Tumia Wakati wa Desemba kwa Hekima
1 Watoto wanaulizwa mara nyingi wataka kufanya nini wakati wa likizo, na wakati wanaporudi shuleni, huenda wakaulizwa watoe ripoti ya yale waliyofanya. Kweli kweli, sisi sote, wachanga na wazee, twafanya vema kujiuliza: ‘Sisi tumepanga kufanya nini wakati wa Desemba? Utakapokuwa umekwisha, je, sisi tutaweza kutoa ripoti ya mwezi wenye mafaa, wenye mazao?’ Tutafanya hivyo tukitii ule ushauri wa ‘kukomboa wakati wenye fursa kwa ajili yetu wenyewe.’—Efe. 5:15, 16, NW.
NUFAISHWA NA MIKUSANYIKO
2 Jambo moja ambalo sisi sote twapaswa kuwa tulitia ndani ya mambo tuliyopangia ni kuhudhuria “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya. Baadaye, twafanya vema kupitia mambo tuliyoandika tuone ni mambo gani tulijifunza na tunayoweza kutumia maishani mwetu tukiwa wasifaji wa Yehova. Kwenye Waefeso 4:25 tunatiwa moyo ‘tuseme kweli kila mmoja na jirani yake.’ Majirani wetu walio karibu zaidi ni washiriki wa familia zetu wenyewe. Twaweza kuzungumza nao au na washiriki wa familia yetu ya kiroho baadhi ya chakula cha kiroho kizuri ajabu tulichoandaliwa wakati wa programu ya mkusanyiko. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tukisaidiana mmoja na mwenzake ‘kuliitia jina la Yehova, ili tumtumikie bega kwa bega.’—Sef. 3:9.
SHIRIKI HUDUMA YA SHAMBANI
3 Wakati wa Desemba, toleo lililodokezwa ni Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia au Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Je, wewe umepanga kushiriki kwa kadiri kubwa iwezekanavyo katika huduma wakati wa mwezi huo, ukitoa fasihi katika kila fursa? Ikiwa tutakuwa katika kundi letu wenyewe, tutataka kuunga mkono mipango ya kawaida ya utumishi wa shambani. Huenda hata tukaweza kushiriki katika kutoa ushahidi jioni. Watu wengi wamo nyumbani jioni na wanaelekea kuwa katika hali ya starehe zaidi, hivyo kuifanya iwe rahisi zaidi kwetu kuongea nao juu ya habari njema za Ufalme ambazo tumefundishwa.—Isa. 50:4.
4 Tufanyapo mipango ya kusafiri, ama kwenda kwenye mkusanyiko au kwa ajili ya likizo, twapaswa kupanga kuchukua fasihi. Fursa za kutoa ushahidi vivi hivi zijitokezapo, twaweza kuelekeza fikira kwa mojapo vichapo. Tuwapo mbali na nyumbani, huenda tukaweza kupata Jumba la Ufalme, kuhudhuria mikutano, na kushiriki utumishi wa shambani pamoja na ndugu na dada wenyeji. Hicho chapaswa kuwa chanzo chema cha kitia-moyo kwa ajili ya wote sisi na hao ndugu tunaoshirikiana nao.—Rum. 1:12.
5 Ikiwa tutakuwa mbali na kundi letu mwishoni mwa mwezi, twapaswa kupelekea mwandishi ripoti yetu ya utumishi wa shambani kwa posta mapema vya kutosha ili itiwe pamoja na ripoti ambayo huipeleka tarehe sita ya mwezi unaofuata.
JITAHIDI KUONGOZA MAFUNZO
6 Kwa kawaida mafunzo machache kidogo huongozwa wakati wa Desemba kwa sababu baadhi ya wanafunzi wa Biblia huenda likizoni. Yule aongozaye huenda pia akaenda lakini wakati tofauti. Badala ya kuacha funzo bila kuongozwa kwa majuma kadhaa, je, hatuwezi kupanga mtu mwingine kundini aongoze funzo hilo wakati hatupo? Ni vizuri funzo liongozwe kwa ukawaida kadiri iwezekanavyo ili kukazia akilini ya mwanafunzi uhitaji wa kulishwa kiroho kwa ukawaida.
7 Tupatapo kupendezwa katika eneo, twapaswa kufuatia kupendezwa huko upesi iwezekanavyo. Mwenye nyumba akichukua baadhi ya fasihi, twaweza kujitolea kumwonyesha jinsi ya kuitumia kwa kuzungumza pamoja naye mafungu machache. Kisha twapaswa kujaribu kupatana na mwenye nyumba juu ya tarehe na wakati dhahiri wa kurudi twendeleze funzo.
8 Sisi sote na tuweze kutazama nyuma kwenye wakati wa Desemba na kuhisi kwamba, tukiwa watumishi walio wakfu wa Yehova, kweli kweli sisi tulitumia wakati wetu kwa hekima katika ‘kushika kielelezo cha maneno yenye uzima’ na katika kusaidia wengine wajifunze maneno hayo yenye uzima ya kweli kutoka kwa Neno la Yehova.—2 Tim. 1:13.