Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 4/15 kur. 18-22
  • Kuvumilia Baada ya Msiba Mkubwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuvumilia Baada ya Msiba Mkubwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUKAMATWA NA KUCHINJWA
  • KUENDELEA KUEPUKA KUWA NA UCHUNGU
  • KUFARIJIWA—SI NA MWANADAMU, BALI NA MUNGU
  • MIAKA YENYE KUSISIMUA ILIYOFUATA BAADA YA VITA
  • FURAHA YA KUVUMILIA
  • Sababu ya Kutoogopa Kusema kwa Ujasiri
    Amkeni!—1995
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
  • Kutoka Magereza Yenye Giza Hadi Milima ya Alps ya Uswisi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 4/15 kur. 18-22

Kuvumilia Baada ya Msiba Mkubwa

Kama inavyosimuliwa na Elise Harms

MIAKA 41 iliyopita, katika Januari 8, 1941, mume wangu, Johannes Harms, aliuawa na Wanazi. Kwa sababu gani? Kwa sababu dhamiri yake haingemruhusu ashiriki katika vita, achinje wanadamu wenzake katika upande mwingine uliokuwa ukipigana na Wanazi. Kwa uthabiti yeye alikataa ‘kumwabudu’ Hitler. Johannes hakuogopa kuendeleza kutokuwamo huko kwa Kikristo hata ilipokuwa ni kupoteza uhai wake mwenyewe.

Sitasahau kamwe barua yenye kugusa moyo aliyompelekea babaye, Martin, kabla tu hajauawa. Mume wangu aliandika hivi:

“Sasa mimi, pia, nimepewa nafasi ya kuuthibitisha uaminifu wangu kwa Bwana kufikia kifo, ndio, uaminifu si kufikia kifo tu, bali hata kuingia katika kifo. Hukumu yangu ya kifo tayari imekwisha kutangazwa nami ninafungwa pingu mchana na usiku​—alama hizi (juu ya karatasi) zimewekwa na pingu​—walakini bado ningali sijashinda kikamilifu. Kuendelea kuwa mwaminifu kunafanywa liwe jambo gumu kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ningali nina nafasi ya kuokoa uhai wangu wa kidunia, bali kwa kufanya hivyo nipoteze uzima ulio kweli kweli. Ndiyo, Shahidi wa Yehova anapewa nafasi ya kuvunja agano lake hata anapokuwa katika nyumba ya kunyongea. Kwa hiyo, ningali katikati ya vita na ningali na ushindi mwingi wa kutimiza kabla sijaweza kusema kwamba ‘nimepigana vita vile vizuri, nimeishika imani; nimewekewa taji ya haki ambayo Mungu aliye hakimu wa haki atanipa.’ Bila shaka vita hiyo ni ngumu, walakini ninashukuru Bwana kwa moyo wote kwamba amenipa nguvu inayohitajiwa kusimama mpaka sasa nikielekeana na kifo na pia amenipa furaha ambayo ningependa kushiriki pamoja na wapendwa wangu wote.

“Babaangu mpendwa, wewe ungali mfungwa, pia, na kama barua hii itakufikia wakati wo wote, mimi sijui. Hata hivyo, ikiwa wakati wo wote utakuwa huru basi endelea kuwa mwaminifu kama ulivyo sasa, kwa maana unajua kwamba ye yote ambaye ameweka mkono wake kwenye jembe na kutazama nyuma haustahili ufalme wa Mungu. . . .

“Wakati wewe, baba mpendwa, utakapokuwa nyumbani tena, basi uhakikishe kumtunza kipekee mpenzi wangu Lieschen, kwa maana itakuwa vigumu sana kwake, kujua kwamba mpenzi wake hatarudi. Ninajua kwamba utafanya hivyo nami ninatangulia kukushukuru. Babaangu mpendwa, kwa roho ninakuita, uendelee kuwa mwaminifu, kama ambavyo nimejaribu kuendelea kuwa mwaminifu, kisha tutaonana tena. Nitakuwa nikikufikiria mpaka dakika ya mwisho.”

Pengine unataka kujua ni jambo gani lililompata babaye Johannes, na mimi baada ya kuuawa kwa Johannes. Je! tumevumilia, tukaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, kama Johannes alivyotutia moyo tufanye?

Baba ya Johannes, Martin, alikuwa katika kambi ya mateso huko Sachsenhausen wakati Johannes alipouawa, naye aliendelea kuwa huko mpaka mwisho wa vita kisha akarudi nyumbani huko Wilheimshaven na akasaidia kujenga upya kundi la Mashahidi wa Yehova huko. Alimtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu mpaka mwaka 1976, akiwa amefikia umri mkubwa wa miaka 90.

Kwa habari yangu, kwa sasa ninaishi katika kijumba kimoja hapa Wilhelmshaven, ambako nilikulia na nikaolewa na Johannes huko-o-o nyuma katika mwaka 1936. Ingawa sina afya nzuri sana, ndiyo, ningali ninatenda nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Je! nimeolewa tena? Hapana. Bila shaka, kulingana na Maandiko nilikuwa huru kuolewa tena. Walakini wazo la kupata furaha katika mikono ya mwanamume mwingine, baada ya Johannes kung’ang’ana sana ili aendelee kuwa mwaminifu​—hapana, kwangu binafsi wazo hilo halikunivutia kamwe.

Kabla sijaeleza yaliyonisaidia nivumilie mambo mbalimbali wakati wa miaka 40 iliyopita, ebu nirudi nyuma na niwaambie hali zilizotokeza kuchinjwa kwa Johannes.

KUKAMATWA NA KUCHINJWA

Johannes alikamatwa katika Septemba 3, 1940. Tangu ndoa yetu huko kulikuwa kufungwa kwake kwa pili. Dada yangu nami tuliweza kumtembelea baada ya kila juma tatu au nne. Wakati wa ziara yetu ya pili tulipata kujua kwamba alikuwa amehukumiwa kifo. Kwa hiyo halikuwa jambo la kunishangaza kabisa alipokatwa kichwa katika Januari 8, 1941, ingawa bado lilikuwa jambo lenye kushtusha sana, bila shaka. Ah! hilo lilinishtua sana.

Walakini nilikuwa najua kwamba Johannes hakuwa amekufa akiwa mhalifu. Vilevile nilikuwa najua kwamba maafisa kwa kurudia-rudia walijaribu njia mbalimbali za kumfanya aikane imani yake. Nilikuwa najua nyakati ngumu alizokuwa amezipitia. Hakukuwa mengi ambayo ningeweza kufanya kumsaidia. Kwa hiyo nilipoarifiwa kwamba alikuwa ameuawa, nilifarijika kujua mambo hayo yalikuwa yamekwisha. Kwa wakati huo nilijisahau, nikawa nikifikiri tu: “Sasa hawawezi kumfanya aikane imani. Hakuna hatari kwamba atakosa kuwa mwaminifu. Amevumilia kwa uaminifu kufikia kifo.”

Tulikuwa tumeoana karibu miaka minne na miezi minane tu iliyokuwa imepita. Kwa kuwa tulikuwa tumeposana kwa miaka mitatu, tungaliweza kuwa tumeoana mapema, walakini wakati wote tuliendelea kuahirisha. Tuliyajua matatizo ambayo pengine tungeyakabili. Hata wakati huo, nyakati zilikuwa zenye hatari katika Ujeremani. Kwa kweli, utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa umepigwa marufuku katika nchi hiyo.

Wakati babaake Johannes (ambaye tayari alikuwa akitumikia kifungo chake cha pili) alipofunguliwa bila kutazamiwa kutoka gerezani, tulikuwa tumetumia pindi hiyo kuoana. Ningali naweza kukumbuka kwamba ilikuwa siku ya masika yenye kuvutia katika Mei wa 1936. Tuliona furaha nyingi pamoja tukiwa wenzi waliooana mpaka Wanazi walipomkamata Johannes.

KUENDELEA KUEPUKA KUWA NA UCHUNGU

Watu wengine huruhusu uadui uwaingize uchungu. Wanaanza kutilia mashaka upendo wa Mungu. Wanamtafutia vikosa, hata kufikia kutilia shaka kuwapo kwake. Wakati Johannes alipouawa, nilijua kwamba hiyo ilikuwa kwa sababu fulani; alikuwa ameuawa kwa ajili ya kuendeleza ukamilifu wake kwa Mungu. Walakini miezi sita tu baada ya kumpoteza Johannes, kifo kilinipiga dharuba jingine​—mamangu alikufa! Jambo hilo, lazima nikubali, karibu linifanye nimwonee Mungu uchungu. Nilitaka kujua: “Kwa sababu gani, katika wakati wangu wa huzuni, yeye (mama), mtu pekee ambaye ningeweza kumtumaini anitegemeze, akafa pia?”

Hata hivyo, muda mfupi baada ya hapo tukaanza kupatwa na maafa makubwa ya vita​—mashambulio mabaya sana ya ndege, kwa mfano, ambayo karibu yaharibu kabisa miji fulani ya Ujeremani. Kwa kuwa nililazimika kufanya kazi ili kujiruzuku nilianza kufikiri hivi: “Ni nani ambaye angemtunza mama wakati huu mgumu, kama angalikuwa bado hai? Kwa kuwa yeye alikuwa kipofu, ni nani ambaye angepata wakati wa kumsaidia afike kwenye maficho ya kujilinda na mashambulio ya ndege?” Lingekuwa jambo gumu kama nini kwake! Polepole nikaupata usawa wangu, nikatambua kwamba nyakati nyingine Yehova anaruhusu mambo ambayo huenda tusiyafahamu, walakini ambayo kwa hakika yanaonyesha yeye ni ‘mpole sana katika shauku ya upendo na mwenye rehema.’ (Yak. 5:11, NW) Nilisadikishwa kwamba maadamu ningeendelea kuwa na maoni yanayofaa na kumtumaini yeye kabisa, sikuzote mambo yangekuwa mazuri kwangu.

Mfano mwingine ni huu. Tulikuwa na kijumba chenye vyumba vinne. Hata hivyo, wakati mume wangu alipouawa, nilipoteza haki kuendelea kuishi humo. Niliamriwa niondoke. Walakini ningeenda wapi? Kama kwamba ni mwujiza, mke wa afisa mmoja wa jeshi, ambaye pamoja na mume wake walikuwa wakihamishwa waende sehemu nyingine alinipangia nivitwae vyumba hivyo vitatu katika kijumba walimokuwa wakiondoka. Bado, nilihama nikiwa na moyo wenye masikitiko mahali hapo ambapo Johannes nami tulikuwa tumeshirikiana pamoja. Hata hivyo, unafikiri ni jambo gani lingetokea karibu miezi sita baadaye? Paliharibiwa kabisa katika shambulio la ndege!

KUFARIJIWA—SI NA MWANADAMU, BALI NA MUNGU

Wakati Johannes alipouawa, nilikuwa nikifanya kazi katika afisi moja. Wakati wafanya kazi wenzangu waliposikia juu ya jambo lililokuwa limetokea, walijaribu, katika njia yao wenyewe, kunifariji. Walikuwa wakinialika kwenye vikusanyiko vya kirafiki. Ingawa nilithamini jitihada zao zenye kusudi zuri, nilipata faraja ya kweli mahali pengine​—katika Yehova Mungu na Neno lake, Biblia.

Inasikitisha kusema kwamba kuna nyakati nyingine, wakati wengine sikuzote hawakuniambia mambo yenye kutia moyo. Ninakumbuka wakati mmoja mwanamke mmoja aliponiambia (na hiyo ilikuwa muda mfupi baada ya Johannes kuuawa): “Ni shauri lako mwenyewe; jambo hilo halingalipasa kutokea. Lilikuwa shauri la Johannes mwenyewe!”

Je! hilo si jambo la ukatili kusema? Ndiyo, katika njia fulani, ingawa​—na nilimwambia hivyo​—yeye alisema kweli. Lilikuwa ‘shauri letu wenyewe.’ Johannes angaliweza kuliepuka. Na kama ningalijaribu kumshawishi aikane imani, pengine mimi, pia, ningaliweza kuliepuka. Walakini nilikuwa na furaha kama nini kwamba sisi wawili tulikuwa tumeendelea kuwa wenye nguvu kiroho na tulikuwa tumevumilia! Nilifurahi kwamba mimi ‘kwa sehemu nilikuwa na lawama.’

Bila shaka, nimekuwa na nyakati fulani za huzuni. Walakini Yehova ni ‘mpole sana katika shauku ya upendo,’ na sikuzote amenifariji. Nyakati nyingine imekuwa ni kwa njia zisizo za kawaida. Ninakumbuka Jumapili moja karibu miezi mitatu baada ya Johannes kuchinjwa. Hali ya hewa haikuwa nzuri. Jambo hilo, pamoja na yale ambayo yalikuwa yamenipata, lilikuwa limenishusha moyo sana. Nilitumia sehemu kubwa ya siku nikilia na kutembea-tembea kutoka chumba hiki mpaka hiki mama yangu akiwa amenifuatia nyuma, akijaribu kunituliza. Niling’ang’ana kuyashinda machozi yangu, walakini sikuweza. Nakumbuka niliwaza hivi: “Ulikuwa ukipokea angaa barua mara moja kwa mwezi, walakini sasa ng’o hutaipata kamwe​—hata mstari mmoja! Kama tu ningaliweza kupokea barua nyingine moja​—nyingine moja tu!”

Baadaye, siku hiyo hiyo, nilikwenda kwenye kabati na nikaanza kutafuta katikati ya baadhi ya vitu vya mume wangu vilivyokuwa vimeletwa nyumbani baada ya yeye kuchinjwa. Kati ya vitu hivyo mlikuwa kifuko cha ngozi kilichokuwa kinatumiwa kuwekwa kalamu na vitu vingine. Ghafula, nikaona kwamba upande mmoja ulikuwa mpana isivyokuwa kawaida. Niliupasua, nikaingiza vidole vyangu nikaanza kuvuta vikaratasi vidogo. Ndiyo, vilikuwa ni barua ambazo Johannes alikuwa ameandika kwa maandishi madogo, kama kitabu kinachoandikwa matukio ya kila siku. Jumla ya barua hizo ilikuwa 20! Unaweza kuwazia namna tu nilivyoona. Barua moja ingalinifanya nifurahi. Walakini lo! 20? Nakumbuka nilimwahidi Yehova: “Sitalalamika tena!”

MIAKA YENYE KUSISIMUA ILIYOFUATA BAADA YA VITA

Wakati wa miaka 40 ambayo imepita sijapata kufikiria juu ya kuacha kamwe. Kwa sababu gani niache? Johannes alikuwa amemtolea Yehova sehemu fulani kwa kuendeleza ukamilifu wake kufikia kifo; ninaweza kufanya sehemu fulani kwa kuvumilia maadamu ningali hai. (Linganisha Warumi 12:1.) Bila shaka, jambo hilo limekuwa si rahisi, nami singaliweza kulifanya kwa uwezo wangu. Sala imekuwa msaada wa maana sana kwangu. Na kuwahubiri wengine juu ya ufalme wa Mungu kumekuwa baraka kweli kweli, pia. Wakati wo wote nilipoona masikitiko yananishinda, nilikuwa nikiondoka nikashiriki katika kuhubiri “habari njema.” Kujaribu kuwafariji wengine kwa ujumbe wa Biblia kulinifanya niyasahau matatizo yangu mwenyewe.

Baadaye, niliweza kuacha kazi yangu ya kimwili. Kisha nikawa na wakati zaidi wa kushiriki katika kuhubiri “habari njema” kwa wengine. Shahidi mmoja alinipa motokaa ndogo ili kwamba niweze kuhubiri katika sehemu za mbali, nami niliweza kuanzisha mafunzo kadha ya Biblia na watu wenye kupendezwa. Nakumbuka moja sana-sana.

Nilitembelea mwanamke mmoja siku ya Alhamisi alasiri na ninakumbuka nilimwambia hivi: “Ingekuwa vizuri sana kama tungezungumza mambo haya kwa utaratibu kwa msaada wa kitabu kimoja.” Yeye alikubali. Kisha nikaongeza hivi: “Nasi tuna mikutano mizuri ajabu. Ninaweza kukuchukua Jumapili, kama ungependa kuja.” Kwa kuwa sikutaka kupoteza wakati, nilisema mambo moja kwa moja!

Alikubali kuja kwenye mkutano. Kwa hiyo alasiri ya Jumapili iliyofuata nilibisha hodi kwenye mlango wake, na nikaambiwa: “Ingia kidogo. Mume wangu bado hajawa tayari kabisa.”

“Ati?” Nadhani nilionyesha mshangao wangu. “Mume wako anataka kuja, pia?”

Naye alikuja. Baadaye, niliwaeleza juu ya mikutano mingine yetu na wakaanza kuihudhuria pia. Karibuni walibatizwa, na funzo la kitabu likaanzishwa katika nyumba yao. Leo, karibu miaka 30 baadaye, lingali linafanyiwa hapo.

FURAHA YA KUVUMILIA

Ninapotazama nyuma, ninaweza kusema kwamba mambo kadha wa kadha yamenisaidia kuvumilia. Kwanza kabisa, Johannes nami tulijaribu kujitayarisha, kufikiria mambo ambayo yangaliweza kutokea kwa namna ya majaribu. Kwa habari yetu, kufikiria hali kabla na kuamua ambayo tulitaka kufanya ndiko kulikotusaidia tuyakabili yalipotokea.

Vilevile tuliepuka kufanya jambo lo lote ambalo lingaliweza kufanya majaribu yawe magumu zaidi. Kwa mfano, tukiwa wenzi wachanga waliooana hatukujiingiza kwenye madeni bila sababu. Jambo hilo kwa hakika lingaliweza kufanya hali iwe ngumu zaidi​—kwetu wawili.

Wakati wa miaka ambayo imepita vilevile nimejifunza kutokutazamia mengi mno kutoka kwa wengine. Nyakati nyingine huenda tukafikiri ndugu zetu Wakristo hawatutembelei mara nyingi kutosha au kutuangalia vya kutosha. Walakini kwa sababu gani nitake kuwanyang’anya wakati na nguvu wanayohitaji kwa ajili ya jamaa yao wenyewe na madaraka mbalimbali ya kundi? Nimepata kuthamini kwamba ikiwa sitazamii mengi mno kutoka kwa wengine, sitakatishwa tamaa kwa urahisi. Tendo lo lote la fadhili na la huruma ninalopokea linamaanisha mengi mno na linanipa sababu zaidi ya kumshukuru Yehova.

Bila shaka, jambo la maana kabisa ambalo limenisaidia kuvumilia limekuwa ni kumtumaini Yehova, na kumweleza matatizo yangu yote katika sala.

Katika barua ya mwisho kabisa ambayo Johannes alipata kuniandikia saa chache tu kabla hajauawa, yeye alitaja wazo hilo ambalo nimeendelea kuwa nalo tangu wakati huo na ambalo vilevile limenitia moyo kuvumilia: “Hatutaki kuwa waaminifu kwa Mungu kwa ajili ya thawabu tu, bali ili tuthibitishe uimara wetu katika utumishi Wake kwamba wanadamu, kama Ayubu, wanaweza kuendeleza ukamilifu chini ya majaribu magumu zaidi.”

Johannes angekuwa na furaha kama nini ikiwa wakati huo angalijua mambo ambayo sasa nayajua! Angalipendezwa kujua kwamba baba yake baada ya miongo mitano ya miaka ya kumtolea Yehova utumishi, aliendelea kuwa mwaminifu kufikia kifo, na kwamba baada ya miaka 41 tangu auawe mimi, ‘mpenzi wake Lieschen,’ ningali kati ya wenye furaha wanaojitahidi kuvumilia kwa uaminifu.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Johannes Harms na hati yake ya kifo iliyotolewa na utawala wa Wanazi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki