Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • fl sura 11 kur. 146-160
  • Kuendelea Kupashana Habari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuendelea Kupashana Habari
  • Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUWA NA MAONI YA MBELE
  • KUMTIA MOYO MTOTO WAKO AWE AKISEMA
  • MIAKA YENYE MAGEUZO
  • KUFAHAMU MAHITAJI YA WATOTO WENYE UMRI WA KATI YA MIAKA 13 NA 19
  • KUTOA SHAURI NA KARIPIO
  • HALI YA KUONA MTU MMOJA MMOJA KUWA ANAFAA
  • KULINDWA KWA ADILI ZA BIBLIA
  • Wazazi Na Watoto—wasilianeni Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kupata Furaha Katika Kulea Watoto
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kuzuia Mtengano Kati Yako na Watoto Nyumbani Mwako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
fl sura 11 kur. 146-160

Sura ya 11

Kuendelea Kupashana Habari

1, 2. Kupashana habari ni nini, na kwa nini ni kwa maana?

KUPASHANA HABARI si kuzungumza tu. Kama mtume Paulo alivyosema: Msikiaji asipoyafahamu maneno yako, ‘utakuwa ukinena hewani tu.’ (1 Wakorintho 14:9) Je! watoto wako wanafahamu unayosema, nawe unafahamu wanayojaribu kukuambia?

2 Ili kuweko kupashana habari kweli kweli, ni lazima kuweko kupeana mawazo, fikira na maoni. Ikiwa upendo unaweza kuitwa kiini cha maisha ya furaha ya jamaa, basi kupashana habari kungeweza kuitwa nguvu zake. Kukosa kupashana habari kati ya wenzi wa ndoa kunaleta matata; hali hiyo ni nzito vilevile au hata inazidi hiyo, inapotokea kati ya wazazi na watoto.

KUWA NA MAONI YA MBELE

3. Ni wakati wa kipindi gani cha maisha ya mtoto ambacho wazazi wamepaswa kutazamia magumu ya kupashana habari?

3 Ukosefu mkubwa wa kupashana habari kati ya wazazi na watoto wao unatokea wakati wa muda ulio kati ya utoto na kukomaa, yaani, miaka ya kuanzia kumi na mitatu kufika kumi na tisa. Imewapasa wazazi wafahamu kwamba hivyo ndivyo itakavyokuwa. Si jambo la busara kwao kutazamia kwamba, kwa sababu miaka ya kwanza ya maisha ya watoto wao haina matata sana, vilevile miaka hiyo itakayofuata itakuwa bila matata. Magumu yatakuja bila shaka, na kupashana habari waziwazi na kwa kufaa kunaweza kuwa njia kuu ya kuyamaliza au kuyapunguza. Wakifahamu hayo, wazazi wanahitaji watazamie mambo ya mbele, wafikirie mambo ya mbele, kwa maana “heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake.”—Mhubiri 7: 8.

4. Je! ni lazima kupashana habari na jamaa kuwe kwa naznna ya mazungumzo? Eleza.

4 Mambo yanayotakiwa ili kuimarisha, kujenga na kuendelea kupashana habari kama jamaa ni mengi. Kwa miaka mingi, mwanamume na mwanamke wanaweza kusitawisha hali ya kutumainiana na kufahamiana sana, hali inayowezesha kupashana habari kuweko hata bila kusema. Kutazama, kutabasamu (kuchekelea) au kugusa peke yake kunaweza kuwasemea mambo mengi. Imewapasa wawe na lengo la kuimarisha msingi uo huo wenye nguvu wa kupashana habari na watoto wao. Kabla mtoto mchanga hajafahamu usemi, ninyi wazazi mwonyesheni hali ya kujisikia salama na ya kupendwa. Wakati watoto wangali wakikua, ikiwa jamaa inafanya kazi pamoja, kucheza pamoja, na zaidi ya hayo, kuabudu pamoja, hapo ndipo njia zenye nguvu za kupashana habari zinapoimarishwa. Lakini kunatakiwa kujitahidi sana lii waendelee kupashana habari hivyo.

KUMTIA MOYO MTOTO WAKO AWE AKISEMA

5-7. (a) Kwa nini Inawafaa wazazi waangalie wasije wakamzuia mtoto kusema? (b) Wazazi wangeweza kufundishaje watoto heshima na adabu?

5 Kuna usemi wa kwamba “watoto wanapaswa kuonwa si kusikiwa.” Ndivyo ilivyo nyakati nyingine. Kama Neno la Mungu linavyosema, inawapasa watoto wajue kwamba kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.” (Mhubiri 3:7) Lakini watoto wanatamani kusikilizwa, na inawapasa wazazi waangalie wasije wakawazuia bure kusema kwa uhuru. Usitazamie kwamba mtoto mdogo ataitikia mambo anayoona kama mtu mzima. Mtu mzima anaona tukio moja kuwa sehemu ya tamasha kubwa inayofuatana na mambo mengi ya maisha. Huenda mtoto akafurahia sana na kuvutwa sana na jambo fulani linalompendeza wakati huo hata asahau karibu mambo mengine yote. Huenda mtoto mdogo akaingia chumbani haraka na kuanza kumsimulia baba au mama yake tukio fulani kwa shauku sana. Mzazi akimzuia mtoto huyo kwa kumwambia kwa ukali “Nyamaza!” au akisema neno jingine la ukali, huenda shauku ya mtoto ikapoa. Huenda mazungumzo ya kitoto yasiwe na maana sana. Lakini, kwa kuwatia moyo watoto wako kusema kiasili, wanaweza kukuambia mambo unayotaka na unayohitaji kujua baadaye maishani.

6 Heshima na adabu zinaleta hali nzuri ya kupashana habari. Imewapasa watoto wajifunze kuwa na heshima, nao wazazi wamepaswa wawawekee watoto mfano wanapozungumza nao, na vilevile katika njia nyingine. Itakuwa lazima kukaripia watoto, nako kumepaswa kutolewe kunapokuwa na uhitaji, hata kwa ukali. (Mithali 3:11, 12; 15:31, 32; Tito 1:13) Walakini, mzazi akizoea kuwakatiza watoto akiwakaripia kila wakati, au zaidi, akiwadharau hata kuwadhihaki wanaposema, inaelekea kwamba watakuwa na mawazo yao wenyewe hata wasiitikie, au watamwendea mtu mwingine wanapotaka kusema neno fulani. Kadiri mtoto wa kiume au wa kike anavyoendelea kuwa mkubwa, ndivyo hali hiyo inavyozidi kuwa kubwa. Kwa nini usifanye hivi, wakati siku hii inapomalizika, fikiri na kuchunguza ulivyozungumza na mtoto wako wa kiume au wa kike, kisha ujiulize hivi: Ni mara ngapi niliposema mambo yaliyoonyesha kuthamini (kushukuru), kutia moyo, kusifu? Kwa upande mwingine, ni mara ngapi niliposema mambo yaliyokuwa tofauti na hayo, yaliyoelekea kumdharau, yaliyoonyesha kutoridhika, uchungu au kuona hasira? Labda utashangazwa na mambo ambayo uchunguzi wako utafunua.—Mithali 12:18.

7 Wazazi wanahitajiwa mara nyingi wawe wavumilivu na wenye kujiweza. Vijana wana maelekeo ya kufanya bila kufikiri. Huenda wakafunua mambo yaliyo katika akili zao bila kufikiri, labda hata kumkata kauli mtu mzima anapozungumza. Mzazi angeweza kumkemea mtoto bila heshima. Lakini labda nyakati nyingine litakuwa jambo la hekima zaidi kusikiliza kwa heshima, ili kwa njia hiyo aweke mfano wa kujiweza, ndipo akiisha kujibu kifupi, amkumbushe mtoto kwa wema juu ya uhitaji wa kuwa na heshima na kufikiria wengine. Hivyo, tena hapa, huenda shauri hili likatumika, kuwa “mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema; wala kukasirika.”—Yakobo 1:19.

8. Wazazi wanawezaje kutia moyo watoto wao wawafikie wakitaka uongozi?

8 Unataka watoto wako wajione huru kutafuta uongozi wako wanapokuwa na magumu. Unaweza kuwatia moyo wafanye hivyo kwa kuonyesha kwamba wewe vilevile unatafuta uongozi katika maisha na unaye mtu wa kumwendea kwa unyenyekevu. Katika kueleza namna anavyopashana habari vizuri na watoto wake wakati wangali wadogo, baba mmoja alisema hivi:

“Mimi ninasali pamoja na watoto wangu karibu kila siku wakati wa kulala. Kwa kawaida wanakuwa kitandani mwao, nami hupiga magoti kando yake na kuwashika mikononi mwangu. Mara nyingi nikitoa sala, nao wanatoa sala yao baadaye. Ni kawaida yao kunibusu na kusema, ‘Baba, nakupenda,’ kisha wanafunua jambo fulani walilo nalo moyoni mwao. Wanapostarehe katika kitanda chao na kuona usalama wa kukumbatiwa na baba yao, wanaweza kueleza tatizo fulani walilo nalo ambalo wanataka kusaidiwa, au labda ni kusema neno tu ili kuonyesha upendo.”

Wakati wa chakula na pindi nyingine, sala zao zinaweza kusaidia sana kusitawisha uhusiano mzuri na watoto wako, ikiwa hazitolewi kwa sababu ni desturi tu kusali—bali zina maana, zinatolewa kutokana na moyo na kuonyesha uhusiano wa kipekee na wa kweli pamoja na Muumba wako wa mbinguni na Baba yako.—1 Yohana 3:21; 4:17, 18.

MIAKA YENYE MAGEUZO

9. Tunaweza kusema nini juu ya magumu na mahitaji ya watoto wanaokomaa, yanapolinganishwa na yale ya watoto wachanga?

9 Muda wa kutoka utoto kuwa mtu aliyekomaa ni wakati wa mageuzo, wakati ambapo mwanao au binti yako hawi mtoto tena, lakini bado kuwa mtu mzima. Miili ya vijana wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa inageuka, na mageuzo hayo yanapasa (yanahusu) maono ya moyoni. Magumu na mahitaji ya vijana wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa ni tofauti na magumu yanayotokea wakati wa kipindi kinachotangulia miaka hiyo. Basi ni lazima wazazi wageuze njia ya kuondolea magumu hayo na njia ya kutimizia mahitaji hayo. Kwa maana njia iliyomfaa mtoto mwenye umri uliotangulia ule wa kuanzia miaka kumi na mitatu kufika kumi na tisa, haitamfaa nyakati zote yule anayetoka utoto kuwa mtu aliyekomaa. Kuna uhitaji wa kutolewa zaidi kwa sababu, na huo unataka kupashana habari nyakati nyingi zaidi, si nyakati chache.

10. (a) Kwa nini maelezo mafupi na mepesi juu ya ngono hayatoshi kwa watoto wanaokomaa? (b) Wazazi wanawezaje kuanza mazungumzo ya ngono pamoja na watoto wao?

10 Kwa mfano, yale maelezo mafupi na mepesi uliyompa mtoto mdogo juu ya ngono, hayatafaa mahitaji ya watoto wanaofikia hali ya kukomaa. Wanaona nyege, lakini haya inawazuia mara nyingi wasimkaribie baba wala mama yao wakiwa na maulizo juu ya hayo. Inawapasa wazazi ndio waanze, na hivyo haitakuwa vyepesi isipokuwa wameimarisha na kuendeleza njia nzuri za kupashana habari, sana sana kwa kuwa wenzi wachangamfu wa watoto wao, katika kufanya kazi na katika kucheza. Mwanzo wa mvulana kutokwa shahawa au msichana kutokwa damu ya mwezi hautaudhi sana ikiwa wamekwisha kutangulia kuelezwa. (Mambo ya Walawi 15:16, 17; 18:19) Labda wakati baba anapotembea na mtoto wake wa kiume, anaweza kuanzisha mazungumzo juu ya kupiga punyeto, akitaja kwamba vijana wengi wa kiume wanasumbuliwa na jambo hilo, kisha aulize hivi, ‘Wewe unafanyaje na jambo hilo?’ au ‘Umeona jambo hilo linakusumbua?’ Hata mazungumzo ya jamaa yanaweza kuwa juu ya magumu yanayokamatana na hayo yanayotokea wakati wa muda wa kutoka utoto kuwa mtu aliyekomaa. Baba na mama, wote wawili, wanaweza kusaidia kwa kutoa shauri lao katika njia ya starehe, lakini ya waziwazi.

KUFAHAMU MAHITAJI YA WATOTO WENYE UMRI WA KATI YA MIAKA 13 NA 19

11. Watoto wanaokomaa ni tofauti na watu wazima katika njia gani?

11 “Kwa mapato yako yote jipatie ufahamu.” (Mithali 4:7) Ninyi wazazi, iweni wenye hekima katika njia za watoto; onyesheni busara juu ya maoni yao. Msisahau namna kuwa mtoto kulivyokuwa na maana kwenu. Kumbukeni, vilevile kwamba, ijapokuwa ye yote ambaye ni mtu mzima sasa alikuwa mtoto wakati mmoja, naye anajua ilikuwa na maana gani kuwa mtoto, hakuna mtoto ambaye amepata kuona mambo ambayo mtu mzima ameona. Mtoto anayekomaa hataki kutendewa tena kama mtoto mdogo, lakini yeye si mtu mzima naye hajawa bado na mapendezi kama yale ya watu wazima. Yeye angali ana uhuru mwingi, naye anahitaji wakati ili autumie.

12. Watoto wenye umri wa kati ya miaka, kumi na mitatu na kumi na tisa wanataka wazazi wao wawatendeeje?

12 Kuna mambo fulani ambayo vijana wanataka sana kutoka kwa wazazi wao katika umri huu wa maisha. Wanataka kufahamika; kuliko wakati wo wote, wanataka watendewe kama watu mmoja mmoja; wanataka maongozi na usimamizi unaopatana na unaofikiria hali yao ya kufikia kuwa mtu mzima; wanataka sana sana wajione kuwa wanahitajiwa na kuthaminiwa.

13. Huenda watoto wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa wakavionaje vizuizi wanavyowekewa na wazazi wao, na kwa sababu gani?

13 Wazazi wasishangae kwa sababu upinzani fulani juu ya vizuizi unaanza kutokea muda huo wa kukomaa. Hiyo ni kwa sababu kijana anaanza kuelekea hali ya kujitegemea mwishowe na tamaa ya kawaida ya kuwa na uhuru mkubwa zaidi wa kutembea na kuchagua. Vitoto vichanga vinavyotaka msaada vinahitaji kutunzwa na wazazi nyakati zote, na watoto ambao ni wakubwa kidogo wanahitaji kulindwa kwa uangalifu vilevile. Lakini wanapokuwa watu wakubwa mambo ya kufanya yanapanuka, navyo vifungo (uhusiano) vya kuwa pamoja na wale wasio ndani ya mpango wa jamaa vinaongezeka na kuwa vyenye nguvu. Kutafuta-tafuta hali ya kujitegemea kunaweza kumfanya mtoto wa kiume au mtoto wa kike kuwa mgumu kidogo kuongozwa. Wazazi hawawezi kuacha mamlaka yao idharauliwe au ipingwe kwa faida ya watoto wao wenyewe. Lakini wanaweza kuzuia hali hiyo kwa hekima na kuendelea kupashana habari na watoto wao, wakikumbuka kinacholeta mwenendo huo unaoelekea kusumbua.

14. Wazazi wanaweza kutimizaje vya kufaa tamaa ya mtoto ya kutaka uhuru mkubwa zaidi?

14 Wazazi wanapaswa kufanya nini ikiwa mtoto wao wa kiume au mtoto wa kike anataka sana kujitegemea zaidi? Nia hiyo inafanana na kunyumbuka kwa uzi wa chuma, ulioshindiliwa na kushikwa mkononi. Ukiachwa kwa ghafula, unaruka bila kuzuiwa na kuingia upande usiokusudiwa mwanzoni. Ukiushika mkononi muda mrefu, utajichosha mwenyewe nao utakosa nguvu. Lakini ukiuachilia polepole katika njia iliyoongozwa, utasimama mahali pake panapofaa.

15. Ni nini kinachoonyesha kwamba ukuzi wa Yesu mpaka kuwa mtu mzima ulisimamiwa na wazazi wake?

15 Tunaona mfano wa ukuzi huo unaoongozwa kuelekea hali ya kujitegemea katika habari ya Yesu alipokuwa kivulana mdogo. Kwa habari ya kipindi chake, kabla hajawa na umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa, habari ya historia katika Luka 2: 40 inasema kwamba “yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake.” Wazazi wake bila shaka walitimiza daraka kubwa katika ukuzi wake, kwa maana, ijapokuwa alikuwa mkamilifu, hekima yake haingejileta yenyewe. Walimpa kwa kawaida hali ya kiroho iliyosaidia malezi yake, kama vile habari inavyoendelea kusimulia. Katika umri wa miaka 12, wakati jamaa hiyo ilipokuwa Yerusalemu ikihudhuria Sikukuu ya Kupitwa, Yesu alikwenda hekaluni akaanza kuzungumza pamoja na waalimu wa dini huko. Kwa wazi wazazi wake walimpa mtoto wao wa kiume mwenye umri wa miaka 12 kadiri hiyo ya uhuru wa kutembea. Waliondoka Yerusalemu pasipo kujua kwamba alikuwa amebaki, labda wakidhani kwamba alikuwa pamoja na rafiki zake wengine au watu wa ukoo wake waliokuwa wakirudi. Baada ya siku tatu walimkuta hekaluni, si akijaribu kufundisha wazee wake, bali “akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” Mama yake alieleza namna walivyokuwa wamehangaika sana, naye Yesu bila dharau, alijibu kwamba alidhani wangejua bila shaka mahali pa kumtafuta wakati wangekuwa tayari kuondoka. Ijapokuwa alitumia uhuru kidogo wa kutembea, habari inasema kwamba tokea hapo “alikuwa akiwatii,” akifuata maongozi na vizuizi vyao alipoingia kipindi chake cha miaka kumi na mitatu mpaka kumi na tisa, naye “akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.”—Luka 2:41-52.

16. Wazazi wanaposumbuliwa na mtoto anayekomaa, imewapasa wakumbuke nini?

16 Vilevile, wazazi wamepaswa wawaruhusu watoto wao wa kiume au wa kike wenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa kadiri ndogo ya kujitegemea, wakiiongeza polepole wakati wanapokaribia hali ya kuwa mtu mzima, na kuwaruhusu wazidi kujifanyia maamuzi yao wenyewe chini ya uongozi na usimamizi wa wazazi wao. Magumu yanapotokea, kufahamu sababu zake kutasaidia wazazi waepuke kufanya mambo madogo yawe makubwa. Mara nyingi mtoto wa miaka ya kati ya kumi na mitatu na kumi na tisa hawaasi wazazi wake kwa makusudi, bali anajaribu kuimarisha kadiri fulani ya kujitegemea asijue namna ya kufanya. Hivyo, huenda wazazi wakafanya makosa, labda hata kufanya makosa madogo yawe makubwa. Ikiwa jambo hilo si zito sana, liachilie. Lakini linapokuwa zito, uwe imara. ‘Usichuje mbu’ wala ‘kumeza ngamia.’—Mathayo 23:24.

17. Imewapasa wazazi wafikirie mambo gani wanapowekea watoto wao wanaokomaa. vizuizi?

17 Kwa kuonyesha usawa mzuri katika vizuizi wanavyowawekea, wazazi wanaweza kusaidia ili uhusiano wao mzuri uendelee pamoja na watoto wao wa kiume na wa kike wanaokomaa. Kumbuka kwamba ijapokuwa “hekima itokayo juu, kwanza ni safi,” vilevile ni “tayari kusikiliza maneno ya watu” na “imejaa rehema,” “haina unafiki.” (Yakobo 3:17) Kuna mambo fulani ambayo Biblia inaonyesha kuwa yasiyokubalika kabisa, kutia na wivi, uasherati, kuabudu sanamu na makosa mazito kama hayo. (1 Wakorintho 6:9, 10) Kwa habari ya mambo mengine. kufaa au ubaya waweza kutegemea kadiri ambayo jambo fulani limefanywa. Chakula ni kizuri, lakini tukila kupita kadiri tunakuwa walafi. Ndivyo ilivyo na namna fulani za tafrija, kama kucheza dansi, kucheza michezo mingine, kufanya karamu za vyakula, au matendo yanayofanana na hayo. Mara nyingi haitegemei jambo linalofanywa, bali namna linavyofanywa na ushirika ambao katika huo linafanywa. Hivyo, kama vile tusingelaumu kula tunapomaanisha ulafi, wazazi hawangetaka kulaumu utendaji wote wa watoto ikiwa kusudi la kweli ni kulaumu hali ya kupita kiasi au kadiri ambayo wengine wanafanya utendaji huo, au kwa kadiri ambayo ingeweza kuruhusu hali fulani zisizofaa zitokee.—Linganisha Wakolosai 2:23.

18. Wazazi wanawezaje kuwaonya watoto wao juu ya watu ambao wanataka kushirikiana nao?

18 Vijana wote wanaona uhitaji wa kuwa na rafiki. Labda wachache wanaweza kuonwa kuwa “bora,” lakini, je! watoto wako mwenyewe hawana makosa fulani? Labda utataka uwazuie wasishirikiane na vijana wengine kwa sababu unaona kwamba hawawezi kuwa rafiki wazuri. (Mithali 13:20; 2 Wathesalonike 3:13, 14; 2 Timotheo 2:20, 21) Kwa habari ya wengine, labda unaona mambo fulani unayopenda na mengine usiyopenda. Badala ya kumzuia mtu kabisa kwa sababu ya kasoro fulani, labda utataka uthamini sifa fulani njema za rafiki za watoto wako, ukiwatajia hizo lakini ukiwaambia uhitaji wa kuepuka mambo fulani yasiyofaa, ukimtia moyo mwanao au binti yako ajionyeshe kuwa nguvu ya kutetea mema katika mambo hayo, kwa faida inayoendelea ya rafiki yake.

19. Kupatana na kanuni iliyoandikwa katika Luka 12:48, watoto wanaweza kusaidiwaje wawa na maoni yanayofaa juu ya uhuru?

19 Njia moja ya kusaidia mwanao au binti yako anayekomaa asitawishe maoni yanayofaa juu ya uhuru alioongezewa, ni kumsaidia ajue kwamba uhuru mkubwa zaidi unaleta daraka kubwa zaidi. “Aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi.” (Luka 12:48) Kadiri watoto wanavyojionyesha kwamba wanaweza kutimiza madaraka zaidi, ndivyo wazazi wanavyoweza kuwaongezea madaraka zaidi—Wagalatia 5:13; 1 Petro 2:16.

KUTOA SHAURI NA KARIPIO

20. Zaidi ya kuwa, na uwezo au mamlaka juu ya watoto, ni nini kinachohitajiwa ili kuzuia kuharibika kwa kupashana habari?

20 Mtu akikushauri lakini hafahamu hali yako, unaona kwamba shauri lake halifai kitu. Ikiwa ana uwezo wa kukulazimisha ufuate matakwa yake, labda utachukia hilo na kuona kama anakuonea. Imewapasa wazazi wakumbuke kwamba “moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa.” (Mithali 15:14; 24:5) Labda una uwezo juu ya watoto wako, lakini, uwezo huo ukitiwa nguvu kwa maarifa na ufahamu, utapata matokeo zaidi katika kupashana habari nao. Kushindwa kuonyesha ufahamu wakati wa kukaripia watoto kunaweza kuleta hali ya mtengano na kuharibika kwa kupashana habari.

21. Wazazi wanapaswa kuwatendeaje watoto wanaoingia katika makosa mazito?

21 Utafanya nini ikiwa mtoto wako anaingia katika taabu, ikiwa anafanya kosa zito au anafanya kosa fulani litakalokushtua? Haikupasi hata kidogo kuachilia makosa. (Isaya 5:20; Malaki 2:17) Lakini ujue kwamba sasa mwanao au binti yako anahitaji msaada wa ufahamu na uongozi wa akili kuliko nyakati zote. Kama Yehova Mungu, labda unaweza kusema, ‘Njoo ili tuyanyoshe mambo; hali hii ni nzito sana, lakini si ngumu sana kutengenezwa.’ (Isaya 1:18, NW) Kuhamaki au kutoa maneno makali ya kulaumu kunaweza kuzuia kupashana habari. Watoto wengi ambao wamefanya makosa wamesema hivi: ‘Singeweza kuwaambia wazazi wangu jambo fulani, maana wangenikasirikia sana.’ Waefeso 4:26 linasema: “Ukikasirika, usiache hasira ikuongoze katika dhambi.” (New English Bible) Zuia hasira yako wakati unaposikiliza anavyosema mwanao au binti yako. Hapo ndipo kusikiliza kwako bila kupendelea kutakapolifanya karipio unalotoa likubalike kwa vyepesi zaidi.

22. Kwa nini haiwapasi wazazi waonyeshe hata kidogo kwamba wamewatupa watoto wao?

22 Labda hue si tukio moja tu, bali ni kipindi chenye matata, ni hali ya kuendelea kuonyesha tabia fulani isiyofaa. Ijapokuwa ni lazima kutia adabu, inawapasa wazazi waepuke kuonyesha kwa maneno wala kwa hali yao kwamba wamemtupa mtoto. Uvumilivu wake utakuwa kipimo cha wengi wa upendo wako. (1 Wakorintho 13:4) Usishinde ubaya kwa ubaya, bali uushinde kwa wema. (Warumi 12:21) Mtoto anaumizwa vibaya ikiwa anaaibishwa mbele ya wengine kwa maneno ya kusema kwamba yeye ni “mvivu,” “mkorofi,” “kinyangarika tu (hafai kitu),” au “yeye ni bure tu.” Upendo hauachi kutumaini. (1 Wakorintho 13:7) Huenda mtoto akaharibika sana kadiri ya kuwa mbaya na kuondoka nyumbani. Ijapokuwa hawakubali hali hiyo, wazazi wanaweza kufanya iwezekane kwake arudi. Namna gani? Kwa kuonyesha kwamba hawamkatai yeye, bali wanakataa mwendo wake. Wanaweza kuendelea kumwonyesha kwamba wanaamini kwamba ana sifa njema ndani yake na kutumaini kwamba hizo zitaleta matokeo mema. Ikiwa hivyo, ataweza kurudi nyumbani kama mwana mpotevu anayesimuliwa katika mfano wa Yesu, akiwa na matumaini ya kwamba kurudi kwake akiwa ametubu kutakubaliwa kwa furaha na shangwe.—Luka 15:11-32.

HALI YA KUONA MTU MMOJA MMOJA KUWA ANAFAA

23. Kwa nini ni jambo la maana kwa watoto wanaokomaa kujiona kwamba ni washiriki bora wa jamaa?

23 Viumbe vyote vya kibinadamu vinataka kukubaliwa na kupokewa, kujiona wako upande fulani. Bila shaka, ili kupokewa na kukubaliwa, mtu hawezi kuwa mwenye kujitegemea mno. Inampasa awe na mwenendo unaokubaliwa na kikundi anachoshirikiana nacho. Vijana wakiwa katika umri wao wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa wanaona uhitaji huo wa kuwa sehemu ya jamaa. Wafanye wajione kwamba ni washiriki bora wa mpango wa jamaa, waisaidie iwe na hali njema, hata waruhusiwe kushiriki mipango na maamuzi fulani ya jamaa.

24. Imewapasa wazazi waepuke kufanya nini ili mtoto mmoja asimwonee wivu mtoto mwenzake?

24 “Tusiwe na tabia ya kujifikiria wenyewe,” asema mtume, “tukiamsha kushindana sisi kwa sisi tukioneana wivu.” (Wagalatia 5:26, NW) Sifa inayotoka kwa mzazi wakati mwana au binti anapofanya vema, itasaidia kuzuia roho hiyo isitokee; lakini kumlinganisha mtoto isivyofaa na mtu mwingine anayeonwa mara nyingi kuwa bora, kutatokeza wivu na chuki. Mtume alisema kwamba imempasa kila mtu “achunguze ili aone kazi yake mwenyewe ilivyo, na hapo ndipo yeye peke yake atakapokuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe, wala si kwa kulinganishwa na mtu mwingine.” (Wagalatia 6:4, NW) Kijana anataka kukubaliwa kama alivyo na kwa lile analoweza kufanya, akipendwa na wazazi wake kwa sababu ya mambo hayo.

25. Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wan wasitawishe hali ya kujiona wanafaa?

25 Wazazi wanaweza kusaidia mwana au binti yao asitawishe hali ya kujiona kuwa anafaa kwa kumzoeza akubali madaraka ya maisha katika mambo yote. Wamekuwa wakilea watoto wao tangu uchanga, katika unyofu, ukweli na katika kutendea wengine vya kufaa; wanaendelea na msingi huo wa kwanza kwa kuonyesha namna sifa hizo zinavyotumika katika jamii ya kibinadamu. Hayo ni pamoja na kuonyesha namna ya kukubali daraka la kazi na kuonekana kuwa mtu wa kutegemeka kuifanya. Katika ‘kuzidi kwake kuendelea katika hekima’ kama kijana mwenye umri wa kati ya miaka kumi na mitatu na kumi na tisa, bila shaka Yesu alijifunza kazi ya uchumi kwa kufanya kazi pamoja na Yusufu, baba yake mlezi, kwa maana hata alipofikia umri wa miaka 30 na kuanza kazi yake kuu ya kuutangaza Ufalme, watu walimtaja kama “seremala.” (Marko 6:3) Wakati wa kipindi cha kuanzia miaka kumi na mitatu kufika kumi na tisa, imewapasa sana sana wavulana wajifunze kufanya kazi na kumfurahisha mkubwa wa kazi au mnunuzi (mtu anayetumikiwa kwa kawaida), hata ijapokuwa kazi hiyo ni ya vivi hivi tu kama vile kutumwa na mkubwa wa kazi. Wanaweza kuonyeshwa kwamba kwa kuwa wenye bidii, na kuwa wafanya kazi waaminifu na wenye kutegemeka, wanajipatia hali ya kujiheshimu na ya kuheshimiwa na kuthaminiwa na wengine. Si kwamba kwa kufanya hivyo wanawaletea sita wazazi wao na jamaa yao peke yao, bali vilevile ‘wanayapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’—Tito 2:6-10.

26. Ni desturi gani ya kale iliyoonyesha kwamba binti alikuwa mshiriki bora wa jamaa?

26 Watoto wa kike vilevile, wanaweza kujifunza ufundi wa kutunza na kupamba nyumba ili wajipatie thamani na sifa ndani na nje ya jamaa yao vilevile. Kufaa kwa mtoto wa kike jamaa yake kunaonyeshwa na mazoea yaliyokuwa katika nyakati za Biblia, ya kulipisha mahari au bei ya bibi-arusi wakati mtoto wa kike alipoozwa. Bila shaka hayo yalionwa kuwa malipo ya kupoteza utumishi wake aliokuwa akitolea jamaa yake.—Mwanzo 34:11, 12; Kutoka 22:16.

27. Kwa nini nafasi za elimu zimepaswa zitumiwe kwa faida nzuri?

27 Nafasi za elimu zimepaswa zitumiwe vizuri ili kutayarisha watoto wajipatie mambo ya lazima ya maisha katika taratibu hii ya mambo. Watoto wanatiwa katika maneno ya mtume yenye kutia moyo kwamba “watu wetu pia wajifunze kudumisha kazi njema [kazi halali ya kuajiriwa, New English Bible] ili wapate mahitaji yao ya lazima, wasije wakawa bila matunda.”—Tito 3:14, NW.

KULINDWA KWA ADILI ZA BIBLIA

28, 29. (a) Ni shauri gani ambalo Biblia inatoa juu ya mashirika? (b) Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao watii shauri hilo?

28 Bila shaka, wazazi wanahangaika sana inapokuwa lazima watoto wao washirikiane na watoto wengine wanaofanya makosa na kujiharibu wenyewe kwa sababu hali, labda mtaa wanamoishi au shule yao inataka hivyo. Huenda wazazi wakaikumbuka kweli ya maneno ya Biblia kwamba “mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” Kwa hiyo hawataki kukubali sababu hii ya mtoto akiomba kufanya jambo fulani: ‘Kila mtu anazoea kufanya hivyo; kwa nini mimi nisifanye?’ Labda si kila mtu anayefanya hivyo, lakini hata iwe hivyo, hiyo si sababu ya kutosha kumruhusu mtoto wako afanye ikiwa ni vibaya au si jambo la hekima kufanya. “Usione wivu kwa watu [au watoto] wabaya, wala usitamani kuwa pamoja nao: inaana moyo wao unafikili mateso, na midomo yao inasema mabaya. Nyumba inajengwa kwa hekima; na inasimamishwa kwa ufahamu.”—1 Wakorintho 15:33, NW; Mezali 24: 1-3, ZSB.

29 Huwezi kumwongoza mtoto wako kupitia kwa shule au kupitia kwa maisha. Lakini, kwa kujenga nyumba yako kwa hekima unaweza kuwapeleka wakiwa na adili njema na kanuni zinazofaa kuwaongoza. “Maneno yao wenye hekima huwa mfano wa michokoo.” (Mhubiri 12:11) Katika nyakati za kale michokoo hiyo ilikuwa fimbo ndefu zenye ncha zilizochongoka. Zilitumiwa kusukuma wanyama wazidi kutembea kuelekea upande unaofaa. Maneno ya Mungu yenye hekima yatatusaidia tuendelee kutembea katika njia inayofaa, na, tukipotea njia, yataifanya dhamiri yetu ituchome tugeuze mwendo wetu. Ili watoto wako wapate hali njema inayoendelea, peleka hekima hiyo waende nayo. Wape hekima hiyo kwa maneno na kwa mifano. Kazia ndani yao kanuni bora, na hizo ndizo watoto wako watataka kuona kwa wengine ambao watachagua wawe wenzao.—Zaburi 119:9, 63.

30. Wazazi wanaweza kuwapaje watoto wao adili za Mungu?

30 Katika yote hayo, kumbuka kwamba inaelekea sana kwamba kanuni bora za adili zitakaziwa ikiwa kuna hali ya nyumbani ambayo katika hiyo kanuni hizo zinaheshimiwa na kufuatwa. Uwe na maoni ambayo unataka watoto wake wawe nayo. Nyumbani mwako, katika mpango wa jamaa, hakikisha kwamba watoto wako wanaona kwamba watu wazima wanawafahamu, wanawapenda, wanawasamehe, wanaruhusiwa kadiri fulani ya uhuru na kujitegemea pamoja na haki na usawa, na kujiona kuwa wanakubaliwa tena wako upande fulani kama wanavyohitaji. Wape katika njia hizo adili za Mungu wazichukue nje ya mpango wa jamaa. Hakuna urithi bora unaoweza kuwapa kuliko huo.—Mithali 20:7.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki