Kuwathamini Mapainia Wetu
1 Wafanyakazi wenzi kwa ajili ya Ufalme wa Mungu huimarishana. (Kol. 4:11) Tunapofikiria kwamba kazi ya msingi ya kundi la Kikristo ni kuhubiri habari njema, kuna sababu zenye kulazimisha kuthamini wafanyakazi wa wakati wote walio miongoni mwetu.—Mk.13:10; Rum. 16:2; Flp. 4:3.
KWA NINI?
2 Katika njia ya moja kwa moja, mapainia hujenga kundi kwa kufanya kazi pamoja na wahubiri wasio na ujuzi mwingi katika zile pande mbalimbali za kazi ya kuhubiri. Hiyo yatia ndani kutoa ushahidi kwa magazeti, kujitayarishia na kufanya ziara za kurudia, na kuanza na kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani kwa mafanikio. Kwa kuongeza, mapainia huweka kielelezo katika kutoa ushahidi wa vivi hivi kijasiri. Tegemezo lao la mipango ya kutoa ushahidi wa kikundi katikati ya juma huwapa fursa ya kusaidia wengine. Uvutano wao chanya shambani waweza kuhisiwa hasa wakati mapainia wanapotegemeza utumishi wa shambani mwishoni mwa juma, wakati ambapo walio wengi wa wahubiri waweza kushiriki.
3 Mapainia husaidia makundi katika kueneza eneo kikamili na mara nyingi. Hilo lawezesha watu kupata kujua vizuri zaidi ujumbe wetu na kuhisi wakistarehe zaidi wakati tunapowazuru kwa sababu wanatujua. Zile saa nyingi ambazo mapainia hutumia katika eneo wakiachia fasihi watu wenye kupendezwa na kusitawisha kupendezwa—kwa kweli, wakipanda na kumwagilia maji mbegu za ukweli—zaweza kuongoza tu kwenye eneo lenye mazao zaidi.—1 Kor. 3:6.
KUNDINI
4 Wengine wametiwa moyo waingie katika utumishi wa wakati wote kwa sababu moyo wao uliguswa na bidii na idili ya mapainia waaminifu. Dada mmoja alikuwa amekuwa akisita-sita juu ya kuwa painia wa kawaida kwa sababu hakukuwa na wowote kundini. Lakini, alipotiwa moyo na mwangalizi wa mzunguko, alisonga mbele akajiandikisha. Upesi wengine wakafuata, na kundi hilo sasa lina hesabu kubwa ya mapainia wenye bidii.
5 Huenda zikawako nyakati ambazo wazee humwomba painia asaidie mhubiri ambaye amekuwa asiye wa kawaida au asiyetenda. Usaidizi huu ungeweza kutia ndani kuongoza funzo la Biblia na mtu huyo. Hivyo imani na bidii ya painia vingeweza kuchangia kuwashwa upya kwa upendo wa mtu huyo kwa ajili ya ukweli na kusaidia kumtendesha tena katika kutimiza wajibu wake mbalimbali wa wakfu wake.—1 The. 5:14.
WATIE MOYO MAPAINIA
6 Mapainia, ingawa wafanya mengi katika kutia wengine moyo, wenyewe huhitaji kutiwa moyo ili waendelee kuonea shangwe utumishi wao. (Rum. 1:12) Je! wewe hunena kwa uchanya juu ya huduma ya painia? Mara ya mwisho ulipompongeza painia kwa sababu ya kazi na roho yake ya kujidhabihu ilikuwa lini? Mapainia huthamini hasa kuwa na mtu wa kufanya kazi naye katika utumishi wa shambani katika zile saa za mchana ambapo ni wahubiri wachache hutoka nje. Je! wewe waweza kuambatana na mapainia na pengine utumie saa ndefu katika kutegemeza kazi ya kuhubiri?
7 Ni jinsi gani nyingine unavyoweza kuwatia moyo mapainia? Licha ya kuwapongeza, waweza kuonyesha uthamini wako kwa wafanyakazi hawa wenye juhudi katika njia dhahiri kwa kushiriki mlo pamoja nao, kwa kujitolea uwasaidie na gharama zao za usafiri, na kwa kuwategemeza kwa njia nyinginezo kwa kadiri uwezayo. Linganisha 1 Wathesalonike 5:12, 13.
8 Wazee na watumishi wa huduma wakiwa wanachukua uongozi kundini, mapainia na wahubiri watatoa utegemezo kamili kwa mipango iliyopangwa vizuri kitengenezo kwa ajili ya utumishi. Sisi sote tutaweza hivyo kutumia vipawa tulivyo navyo katika “kuhudumiana.”—1 Pet. 4:10, 11.