Matangulizi ya Kutumia Katika Huduma ya Shambani
Maelezo: Unapaswa kufikiria kwa uangalifu mambo matatu unapochagua utangulizi wa kutumia ukiwa katika huduma ya shambani: (1) Ujumbe tulioagizwa kuhubiri ni “habari njema ya ufalme.” (Mt. 24:14) Hata wakati hatuuzungumzi moja kwa moja, tunapaswa kukumbuka kuwasaidia watu waone wanauhitaji, au labda kuondoa vitu vinavyowazuia wasiwe na nia ya kuufikiria. (2) Kuhangaikia kikweli hali njema ya watu tunaokuta kutatusaidia, kama Yesu, tuifikie mioyo. (Marko 6:34) Huenda kupendezwa kikweli huko kukaonyeshwa na tabasamu changamfu na urafiki, nia ya kusikiliza wanaposema kisha kubadili maneno yetu yafae hali yao, pia jinsi tunavyotumia maswali yanayowatia moyo kujieleza wenyewe ili tuelewe maoni yao vizuri. Andiko la 1 Wakorintho 9:19-23 linaonyesha kwamba mtume Paulo alibadili mahubiri yake ya habari njema ili yafae hali za watu aliosema nao. (3) Katika sehemu fulani za ulimwengu, wageni wanatazamiwa kufuata desturi fulani kabla ya kusema sababu ya ziara yao. Kwingineko huenda mwenye nyumba akamtazamia mgeni asiyekaribishwa aseme kusudi lake bila kupoteza wakati.—Linganisha na Luka 10:5.
Matangulizi yafuatayo yanaonyesha jinsi Mashahidi fulani wenye uzoefu wanavyoanza mazungumzo. Ikiwa matangulizi unayotumia sasa hayafungui sana njia ya kuwa na mazungumzo, jaribu baadhi ya mapendekezo haya. Unapofanya hivyo, jaribu kutumia maneno yako mwenyewe. Pia, utafaidika kutokana na mapendekezo ya Mashahidi wengine katika kutaniko lako ambao wanafanikiwa kuwafikia watu.
BIBLIA/MUNGU
● ‘Hujambo. Nimekutembelea kifupi tu ili nikueleze ujumbe muhimu. Tafadhali ona Biblia inavyosema. (Soma andiko, kama vile Ufunuo 21:3, 4.) Unaonaje kuhusu mambo hayo? Je, yanakupendeza?’
● ‘Tunaongea na jirani zetu kuhusu mahali pa kupata msaada unaofaa ili kukabiliana na matatizo ya maisha. Zamani, watu walitafuta shauri katika Biblia. Lakini tunaishi wakati ambapo mitazamo inabadilika. Una maoni gani kuhusu jambo hilo? Je, unaamini Biblia ni Neno la Mungu au unaona kwamba hiyo ni kitabu kizuri tu kilichoandikwa na wanadamu? . . . Ikiwa imetoka kwa Mungu, unafikiri mtu anaweza kuhakikishaje jambo hilo?’ (Ona ukurasa wa 32-42, chini ya kichwa “Biblia.”)
● ‘Nimefurahi kukukuta nyumbani. Ninashiriki pamoja na jirani zangu wazo lenye kutia moyo kutoka katika Biblia (au, Maandiko Matakatifu). Je, umewahi kujiuliza: . . . ? (Uliza swali linaloongoza kwenye kichwa cha mazungumzo yako.)’
● ‘Tunawatia watu moyo waisome Biblia yao. Majibu inayotoa kwa maswali muhimu mara nyingi huwashangaza watu. Kwa mfano: . . . (Zab. 104:5; au Dan. 2:44; au andiko lingine).’
● ‘Leo tunawatembelea jirani zetu kifupi tu. Watu fulani tunaosema nao wanamwamini Mungu. Wengine hushindwa kumwamini. Wewe unaonaje? . . . Biblia inatutia moyo tufikirie maana ya ulimwengu wote unaoonekana. (Zab. 19:1) Yule ambaye sheria zake zinaongoza sayari hizo za mbinguni ametupatia pia mwelekezo wenye thamani. (Zab. 19:7-9)’ (Ona pia ukurasa wa 215-221, 390-394, chini ya vichwa “Mungu” na “Uumbaji.”)
