Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 4/15 kur. 23-24
  • Maswali kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Habari Zinazolingana
  • Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?
    Amkeni!—1995
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Uwe Mshikamanifu kwa Mwenzi Wako
    Unaweza Kuwa na Familia Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 4/15 kur. 23-24

Maswali kutoka kwa Wasomaji

● Wakati mwenzi asiye na hatia arudiapo kufanya ngono na mwenzi mzinifu baada ya kupata habari kwamba amezini, je! kurudia ngono jinsi hiyo ni ushuhuda wa kwamba mwenzi asiye na hatia amemsamehe mwenziwe?

Kufanya ngono nje ya ndoa kunatokeza msingi wa talaka, ikiwa mwenzi asiye na hatia anaitaka; kwa njia iyo hiyo, ikiwa ngono inarudiwa, inapasa ifahamike kwamba kufanya hivyo ni kutoa msamaha na kuziba pengo lililotokea kati yao. Ama sivyo, hakuna upatano halisi wa kufanya ngono bila kutoa msamaha.​—Mt. 19:9; 5:37.

Wakati kunapokuwa na toba ya kweli upande wa mwenzi mzinifu, na wenzi wote wawili wanataka kwa unyofu wa moyo kutatua pamoja matatizo ambayo yametokea, kwa uhakika ingefaa sana mwenye kukosa aonyeshwe rehema na kusamehewa. Zinapasa jitihada zote ziwezekanazo zifanywe ili kuhifadhi uhusiano wa ndoa uliopo, huku wakijua kwamba inaelekea uhusiano wao utakuwa wenye kutatiza-tatiza na kutakuwako matatizo ya kutatuliwa kwa muda fulani. Kwa njia hiyo inaweza kuwa baraka si kwa wenzi waliooana tu na watoto wo wote ambao wangali nyumbani, bali pia jambo hilo litamshinda nguvu mvunjaji mkuu wa ndoa, Shetani yule Ibilisi.

Katika visa fulani, huenda ikawa vigumu sana mwenzi asiye na hatia kupata msingi halisi wa kuiendeleza ndoa. Hata kabla uzinifu haujatokeza, huenda kukawa kumekuwako matatizo mazito sana katika kutumia kanuni za Biblia zinazohusiana na ukichwa na utii. Huenda kukawa kumekuwa hakuna kupashana habari kwa wingi, na hali ya kupendana na kuheshimiana ikawa chini sana. Huenda uchungu, mfundo (hali ya mtu kujisikia ameudhiwa) au mambo mengine yakawa yaliwazuia wasipane haki ya ngono. Je! kutakuwa na maendeleo ya kweli katika kujaribu kuyatatua matatizo haya mazito, yaliyotia mizizi imara, msamaha ukitolewa? Huenda mwenzi asiye na hatia akajisikia kwamba ni vigumu sana kuwa na uwezekano wa kufanya maendeleo na huenda akachagua kumtaliki mwenzi huyo mzinifu, ingawa kufanya hivyo kutamaanisha afanye marekebisho maishani, kama vile kukabiliana na uchungu wa moyoni unaotokana na talaka, labda uhitaji wa kupanga makao mahali pengine, kutunza watoto wo wote wanaohusika, na kadhalika. Vilevile, unaopasa kukumbukwa ni uhakika wa kwamba Yehova ‘huchukia kutaliki.’​—Mal. 2:16, NW.

Haya yote ni mambo ya hakika ambayo mwenzi asiye na hatia lazima ayafikirie katika kuamua kama atasamehe au hatasamehe. Anapaswa kufanya hivyo kabla ya kurudia ngono, kabla ya kuanza upya mapendeleo ya unyumba ambayo ni haki ya wale tu waliooana. Kuzungumza mambo yaliyotukia, kuzizungumza pande zilizotokeza tatizo, kujaribu kufikia ufahamiano, na kuamua kama wote wawili wana nia ya kujitahidi kikweli wasitawishe upendo na heshima katika ndoa, hayo yote ni mambo yanayoweza kufanywa bila kumfanya yule mwingine adhani unatoa msamaha. Lakini wakati mwenzi asiye na hatia anapovutwa na maono yake mwenyewe ya moyoni kiasi cha kuweza kufanya ngono na mwenzi mzinifu, itachukuliwa kwamba mwenzi asiye na hatia anatoa msamaha wa kabisa, wala hatatumia kule kutokuaminika kwa mwenziwe anakokujua kama msingi wa kupata talaka ya Kimaandiko yenye kuruhusu kuoa au kuolewa tena.

Kwa kutoa msamaha kwa njia hiyo yenye upatani, mwenzi asiye na hatia anamwiga Yehova katika kusamehe, bila ya kumhesabia mwenye hatia dhambi zake za zamani na kuendelea kumkumbusha-kumbusha lililotukia zamani. (Zab. 103:3, 8-14; Isa. 55:7; Efe. 4:32; 1 Pet. 4:8; 1 Yohana 1:9) Bila shaka, hilo linamwekea msamehewa daraka la kuthamini hivyo na kuepuka kurudia kosa hilo.

Ni jambo lenye kukubaliwa kwamba nyakati nyingine matatizo makubwa yenye kuhuzunisha sana, yasiyokuwa yametazamiwa, husitawi baadaye hata kwamba, kama yangalijulikana mwanzoni, yangaliweza kumfanya mwenzi asiye na hatia amnyime mwenziwe msamaha, hata kukataa kurudia ngono. Walakini, badala ya matatizo hayo kutoa msingi wa kuibadili hali ya ndoa, uwezekano wa kutokeza kwa matatizo hayo unazidi kukazia umaana wa mwenzi asiye na hatia kupima mambo yote kwa uangalifu asifanye uamuzi wa haraka-haraka anapokabiliwa na uamuzi wa kama atasamehe au hatasamehe.

Hali ingekuwa iyo hiyo hata wakati mimba inapotokea kwa sababu ya uzinifu uliofanywa na mke, na mimba hiyo haijulikani wakati ngono inaporudiwa na mwanamume pamoja na mkewe. Uwezekano wa mimba kwa uhakika ni jambo ambalo mume angetaka kufikiria katika kuamua kama anaweza kumsamehe mkewe na kumchukua tena. Hekima ambayo imeonekana inafaa ingeagiza kwamba mume angoje mpaka wakati ambao inaweza kujulikana kabisa kama mkewe ana mimba ya mtoto wa mwanamume mwingine. Kama mume akimsamehe mke na kufanya ngono naye kabla ya kujua hayo, sasa namna gani? Mume angalipaswa kuwa ameamua mapema kwamba ana nia ya kuukubali uwezekano wa mkewe kuwa na mimba na kwamba, mkewe akijifungua mtoto, huyo mume angemkubali mtoto huyo akae ndani ya nyumba yake na kumtunza kama mtoto wake mwenyewe.

Inafahamika kwamba wakati “uasherati” upande wa mwenzi wa ndoa mwenye kuamini unapojulikana, baraza ya wazee katika kundi inapaswa ifahamishwe. (Mt. 19:9) Ikiwa mwenye hatia hafanyi hivyo, basi mwenzi asiye na hatia angekuwa na daraka la kutoa habari za kosa hilo kwa faida za kuliendeleza kundi la Yehova likiwa safi. Kama kuna toba ya kweli upande wa mwenye hatia, huenda mtu huyo akabakizwa ndani ya kundi, na ndivyo ingekuwa hata ingawa mwenzi asiye na hatia anaweza kuchagua kutokumsamehe. Kama hakuna toba, yule mwenzi mwenye hatia angetengwa na ushirika, hata ingawa mwenzi asiye na hatia anaweza kuchagua kumsamehe na kuendelea kuishi na mwenzi huyo aliyetengwa na ushirika.

Yote hayo yanakazia kwamba madaraka ya ndoa hayawezi kuchukuliwa kivivi-hivi tu. “Uasherati” tu ukifanywa na mwenzi wa mtu ndio unaompa mwenzi yule mwingine sababu za Kimaandiko za kuivunja ndoa kwa kusudi la kuoa au kuolewa tena. Lakini mambo ya unyumba (ngono) yakiisha kurudiwa, lazima kundi la Kikristo liwe na upatani kama ule ambao mume na mke huyo lazima wawe nao, kwa kufuata maoni ya kwamba “uasherati” wa zamani unaojulikana umekwisha kuacha kuwa msingi wa kuivunja ndoa. Wakimtegemea Yehova, mume na mke hao wanapaswa watie bidii sana kusitawisha upendo na heshima katika uhusiano wao, ili wawe na furaha na ufanisi wa kutosha katika ndoa yao.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki