Maoni ya Biblia
Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?
“SAMEHENI, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu.” (Marko 11:25) Maneno hayo ya Yesu yanazusha maswali fulani magumu katika kisa cha ndoa kuvurugwa na uzinzi: Je, ni lazima Mkristo asiye na hatia amsamehe mwenzi wake na kudumisha ndoa? Ikiwa anaamua kutaliki, je, anahatarisha uhusiano wake mwenyewe pamoja na Mungu? Ebu tuone jinsi Biblia isaidiavyo kujibu maswali haya.
Je, Ni Lazima Usamehe Sikuzote?
Je, maneno ya Yesu, “sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu,” yanamaanisha kwamba katika hali zote—kutia ndani mwenzi anapofanya uzinzi—Mkristo anawajibika kusamehe? Taarifa ya Yesu yapasa kueleweka kwa kufikiria maelezo mengine aliyotoa kuhusu msamaha.
Kwa kielelezo, twajifunza kanuni ya maana kuhusu msamaha kutokana na maneno ya Yesu kwenye Luka 17:3, 4: ‘Kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe.’ Kwa hakika katika visa vya dhambi nzito, aliyekosewa anatiwa moyo kujaribu kusamehe ikiwa kuna toba ya unyofu. Yehova mwenyewe huona mambo kwa njia hiyo; ili kupata msamaha wa kimungu, ni lazima tuwe wenye kutubu kwa unyofu.—Luka 3:3; Matendo 2:38; 8:22.
Hata hivyo, hili pia laonyesha kwamba ikiwa mwenzi mzinzi ni asiyetubu, akikataa kukubali daraka kwa dhambi yake, ni jambo lenye kueleweka kwamba mwenzi wa ndoa asiye na hatia anaweza kuchagua kutosamehe.—Linganisha 1 Yohana 1:8, 9.
Msamaha—Namna Gani Athari?
Ingawa hivyo, namna gani ikiwa mzinzi ni mwenye kutubu? Kunapokuwa na toba, kuna msingi wa msamaha. Lakini, je, msamaha wamaanisha kwamba mkosaji anaondolewa athari yote ya mwendo wake wenye makosa? Fikiria vielelezo fulani vya msamaha wa Yehova.
Waisraeli walipoasi baada ya kusikiliza wale wapelelezi kumi waliotoa ripoti mbaya kuhusu bara la Kanaani, Musa alimsihi Yehova hivi: “Nakusihi, usamehe uovu wa watu hawa.” Yehova aliitikia hivi: “Mimi nimewasamehe kama neno lako lilivyokuwa.” Je, hili lilimaanisha kwamba wakosaji waliondolewa athari yoyote ya matendo yao? Yehova aliendelea hivi: ‘Lakini watu hawa wote ambao hawakuisikiza sauti yangu, hawataiona hiyo nchi niliyowaapia baba zao.’ (Hesabu 14:19-23) Yehova alitimiza alichosema; kizazi hicho cha watu wazima—isipokuwa Yoshua na Kalebu—hakikuona Bara Lililoahidiwa.—Hesabu 26:64, 65.
Vivyo hivyo, wakati nabii Nathani alipomkemea Mfalme Daudi kwa dhambi yake na Bathsheba, Daudi mwenye kutubu alikubali hivi: “Nimemfanyia BWANA dhambi.” Halafu Nathani akamwambia Daudi hivi: “BWANA naye ameiondoa dhambi yako.” (2 Samweli 12:13) Hata hivyo, ingawa Yehova alimsamehe Daudi, kwa muda wote uliobaki wa maisha yake Daudi aliteseka kwa athari ya dhambi yake.—2 Samweli 12:9-14; ona pia 2 Samweli, sura 24.
Vielelezo hivi vya msamaha wa kimungu vinakazia somo muhimu: Hatuwezi kutenda dhambi na kuwa huru kutokana na adhabu. (Wagalatia 6:7, 8) Ingawa mtenda-dhambi mwenye kutubu anaweza kupata msamaha, si lazima akose kupata athari ya mwendo wake wenye makosa. Je, hili lamaanisha kwamba mwenzi asiye na hatia anaweza kusamehe mzinzi—angalau katika maana ya kwamba anaachilia mbali chuki kali—na bado aamue kumtaliki?
Msamaha na Talaka
Wakati wa huduma yake, katika pindi tatu Yesu alizungumza kuhusu talaka. (Mathayo 5:32; 19:3-9; Luka 16:18) Kwa kupendeza, hakuna mara moja kati ya yoyote ya haya mazungumzo Yesu alitaja msamaha. Kwa kielelezo, kama ipatikanavyo kwenye Mathayo 19:9, yeye alisema hivi: “Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini.” Kwa kusema “isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati,” Yesu alikubali kwamba ukosefu wa adili katika ngono ungempa mwenzi asiye na hatia haki, au “msingi” wa kimaandiko wa kutaliki. Hata hivyo, Yesu hakusema kwamba mwenzi asiye na hatia angepaswa kutaliki. Walakini, yeye alimaanisha kwa wazi kwamba mwenzi huyo aweza kufanya hivyo.
Ndoa ni kifungo ambacho hufunga watu wawili pamoja. (Warumi 7:2) Lakini mmoja wao akikosa kuwa mwaminifu, kifungo hicho chaweza kuhatarishwa. Katika hali kama hizo mwenzi asiye na hatia kwa hakika anakabiliwa na maamuzi mawili. Kwanza, je, asamehe? Kama tulivyoona, jambo la maana hapa ni ikiwa mzinzi ni mwenye kutubu kwa unyofu au sivyo. Wakati kuna toba, mwenzi asiye na hatia baada ya muda huenda akasamehe—angalau katika maana ya kuachilia mbali chuki.
Uamuzi wa pili ni, je, afanye mipango ya kupata talaka? Kwa nini swali hili lazuka ikiwa amemsamehe?a Namna gani ikiwa ana mahangaiko yenye msingi kuhusu usalama wake na wa watoto wake, hasa ikiwa mumeye alikuwa amekuwa mwenye kutenda vibaya katika wakati uliopita? Au namna gani ikiwa kuna hofu za kuambukizwa na ugonjwa unaopitishwa kingono? Au namna gani ikiwa yeye ahisi kwa kina kwamba kwa sababu ya usaliti wa mumeye, yeye hawezi tena kumtumaini katika uhusiano wa mume-na-mke? Katika hali kama hizo ni jambo lenye kueleweka kwamba mwenzi asiye na hatia angeweza kumsamehe mwenzi aliyekosa (katika maana ya kuachilia mbali chuki) na bado aamue kumtaliki kwa sababu hatamani kuendelea kuishi pamoja naye. Kuachilia chuki kwaweza kumsaidia aendelee na maisha yake. Kwaweza pia kumsaidia kuweka shughuli zozote pamoja na mzinzi kuwa za upole zaidi.
Kupata talaka kutoka kwa mwenzi asiye mwaminifu ni uamuzi wa kibinafsi, mmoja ambao mwenzi asiye na hatia apaswa kuufanya baada ya kupima mambo yote yanayohusika kwa uangalifu na kwa sala. (Zaburi 55:22) Wengine hawana haki ya kujaribu kuamrisha au kumsonga mwenzi asiye na hatia katika kuamua njia moja au nyingine. (Linganisha Wagalatia 6:5.) Kumbuka, Yesu hakusema lile ambalo mwenzi asiye na hatia apaswa kufanya. Kwa wazi, basi Yehova hachukizwi na wale ambao wanachagua kutaliki juu ya misingi ifaayo ya Kimaandiko.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kurudia mahusiano ya kingono, mwenzi asiye na hatia angekuwa akionyesha kwamba aliamua kupatana na mwenzi wake aliyekosa. Kwa hivyo angekuwa akiharibu msingi wowote wa Kimaandiko kwa ajili ya talaka.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]
Life