-
Je, Unyoofu Umepitwa na Wakati?Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 1
-
-
HABARI KUU | KWA NINI UWE MNYOOFU?
Je, Unyoofu Umepitwa na Wakati?
Hitoshi alikuwa mhasibu katika kampuni ya uwakala wa ajira huko Japani. Alipokuwa akifanya hesabu pamoja na bosi wake, Hitoshi aliambiwa aandike ripoti ya uwongo. Hitoshi alimweleza kwamba dhamiri yake haimruhusu kudanganya. Baada ya muda, Hitoshi alifukuzwa kazi.
Kwa miezi kadhaa, Hitoshi alivunjika moyo kwa sababu ya kukosa ajira. Kwa mfano, katika mahojiano ya kazi fulani, Hitoshi alieleza kwamba hangeweza kudanganya. Yule aliyemhoji akamwambia, “Unastaajabisha sana!” Ingawa watu wa familia na marafiki walimtia moyo awe imara na aendelee kuwa mnyoofu, Hitoshi alianza kuwa na mashaka. Kwa mfano, alisema hivi: “Nilianza kufikiria ikiwa ni jambo linalofaa kuwa mnyoofu kuhusu imani yangu.”
Mambo aliyokabili Hitoshi yanatukumbusha kwamba si kila mtu anapenda unyoofu. Kwa kweli, wengine wanaona unyoofu kuwa kizuizi hasa katika biashara. Mwanamke mmoja huko Afrika Kusini alisema hivi, “Nimezungukwa na watu wasio wanyoofu, na wakati mwingine ni vigumu kuwa mnyoofu.”
Kusema uwongo ni aina moja ya ukosefu wa unyoofu ulioenea sana leo. Miaka kadhaa iliyopita, utafiti uliofanywa na mwanasaikolojia Robert S. Feldmana wa chuo kikuu cha Massachusetts Amherst ulionyesha kwamba asilimia 60 ya watu hudanganya angalau mara moja katika kila mazungumzo ya dakika kumi. Feldman alisema hivi: “Matokeo hayo yalitushangaza sana, hatukutarajia uwongo uwe sehemu ya kawaida katika maisha yetu ya kila siku.” Inashangaza kwamba watu wengi wanachukia kudanganywa ilhali wao wenyewe husema uwongo.
Kwa nini kusema uwongo, kuiba, na aina nyingine za kukosa unyoofu ni mambo ya kawaida leo? Kukosa unyoofu kunawezaje kuiathiri jamii? Zaidi ya yote, tunawezaje kuepuka kunaswa na mazoea ya kukosa unyoofu?
-
-
Athari za Kukosa UnyoofuMnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 1
-
-
HABARI KUU | KWA NINI UWE MNYOOFU?
Athari za Kukosa Unyoofu
“Kwa kawaida, kuna matatizo ambayo yanaweza kusuluhishwa ikiwa mtu atakosa unyoofu.”—Samantha, Afrika Kusini.
Je, unakubaliana na maneno hayo? Kama Samantha, sote tumewahi kukabili hali ngumu. Jinsi tunavyotenda tunapokabili hali inayojaribu unyoofu wetu, kutaonyesha wazi viwango tunavyofuata. Kwa mfano, huenda tukakosa kuwa wanyoofu ili kuepuka aibu. Hata hivyo, kukosa unyoofu husababisha matokeo mabaya ukweli unapojulikana. Fikiria mambo yafuatayo.
KUKOSA UNYOOFU HUFANYA WATU WASIKUAMINI
Mahusiano hujengwa na uaminifu. Watu wawili wanapoaminiana, wanahisi wakiwa salama salimini. Lakini uaminifu hautokei mara moja tu. Uaminifu hujengeka watu wanapotumia wakati mwingi pamoja, wanapowasiliana kwa unyoofu, na wanapotenda bila ubinafsi. Hata hivyo, tendo moja tu la kukosa unyoofu linaweza kufanya tusiaminiwe. Na uaminifu unapovunjika, inaweza kuwa vigumu sana kuujenga upya.
Je, umewahi kudanganywa na mtu ambaye ulifikiri ni rafiki mzuri? Ikiwa ndivyo, ulihisije? Huenda ulivunjika moyo na kuhisi umesalitiwa. Jambo hilo linaeleweka. Bila shaka, kukosa unyoofu kunaweza kuharibu uhusiano mzuri.
UDANGANYIFU HUZAA UDANGANYIFU
Uchunguzi uliofanywa na profesa wa uchumi Robert Innes wa Chuo Kikuu cha California, ulionyesha kwamba “ukosefu wa unyoofu huambukiza.” Hivyo, kukosa unyoofu kunaweza kulinganishwa na virusi kwani kadiri unavyoshirikiana na mtu mwongo, ndivyo unavyokuwa katika mazingira hatari zaidi ya “kuathiriwa” na uwongo.
Unawezaje kuepuka kunaswa na mtego wa kukosa unyoofu? Biblia inaweza kukusaidia. Tafadhali chunguza kanuni chache za Biblia.
-
-
Faida ya Kuwa MnyoofuMnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2016 | Na. 1
-
-
HABARI KUU | KWA NINI UWE MNYOOFU?
Faida ya Kuwa Mnyoofu
“Tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.
Katika Biblia, neno la awali la Kigiriki ambalo nyakati nyingine hutafsiriwa kuwa “unyoofu” linamaanisha “kitu ambacho kiasili ni kizuri.” Linaweza pia kumaanisha kitu kizuri kinachofaa kulingana na maadili.
Wakristo wanachukua kwa uzito maneno ya mtume Paulo yaliyoongozwa na roho takatifu: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” Hilo linahusisha nini?
KUPAMBANA NA MWELEKEO WETU
Watu wengi hujitazama katika kioo kila asubuhi kabla ya kutoka nyumbani. Kwa nini? Kwa sababu wanataka kuonekana vizuri. Hata hivyo kuna jambo muhimu zaidi kuliko mtindo wetu wa kunyoa au mavazi ya kisasa. Utu wetu unaweza kuboresha au kuharibu mwonekano wetu.
Neno la Mungu linaeleza waziwazi kwamba tuna mwelekeo wa kufanya mambo mabaya. “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea,” linasema andiko la Mwanzo 8:21. Hivyo, ili tuwe wanyoofu, tunapaswa kujitahidi kupambana na mwelekeo wa dhambi tuliorithi. Mtume Paulo alitoa maelezo ya kina kuhusu pambano lake dhidi ya dhambi kwa kusema hivi: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo vyangu.”—Waroma 7:22, 23.
Kwa mfano, si lazima tufanye mambo mabaya hata kama moyo wetu unatuchochea kufanya mambo hayo au tuna mwelekeo wenye nguvu wa kutokuwa wanyoofu. Tuna uhuru wa kuamua cha kufanya. Tunapoamua kukataa mawazo mabaya, tunaweza kubaki wanyoofu licha ya kuzungukwa na ukosefu wa unyoofu.
KUSHINDA PAMBANO
Ili tuwe wanyoofu, tunahitaji viwango vya juu vya maadili. Kwa kusikitisha, watu wengi wanatumia wakati mwingi kuamua aina ya mavazi watakayovaa badala kufikiria maadili yao. Matokeo ni kwamba wanatetea ukosefu wao wa unyoofu ili wasiwajibike. Kitabu The (Honest) Truth About Dishonesty kinaelezea jambo hilo hivi: “Kwa kweli, tunadanganya ili tuendelee kuonekana kuwa watu wanyoofu.” Je, kuna viwango vyovyote vinavyoweza kutusaidia kuamua ikiwa kuna aina yoyote ya ukosefu wa unyoofu ambayo ni sawa? Bila shaka, vipo.
Mamilioni ya watu duniani pote wamegundua kwamba Biblia inaweza kutimiza kwa ukamili jambo hilo. Biblia ina viwango vya juu vya maadili kuliko vyote. (Zaburi 19:7) Inatupatia mwongozo wenye kutegemeka kuhusu mambo kama vile maisha ya familia, kazi, maadili, na hali ya kiroho. Mwongozo huo umewafaa watu kwa muda mrefu sana. Sheria na kanuni za Biblia zinatumiwa na watu wa mataifa, jamii, makabila na vikundi vya watu wote. Kwa kuisoma Biblia, kutafakari, na kutumia ushauri wake, tunaweza kuuzoeza moyo wetu uwe mnyoofu na mwadilifu.
Pamoja na kupata ujuzi sahihi wa Biblia, kuna mambo mengine yanayohitajika ili kupambana na ukosefu wa unyoofu. Tunaishi katika ulimwengu uliopotoka kiadili ambao unatushinikiza tupende mambo mabaya. Ndiyo sababu tunahitaji kusali ili kuomba msaada na utegemezo wa Mungu. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Kwa kufanya hivyo, tunaweza kupata ujasiri wa kusimama imara ili kutetea mambo mema na kuwa wanyoofu katika mambo yote.
BARAKA ZA UNYOOFU
Hitoshi, aliyenukuliwa katika makala ya kwanza, alinufaika kwa sababu ya kujulikana kuwa mfanyakazi mnyoofu. Sasa anafanya kazi kwa mwajiri ambaye anathamini unyoofu wake. Hitoshi anaeleza hivi: “Ninashukuru kwamba niliweza kupata kazi inayoniruhusu niendelee kuwa na dhamiri safi.”
Wengine pia wamenufaika kwa kuwa wanyoofu. Fikiria mifano ya wale ambao wamenufaika kwa kutumia kanuni ya Biblia ya “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”
Dhamiri Safi
“Niliacha shule nikiwa na umri wa miaka 13 ili kufanya kazi na wezi. Matokeo ni kwamba, asilimia 95 ya mapato yangu yalitokana na wizi. Niliolewa na hatimaye mimi na mume wangu tukaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Tulijifunza kwamba Yehovaa Mungu anachukia ukosefu wa unyoofu, hivyo tuliamua kubadili maisha yetu. Mwaka wa 1990 tukawa Mashahidi wa Yehova kwa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.”—Methali 6:16-19
“Zamani, nyumba yangu ilijaa vitu vya wizi lakini sasa sina tena vitu hivyo na hilo linafanya niwe na dhamiri safi. Ninapofikiria miaka mingi niliyoishi bila kuwa mnyoofu, ninamshukuru Yehova kwa rehema yake kubwa. Ndiyo sababu ninaridhika ninapoenda kulala kila siku huku nikijua kwamba Yehova anapendezwa nami.”—Cheryl, Ireland.
“Bosi wangu alipojua kwamba nilikataa kupokea rushwa kutoka kwa mteja, aliniambia hivi: ‘Mungu wako amekufanya kuwa mtu anayeaminika! Ni baraka kubwa kuwa nawe katika kampuni yetu.’ Kuwa mnyoofu katika mambo yote kumenifanya niwe na dhamiri safi mbele za Yehova Mungu. Pia kunanifanya niwe huru kuwahimiza watu wa familia yangu na watu wengine wafanye hivyo.”—Sonny, Hong Kong.
Amani ya Akili
“Mimi ni meneja katika benki ya kimataifa. Katika kazi hii mara nyingi unyoofu huwekwa pembeni ili kupata mali. Maoni ya watu wengi ni, ‘hakuna shida yoyote ukikosa unyoofu kidogo ili kupata mali na kuboresha uchumi.’ Lakini nina amani ya akili kwa sababu ya kuwa mnyoofu. Nimeazimia kuendelea kuwa mnyoofu na kukabili hali yoyote itakayotokea kwa sababu ya kufanya hivyo. Waajiri wangu wanajua kwamba sitawadanganya na wala sitadanganya kwa niaba yao.”—Tom, Marekani.
Kuheshimika
“Msimamizi wangu alinichochea nidanganye kuhusu kupotea kwa vitu fulani kazini lakini nilikataa. Wezi walipogunduliwa, mwajiri wangu alinishukuru kwa sababu ya unyoofu wangu. Inahitaji ujasiri kuwa mnyoofu katika ulimwengu huu wenye ukosefu wa unyoofu. Lakini mwishowe tunaweza kuaminiwa na kuheshimiwa.”—Kaori, Japani.
Dhamiri safi, amani ya akili, na kuheshimika ni baraka zinazoonyesha kwamba unyoofu una faida. Bila shaka unakubaliana na jambo hilo.
a Yehova ni jina la Mungu linalotajwa katika Biblia.
-