FAMILIA/WATOTO
● ‘Tunazungumza na watu wanaotaka kujua jinsi tunavyoweza kukabiliana na matatizo ya maisha ya familia. Sote tunajaribu kufanya yote tuwezayo, lakini kama kuna jambo linaloweza kutusaidia tupate mafanikio zaidi, tutafurahi kulijua, sivyo? . . . (Kol. 3:12, 18-21) Biblia inatupatia tumaini kwamba familia zetu zitafurahia wakati ujao ulio mzuri sana. (Ufu. 21:3, 4)’
● ‘Sote tunataka watoto wetu wawe na maisha yenye furaha. Lakini unafikiri kuna sababu nzuri ya kutazamia kwamba ulimwengu wa leo wenye matatizo utabadilika na kuwa mzuri? . . . Basi, unafikiri watoto wetu watakabili ulimwengu wa aina gani watakapokua? . . . Biblia inaonyesha kwamba Mungu ataifanya dunia hii iwe makao mazuri ajabu. (Zab. 37:10, 11) Lakini ili watoto wetu waishi humo, itategemea sana mambo ambayo sisi hufanya. (Kum. 30:19)’
FUNZO LA BIBLIA NYUMBANI
● ‘Nimekutembelea ili nikuonyeshe jinsi unavyoweza kujifunza Biblia nyumbani bila malipo. Ukipenda, ninaweza kuchukua dakika chache tu nikuonyeshe jinsi watu katika nchi 200 hivi wanavyozungumza Biblia nyumbani wakiwa vikundi vya familia. Tunaweza kutumia kichwa chochote kati ya vichwa hivi kama msingi wa mazungumzo yetu. (Onyesha mambo yaliyomo katika kitabu cha funzo.) Ni kichwa kipi hasa kinachokupendeza?’
● ‘Tunawaonyesha jirani zetu kichapo hiki kinachowasaidia watu kujifunza Biblia. (Onyesha.) Umewahi kukiona? . . . Kama una dakika chache tu, ningependa kukuonyesha jinsi kinavyoweza kutumiwa pamoja na Biblia yako mwenyewe.’
HAR-MAGEDONI
● ‘Watu wengi wanahangaika juu ya Har–Magedoni. Wamesikia viongozi wa ulimwengu wakitumia neno hilo kuhusu vita vikuu vya nyukilia. Kwa maoni yako, Har–Magedoni itamaanisha nini kwa wanadamu? . . . Kwa kweli, jina Har–Magedoni linatoka katika Biblia, nalo linamaanisha jambo tofauti kabisa na lile linaloonyeshwa na matumizi ya ujumla ya neno hilo. (Ufu. 16:14, 16) Biblia inaonyesha pia kwamba kuna mambo ambayo sisi binafsi tunaweza kufanya ili tuje kuokolewa. (Sef. 2:2, 3)’ (Ona pia ukurasa wa 84-88 chini ya kichwa “Har–Magedoni.”)
KAZI/NYUMBA
● ‘Tumekuwa tukizungumza na jirani zako kuhusu jambo linaloweza kufanywa ili kuhakikisha kwamba kila mtu ana kazi na nyumba. Unasadiki kwamba tunaweza kuzitazamia serikali za wanadamu zitimize hilo? . . . Lakini kuna mtu anayejua jinsi ya kutatua matatizo hayo; huyo ni Muumba wa wanadamu. (Isa. 65:21-23)’
● ‘Tunazungumza na jirani zetu wazo fulani kuhusu serikali nzuri. Watu wengi wanatamani kuwa na serikali isiyo na ufisadi, ambayo inampa kila mtu kazi na nyumba nzuri. Unafikiri ni serikali gani inayoweza kufanya yote hayo? . . . (Zab. 97:1, 2; Isa. 65:21-23)’ (Ona pia ukurasa wa 265-269, chini ya kichwa “Serikali.”)
MAISHA/FURAHA
● ‘Tunawatembelea jirani zetu tukitafuta watu wanaotaka sana kujua kusudi la maisha. Watu wengi hupata kiasi fulani cha furaha. Lakini wanakabili matatizo mengi pia. Umri wetu unapozidi kusonga, tunatambua kwamba maisha ni mafupi sana. Je, hivi ndivyo maisha yamekusudiwa yawe? Unaonaje jambo hilo? . . . (Toa maelezo kuhusu kusudi la kwanza la Mungu kama lilivyoonyeshwa katika Edeni; kisha kuhusu Yohana 17:3 na Ufunuo 21:3, 4)’ (Ona pia ukurasa wa 327-332, chini ya kichwa “Uhai.”)
● ‘Leo tunawauliza jirani zetu jambo wanalofikiria wanaposoma katika Biblia zao maneno “uzima wa milele.” Maneno hayo ni ya pekee kwa sababu yanapatikana katika Biblia mara 40 hivi. Uzima huo unaweza kumaanisha nini kwetu? . . . Tunaweza kuupataje? (Yoh. 17:3; Ufu. 21:4)’
● ‘Tunaongea na watu wanaohangaikia kwelikweli ubora wa maisha leo. Wengi wetu tunafurahia kuwa hai, lakini wengi hujiuliza, Je, inawezekana kuwa na maisha yenye furaha ya kweli? Unaonaje hilo? . . . Kwa maoni yako, ni kitu gani kikubwa zaidi kinachowazuia watu wasiwe na furaha leo? . . . (Zab. 1:1, 2; tumia maandiko zaidi yafae jambo linalomhangaisha mwenye nyumba)’
MATUKIO YA SASA
● ‘Habari ya jioni. Jina langu ni ——. Mimi ni jirani yako kutoka (taja jina la barabara au eneo). Je, ulitazama habari za televisheni jana jioni? . . . Habari hizo juu ya (taja jambo la sasa linalowahangaisha watu)—unazionaje habari hizo? . . . Mara nyingi watu huuliza, Ulimwengu huu unaelekea wapi? Sisi Mashahidi wa Yehova tunaamini kwamba tunaishi katika wakati ambao Biblia inauita “siku za mwisho.” Ona maelezo haya marefu katika 2 Timotheo 3:1-5.’ (Ona pia ukurasa wa 284-293.)
● ‘Je, ulisoma jambo hili katika gazeti juma hili? (Onyesha gazeti lililo na habari hizo.) Unaonaje . . . ?’
● ‘Ningependa kukuuliza swali. Kama ungekuwa na uwezo wa kuchagua, ungependa tatizo gani litatuliwe kwanza kati ya matatizo mengi yanayoukabili ulimwengu? (Ukiisha kujua jambo linalomhangaisha zaidi mwenye nyumba, litumie kuwa msingi wa mazungumzo yako.)’
SIKU ZA MWISHO
● ‘Tumekutembelea ili tuzungumzie maana ya mambo tunayoona yakitendeka ulimwenguni leo. Watu wengi hawapendezwi sana na Mungu na viwango vyake vya maisha vilivyoandikwa katika Biblia. Jambo hilo limeathiri sana mtazamo wa watu kuhusu mtu na mwenzake. Tafadhali niruhusu nishiriki pamoja nawe masimulizi haya yaliyoandikwa katika 2 Timotheo 3:1-5 kisha uniambie kama unafikiri yanapatana na hali za ulimwengu wa leo au sivyo. (Soma) . . . Je, kuna sababu nzuri ya kutazamia hali bora wakati ujao? (2 Pet. 3:13)’
● ‘Watu wengi wanaamini kwamba wakati wa ulimwengu huu unakaribia haraka mwisho wake. Wanasema kwamba wakati wetu ni “siku za mwisho.” Lakini unajua kwamba Biblia inatuambia jinsi tunavyoweza kuokoka mwisho wa ulimwengu wa sasa na kuendelea kuishi katika dunia itakayofanywa kuwa paradiso? (Sef. 2:2, 3)’ (Ona pia ukurasa wa 284-293, chini ya kichwa “Siku za Mwisho.”)
Ona pia “Matukio ya Sasa” katika orodha hii ya matangulizi yaliyopendekezwa.
