayubu aliweza kuvumiliaje majaribu hayo yote? Jambo moja hasa lililomtegemeza Ayubu lilikuwa tumaini. “Yako matumaini ya mti,” akajulisha. “Ukikatwa utachipuka tena, wala machipukizi yake hayatakoma.” (Ayubu 14:7) Ayubu alikuwa na tumaini gani? Kama ionyeshwavyo katika mistari michache baadaye, yeye alisema hivi: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa [au, hamu] ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Naam, Ayubu alitazama ng’ambo ya maumivu yake ya wakati huo. Alijua kwamba majaribu yake yasingedumu milele. Zaidi sana, angalipaswa avumilie hadi kifo. Tazamio lake lenye tumaini lilikuwa kwamba Yehova, anayetamani kwa upendo kuwafufua wafu, angemrudisha kwenye uhai.—Matendo 24:15.

      16. (a) Tunajifunza nini juu ya uvumilivu kutokana na kielelezo cha Ayubu? (b) Tumaini la Ufalme lapaswa liwe halisi kwetu kwa kadiri gani, na kwa nini?

      16 Tunajifunza nini kutokana na uvumilivu wa Ayubu? Ili kuvumilia hadi mwisho, ni lazima tusikose kamwe kuwa na tumaini letu. Kumbuka pia, uhakika wa tumaini la Ufalme humaanisha kwamba kuteseka kokote tunakokabili ni ‘kwa muda tu’ kwa kulinganishwa. (2 Wakorintho 4:16-18) Tumaini letu lenye thamani kubwa linategemea kwa uthabiti ahadi ya Yehova juu ya wakati fulani ujao ulio karibu ambapo “atafuta kila chozi katika macho [yetu], wala mauti haitakuwapo tena, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Tumaini hilo, ambalo “halitahayarishi,” ni lazima lilinde fikira zetu. (Warumi 5:4, 5; 1 Wathesalonike 5:8) Ni lazima liwe halisi kwetu—halisi sana hivi kwamba kwa macho ya imani, twaweza kujiona wenyewe tukiwa katika ulimwengu mpya—wakati ambapo hatung’ang’ani tena na ugonjwa na mshuko wa moyo bali tukiamka kila siku katika afya njema na wenye akili isiyojaa matatizo; wakati ambapo hatuhangaiki tena juu ya misongo mikubwa ya kiuchumi bali tukiishi katika usalama; wakati ambapo hatuombolezi kifo cha wapendwa bali tukiwa na msisimuko wa kuwaona wakiwa wamefufuliwa. (Waebrania 11:1) Bila tumaini hilo tunaweza kulemewa sana na majaribu yetu ya wakati huu hivi kwamba tunakata tamaa. Tukiwa na tumaini letu, tuna kichocheo kilichoje cha kuendelea kupiga vita, ili kuendelea kuvumilia hadi mwisho!

      17. (a) Yesu alivumilia majaribu gani? (b) Kule kuteseka kwingi ambako Yesu alivumilia kwaweza labda kuonwa kutokana na jambo gani? (Ona kielezi-chini.)

      17 Biblia yatuhimiza ‘tumtazame kwa mkazo’ Yesu na ‘kumfikiria kwa ukaribu.’ Yeye alivumilia majaribu gani? Baadhi yayo yalitokana na dhambi na kutokamilika kwa wengine. Yesu alivumilia ‘maongezi-kinyume yenye kufanywa na watenda dhambi’ na pia matatizo yaliyotokea miongoni mwa wanafunzi wake, kutia ndani mabishano yao ya mara kwa mara juu ya ni nani aliyekuwa mkuu zaidi. Zaidi ya hayo, alikabili mtihani wa imani usio na kifani. ‘Alivumilia mti wa mateso.’ (Waebrania 12:1-3, NW; Luka 9:46; 22:24) Ni vigumu hata kuwazia kule kuteseka kiakili na kimwili kulikohusika katika maumivu ya kutundikwa na ile aibu ya kuuawa akiwa mkufuru.a

      18. Kulingana na mtume Paulo, ni mambo gani mawili yaliyomtegemeza Yesu?

      18 Ni nini kilichomwezesha Yesu avumilie hadi mwisho? Mtume Paulo ataja mambo mawili yaliyomtegemeza Yesu: “maombi na dua” na pia “furaha iliyowekwa mbele yake.” Yesu, yule Mwana mkamilifu wa Mungu, hakuona aibu kuomba msaada. Alisali “pamoja na kulia sana na machozi.” (Waebrania 5:7; 12:2) Hasa wakati jaribu lake kuu zaidi lilipokuwa likikaribia ndipo aliona ni lazima kusali mara kwa mara na kwa bidii ili kupata nguvu. (Luka 22:39-44) Kwa kuitikia maombi ya Yesu, Yehova hakuliondoa lile jaribu, bali alimwimarisha Yesu kulivumilia. Yesu alivumilia pia kwa sababu alitazama ng’ambo ya mti wa mateso hadi kwenye thawabu yake—ile furaha ambayo angekuwa nayo katika kuchangia utakaso wa jina la Yehova na kufidiwa kwa familia ya kibinadamu kutoka katika kifo.—Mathayo 6:9; 20:28.

      19, 20. Kielelezo cha Yesu kinatusaidiaje kuwa na maoni halisi juu ya yale yanayohusika katika uvumilivu?

      19 Kutokana na kielelezo cha Yesu, twajifunza mambo kadhaa yanayotusaidia kuwa na maoni halisi juu ya yale yanayohusika katika uvumilivu. Mwendo wa uvumilivu si rahisi. Ikiwa tunaona vigumu kuvumilia jaribu fulani, kuna faraja kujua kwamba ilikuwa vivyo hivyo hata kwa Yesu. Ili kuvumilia hadi mwisho, ni lazima tusali mara kwa mara ili kupata nguvu. Nyakati fulani, tunapokuwa chini ya jaribu huenda tukahisi hatustahili kusali. Lakini Yehova hutualika tumwagie mioyo yetu ‘kwa sababu yeye hutujali.’ (1 Petro 5:7, NW) Na kwa sababu ya yale ambayo Yehova ameahidi katika Neno lake, amejiwajibisha kutoa “nguvu inayozidi iliyo ya kawaida” kwa wale wanaomwitia kwa imani.”—2 Wakorintho 4:7-9, NW.

      20 Nyakati fulani ni lazima tuvumilie kwa machozi. Kwa Yesu maumivu ya mti wa mateso hayakuwa sababu hasa ya kushangilia. Badala ya hivyo, furaha ilikuwa katika ile thawabu iliyowekwa mbele yake. Katika hali yetu si jambo halisi kutazamia kwamba sikuzote tutahisi uchangamfu na msisimuko tunapokuwa chini ya jaribu. (Linganisha Waebrania 12:11.) Hata hivyo, kwa kutazama mbele kwenye thawabu, huenda tukaweza ‘kuhesabu ya kuwa ni furaha tupu’ hata tunapokabili hali zenye kujaribu zaidi. (Yakobo 1:2-4; Matendo 5:41) Jambo la maana ni kwamba tuendelee kuwa thabiti—hata ikiwa ni lazima iwe kwa machozi. Kwa vyovyote vile, Yesu hakusema, ‘Mwenye kulia machozi machache zaidi, ndiye atakayeokoka’ bali, “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.”—Mathayo 24:13.

      21. (a) Kwenye 2 Petro 1:5, 6, tunahimizwa kutia nini katika uvumilivu wetu? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?

      21 Hivyo uvumilivu ni wa muhimu ili kupata wokovu. Hata hivyo, kwenye 2 Petro 1:5, 6, tunahimizwa kutia ujitoaji kimungu katika uvumilivu wetu. Ujitoaji kimungu ni nini? Unahusianaje na uvumilivu, na wewe unaweza kuupataje? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kule kuteseka kwingi ambako Yesu alivumilia kwaweza labda kuonwa kutokana na jambo la kwamba mwili wake mkamilifu ulikufa baada ya muda wa saa chache tu ukiwa mtini, ilihali wale watenda maovu waliotundikwa kando yake walilazimika kuvunjwa miguu ili kuharakisha kifo. (Yohana 19:31-33) Hawakuwa wamepatwa na kule kuteseka kiakili na kimwili kulikompata Yesu katika lile jaribu la usiku kucha bila usingizi kabla ya kutundikwa, labda kufikia hatua ambayo hangeweza hata kuchukua mti wake mwenyewe wa mateso.—Marko 15:15, 21.

  • Tieni Ujitoaji Kimungu Katika Uvumilivu Wenu
    Mnara wa Mlinzi—1993 | Septemba 15
    • Tieni Ujitoaji Kimungu Katika Uvumilivu Wenu

      “Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW], na katika saburi yenu utauwa [ujitoaji kimungu, NW].”—2 PETRO 1:5, 6.

      1, 2. (a) Kuanzia miaka ya 1930, ni nini kilichowapata Mashahidi wa Yehova katika mabara yaliyokuwa chini ya utawala wa Nazi, na kwa nini? (b) Watu wa Yehova walikabilianaje waliponyanyaswa kwa ukatili?

      KILIKUWA kipindi chenye giza katika historia ya karne ya 20. Kuanzia miaka ya 1930, maelfu ya Mashahidi wa Yehova katika mabara yaliyokuwa chini ya utawala wa Nazi walikamatwa isivyo haki na kufungwa katika kambi za mateso. Kwa nini? Kwa sababu walithubutu kuendelea kutokuwamo na kukataa kusema heil Hitler. Walitendwaje? “Hakuna kikundi kingine cha wafungwa . . . kilichopatwa na ukatili wa askari wa SS wa njia ile ambayo Wanafunzi wa Biblia [Mashahidi wa Yehova] walipatwa nao. Ulikuwa ukatili wenye mfululizo wa mateso mengi ya kimwili na kiakili, ambao hakuna lugha ulimwenguni inayoweza kueleza.”—Karl Wittig, aliyekuwa ofisa wa serikali ya Ujerumani.

      2 Mashahidi walikabilianaje? Katika kitabu chake The Nazi State and the New Religions: Five Case Studies in Non-Conformity, Dakt. Christine E. King alisema hivi: “Serikali ilikosa kufanikiwa dhidi ya Mashahidi tu [tofauti na vikundi vingine vya kidini].” Naam, Mashahidi wa Yehova kwa ujumla walisimama imara, hata ingawa kwa mamia yao, hilo lilimaanisha kuvumilia hadi kifo.

      3. Ni nini kimewawezesha Mashahidi wa Yehova wavumilie majaribu makali?

      3 Ni nini kimewawezesha Mashahidi wa Yehova wavumilie majaribu hayo si katika Ujerumani wa Nazi tu bali ulimwenguni pote? Baba yao wa kimbingu amewasaidia wavumilie kwa sababu ya ujitoaji kimungu wao. “Bwana [Yehova, NW] ajua kuwaokoa watauwa [watu wenye ujitoaji kimungu, NW] na majaribu,” mtume Petro aeleza. (2 Petro 2:9) Mapema zaidi katika barua iyo hiyo, Petro alikuwa amewashauri Wakristo hivi: “Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW], na katika saburi yenu utauwa [ujitoaji kimungu, NW].” (2 Petro 1:5, 6) Kwa hiyo uvumilivu unahusiana kwa ukaribu na ujitoaji kimungu. Kwa kweli, ili kuvumilia hadi mwisho, ni lazima ‘tufuatie ujitoaji kimungu’ na kuudhihirisha. (1 Timotheo 6:11, NW) Lakini ujitoaji kimungu ni nini hasa?

      Maana ya Ujitoaji Kimungu

      4, 5. Ujitoaji kimungu ni nini?

      4 Nomino ya Kigiriki kwa neno “ujitoaji kimungu” (eu·seʹbei·a) yaweza kutafsiriwa kihalisi kuwa “kustahi kunakofaa.”a (2 Petro 1:6, Kingdom Interlinear) Hilo huonyesha hisia changamfu ya moyoni kumwelekea Mungu. Kulingana na W. E. Vine, kivumishi eu·se·besʹ, kinachomaanisha kihalisi “-enye staha inayofaa,” humaanisha “ile nishati ambayo, ikielekezwa na kicho kitakatifu kwa Mungu, huonekana katika utendaji wa kujitoa.”—2 Petro 2:9, Int.

      5 Kwa hiyo usemi “ujitoaji kimungu” unarejezea staha au ujitoaji kwa Yehova ambao hutusukuma kufanya yale yanayompendeza. Hayo yanafanywa hata tunapokabili majaribu magumu kwa sababu tunampenda Mungu kutoka moyoni. Ni ushikamano wa kibinafsi kwa Yehova, wenye uaminifu-mshikamanifu ambao huonekana katika njia tunayoishi maisha zetu. Wakristo wa kweli wanahimizwa kusali kwamba waweze kuongoza “maisha ya utulivu na amani katika utauwa [ujitoaji kimungu, NW] wote.” (1 Timotheo 2:1, 2) Kulingana na watunga-kamusi J. P. Louw na E. A. Nida, “katika lugha kadhaa [eu·seʹbei·a] katika 1 Tm 2.2 laweza kutafsiriwa kwa kufaa kuwa ‘kuishi kama vile Mungu angetaka tuishi’ au ‘kuishi kama vile Mungu ametuambia twapaswa kuishi.’”

      6. Kuna uhusiano gani kati ya uvumilivu na ujitoaji kimungu?

      6 Sasa tunaweza kufahamu vizuri zaidi uhusiano kati ya uvumilivu na ujitoaji kimungu. Kwa sababu tunaishi kama vile Mungu angetaka tuishi—kwa ujitoaji kimungu—tunapatwa na chuki ya ulimwengu, ambayo sikuzote huleta majaribu ya imani. (2 Timotheo 3:12) Lakini hakuna njia yoyote tungechochewa kuvumilia majaribu hayo ikiwa isingekuwa kwa sababu ya ushikamano wetu wa kibinafsi kwa Baba yetu wa kimbingu. Zaidi ya hayo, Yehova huitikia ujitoaji huo wa kuhisiwa moyoni. Ebu wazia jinsi ambavyo ni lazima iwe anahisi anapoangalia chini kutoka mbinguni na kuona wale ambao, kwa sababu ya ujitoaji wao kwake, wanajitahidi kumpendeza kujapokuwa upinzani wa kila aina. Haishangazi kwamba ana nia ya “kuwaokoa watauwa [watu wenye ujitoaji kimungu, NW] na majaribu”!

      7. Kwa nini ni lazima ujitoaji kimungu ukuzwe?

      7 Hata hivyo, hatuzaliwi tukiwa na ujitoaji kimungu, wala hatuupati moja kwa moja kutoka kwa wazazi wanaomwogopa Mungu. (Mwanzo 8:21) Badala ya hivyo, ni lazima ukuzwe. (1 Timotheo 4:7, 10) Ni lazima tujitahidi kutia ujitoaji kimungu katika uvumilivu wetu na imani yetu. Petro asema hilo huhitaji ‘kujitahidi sana.’ (2 Petro 1:5) Basi, tunaweza kupataje ujitoaji kimungu?

      Tunapataje Ujitoaji Kimungu?

      8. Kulingana na mtume Petro, ni nini ufunguo wa kupata ujitoaji kimungu?

      8 Mtume Petro alieleza ufunguo wa kupata ujitoaji kimungu. Alisema hivi: “Neema na iwe kwenu na amani iongezwe katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu. Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa [ujitoaji kimungu, NW], kwa kumjua [ujuzi sahihi juu ya, NW] yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe.” (2 Petro 1:2, 3) Kwa hiyo ili kutia ujitoaji kimungu katika imani yetu na uvumilivu wetu, ni lazima tukue katika ujuzi sahihi, yaani, ujuzi wote au kamili, juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo.

      9. Ni kielezi gani kinachoweza kuonyesha kwamba kuwa na ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo kwahusisha zaidi ya kujua tu wao ni nani?

      9 Ni nini maana ya kuwa na ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo? Kwa wazi, kunatia ndani zaidi ya kujua wao ni nani. Kwa kutoa kielezi: Huenda ikawa unajua jirani yako ni nani na huenda hata ukamsalimu kwa jina. Lakini, je, ungemkopesha kiasi kikubwa cha fedha? Sivyo, isipokuwa tu kama ungemjua yeye ni mtu wa aina gani. (Linganisha Mithali 11:15.) Vivyo hivyo, kumjua Yehova na Yesu kwa usahihi, au kikamili, hakumaanishi kuamini tu kwamba wako na kujua majina yao. Ili kuwa na nia ya kuvumilia majaribu kwa ajili yao hata hadi kifo, ni lazima tuwajue kikweli kwa ukaribu sana. (Yohana 17:3) Hilo lahusisha nini?

      10. Kuwa na ujuzi sahihi juu ya Yehova na Yesu kwahusisha mambo gani mawili, na kwa nini?

      10 Kuwa na ujuzi sahihi, au kamili, juu ya Yehova na Yesu huhusisha mambo mawili: (1) kupata kuwajua wakiwa watu—sifa zao, hisia zao, na njia zao—na (2) kuiga kielelezo chao. Ujitoaji kimungu huhusisha ushikamano wa kibinafsi kwa Yehova, wenye kuhisiwa moyoni, na unadhihirishwa kwa njia tunayoishi maisha zetu. Kwa hiyo, ili kuupata ni lazima tumjue Yehova binafsi na kufahamu kikamili mapenzi yake na njia zake kadiri hilo liwezekanavyo kibinadamu. Ili kumjua Yehova kikweli, ambaye tumeumbwa kwa mfano wake, ni lazima tutumie ujuzi huo na kujitahidi kuwa kama yeye. (Mwanzo 1:26-28; Wakolosai 3:10) Na kwa kuwa Yesu alimwiga Yehova kikamilifu katika yale aliyosema na kufanya, kumjua Yesu kwa usahihi ni msaada wenye thamani katika kukuza ujitoaji kimungu.—Waebrania 1:3.

      11. (a) Tunaweza kupataje ujuzi sahihi juu ya Mungu na Kristo? (b) Kwa nini ni jambo la maana kutafakari juu ya yale tunayosoma?

      11 Lakini, tunaweza kupataje ujuzi huo sahihi juu ya Mungu na Kristo? Kwa kujifunza Biblia na vichapo vyenye msingi wa Biblia kwa bidii-nyendelevu.b Hata hivyo, ikiwa funzo letu la Biblia la kibinafsi litatokeza kupata kwetu ujitoaji kimungu, ni muhimu kwetu kuchukua wakati wa kutafakari, yaani, kufikiria, au kutia maanani, yale tunayosoma. (Linganisha Yoshua 1:8.) Kwa nini hilo ni la maana? Kumbuka kwamba ujitoaji kimungu ni hisia changamfu, yenye kuhisiwa moyoni kuelekea Mungu. Katika Maandiko, kutafakari hushirikishwa tena na tena na moyo wa kitamathali—mtu wa ndani. (Zaburi 19:14; 49:3; Mithali 15:28) Tunapofikiria kwa uthamini yale tunayosoma, yanachujwa hadi kwenye mtu wa ndani, hivyo yakichochea hisia zetu, yakigusa hisiamoyo zetu, na kuvuta fikira zetu. Ndipo tu kujifunza kunapoweza kuimarisha ushikamano wetu wa kibinafsi kwa Yehova na kutusukuma kuishi katika njia inayompendeza Mungu hata tunapokabili hali ngumu au majaribu makali.

      Kuzoea Ujitoaji Kimungu Nyumbani

      12. (a) Kulingana na Paulo, Mkristo anaweza kuzoeaje ujitoaji kimungu nyumbani? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli huwajali wazazi waliozeeka?

      12 Ujitoaji kimungu unapaswa kuzoewa nyumbani kwanza. Mtume Paulo asema hivi: “Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao [ujitoaji kimungu, NW] kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu.” (1 Timotheo 5:4) Kama vile Paulo anavyosema, kuwatunza wazazi waliozeeka, ni wonyesho wa ujitoaji kimungu. Wakristo wa kweli huandaa msaada huo si kwa sababu tu ya kuhisi wajibu bali kwa sababu ya kuwapenda wazazi wao. Lakini, zaidi ya hayo, wanatambua umaana ambao Yehova huweka juu ya mtu kuitunza familia yake. Wanafahamu sana kwamba kukataa kuwasaidia wazazi wao wanapokuwa na uhitaji kungekuwa sawasawa na ‘kuikana imani ya Kikristo.’—1 Timotheo 5:8.

      13. Kwa nini kuzoea ujitoaji kimungu nyumbani kwaweza kuwa jambo gumu, lakini ni uradhi gani unaotokana na mtu kuwatunza wazazi wake?

      13 Kwa kweli, si rahisi sikuzote kuzoea ujitoaji kimungu nyumbani. Huenda ikawa washiriki wa familia wako mbalimbali sana. Huenda ikawa watoto ambao wamekuwa watu wazima wanalea familia zao wenyewe na huenda ikawa wanang’ang’ana kiuchumi. Asili au kadiri ya utunzaji unaohitajiwa na mzazi yaweza kuathiri afya ya kimwili, kiakili, na kihisiamoyo ya wale wanaoandaa msaada huo. Hata hivyo, mtu aweza kuwa na uradhi wa kweli akijua kwamba kuwatunza wazazi wake si “kuwalipa” tu bali pia kwampendeza Yule “aliye asili ya jamaa zote [kila familia, NW] duniani na mbinguni.”—Waefeso 3:14, 15, HNWW.

      14, 15. Simulia kielelezo cha utunzaji wa kuonyesha kumwogopa Mungu kwa upande wa watoto kwa mzazi fulani.

      14 Fikiria kielelezo kimoja chenye kugusa moyo kwelikweli. Ellis na ndugu na dada zake watano wana kazi ngumu ya kumtunza baba yao nyumbani. “Katika 1986 baba yangu alipatwa na ugonjwa wa ghafula, uliompooza kabisa,” aeleza Ellis. Hao watoto sita hushiriki katika kutunza mahitaji ya baba yao, kuanzia kumwogesha hadi kuhakikisha kwamba anageuzwa kwa ukawaida ili asipatwe na vidonda vinavyosababishwa na kulala kwa upande mmoja tu kitandani. “Sisi humsomea vitabu, huongea naye, humchezea muziki. Hatujui kwa hakika kama anafahamu yale yanayoendelea karibu na yeye, lakini sisi humtendea kama kwamba anafahamu kila kitu kikamili.”

      15 Kwa nini watoto hao humtunza baba yao hivyo? Ellis aendelea hivi: “Baada ya kifo cha mama yetu katika 1964, Baba alitulea akiwa peke yake. Wakati huo, tulikuwa na miaka kuanzia 5 hadi 14. Wakati huo alitusaidia sisi; sasa tunamsaidia.” Kwa wazi, si rahisi kuandaa msaada huo, na watoto hao huvunjika moyo nyakati nyingine. “Lakini tunatambua kwamba hali ya baba yetu ni tatizo la muda tu,” asema Ellis. “Tunatazamia wakati baba yetu anaporudishwa kwenye afya njema na tunapoweza kuungana tena na mama yetu.” (Isaya 33:24; Yohana 5:28, 29) Kwa hakika, ni lazima iwe utunzaji huo wa kujitoa kwa mzazi huchangamsha moyo wa Yule ambaye huwaamuru watoto kuwaheshimu wazazi wao!c—Waefeso 6:1, 2.

      Ujitoaji Kimungu na Huduma

      16. Ni nini inayopaswa kuwa sababu kuu ya yale tunayofanya katika huduma?

      16 Tunapokubali mwaliko wa Yesu wa ‘kumfuata daima,’ tunapata utume wa kimungu wa kuhubiri habari njema za Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 16:24, NW; 24:14; 28:19, 20) Kwa wazi, kushiriki katika huduma ni wajibu wa Kikristo katika “siku [hizi] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, ni lazima kusudi letu la kuhubiri na kufundisha liwe zaidi ya kutimiza kazi fulani au wajibu tu. Lazima kumpenda Yehova kuwe sababu kuu ya yale tunayofanya na kadiri ya yale tunayofanya katika huduma. “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake,” akasema Yesu. (Mathayo 12:34) Naam, mioyo yetu inapofurika kwa kumpenda Yehova, tunahisi kusukumwa kuwatolea wengine ushahidi juu yake. Kumpenda Mungu kunapokuwa kichocheo chetu, huduma yetu ni wonyesho wenye maana wa ujitoaji kimungu wetu.

      17. Tunaweza kusitawishaje kichocheo kifaacho kwa ajili ya huduma?

      17 Tunaweza kusitawishaje kichocheo kifaacho kwa ajili ya huduma? Fikiria kwa uthamini sababu tatu ambazo Yehova ametupa sisi za kumpenda. (1) Twampenda Yehova kwa sababu ya yale ambayo ametufanyia tayari. Asingaliweza kuonyesha upendo mwingi zaidi ya kuandaa fidia. (Mathayo 20:28; Yohana 15:13) (2) Twampenda Yehova kwa sababu ya yale anayotufanyia sasa. Tuna uhuru wa kusema pamoja na Yehova, anayejibu sala zetu. (Zaburi 65:2; Waebrania 4:14-16) Tunapotanguliza masilahi ya Ufalme, tunapata mahitaji ya uhai. (Mathayo 6:25-33) Tunapokea ugavi wa kawaida wa chakula cha kiroho ambao hutusaidia kukabiliana na matatizo tunayopata. (Mathayo 24:45) Na tuna baraka ya kuwa sehemu ya udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote ambao kwa kweli hututenga kando na ile sehemu nyingine yote ya ulimwengu. (1 Petro 2:17) (3) Pia sisi twampenda Yehova kwa sababu ya yale atakayotufanyia bado. Kwa sababu ya upendo wake, ‘tunashika imara uhai ulio kwelikweli’—uhai wa milele katika wakati ujao. (1 Timotheo 6:12, 19, NW) Tunapofikiria upendo wa Yehova kwa ajili yetu, kwa hakika mioyo yetu itatusukuma kushiriki kwa kujitoa katika kuwaambia wengine juu yake na makusudi yake yenye thamani kubwa! Wengine hawatalazimika kutuambia jambo la kufanya au kadiri ya kufanya katika huduma. Mioyo yetu itatusukuma kufanya yale tuwezavyo.

      18, 19. Dada mmoja alishinda kizuizi kipi ili kushiriki katika huduma?

      18 Hata tunapokabili hali ngumu, moyo uliochochewa na ujitoaji kimungu utasukumwa kusema. (Linganisha Yeremia 20:9.) Hilo laonyeshwa katika hali ya Stella, ambaye ni mwanamke Mkristo mwenye haya sana. Alipoanza kujifunza Biblia kwa mara ya kwanza, alifikiri, ‘Singeweza kamwe kwenda nyumba kwa nyumba!’ Yeye aeleza hivi: “Nilikuwa mnyamavu sana sikuzote. Sikuweza kamwe kuwakaribia wengine ili kuanza mazungumzo.” Alipoendelea kujifunza, kumpenda kwake Yehova kulikua, akasitawisha tamaa yenye bidii ya kusema na wengine juu yake. “Nakumbuka nikimwambia mwalimu wangu wa Biblia, ‘Nataka sana kuongea, lakini siwezi hata kidogo, na hilo hunisumbua kwelikweli.’ Sitasahau kamwe lile aliloniambia: ‘Stella, uwe na shukrani kwamba wataka kuongea.’”

      19 Upesi, Stella alijipata akimtolea jirani yake ushahidi. Halafu akachukua hatua iliyokuwa kubwa sana kwake—alishiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza. (Matendo 20:20, 21) Yeye akumbuka hivi: “Nilikuwa nimeandika utoaji wangu. Lakini niliogopa sana hivi kwamba ingawa ulikuwa mbele yangu, nilikuwa mwoga mno kutazama maandishi yangu!” Sasa, baada ya miaka 35 na zaidi, Stella angali mwenye haya sana kiasili. Lakini, aipenda huduma ya shambani na aendelea kuwa na ushiriki wenye maana katika huduma hiyo.

      20. Ni kielelezo kipi kinachoonyesha kwamba wala mnyanyaso wala kufungwa gerezani hakuwezi kufunga vinywa vya Mashahidi wa Yehova wenye kujitoa?

      20 Wala mnyanyaso wala kufungwa gerezani hakuwezi kufunga vinywa vya Mashahidi wa Yehova wenye kujitoa. Fikiria kielelezo cha Ernst na Hildegard Seliger wa Ujerumani. Kwa sababu ya imani yao, kati yao walitumia zaidi ya miaka 40 katika kambi za mateso za Nazi na magereza ya Kikomunisti. Hata wakiwa gerezani, waliendelea kutolea ushahidi wafungwa wengine. Hildegard alikumbuka hivi: “Maofisa wa gereza waliniona mimi kuwa hatari sana, kwa sababu, kama vile mlinzi mmoja mwanamke alivyosema, nilisema juu ya Biblia siku nzima. Kwa hiyo niliwekwa katika seli ya chini ya ardhi.” Baada ya wao kupewa uhuru wao hatimaye, Ndugu na Dada Seliger walitoa wakati wao wote kwenye huduma ya Kikristo. Wote wawili walitumikia kwa uaminifu hadi vifo vyao, Ndugu Seliger katika 1985 na mke wake katika 1992.

      21. Ni lazima tufanye nini ili kutia ujitoaji kimungu katika uvumilivu wetu?

      21 Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii-nyendelevu na kuchukua wakati wa kutafakari kwa uthamini juu ya yale tunayojifunza, tutakua katika ujuzi sahihi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kisha, hilo litatufanya tupate kiwango kikamilifu zaidi cha ile sifa yenye thamani kubwa—ujitoaji kimungu. Bila ujitoaji kimungu hakuna njia ya kuvumilia majaribu mbalimbali tunayopatwa nayo tukiwa Wakristo. Kwa hiyo acheni tufuate shauri la mtume Petro, tukiendelea ‘kutia katika imani yetu uvumilivu na katika uvumilivu wetu ujitoaji kimungu.’—2 Petro 1:5, 6, NW.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki