-
Je, Unahisi Uko Karibu na Mungu?Mnara wa Mlinzi—2014 | Desemba 1
-
-
HABARI KUU | UNAWEZA KUMKARIBIA MUNGU
Je, Unahisi Mungu Yuko Karibu na Wewe?
“Kuwa na uhusiano mzuri na Mungu kunakufanya uhisi usalama, utulivu, na amani. Unahisi kwamba Mungu anakutakia mema siku zote.”—CHRISTOPHER, MWANAMUME KIJANA NCHINI GHANA.
“Mungu hukuona unapoteseka, naye anakupenda kuliko unavyoweza kuwazia.” —HANNAH, MSICHANA MWENYE UMRI WA MIAKA 13, ALASKA, MAREKANI.
“Inafariji na kufurahisha sana kutambua kwamba una uhusiano mzuri na Mungu!”—GINA, MWANAMKE KUTOKA JAMAIKA MWENYE UMRI WA MIAKA 40 HIVI.
Watu wengi huhisi kama Christopher, Hannah, na Gina. Wanaamini kwamba Mungu ni rafiki yao. Vipi wewe? Je, unahisi kwamba uko karibu na Mungu? Au, je, unataka kumkaribia au kuboresha uhusiano wako na Mungu? Huenda ukajiuliza hivi: ‘Inawezekanaje mwanadamu awe na uhusiano mzuri na Mungu Mweza-Yote? Ikiwa inawezekana, jinsi gani?’
INAWEZEKANA KUMKARIBIA MUNGU
Biblia inasema kwamba inawezekana kuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Pia inasema kwamba Mungu alimwita Abrahamu, aliyekuwa Mwebrania ‘rafiki yake.’ (Isaya 41:8) Pia kumbuka mwaliko unaotolewa kwenye andiko la Yakobo 4:8: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” Kwa hiyo, ni wazi kwamba inawezekana kuwa na uhusiano mzuri au urafiki na Mungu. Lakini kwa sababu hatuwezi kumwona Mungu, inawezekanaje ‘kumkaribia’ na kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye?
Ili kupata jibu la swali hilo, fikiria jinsi urafiki kati ya wanadamu unavyositawishwa. Kwa kawaida, watu hujuana majina na kisha kuanzisha urafiki. Halafu, kadiri wanavyoendelea kuwasiliana ndivyo urafiki wao unavyositawi. Urafiki wao huzidi kuimarika wanapoendelea kutendeana mambo mema. Ndivyo ilivyo pia tunapotaka kuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Acheni tuchunguze jinsi ya kufanya hivyo.
-
-
Je, Unalijua na Kulitumia Jina la Mungu?Mnara wa Mlinzi—2014 | Desemba 1
-
-
HABARI KUU | UNAWEZA KUMKARIBIA MUNGU
Je, Unalijua na Kulitumia Jina la Mungu?
Je, una rafiki ambaye hujui jina lake? Bila shaka hapana. Irina, mwanamke kutoka Bulgaria anasema, “Huwezi kuwa rafiki ya Mungu ikiwa hujui jina lake.” Kama ilivyotajwa kwenye makala iliyotangulia, inafurahisha kwamba Mungu anataka uwe rafiki yake. Hiyo ndiyo sababu katika Biblia, amejitambulisha kwako kwa maneno haya: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.”—Isaya 42:8.
Kwenye Biblia, Mungu amejitambulisha kwako kwa maneno haya: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.”—Isaya 42:8
Je, kweli Yehova anataka ujue na kulitumia jina lake? Fikiria jambo hili: Jina la Mungu, linaloandikwa kwa herufi nne za Kiebrania zinazojulikana kama Tetragramatoni, linapatikana katika maandishi ya awali ya Maandiko ya Kiebrania mara 7,000 hivi. Hakuna jina lingine lolote katika Biblia linalotajwa mara nyingi kadiri hiyo. Bila shaka hilo linatuthibitishia kwamba Yehova anataka tulijue na kulitumia jina lake.a
Kwa kawaida, ukitaka mtu awe rafiki yako, mnaanza kwa kujuana majina. Je, unalijua jina la Mungu?
Hata hivyo, baadhi ya watu wanahisi kwamba kwa sababu Mungu ni mtakatifu na mweza-yote, ni ukosefu wa heshima kutumia jina lake. Ni wazi kwamba haifai kutumia jina la Mungu katika njia isiyofaa, kama vile tu isivyofaa kutumia vibaya jina la rafiki yako mpendwa. Hata hivyo, ni mapenzi ya Yehova kwamba watu wanaompenda waliheshimu na kulitangaza jina lake. (Zaburi 69:30, 31; 96:2, 8) Kumbuka kwamba Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” Tunaweza kushiriki kulitakasa jina la Mungu kwa kuwaambia wengine kuhusu jina hilo. Kufanya hivyo kutatufanya tumkaribie.—Mathayo 6:9.
Biblia inaonyesha kwamba Mungu huwakazia fikira “wale wanaolifikiria jina lake.” (Malaki 3:16) Kuhusu mtu wa namna hiyo, Yehova anaahidi hivi: “Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu. Ataniitia, nami nitamjibu. Nitakuwa pamoja naye katika taabu.” (Zaburi 91:14, 15) Kujua na kutumia jina la Mungu, Yehova, ni muhimu ikiwa tunataka kufurahia uhusiano mzuri pamoja naye.
a Kwa kusikitisha, tafsiri nyingi za Biblia hazina jina la Mungu, licha ya kwamba linapatikana mara nyingi kwenye Maandiko ya Kiebrania yanayojulikana kama Agano la Kale. Badala yake jina la Mungu limeondolewa na mahali pake pakachukuliwa na majina ya cheo kama vile Bwana au Mungu. Kwa habari zaidi kuhusu jina la Mungu, ona ukurasa wa 195-197 kwenye kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Je, Unawasiliana na Mungu?Mnara wa Mlinzi—2014 | Desemba 1
-
-
HABARI KUU | UNAWEZA KUMKARIBIA MUNGU
Je, Unawasiliana na Mungu?
Marafiki hufanya yote wawezayo ili kuwasiliana, iwe ni kwa simu, barua-pepe, video, au barua, nao huwasiliana mara nyingi iwezekanavyo. Kwa hiyo, ili tuwe karibu na Mungu, tunahitaji kuwasiliana naye kwa ukawaida. Lakini, tunawezaje kufanya hivyo?
Tunaweza kuwasiliana na Mungu kupitia sala. Hata hivyo, kusali kwa Mungu ni tofauti na kuzungumza na mwanadamu mwenzako. Tunahitaji kutambua kwamba tunaposali tunazungumza na Muumba wetu, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu mzima. Kutambua hilo kutatuchochea tusali kwa heshima kubwa na staha. Ili Mungu asikilize sala zetu, tunapaswa kutimiza mambo fulani. Acheni tuchunguze baadhi ya mambo hayo.
Kwanza, tunapaswa kusali kwa Yehova Mungu tu—si kwa Yesu, “mtakatifu fulani,” au sanamu. (Kutoka 20:4, 5) Biblia inasema hivi waziwazi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Wafilipi 4:6) Pili, tunapaswa kusali kupitia jina la Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Tatu, tunapaswa kusali kuhusu mambo yanayopatana na mapenzi ya Mungu. Biblia inasema hivi: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”a—1 Yohana 5:14.
Marafiki wanaopendana huwasiliana mara nyingi iwezekanavyo
Ni kweli kwamba uhusiano hauwezi kusitawi ikiwa mtu mmoja ndiye anayezungumza nyakati zote. Kama marafiki wanavyofurahia kila mmoja wao anapochangia mazungumzo, tunapaswa kumruhusu Mungu azungumze nasi na kumsikiliza anapofanya hivyo. Je, unajua jinsi Mungu anavyozungumza nasi?
Leo, Yehova Mungu huzungumza nasi kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa nini tunasema hivyo? Fikiria mfano huu: Tuseme umepokea barua kutoka kwa rafiki yako mpendwa. Baada ya kuisoma, huenda ukafurahi kuwaeleza hivi wengine, “Nimezungumza na rafiki yangu!” Unasema hivyo hata ingawa ulisoma tu barua, hukuzungumza naye ana kwa ana. Vivyo hivyo, unaposoma Biblia, unamruhusu Yehova azungumze nawe. Hiyo ndio sababu, Gina, aliyetajwa kwenye makala iliyopita, anasema hivi: “Nafikiri kwamba ikiwa ninataka Mungu awe rafiki yangu, ninapaswa kuisoma ‘barua’ yake, yaani, Biblia.” Anaendelea kusema hivi, “Kusoma Biblia kila siku kumenifanya nimkaribie Mungu.” Je, unamruhusu Yehova azungumze nawe kwa kusoma Neno lake, Biblia, kila siku? Kufanya hivyo kutakusaidia umkaribie Mungu.
a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi unavyoweza kumkaribia Mungu kupitia sala, ona sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Je, Wewe Hufanya Yale Ambayo Mungu Anataka?Mnara wa Mlinzi—2014 | Desemba 1
-
-
HABARI KUU | UNAWEZA KUMKARIBIA MUNGU
Je, Wewe Hufanya Yale Ambayo Mungu Anataka?
“Ukitaka chochote, wewe sema tu, nami nitafanya.” Bila shaka huwezi kumwambia maneno hayo mtu usiyemjua au usiyemfahamu vizuri. Hata hivyo, haitakuwa vigumu kwako kumwambia maneno hayo rafiki yako mpendwa. Marafiki wa kweli hutendeana mambo mema.
Biblia inaonyesha kwamba Yehova hufanya kwa ukawaida mambo ambayo anajua yatawafurahisha waabudu wake. Kwa mfano, Mfalme Daudi, ambaye alifurahia uhusiano mzuri na Mungu, alisema hivi: “Wewe mwenyewe umefanya mambo mengi, Ee Yehova Mungu wangu, naam, kazi zako za ajabu na mawazo yako kutuelekea. . . . Zimekuwa nyingi sana kuliko vile ninavyoweza kusimulia.” (Zaburi 40:5) Isitoshe, Yehova anawatendea mema hata wale ambao bado hawamtumikii, ‘akijaza mioyo yao kikamili kwa chakula na uchangamfu.’—Matendo 14:17.
Tunafurahia kuwatendea mema watu tunaowapenda na kuwaheshimu
Kwa sababu Yehova anapenda kufanya mambo yanayowafurahisha viumbe wake, ni wazi kwamba anatarajia wale ambao wanataka kuwa rafiki zake wafanye mambo yatakayofanya ‘moyo wake ushangilie.’ (Methali 27:11) Unaweza kufanya mambo gani hususa ili umpendeze Mungu? Biblia inatuambia hivi: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Waebrania 13:16) Je, inamaanisha kwamba ili tumpendeze Yehova, inatosha tu kutenda mema na kushiriki vitu na wengine?
Biblia inasema hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 11:6) Kwa kweli, “Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova” na ndipo akaitwa “rafiki ya Yehova.” (Yakobo 2:23) Yesu Kristo pia alisisitiza umuhimu wa kuwa na “imani katika Mungu” ili tubarikiwe na Mungu. (Yohana 14:1) Kwa hiyo unawezaje kusitawisha imani inayohitajika ili kuwa rafiki ya Mungu? Kwanza, unahitaji kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu, Biblia. Kwa kufanya hivyo, utapata “ujuzi sahihi wa mapenzi yake” na hivyo utajua jinsi ya “kumpendeza yeye kikamili.” Kisha, kadiri unavyozidi kupata ujuzi huo na kutumia yale unayojifunza, imani yako kwa Mungu itazidi kuimarika naye ataendelea kukukaribia.—Wakolosai 1:9, 10.
-
-
Hii Ni Njia Bora ya MaishaMnara wa Mlinzi—2014 | Desemba 1
-
-
HABARI KUU | UNAWEZA KUMKARIBIA MUNGU
Hii Ni Njia Bora ya Maisha
Unapaswa kufanya nini ili umkaribie Mungu? Tumechunguza hatua kadhaa unazoweza kuchukua ili uwe rafiki ya Mungu:
Unahitaji kujua na kulitumia jina la Mungu, Yehova.
Zungumza naye kwa ukawaida kwa kusali na kusoma Neno lake, Biblia.
Endelea kufanya mambo yanayompendeza Yehova.
Ili umkaribie Mungu unahitaji kutumia jina lake, usali kwake, kujifunza Biblia, na kufanya mambo yanayompendeza
Kwa msingi wa mambo hayo, je, unafikiri kwamba unafanya mambo yanayohitajika ili kumkaribia Mungu? Je, unahisi kuna mambo unayohitaji kurekebisha? Kwa kweli, jitihada inahitajika, lakini utapata matokeo mazuri.
Jennifer mwanamke anayeishi Marekani anasema hivi: “Kila jitihada unayofanya ili kumkaribia Mungu ina faida. Urafiki na Mungu unaleta baraka nyingi kutia ndani: kumtumaini, kumjua vizuri zaidi, na zaidi ya yote, kumpenda. Hii ni njia bora ya maisha!”
Ikiwa ungependa kuwa na uhusiano mzuri na Mungu, Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia ufanye hivyo. Watapanga kujifunza Biblia pamoja nawe, bila malipo. Pia unakaribishwa kuhudhuria mikutano yao ya Biblia kwenye Jumba la Ufalme, ambapo utafurahia kushirikiana na watu wanaothamini uhusiano wao na Mungu.a Unapoendelea kufanya hivyo, wewe pia utahisi kama alivyohisi mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Lakini mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.”—Zaburi 73:28.
a Ili kuomba ufundishwe Biblia au kujua mahali lilipo Jumba la Ufalme lililo karibu nawe, tafadhali zungumza na mtu aliyekuletea gazeti hili au tembelea Tovuti yetu, www.jw.org/sw, na utazame kichwa WASILIANA NASI.
-