-
Hakuna Anayeweza Kuwatumikia Mabwana WawiliMnara wa Mlinzi—2014 | Aprili 15
-
-
Hakuna Anayeweza Kuwatumikia Mabwana Wawili
“Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili . . . Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”—MT. 6:24.
1-3. (a) Watu wengi wanakabili matatizo gani ya kifedha, na baadhi yao hujaribu kuyatatua jinsi gani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Wazazi wanaohama huwa na mahangaiko gani kuhusu kulea watoto wao?
“MUME wangu, James, alirudi nyumbani kila siku akiwa amechoka sana baada ya kazi. Isitoshe, mshahara wake haukutosha mahitaji yetu ya kila siku,” akasema Marilyn.a Aliendelea kusema hivi: “Nilitaka kumpunguzia mzigo na kumnunulia mwana wetu, Jimmy, baadhi ya vitu vizuri ambavyo wanashule wenzake walikuwa navyo.” Marilyn alitaka pia kuwasaidia watu wao wa ukoo na kuweka pesa zitakazowasaidia wakati ujao. Tayari rafiki zake wengi walikuwa wamehamia nchi nyingine kufanya kazi ili wapate pesa zaidi. Hata hivyo, alikuwa na wasiwasi kuhusu uamuzi wake wa kuhamia nchi nyingine. Kwa nini?
2 Marilyn aliogopa kuiacha familia yake aliyoithamini sana na kuacha ratiba yao ya mambo ya kiroho. Hata hivyo, akawaza kwamba wengine wamehamia nchi nyingine kwa muda na familia zao zinaonekana zinaendelea vizuri kiroho. Hata hivyo, alifikiria pia jinsi ambavyo angemlea Jimmy akiwa mbali. Je, angefanikiwa kumlea mwana wake “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova” kwa kutumia Intaneti?—Efe. 6:4.
3 Marilyn alitafuta ushauri. Mume wake alimwambia kwamba hangependa ahamie nchi nyingine, lakini hatamzuia kufanya hivyo. Wazee na wengine kutanikoni walimshauri asiende, lakini dada kadhaa walimtia moyo ahamie nchi nyingine. Dada hao walimwambia hivi: “Nenda ikiwa unaipenda familia yako. Unaweza kuendelea kumtumikia Yehova huko.” Ijapokuwa alikuwa na shaka, Marilyn alimwacha James na Jimmy na kuhamia nchi nyingine ili kufanya kazi. Aliwaahidi hivi: “Nitarudi karibuni.”
WAJIBU WA FAMILIA NA KANUNI ZA BIBLIA
4. Kwa nini watu wengi huhamia nchi nyingine? Na mara nyingi ni nani huwatunza watoto wao?
4 Yehova hataki watumishi wake wawe maskini kabisa, na tangu zamani watu wamekuwa wakihamia maeneo mengine ili kukabiliana na umaskini. (Zab. 37:25; Met. 30:8) Ili familia yake isife njaa, Yakobo, mzee wa ukoo aliwatuma wanawe Misri kununua chakula.b (Mwa. 42:1, 2) Hata hivyo, watu wengi leo hawahamii nchi nyingine ili kukabiliana na njaa. Huenda wakafanya hivyo ili kulipa deni kubwa. Wengine huhama kwa kuwa wanatamani tu kuboresha hali ya kifedha ya familia yao. Ili kufanya hivyo, wengi huhamia eneo au nchi nyingine mbali na familia zao. Watu wengi wanapohama, wanawaacha watoto wao wadogo watunzwe na mzazi anayebaki, mtoto wao mkubwa, babu na nyanya (bibi), watu wengine wa ukoo, au marafiki. Ijapokuwa watu wengi wanaohamia nchi nyingine huhuzunika sana kumwacha mwenzi wa ndoa au watoto wao, wanahisi kwamba hawana budi kufanya hivyo.
5, 6. (a) Yesu alifundisha nini kuhusu furaha na usalama? (b) Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kuhusu mambo gani ya kimwili? (c) Yehova anatubariki kwa njia gani?
5 Katika siku za Yesu pia, watu wengi walikuwa maskini na huenda walifikiri kwamba wangekuwa na furaha na usalama zaidi ikiwa wangepata pesa nyingi. (Marko 14:7) Lakini Yesu hakutaka watu watumaini pesa. Alitaka wamtegemee Yehova, Chanzo cha utajiri wa kudumu. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema kwamba furaha na usalama wa kweli hautegemei vitu vya kimwili au jitihada zetu, badala yake unategemea urafiki wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni.
6 Katika sala yake ya kielelezo, Yesu hakutufundisha tusali tupate usalama wa kifedha, alitufundisha tuombe mahitaji yetu ya kila siku, yaani, “mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” Aliwaambia wasikilizaji wake hivi waziwazi: “Acheni kujiwekea hazina duniani . . . Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni.” (Mt. 6:9, 11, 19, 20) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatubariki kama alivyoahidi. Baraka za Mungu si kibali chake tu, bali pia anahakikisha kwamba tunapata vitu tunavyohitaji kikweli. Kwa kweli, njia pekee ya kupata furaha na usalama wa kweli ni kumtegemea Baba yetu anayetujali badala ya kutegemea pesa.—Soma Mathayo 6:24, 25, 31-34.
7. (a) Yehova amewapa nani daraka la kuwalea watoto? (b) Kwa nini wazazi wote wawili wanahitaji kushirikiana katika kuwalea watoto?
7 ‘Kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu’ kunatia ndani kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu wajibu wa kutunza familia. Sheria ya Musa ina kanuni hii inayowahusu pia Wakristo: Wazazi wanahitaji kuwapa watoto wao mazoezi ya kiroho. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.) Mungu amewapa daraka hilo wazazi, bali si babu, nyanya, au mtu mwingine yeyote. Mfalme Sulemani alisema hivi: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Met. 1:8) Yehova alikusudia wazazi wote wawili wawepo ili kuwaongoza na kuwafundisha watoto wao. (Met. 31:10, 27, 28) Watoto hujifunza mambo mengi, hasa mambo ya kiroho, kwa kuwasikiliza wazazi wakiongea kumhusu Yehova kila siku na kupitia mfano wao.
MATOKEO YASIYOTARAJIWA
8, 9. (a) Inakuwaje mzazi anapoishi mbali na familia? (b) Ni madhara gani ya kihisia na kimaadili yanayotokea wazazi wanapoishi mbali na watoto wao?
8 Kabla ya kuhamia nchi nyingine, watu hujaribu kufikiria mambo watakayohitaji kudhabihu na hatari zinazohusika, lakini ni wachache tu wanaofikiria madhara ya kuiacha familia yao. (Met. 22:3)c Baada ya kuhama, Marilyn alianza kuumia sana moyoni kwa sababu ya kuiacha familia yake. Mume na mtoto wake waliumia pia. Mtoto wake, Jimmy, alimuuliza hivi tena na tena: “Kwa nini uliniacha?” Na kadiri miaka ilivyopita, Marilyn alishtuka alipogundua kwamba familia yake imebadilika. Hisia na upendo wa Jimmy kumwelekea ulipungua. Marilyn anasema hivi kwa huzuni: “Hakunipenda tena kama zamani.”
9 Wazazi wanapoishi mbali na watoto wao, wote wanaweza kuathiriwa kihisia na kimaadili.d Watoto wenye umri mdogo zaidi ndio huumia zaidi mzazi anapoishi mbali kwa muda mrefu. Marilyn alimwambia Jimmy kwamba alihamia nchi nyingine kwa faida yake. Hata hivyo, Jimmy alihisi kwamba mama amemwacha. Mwanzoni, alimkosa sana mama yake. Lakini baadaye, Jimmy hakutaka kumwona mama yake alipowatembelea. Kama ilivyo kawaida kwa watoto walioachwa, Jimmy alihisi kwamba mama yake hakustahili tena kupendwa na kuonyeshwa utii.—Soma Methali 29:15.
Huwezi kumkumbatia mtoto wako kupitia Intaneti (Tazama fungu la 10)
10. (a) Matokeo yanakuwa nini mzazi akimpa mtoto zawadi badala ya kutumia wakati pamoja naye? (b) Watoto hukosa nini mzazi akiishi mbali nao?
10 Ijapokuwa Marilyn alimtumia mwana wake pesa na zawadi ili ahisi kwamba hajamwacha, aliona kwamba alikuwa akijitenga na mtoto wake na bila kukusudia alikuwa akimfundisha kutanguliza mambo ya kimwili badala ya mambo ya kiroho na mahusiano ya familia. (Met. 22:6) Jimmy alimwambia hivi: “Usirudi. Endelea tu kunitumia zawadi.” Marilyn alianza kugundua kwamba hangeweza ‘kumlea mwana wake kupitia vyombo vya mawasiliano,’ kama vile barua, simu, au kuwasiliana naye kupitia video. Anasema hivi: “Huwezi kumkumbatia au kumbusu mtoto wako kupitia Intaneti.”
Unaweza kukabili hatari gani ukiishi mbali na mwenzi wako? (Tazama fungu la 11)
11. (a) Ndoa itaathiriwaje ikiwa wenzi wa ndoa hawaishi pamoja kwa sababu ya kazi ya kimwili? (b) Dada mmoja alitambuaje umuhimu wa kurudi ili kuishi na familia yake?
11 Uhusiano wa Marilyn na Yehova, na uhusiano wake na mume wake, James, ulidhoofika pia. Alishirikiana na kutaniko na kuhubiri siku moja kwa juma au nyakati nyingine alishindwa kufanya hivyo, naye alilazimika kukabiliana daima na mwajiri wake aliyekuwa akimtongoza. Kwa kuwa walikuwa mbali wasiweze kutegemezana wakati wa matatizo, Marilyn na James walisitawisha mahusiano ya kimahaba nje ya ndoa na karibu wafanye uzinzi. Marilyn aligundua kwamba ingawa yeye na mume wake hawakufanya uzinzi, kuishi mbali kuliwafanya wasifuate shauri la Biblia kuhusu kutosheleza mahitaji ya kihisia na ya kingono ya mwenzi wao wa ndoa. Hawakuweza kuzungumza wakati wowote, kutazamana, kutabasamu, kushikana mikono kwa wororo, kukumbatiana kwa uchangamfu, ‘kuonyeshana mapenzi,’ au kumpa mwenzi wao “haki” ya ndoa. (Wim. 1:2; 1 Kor. 7:3, 5) Pia hawakuweza kumwabudu Yehova kikamili wakiwa na mwana wao. Marilyn anasema hivi: “Niliposikia katika kusanyiko kwamba ni muhimu sana kufanya ibada ya familia kwa ukawaida ili tuokoke siku kuu ya Yehova, niliona wazi kwamba ninahitaji kurudi nyumbani. Nilihitaji kuanza kujenga tena hali yangu ya kiroho na maisha yangu ya familia.”
MASHAURI MAZURI NA MABAYA
12. Ni mashauri gani ya Kimaandiko tunayoweza kuwapa wale wanaoishi mbali na familia zao?
12 Kila mtu alikuwa na maoni tofauti kuhusu uamuzi wa Marilyn wa kurudi nyumbani. Wazee wa kutaniko katika nchi aliyohamia walimpongeza kwa sababu ya imani na ujasiri wake. Hata hivyo, baadhi ya wale waliohamia nchi nyingine mbali na wenzi wao wa ndoa na familia yao hawakufurahishwa na uamuzi wake. Badala ya kuiga mfano wake mzuri, walijaribu kumshauri asirudi nyumbani. Walimwambia hivi: “Utarudi huku hivi karibuni. Utapataje riziki ukirudi nyumbani?” Badala ya kusema maneno kama hayo yenye kuvunja moyo, Wakristo wenzetu wanapaswa “kuziamsha akili za wanawake vijana wawapende waume zao, wawapende watoto wao, wawe . . . wafanyakazi nyumbani,” yaani, katika nyumba zao wenyewe, “ili neno la Mungu lisitukanwe.”—Soma Tito 2:3-5.
13, 14. Kwa nini imani inahitajiwa ili kumtanguliza Yehova badala ya mapendezi ya watu wa ukoo? Toa mfano.
13 Wengi wanaoacha familia zao na kuhamia nchi nyingine ili kufanya kazi, wamelelewa katika nchi zenye utamaduni unaoheshimu sana desturi na mapendezi ya watu wa ukoo, hasa wazazi. Kwa kweli, Mkristo anaonyesha imani anapoamua kumpendeza Yehova badala ya kufuata desturi au mapendezi ya familia.
14 Carin anasema hivi: “Mwana wetu Don alipozaliwa, mimi na mume wangu tulikuwa tukifanya kazi katika nchi nyingine, na nilikuwa nimeanza tu kujifunza Biblia. Kila mtu katika familia yetu alitarajia kwamba ningempeleka Don nyumbani ili wazazi wangu wamlee hadi hali yetu ya kiuchumi itakapokuwa nzuri.” Carin aliposisitiza kwamba anataka kumlea Don, watu wa ukoo pamoja na mume wake walimcheka na kusema kwamba yeye ni mvivu. Carin anasema hivi: “Kusema kweli, wakati huo sikuelewa kikamili kwa nini haikufaa kumpeleka Don kwa wazazi wangu ili wamlee kwa miaka michache. Hata hivyo, nilijua kwamba tukiwa wazazi, Yehova ametupatia kazi ya kumlea mwana wetu.” Carin alipokuwa mjamzito tena, mume wake asiye mwamini alisisitiza atoe mimba hiyo. Lakini uamuzi mzuri aliofanya Carin mwanzoni uliimarisha imani yake, na kwa mara nyingine tena alishikamana na sheria za Yehova. Sasa yeye, mume wake, na watoto wao, wanafurahi kwamba waliendelea kukaa pamoja. Huenda mambo yangekuwa tofauti kabisa ikiwa Carin angewapeleka watoto wake wakalelewe na watu wengine.
15, 16. (a) Dada mmoja aliyelelewa na watu wa ukoo alikabili hali gani? (b) Kwa nini aliamua kumlea binti yake?
15 Shahidi anayeitwa Vicky anasema hivi: “Nililelewa na nyanya yangu kwa miaka kadhaa na dada yangu mdogo alilelewa na wazazi wangu. Niliporudi nyumbani, upendo wangu kuwaelekea wazazi wangu ulikuwa umepungua. Dada yangu alikuwa na uhusiano wa karibu na wazazi wetu, aliwakumbatia na kuongea nao kwa uhuru. Hata hivyo, sikuwa na uhusiano wa karibu na wazazi wangu, na hata nikiwa mtu mzima bado si rahisi kuwaeleza ninavyohisi. Mimi na dada yangu tumewahakikishia wazazi wetu kwamba tutawatunza watakapozeeka. Lakini nitawatunza ili kutimiza wajibu tu, tofauti na dada yangu atakayewatunza kwa sababu anawapenda.”
16 Vicky anaendelea kusema hivi: “Sasa mama yangu anataka kumlea binti yangu kama nyanya alivyonilea. Nilikataa kwa busara. Mimi na mume wangu tunataka kumlea mtoto wetu katika njia za Yehova. Singependa kuharibu uhusiano wangu na binti yangu.” Vicky ametambua kwamba njia pekee ya kufanikiwa ni kumtanguliza Yehova na kanuni zake badala ya mali au mapendezi ya watu wa ukoo. Yesu alisema hivi waziwazi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili,” Mungu na Utajiri.—Mt. 6:24; Kut. 23:2.
YEHOVA ‘HUFANIKISHA’ JITIHADA ZETU
17, 18. (a) Sikuzote Wakristo wana uhuru wa kuchagua nini? (b) Ni maswali gani tutakayozungumzia katika makala inayofuata?
17 Baba yetu, Yehova, ameazimia kutusaidia kupata mahitaji yetu ya lazima ikiwa tunatanguliza masilahi ya Ufalme na uadilifu wake maishani mwetu. (Mt. 6:33) Hivyo, sikuzote Wakristo wa kweli wana uhuru wa kuchagua jambo la kutanguliza. Yehova anaahidi kuandaa “njia ya kutokea” na hivyo hatuhitaji kulegeza kanuni za Biblia hata tukikabili hali yoyote ngumu. (Soma 1 Wakorintho 10:13.) Tukiendelea ‘kumngojea Yehova kwa kutamani’ na ‘tukimtegemea’ kwa kusali ili atupatie hekima na mwongozo wake na tukifuata amri na kanuni zake, yeye “mwenyewe atatenda.” (Zab. 37:5, 7) Atatubariki kabisa tukijitahidi kutoka moyoni kumtumikia yeye peke yake akiwa Bwana wa pekee wa kweli. Tukimtanguliza, ‘atafanikisha’ maisha yetu.—Linganisha na Mwanzo 39:3.
18 Tunaweza kufanya nini ili kuondoa madhara yanayosababishwa na familia kutengana? Tunaweza kuchukua hatua gani zinazofaa ili kuandaa mahitaji ya kimwili ya familia yetu bila kuishi mbali nao? Na tunawezaje kuwatia wengine moyo kwa upendo kufanya maamuzi yanayofaa kuhusiana na jambo hilo? Makala inayofuata itazungumzia maswali hayo.
-
-
Uwe Hodari—Yehova Ni Msaidizi Wako!Mnara wa Mlinzi—2014 | Aprili 15
-
-
Uwe Hodari Yehova Ni Msaidizi Wako!
“Tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu.’”—EBR. 13:6.
1, 2. Wahamiaji wengi hukabili changamoto gani wanaporudi nyumbani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)
“NILIPATA pesa nyingi sana nilipokuwa nikifanya kazi katika nchi nyingine. Hata hivyo, nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilitambua kwamba nina daraka muhimu zaidi la kuitunza familia yangu kiroho wala si kimwili tu. Hivyo, nilirudi nyumbani,” anasema Eduardo.a—Efe. 6:4.
2 Eduardo alijua kwamba Yehova alipendezwa na uamuzi wake wa kurudi ili kuishi na familia yake. Hata hivyo, sawa na Marilyn aliyetajwa katika makala iliyotangulia, Eduardo alihitaji kujitahidi sana kurekebisha uhusiano wake na familia yake. Alikabili pia changamoto ya kuiandalia familia yake mahitaji yao chini ya hali ngumu zaidi ya kiuchumi. Angepataje riziki? Washiriki wengine wa kutaniko wangemsaidiaje?
KUREKEBISHA HALI YA KIROHO NA MAISHA YA FAMILIA
3. Watoto huathiriwaje mzazi anapoishi mbali?
3 Eduardo anasema hivi: “Nilitambua kwamba niliwapuuza watoto wangu walipohitaji sana mwongozo na upendo. Sikuwapo ili kuwasomea masimulizi ya Biblia, kusali nao, kuwakumbatia, na kucheza nao.” (Kum. 6:7) Anna, binti yake mkubwa, anasema hivi: “Baba alipoondoka nyumbani sikuhisi nikiwa salama. Aliporudi, tulimwona kama mgeni tu. Aliponikumbatia, nilihisi ni kana kwamba ninakumbatiwa na mtu nisiyemjua.”
4. Kwa nini mume hawezi kutimiza daraka lake akiwa kichwa cha familia ikiwa anaishi mbali?
4 Baba hawezi kutimiza daraka lake akiwa kichwa cha familia ikiwa anaishi mbali. Ruby, mke wa Eduardo, anasema hivi: “Nililazimika kutimiza daraka la Mama na Baba hivyo nikazoea kufanya maamuzi mengi katika familia. Eduardo aliporudi, nilihitaji kujifunza kujitiisha chini yake nikiwa mke Mkristo. Hata sasa, nyakati nyingine ninahitaji kujikumbusha kwamba mume wangu yupo.” (Efe. 5:22, 23) Eduardo anaongezea hivi: “Binti zangu walizoea kumwomba mama yao ruhusa kabla ya kufanya jambo fulani. Tukiwa wazazi, tuligundua kwamba watoto wetu walihitaji kuona kwamba tuna umoja, nami nilihitaji kujifunza kuiongoza familia yangu kwa njia ya Kikristo.”
5. Baba mmoja alianzaje kurekebisha uhusiano wake na familia yake? Matokeo yalikuwa nini?
5 Eduardo aliazimia kufanya yote awezayo ili kurekebisha uhusiano wake pamoja na familia yake na kuimarisha hali yao ya kiroho. Anasema hivi: “Lengo langu lilikuwa kuwafundisha kweli watoto wangu kwa maneno na matendo, yaani, kuonyesha kwamba ninampenda Yehova badala ya kusema tu.” (1 Yoh. 3:18) Je, Yehova alimbariki Eduardo kwa sababu ya kutenda kwa imani? Anna anasema hivi: “Ninatiwa moyo sana ninapomwona akifanya yote awezayo ili kuwa baba mzuri na kujitahidi kuwa tena na uhusiano wa karibu pamoja nasi. Tulifurahi pia kumwona akijitahidi kufikia mapendeleo kutanikoni. Ulimwengu ulijaribu kututenganisha na Yehova. Lakini tuliona wazazi wetu wakichukua kweli kwa uzito, nasi pia tulijitahidi kufanya hivyo. Baba alituahidi kwamba hatatuacha tena, na hajatuacha. Ikiwa angetuacha, huenda leo nisingekuwa katika tengenezo la Yehova.”
KUKUBALI MAJUKUMU
6. Baadhi ya wazazi walijifunza nini kuhusu kulea watoto katika kipindi cha vita?
6 Mambo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba wakati wa vita katika nchi za Balkani, watoto wa Mashahidi wa Yehova walikuwa na furaha licha ya kwamba waliishi chini ya hali ngumu. Kwa nini? Kwa sababu wazazi ambao hawangeweza kwenda kazini walibaki nyumbani na kujifunza, kucheza, na kuzungumza nao. Tunajifunza nini? Wazazi wanahitaji kutumia wakati pamoja na watoto wao badala ya kuwapa tu pesa au zawadi. Kwa kweli, kama Neno la Mungu linavyosema, watoto watanufaika wakitunzwa na kuzoezwa na wazazi wao.—Met. 22:6.
7, 8. (a) Baadhi ya wazazi wanaorudi wanafanya kosa gani? (b) Wazazi wanaorudi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao kushinda hisia zisizofaa?
7 Inasikitisha kwamba baadhi ya wazazi wanaporudi na kukataliwa na watoto wao, wanasema hivi: “Mbona huna shukrani licha ya kwamba nimejidhabihu sana kwa ajili yako?” Hata hivyo, huenda watoto wao wana mtazamo huo usiofaa kwa sababu wazazi waliwaacha. Mzazi atafanya nini ili kurekebisha hali hiyo?
8 Mwombe Yehova akusaidie kuelewa vizuri hisia za familia yako. Kisha, unapozungumza na familia yako, kubali kwamba umechangia tatizo hilo. Kuwaomba msamaha kutoka moyoni kunaweza kusaidia. Mwenzi wako na watoto wanapoona kwamba unajitahidi sana kurekebisha hali, watatambua unyoofu wako. Ukiazimia na kuonyesha subira, huenda familia yako ikaanza tena kukupenda na kukuheshimu.
‘KUWAANDALIA MAHITAJI WALIO WAKO MWENYEWE’
9. Kwa nini hatuhitaji kutafuta vitu vingi vya kimwili ili ‘tuwaandalie mahitaji walio wetu’?
9 Mtume Paulo aliagiza kwamba Wakristo waliozeeka wakishindwa kupata riziki, watoto wao na wajukuu watahitaji “kuwalipa wazazi na wazazi wa wazazi wao malipo yanayowastahili.” Lakini Paulo aliwahimiza pia Wakristo wote waridhike na mahitaji yao ya kila siku, yaani, chakula, mavazi, na makao. Hatupaswi kujitahidi daima kuwa na maisha ya hali ya juu au kupata usalama wa kifedha. (Soma 1 Timotheo 5:4, 8; 6:6-10.) Ili ‘kuwaandalia mahitaji walio wake mwenyewe,’ Mkristo hahitaji kutafuta utajiri katika ulimwengu huu utakaopitilia mbali hivi karibuni. (1 Yoh. 2:15-17) Hatupaswi kuruhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri” au “mahangaiko ya maisha” yahatarishe azimio la familia yetu la ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli’ katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu!—Marko 4:19; Luka 21:34-36; 1 Tim. 6:19.
10. Tunawezaje kuonyesha hekima ya Mungu inapohusu madeni?
10 Yehova anajua kwamba tunahitaji kiasi fulani cha pesa. Hata hivyo, pesa haziwezi kutulinda na kututegemeza kama hekima ya Mungu inavyoweza kutulinda. (Mhu. 7:12; Luka 12:15) Watu wengi hupuuza hatari ya kwenda kufanya kazi katika nchi nyingine na uhakika wa kwamba huenda wasipate pesa. Ukweli ni kwamba kuna hatari kubwa sana. Watu wengi hurudi nchini mwao wakiwa na madeni makubwa hata zaidi. Badala ya kuwa huru kumtumikia Mungu, wanawatumikia tu wale wanaowadai pesa. (Soma Methali 22:7.) Jambo la hekima ni kuepuka madeni.
11. Kufuata bajeti kunaisaidiaje familia kupunguza matatizo ya kiuchumi?
11 Eduardo aligundua kwamba alihitaji kuwa na maoni yanayofaa kuhusu pesa ili akae na familia yake kama alivyoazimia. Yeye na mke wake walipanga bajeti ya vitu walivyohitaji kikweli. Ni kweli kwamba hawakuzoea bajeti kama hiyo yenye vitu vichache. Hata hivyo, wote walishirikiana kwa kutonunua vitu wasivyohitaji.b Eduardo anasema hivi: “Kwa mfano, niliwapeleka watoto wangu katika shule nzuri ya serikali badala ya shule ya kibinafsi.” Eduardo na familia yake walisali ili apate kazi ya kimwili ambayo haingevuruga ratiba yao ya kiroho. Yehova alijibuje sala zao?
12, 13. Baba mmoja alichukua hatua gani zinazofaa ili kuandaa mahitaji ya familia yake? Yehova alibarikije azimio lake la kuishi maisha rahisi?
12 Eduardo anakumbuka hivi: “Mambo hayakuwa rahisi miaka miwili ya kwanza. Pesa zilianza kupungua, mshahara wangu mdogo haukuweza kulipia gharama zetu zote, na nilichoka kimwili. Hata hivyo, tuliweza kuhudhuria mikutano yote na kushiriki pamoja katika huduma.” Eduardo aliazimia kutokubali kazi yoyote itakayomfanya aiache familia yake kwa miezi au miaka kadhaa. Anasema hivi: “Badala yake, nilijifunza kazi tofauti-tofauti ili nifanye kazi yoyote ninayopata.”
13 Eduardo alilazimika kulipa riba kubwa kwa sababu alilipa madeni yake kidogo-kidogo. Hata hivyo, aliona kwamba kuwa na familia yake, kama Yehova anavyotaka wazazi wafanye, hakuwezi kulinganishwa na riba anayolipa. Eduardo anasema hivi: “Ingawa sasa ninapata mshahara ambao hauzidi asilimia 10 ya mshahara niliopata katika nchi nyingine, hatujawahi kulala njaa. ‘Mkono wa Yehova si mfupi.’ Hata tuliamua kufanya upainia. Jambo la kushangaza ni kwamba baada ya kufanya hivyo, hali yetu ya kifedha iliboreka na ikawa rahisi zaidi kupata mahitaji muhimu ya kimwili.”—Isa. 59:1.
KUKABILIANA NA SHINIKIZO LA FAMILIA
14, 15. Familia zinawezaje kukabiliana na shinikizo la kutafuta mali badala ya kutanguliza mambo ya kiroho? Na mfano wao mzuri huenda ukawa na matokeo gani?
14 Katika nchi nyingi, watu wanahisi kwamba wana daraka la kuwapa pesa na zawadi watu wao wa ukoo na marafiki. Eduardo anasema hivi: “Hiyo ni sehemu ya utamaduni wetu, nasi tunafurahia sana kutoa. Hata hivyo kuna mipaka. Kwa busara, mimi huwaambia watu wangu wa ukoo kwamba nitawasaidia kadiri niwezavyo bila kuhatarisha hali yetu ya kiroho na kuvuruga ratiba ya familia yangu.”
15 Wale wanaokataa kuacha familia zao ili kufanya kazi nchi nyingine na pia wahamiaji wanaorudi nyumbani, mara nyingi hudhihakiwa na kukasirikiwa na watu wa ukoo waliotamauka kwa sababu walitarajia kwamba wangewaandalia riziki. Baadhi yao husema kwamba watu hao hawapendi familia zao. (Met. 19:6, 7) Anna, binti ya Eduardo anasema hivi: “Hata hivyo, tunapokataa kutafuta mali ili kufuatilia mambo ya kiroho, hatimaye baadhi ya watu wetu wa ukoo huenda wakatambua kwamba maisha yetu ya Kikristo ni muhimu sana. Lakini watajuaje jambo hilo tukifanya wanavyotaka?”—Linganisha na 1 Petro 3:1, 2.
KUDHIHIRISHA IMANI KATIKA MUNGU
16. (a) Mtu anawezaje ‘kujidanganya mwenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli’? (Yak. 1:22) (b) Yehova hubariki maamuzi ya aina gani?
16 Dada mmoja aliyehamia nchi nyingine yenye ufanisi na kuwaacha watoto na mwenzi wake, aliwaambia hivi wazee wa kutaniko lake jipya: “Familia yetu imejidhabihu sana ili nije hapa. Hata mume wangu aliacha pendeleo la kuwa mzee. Hivyo, ninatumaini kabisa kwamba Yehova atabariki uamuzi wangu wa kuhamia hapa.” Sikuzote Yehova hubariki maamuzi yanayoonyesha kwamba tuna imani kumwelekea, lakini atabariki namna gani uamuzi usiopatana na mapenzi yake, hasa ikiwa tunaacha mapendeleo matakatifu kwa sababu zisizofaa?—Soma Waebrania 11:6; 1 Yohana 5:13-15.
17. Kwa nini tunahitaji kutafuta mwongozo wa Yehova kabla ya kufanya maamuzi, na tutafanyaje hivyo?
17 Tafuta mwongozo wa Yehova kabla ya kufanya maamuzi wala si baada ya kufanya maamuzi. Sali ili akupe roho yake takatifu, hekima, na mwongozo. (2 Tim. 1:7) Jiulize hivi: ‘Je, niko tayari kumtii Yehova chini ya hali zozote zile? Hata nikiteswa?’ Ikiwa ni hivyo, je, uko tayari kumtii hata ikimaanisha kuishi maisha rahisi zaidi? (Luka 14:33) Waombe wazee mashauri na ufuate mashauri yao yanayotegemea Biblia. Ukifanya hivyo, utaonyesha kwamba unaamini ahadi ya Yehova ya kukusaidia. Wazee hawatakufanyia maamuzi, lakini wanaweza kukusaidia kufanya maamuzi ambayo mwishowe yatakuletea furaha.—2 Kor. 1:24.
18. Ni nani mwenye daraka la kuiandalia familia? Wakristo wengine wanaweza kusaidia katika hali gani?
18 Yehova amempa kichwa cha familia “mzigo” wa kuiandalia familia yake mahitaji ya kila siku. Tunapaswa kuwapongeza na kusali kwa ajili ya wote wanaotimiza daraka lao bila kumwacha mwenzi au watoto wao hata ingawa wanashinikizwa na kushawishiwa kufanya hivyo. Hali zisizotarajiwa, kama vile misiba au matatizo ya kiafya, zinatupa nafasi ya kuonyeshana upendo wa kweli wa Kikristo na hisia-mwenzi. (Gal. 6:2, 5; 1 Pet. 3:8) Je, unaweza kutoa michango ya pesa wakati wa dharura au kumsaidia Mkristo mwenzako kupata kazi katika eneo lenu? Ukifanya hivyo, unaweza kupunguza mkazo ambao huenda anakabili wa kutaka kuiacha familia ili kutafuta kazi katika eneo au nchi nyingine.—Met. 3:27, 28; 1 Yoh. 3:17.
KUMBUKA KWAMBA YEHOVA NI MSAIDIZI WAKO!
19, 20. Kwa nini Wakristo wanaweza kuridhika kwa kujua kwamba Yehova atawasaidia?
19 Maandiko yanatuhimiza hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’ Hivi kwamba tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?’” (Ebr. 13:5, 6) Hilo linawezekanaje?
20 Ndugu ambaye amekuwa mzee wa kutaniko kwa miaka mingi katika nchi inayositawi anasema hivi: “Mara nyingi watu husema kwamba Mashahidi wa Yehova wana furaha. Husema pia kwamba hata Mashahidi walio maskini huvaa na kuonekana wakiwa nadhifu kuliko watu wengine.” Hilo linapatana na ahadi ya Yesu kwa wale wanaotafuta kwanza Ufalme. (Mt. 6:28-30, 33) Naam, Baba yetu wa mbinguni, Yehova, anakupenda na anataka wewe na watoto wako muwe na maisha bora. “Macho yake [Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Nya. 16:9) Ametupatia amri zake kwa faida yetu, kutia ndani amri kuhusu maisha ya familia na mahitaji ya kimwili. Tunapozifuata, tunaonyesha kwamba tunampenda na tunamtegemea. “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yoh. 5:3.
21, 22. Kwa nini umeazimia kumtegemea Yehova?
21 Eduardo anasema hivi: “Ninajua kwamba sitaupata tena wakati niliopoteza nilipoishi mbali na mke na watoto wangu, lakini sikazii fikira jambo hilo. Rafiki zangu wengi ni matajiri lakini hawana furaha. Familia zao zina matatizo makubwa lakini familia yetu ina furaha sana! Ninatiwa moyo kuona ndugu wengine katika nchi hii wakitanguliza mambo ya kiroho maishani mwao ijapokuwa ni maskini. Sote tunajionea ukweli wa ahadi ya Yesu.”—Soma Mathayo 6:33.
22 Uwe hodari! Chagua kumtii na kumtegemea Yehova. Acha upendo wako kumwelekea Mungu, mwenzi wako wa ndoa, na watoto wako ukuchochee kutimiza daraka lako la kiroho kuelekea familia yako. Ukifanya hivyo, utajionea wazi kwamba ‘Yehova ni msaidizi wako.’
-