Wafanya Kazi Stadi Wanaotumia Neno la Mungu Sawasawa
1 Wahudumu Wakristo kwa kufaa wanarejezewa kuwa “wafanya kazi pamoja na Mungu.” (1 Kor. 3:9) Wapasa uwe mradi wetu kusitawisha ustadi tukiwa wafanya kazi wanaolitumia “neno la ukweli sawasawa.”—2 Tim. 2:15, NW.
2 Ili kutusaidia tuwe stadi katika huduma ya Kikristo, Sosaiti imetia sehemu kadhaa za kipekee ndani ya New World Translation of the Holy Scriptures. Je! unazoeleana nayo? Je! wewe unatumia sehemu hizo katika huduma ya shambani yako na katika funzo lako la Biblia la kibinafsi?
UANDALIZI WENYE MANUFAA NYINGI
3 Wakati New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilipotolewa mwaka 1950, tulikuta marejezo ya habari hususa mahali pengine, vielezi-chini, nyongeza, na marejezo ya kufululiza kuwa msaada mkubwa katika huduma yetu, katika kutayarisha kwa ajili ya mikutano ya kundi na kwa ujumla katika funzo la kibinafsi. Halafu, mwaka 1984, jinsi tulivyosisimuka kupokea New World Translation Reference Bible! Jinsi huo ulivyo uandalizi murua (bora sana) wa kutusaidia katika jitihada yetu ya kuwa wafanya kazi stadi wanaotumia Neno la Mungu sawasawa! Kupitia utumizi wa bidii wa uandalizi huu wenye manufaa nyingi, sasa tuna vifaa bora zaidi ya wakati mwingineo uliotangulia kujenga sifa za kiroho zilizo madhubuti ndani yetu wenyewe na ndani ya wengine.—Mt. 7:24; 1 Tim. 4:16; Ebr. 5:14.
4 Unaposhiriki katika huduma, huenda ukakuta Mkatoliki mwenye moyo mweupe ambaye anataja Mathayo 16:18 kuwa uthibitisho kwamba Petro ndiye mwamba ambao juu yake Kanisa Katoliki limejengwa. Inapotukia hivyo, unaweza kufungua andiko hilo katika New World Translation yenye marejezo ya habari hususa mahali pengine na kupata maandiko matano yaliyorejezwa juu ya neno “rock-mass” (“tungamo-mwamba”). Maandiko hayo yanaonyesha kwamba Kristo, wala si Petro, ndiye Msingi wa kundi. Kwa kurejezea andiko ilo hilo katika New World Translation Reference Bible, utapata habari za ziada katika kielezi-chini juu ya “rock-mass” (“tungamo-mwamba”), zikieleza juu ya maana yalo katika Kigiriki cha awali.
5 Mkato mwingine unaosema “Vichwa vya Biblia kwa Ajili ya Mazungumzo” ni sehemu nyingine ambayo imethibitika kuwa msaada katika huduma ya shambani. Unapofanya kazi katika eneo linaloenezwa mara nyingi, huenda ukataka kuchagua kichwa tofauti na kile kinachoonyeshwa katika Huduma ya Ufalme Yetu. Chini ya vichwa kama vile “Dunia,” “Ufalme,” na “Siku za Mwisho,” utakuta maandiko ambayo yangeweza kutumiwa katika utoaji wa nyumba kwa nyumba au mazungumzo ya Kimaandiko kwenye ziara ya kurudia.
Visaidia-Kumbukumbu
6 Ikiwa huwezi kukumbuka mahali ambako andiko fulani liko unapokuwa na mazungumzo ya Biblia, unaweza kufungua kwenye “Maneno ya Biblia Yaliyofahirisiwa” upande wa nyuma wa Biblia yako na kupata msaada unaohitajiwa. Je! wewe unatumia sehemu hii yenye manufaa?
7 Kifunguzi kwenye ukurasa 5 kinatoa kithibitisho kinachosadikisha kwamba New World Translation ni kazi iliyofanywa kwa ufundi wa kiusomi. Nyongeza inaandaa ufafanuzi ulio wazi juu ya ni kwa nini matumizi ya jina la kimungu yanafaa. Pia inathibitisha Kimaandiko maana ya “Gehena,” “Hadesi,” “Sheoli,” na “Soul” (“nafsi”). Kuongezea hayo, kwa kurejeza kwenye “Dawati la Vitabu vya Biblia” kwenye kurasa 1546-7, tunaweza kujua ni nani aliyeandika kila kitabu, kiliandikiwa wapi, kiliandikwa lini, na muda uliochukuliwa.
8 Kweli kweli, Yehova ameandaa tunachohitaji ili tuwe na “vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Tim. 3:17, NW) Kwa kutumia New World Translation pamoja na vichapo vya Biblia tutakavyokuwa tukitoa, tunaweza kufanya kwa matokeo mazuri kazi tuliyogawiwa. (Luka 6:47, 48) Tujithibitishapo kuwa wafanya kazi stadi, wanaotumia Neno la Mungu sawasawa, tunaweza kutazamia kwa uhakika Bwana kusema: “Vema”!—Mt. 25:21.