UFALME
● ‘Ninaposema na jirani zangu, nimeona kwamba wengi wanatamani kuishi chini ya serikali inayoweza kweli kutatua matatizo makubwa yanayotukabili leo—uhalifu na gharama kubwa za maisha (au lolote linalowasumbua wengi wakati huu). Hilo lingekuwa jambo zuri, sivyo? . . . Je, kuna serikali kama hiyo leo? . . . Kwa kweli watu wengi wamesali kwa ajili ya serikali inayoweza kufanya mambo hayo. Labda wewe pia umesali kwa ajili yake, lakini watu wengi hawaamini kwamba hiyo ni serikali. (Dan. 2:44; Zab. 67:6, 7; Mik. 4:4)’ (Ona pia ukurasa wa 311-319 na 265-269, chini ya vichwa “Ufalme” na “Serikali.”)
● ‘Tunawauliza jirani zetu swali fulani. Tungependa kusikia maoni yako kuhusu hilo. Yesu alitufundisha tusali Ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yafanywe duniani kama mbinguni. Je, unafikiri sala hiyo itajibiwa ili mapenzi ya Mungu yafanywe kikweli hapa duniani? . . . (Isa. 55:10, 11; Ufu. 21:3-5)’
● ‘Ninazungumza na jirani zangu suala ambalo ni lazima sote tukabili: Je, tunapenda serikali ya Mungu, au tunapendelea zaidi utawala wa wanadamu? Kwa sababu ya hali zilizo ulimwenguni leo, je, unafikiri tunahitaji jambo lingine badala ya lile ambalo wanadamu wamefanya? . . . (Mt. 6:9, 10; Zab. 146:3-5)’
UHALIFU/USALAMA
● ‘Hujambo. Tunazungumza na watu juu ya usalama wao. Kuna uhalifu mwingi katika ujirani wetu, nao unaathiri maisha yetu. Unafikiri kwamba wakati utafika ambapo watu kama mimi na wewe watatembea barabarani usiku bila kuogopa? (Au, unafikiri kwamba kuna mtu yeyote aliye na suluhisho kamili la tatizo hili?) . . . (Met. 15:3; Zab. 37:10, 11)’
● ‘Jina langu ni——. Mimi ni jirani yako. Nilipokuwa nikitembea asubuhi hii, niliona kwamba kila mtu anazungumza juu ya (taja uhalifu fulani uliotukia hivi karibuni katika ujirani au jambo lingine linalowahangaisha watu kwenu). Unaonaje kuhusu jambo hilo? . . . Je, unafikiri kuna lolote linaloweza kufanya maisha yetu yawe salama zaidi? . . . (Met. 1:33; 3:5, 6)’
UKOSEFU WA HAKI/KUTESEKA
● ‘Umewahi kujiuliza: Je, kweli Mungu anahangaishwa na ukosefu wa haki na kuteseka kunakowapata wanadamu? . . . (Mhu. 4:1; Zab. 72:12-14)’ (Ona pia vichwa “Kuteseka” na “Kitia-Moyo.”)
UPENDO/FADHILI
● ‘Tumeona kwamba watu wengi wanahangaikia sana ukosefu wa upendo wa kweli ulimwenguni. Je, wewe pia unaona hivyo? . . . Kwa maoni yako, kwa nini kuna mwelekeo huo? . . . Unajua kwamba Biblia ilitabiri hali hii? (2 Tim. 3:1-4) Inaeleza pia sababu ya kuwapo hali hiyo. (1 Yoh. 4:8)’
● ‘Jina langu ni——. Mimi ni mmoja wa jirani zako. Ninawatembelea jirani zangu kifupi tu ili niongee nao kuhusu jambo linalonihangaisha sana, nami nina hakika wewe pia umeliona. Fadhili hazigharimu sana, lakini zinaonekana kuwa haba sana leo. Je, umewahi kujiuliza kwa nini kuna hali hiyo? . . . (Mt. 24:12; 1 Yoh. 4:8)’
UZEE/KIFO
● ‘Je, umewahi kujiuliza kwa nini tunazeeka na kufa? Kasa wengine wa baharini huishi mamia ya miaka. Miti fulani imeishi maelfu ya miaka. Lakini wanadamu huishi miaka 70 au 80 tu kisha hufa. Umewahi kujiuliza ni kwa nini? . . . (Rom. 5:12) Je, hali hiyo itapata kubadilika? . . . (Ufu. 21:3, 4)’
● ‘Umewahi kujiuliza: Je, kifo ndio mwisho wa mambo yote? Au kuna jambo lingine baada ya kifo? . . . Biblia inajibu swali lolote tunaloweza kuwa nalo juu ya kifo. (Mhu. 9:5, 10) Inaonyesha pia kwamba kuna tumaini la kweli kwa watu walio na imani. (Yoh. 11:25)’ (Ona pia ukurasa wa 100-106 na 107, chini ya vichwa “Kifo” na “Kitia-Moyo.”)
VITA/AMANI
● ‘Karibu kila mtu siku hizi anahangaika kwa sababu ya hatari ya vita vya nyukilia. Unafikiri tutapata kuona amani ya kweli katika dunia hii? . . . (Zab. 46:8, 9: Isa. 9:6, 7)’
● ‘Ninatafuta watu ambao wangependa kuishi katika ulimwengu usio na vita. Katika karne iliyopita peke yake kumekuwako mamia ya vita, kutia ndani vita viwili vya ulimwengu. Sasa tunakabiliwa na hatari ya vita vya nyukilia. Unafikiri ni jambo gani linalohitajiwa ili vita hivyo viepukwe? . . . Ni nani anayeweza kuleta ulimwengu wenye amani? . . . (Mik. 4:2-4)’
● ‘Tunaona kwamba karibu kila mtu anasema anataka amani ya ulimwengu. Viongozi wengi wa ulimwengu husema hivyo pia. Kwa nini, basi, ni shida sana kuipata? . . . (Ufu. 12:7-12)’
WAKATI UJAO
● ‘Habari ya asubuhi. . . . Tunajaribu kushiriki pamoja na jirani zetu maoni yanayofaa kuhusu wakati ujao. Je, hivyo ndivyo unavyoyaona maisha? . . . Je, unaona kwamba hali fulani hufanya jambo hilo liwe gumu? . . . Nimeona kwamba Biblia husaidia sana kuhusu jambo hili. Inasimulia kikweli hali zilizopo leo, lakini inaeleza pia maana ya hali hizo na kutuambia matokeo yake. (Luka 21:10, 11, 31)’
● ‘Hujambo. Jina langu ni ——. Jina lako ni nani? . . . Ninawatia moyo vijana kama wewe waufikirie wakati ujao ulio mzuri ajabu ambao Biblia inatuahidi. (Soma andiko, kama vile Ufunuo 21:3, 4.) Je, jambo hilo linakupendeza?’
WATU WENGI WANAPOSEMA: ‘NINA DINI YANGU MWENYEWE’
● ‘Habari ya asubuhi. Tunatembelea familia zote katika mtaa wenu (au, katika eneo hili), nasi tunaona kwamba wengi wao wana dini yao wenyewe. Bila shaka wewe pia una yako. . . . Lakini, bila kujali dini yetu, sote tunapatwa na matatizo yaleyale—gharama za juu za maisha, uhalifu, magonjwa—sivyo? . . . Je, unafikiri kwamba kuna utatuzi wowote wa kweli kwa mambo hayo? . . . (2 Pet. 3:13; n.k.)’
WATU WENGI WANAPOSEMA ‘NINA SHUGHULI’
● ‘Hujambo. Tunatembelea kila mtu katika mtaa huu tukiwa na ujumbe muhimu. Bila shaka una shughuli nyingi, kwa hiyo nitasema kwa ufupi.’
● ‘Habari. Jina langu ni ——. Kusudi langu la kuja hapa ni kuongea nawe baraka za Ufalme wa Mungu na jinsi tunavyoweza kuzipata. Lakini naona kwamba una shughuli nyingi (au, unataka kuondoka). Je, nikueleze jambo fupi tu?’
KATIKA ENEO LINALOHUBIRIWA MARA NYINGI
● ‘Nimefurahi kukukuta nyumbani. Tunafanya ziara ya kila juma katika mtaa huu, nasi tuna jambo zaidi la kushiriki pamoja nawe kuhusu mambo mazuri ajabu ambayo Ufalme wa Mungu utawafanyia wanadamu.’
● ‘Hujambo. Nimefurahi kukuona tena. . . . Je, kila mtu nyumbani ni mzima? . . . Nimepitia kidogo hapa ili nishiriki pamoja nawe wazo fulani kuhusu . . . ’
● ‘Habari ya asubuhi. . . . Nimekuwa nikitafuta nafasi nyingine ya kuongea na wewe. (Kisha taja jambo hususa unalotaka kuzungumzia.)’