Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • na kur. 17-22
  • Jina la Mungu na Watafsiri wa Biblia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jina la Mungu na Watafsiri wa Biblia
  • Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Iliyowafanya Waache Kulitumia
  • Sababu Iliyofanya Wengine Walitie Jina Hilo Katika Tafsiri Zao
  • Jina la Mungu Katika Nyakati za Baadaye
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • A4 Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania
    Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Pata Habari Zaidi
Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
na kur. 17-22

Jina la Mungu na Watafsiri wa Biblia

MAPEMA katika karne ya pili, baada ya kufa kwa yule wa mwisho wa mitume, kujitenga na imani ya Kikristo kulikotabiriwa na Yesu na wafuasi wake kulianza bila mchezo. Falsafa na mafundisho ya kipagani yaliingia polepole katika kundi. Madhehebu na migawanyiko ilitokea, na ule usafi wa awali wa imani ulichafuliwa. Na jina la Mungu likaacha kutumiwa.

Ukristo huo wenye kuasi imani ulipoenea, ulitokea uhitaji wa kutafsiri Biblia kutoka lugha zayo za awali za Kiebrania na Kigiriki kuingizwa katika lugha nyingine. Watafsiri walitafsiri jina la Mungu namna gani katika tafsiri zao? Kwa kawaida, walitumia neno “Bwana” linalolingana nalo. Tafsiri ya Kilatini yenye uvutano sana ya wakati huo ilikuwa ni Vulgate, tafsiri ya Biblia ya Jerome katika Kilatini cha kila siku. Jerome alitafsiri Tetragramatoni (YHWH) kwa kutumia Dominus, “Bwana” badala yake.

Mwishowe, lugha mpya, kama vile Kifaransa, Kiingereza na Kispania, zilianza kutokea Ulaya. Ingawa hivyo, Kanisa Katoliki lilivunja moyo wa kuitafsiri Biblia katika lugha hizo mpya. Hivyo, ingawa Wayahudi wenye kutumia Biblia katika lugha ya awali ya Kiebrania walikataa kulitamka jina la Mungu walipoliona, “Wakristo” wengi waliisikia Biblia ikisomwa katika tafsiri za Kilatini ambazo hazikutumia jina hilo.

Baadaye, jina la Mungu lilirudia kutumiwa. Mwaka wa 1278 lilionekana katika Kilatini katika kitabu Pugio fidei (Jisu la Imani), kilichoandikwa na Raymundus Martini, mtawa wa kiume Mspania. Raymundus Martini alitumia endelezo la Yohoua.a Muda si muda, mwaka wa 1303, Porchetus de Salvaticis akamaliza kuandika kitabu kiitwacho Victoria Porcheti adversus impios Hebraeos (Ushindi wa Porchetus Juu ya Waebrania Wasiomwogopa Mungu). Katika kitabu hicho yeye, pia, alilitaja jina la Mungu, akiliendeleza kwa njia mbalimbali kuwa Iohouah, Iohoua na Ihouah. Ndipo, mwaka wa 1518, Petrus Galatinus akachapisha kitabu kiitwacho De arcanis catholicae veritatis (Kuhusu Siri za Ukweli Ulioenea Mahali Pote) ambacho katika hicho anaendeleza jina la Mungu kuwa Iehoua.

Jina hilo lilionekana kwanza katika Biblia ya Kiingereza mwaka wa 1530, wakati William Tyndale alipochapisha tafsiri ya vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Katika hivyo alitia lile jina la Mungu, ambalo kwa kawaida linaendelezwa kuwa Iehouah, katika mistari kadha,b na katika taarifa iliyo katika chapa hiyo, akaandika hivi: “Iehovah ni jina la Mungu . . . Isitoshe kila unapoona BWANA katika herufi kubwa (isipokuwa kuwe na kosa la kuchapa) ni Iehovah katika Kiebrania.” Kutokana na hiyo likaja zoea la kutumia jina la Yehova katika mistari michache tu na kuandika “BWANA” au “MUNGU” mahali pengine pengi ilipoonekana Tetragramatoni katika maandishi ya awali ya Kiebrania.

Mwaka wa 1611 ikachapishwa tafsiri ya Kiingereza iitwayo Authorized Version, ambayo ikaja kutumiwa sana mahali pote. Katika tafsiri hiyo, jina hili lilionekana mara nne katika maandishi muhimu. (Kutoka 6:3; Zaburi 83:18; Isaya 12:2; 26:4) “Yah,” (“YAHU”) kikiwa kifupi cha kimashairi cha jina hilo, kilionekana katika Zaburi 68:4. Na jina hilo likaonekana likiwa kamili katika majina ya mahali kama vile “Yehova-yire.” (Mwanzo 22:14; Kutoka 17:15; Waamuzi 6:24) Ingawa hivyo, kwa kufuata mfano wa Tyndale, mara nyingi watafsiri walitumia “BWANA,” au “MUNGU” badala ya jina la Mungu. Lakini ikiwa jina la Mungu lingeweza kuonekana katika mistari minne, kwa nini halingeweza kuonekana katika maelfu mengine yote ya mistari iliyo na jina hilo katika Kiebrania cha awali?

Jambo fulani kama hilo lilikuwa likitukia katika lugha ya Kijeremani. Mwaka wa 1534 Martin Lutheri alichapisha tafsiri yake kamili ya Biblia, ambayo alitegemeza juu ya lugha za awali. Kwa sababu fulani hakulitia ndani jina la Mungu bali akatumia maneno kama HERR (“BWANA”), badala yalo. Ingawa hivyo, yeye alilijua jina la Mungu, kwa kuwa katika mahubiri aliyotoa mwaka wa 1526 juu ya Yeremia 23:1-8, alisema hivi: “Jina hili Yehova, Bwana, ni la Mungu wa kweli pekee.”

Mwaka wa 1543 Lutheri aliandika hivi kwa unyofu wenye kuonyesha tabia yake: “Ati sasa [Wayahudi] wanadai jina Yehova halitamkiki, hawajui wasemalo . . . Ikiwa linaweza kuandikwa kwa kalamu na wino, kwa nini lisisemwe, jambo ambalo ni afadhali kuliko kuandikwa kwa kalamu na wino? Kwa nini hawaliiti pia lisiloandikika, lisilosomekeka au lisilofikirika? Mambo yote yakiisha fikiriwa, kuna kosa kubwa.” Ingawa hivyo, Lutheri hakuwa amesahihisha makosa katika tafsiri yake ya Biblia. Hata hivyo, miaka ya baadaye Biblia nyingine za Kijeremani zikawa na jina hilo katika maandishi ya Kutoka 6:3.

Katika karne zilizofuata, watafsiri wa Biblia waliingia katika mmojapo pande mbili. Baadhi yao waliepuka kutumia jina la Mungu, hali wengine wakalitumia sana katika Maandiko ya Kiebrania, ama kwa namna ya Yehova ama kwa namna ya Yahweh. Na tuzichunguze tafsiri mbili zilizoepuka jina hilo, tuone kwa nini, kulingana na wenye kuzitafsiri, ilifanywa hivyo.

Sababu Iliyowafanya Waache Kulitumia

Wakati J. M. Powis Smith na Edgar J. Goodspeed walipotoa tafsiri ya kisasa ya Biblia mwaka wa 1935, wasomaji walikuta kwamba maneno BWANA na MUNGU yalikuwa yametumiwa mahali pengi sana kuwa badala ya jina la Mungu. Sababu ya kufanya hivyo ilielezwa hivi katika dibaji: “Katika tafsiri hii sisi tumefuata pokeo la kidini la Wayahudi na tumetumia ‘Bwana’ badala ya jina ‘Yahweh’ na maneno ‘Bwana Mungu’ badala ya maneno ‘Bwana Yahweh.’ Mahali pote ambapo ‘Bwana’ au ‘Mungu’ linawakilisha jina la awali ‘Yahweh’ tumetumia herufi kubwa za maandishi madogo.”

Halafu, tofauti kabisa na pokeo la Wayahudi waliosoma YHWH lakini wakalitamka “Bwana,” dibaji hiyo yasema: “Kwa hiyo ye yote anayetaka kutunza ladha ya maandishi ya awali anapaswa kusoma ‘Yahweh’ po pote anapoona BWANA au MUNGU”!

Wakati wa kusoma hayo, mara hiyo ulizo hili linakuja akilini: Ikiwa kusoma “Yahweh” badala ya “BWANA” kunatunza “ladha ya maandishi ya awali,” kwa nini watafsiri hawakutumia “Yahweh” katika tafsiri yao? Kwa nini wao, kwa maneno yao wenyewe, ‘walitumia’ neno “BWANA” ‘badala ya’ jina la Mungu na kwa njia hiyo wakafunika ladha ya maandishi ya awali?

Watafsiri hao wanasema ati walikuwa wakifuata pokeo la kidini la Wayahudi. Lakini je, hilo ni jambo la hekima kwa Mkristo kufanya? Kumbuka, ni Wafarisayo, watunzaji wa pokeo la kidini la Kiyahudi, waliomkataa Yesu naye akawaambia hivi: “Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu.” (Mathayo 15:6) Kweli kweli kubadili kwa namna hiyo kunapunguza nguvu za Neno la Mungu.

Mwaka wa 1952 tafsiri ya Revised Standard Version ya Maandiko ya Kiebrania ilichapishwa katika Kiingereza, na Biblia hiyo, pia, ikatumia maneno yaliyo badala ya jina la Mungu. Jambo hilo lilistahili kuangaliwa kwa sababu tafsiri ile ya awali ya American Standard Version ambayo ilisahihishwa ikawa Revised Standard Version, ililitumia jina Yehova katika Maandiko ya Kiebrania yote. Kwa sababu hiyo kuondolewa kwa jina hilo kulikuwa ni kuondoka kukubwa katika matumzi yalo. Kwa nini jambo hilo lilifanywa?

Katika dibaji ya Revised Standard Version, tunasoma hivi: “Kamati imerudia zoea lenye kujulikana zaidi la King James Version [yaani, kuachwa kwa jina la Mungu]: (1) neno hili ‘Yehova’ haliwakilishi kwa usahihi namna yo yote ya Jina lililotumiwa wakati wo wote katika Kiebrania; na (2) kutumiwa kwa jina lo lote la kipekee la yule Mungu mmoja tu, kana kwamba kulikuwako miungu mingine ambayo angepaswa ajitofautishe nayo, kuliachwa katika dini ya Kiyahudi kabla ya wakati wa Kikristo na hakuifai kabisa ile imani ya Kanisa la Kikristo iliyokubaliwa na watu wengi.”

Je! hizo ni sababu za kutosha? Basi, kama ilivyozungumzwa mapema, jina Yesu haliwakilishi kwa usahihi namna ya awali ya jina la Mwana wa Mungu lililotumiwa na wafuasi wake. Hata hivyo hiyo haikuifanya Kamati hiyo iepuke kutumia jina hilo na badala yalo itumie mitajo kama “Mpatanishi” au “Kristo.” Ni kweli mitajo hiyo inatumiwa, lakini ni kuongezea jina la Yesu, si kuwa badala yalo.

Kwa habari ya ile sababu ya kwamba hakuna miungu mingine ambayo Mungu wa kweli angepaswa ajitofautishe nayo, hiyo si kweli kabisa. Kuna mamilioni ya miungu inayoabudiwa na wanadamu. Mtume Paulo alisema hivi: ‘Kuna miungu mingi.’ (1 Wakorintho 8:5; Wafilipi 3:19) Bila shaka, kuna Mungu mmoja tu wa kweli, kama Paulo anavyoendelea kusema. Kwa sababu hiyo, faida moja kubwa ya kutumia jina la Mungu ni kwamba kunaendelea kumfanya awe tofauti na miungu yote ya uwongo. Isitoshe, ikiwa kutumiwa kwa jina la Mungu ‘hakufai kabisa,’ mbona linaonekana mara karibu 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania ya awali?

Ukweli ni kwamba, watafsiri wengi hawakudhani kwamba jina hilo, pamoja na namna nyingi za kisasa za kulitamka, halifai kuwa katika Biblia. Wamelitia katika tafsiri zao, na nyakati zote matokeo yamekuwa tafsiri inayompa heshima nyingi zaidi yule Mtunga-Biblia na inashikamana kwa uaminifu zaidi na maandishi ya awali. Tafsiri fulani zenye kutumiwa kila mahali zilizo na jina hilo ndani yake ni tafsiri (ya Kispania, iliyochapishwa mwaka wa 1602) iitwayo Valera, tafsiri (ya Kireno, iliyochapishwa mwaka wa 1681) iitwayo Almeida, tafsiri ya awali (ya Kijeremani, iliyochapishwa mwaka wa 1871) iitwayo Elberfelder, na pia American Standard Version (ya Kiingereza, iliyochapishwa mwaka wa 1901). Tafsiri fulani, hasa inayojulikana sana kuwa The Jerusalem Bible, inatumia pia bila kigeugeu jina la Mungu lakini kwa maendelezo ya Yahweh.

Sasa yasome maelezo ya watafsiri fulani waliolitia jina hilo katika tafsiri zao kisha ulinganishe sababu walizotoa na zile za wale walioacha kutumia jina hilo.

Sababu Iliyofanya Wengine Walitie Jina Hilo Katika Tafsiri Zao

Haya ndiyo maelezo ya watafsiri wa American Standard Version ya mwaka wa 1901: “[Watafsiri] walisadiki kwa umoja kwamba ushirikina wa Kiyahudi, ulioliona Jina la Kimungu kuwa takatifu mno lisiweze kutamkwa, haupasi tena utawale katika Kiingereza wala katika tafsiri nyingineyo ya Agano la Kale . . . Hilo Jina la Ukumbusho, linaloelezwa katika Kut. 3:14, 15, na kukaziwa kuwa hivyo mara nyingi katika maandishi ya awali ya Agano la Kale, linamtaja Mungu kuwa Mungu wa kibinafsi, kuwa Mungu wa agano, ndiye Mungu wa ufunuo, ndiye Mkombozi, aliye Rafiki ya watu wake . . . Jina hilo la kibinafsi, lenye mahusiano mengi matakatifu, sasa linarudishwa mahali linapopasa kuwa bila kupingwa katika maandishi matakatifu.”

Hali moja na hiyo, katika dibaji ya tafsiri ya awali katika Kijeremani iitwayo Elberfelder Bibel tunasoma hivi: “Yehova. Sisi tumetunza jina hili la Mungu wa Agano wa Israeli kwa sababu msomaji amelizoea kwa miaka mingi.”

Steven T. Byington, mtafsiri wa The Bible in Living English, anaeleza sababu gani yeye anatumia jina la Mungu: “Maendelezo na matamshi si ya maana sana. Kilicho cha maana sana ni kufanya iwe wazi kwamba hilo ni jina la kibinafsi. Kuna maandiko kadha ambayo hayawezi kufahamika vya kufaa ikiwa tunatafsiri jina hilo kwa kutumia neno la kutaja watu wengi kama ‘Bwana,’ au, lililo baya kuliko hilo, kwa kutumia neno la sifa [kwa mfano, Mwenyezi-Mungu] la namna ya mtajo.”

Kisa cha tafsiri nyingine, ya J. B. Rotherham, ni chenye kupendeza. Yeye alitumia jina la Mungu katika tafsiri yake lakini akapendelea namna ya Yahweh. Ingawa hivyo, katika kitabu alichoandika baadaye, Studies in the Psalms, kikachapishwa mwaka wa 1911, alirudia matumizi ya namna ya Yehova. Kwa nini? Anaeleza hivi: “JEHOVAH.—Matumizi hayo ya namna ya Kiingereza ya jina la Ukumbusho (Kut. 3:18) katika tafsiri ya sasa ya Zaburi hayatokani na kuwa na shaka lo lote juu ya matamshi yaliyo sahihi zaidi, yakiwa Yahwéh; bali ni kutokana na ushahidi tu unaofaa uliochaguliwa kibinafsi kwa kutaka kuendeleza hali ya kupatana na jinsi watu wengi wanavyosikia na kuona kisa cha aina hii, ambacho katika hicho jambo kuu ni kutambuliwa vyepesi kulikokusudiwa kwa lile jina la Kimungu.”

Katika Zaburi 34:3 waabudu wa Yehova wanatiwa moyo hivi: “Tumkuzeni Jehova, nyinywi na mimi, naswi tutukuze jina lakwe pamoja.” (OTSWMSA) Wasomaji wa tafsiri za Biblia zinazoacha kutumia jina la Mungu wanaweza kuitikiaje kikamili kitia-moyo hicho? Wakristo wanafurahi kwa vile angalau watafsiri fulani wamejipa moyo kiasi cha kulitia jina la Mungu katika tafsiri zao za Maandiko ya Kiebrania, na kwa njia hiyo wanahifadhi ambayo Smith na Goodspeed wanaiita “ladha ya maandishi ya awali.”

Ingawa hivyo, tafsiri nyingi, hata zinapotia jina la Mungu katika Maandiko ya Kiebrania, zinaacha kulitumia katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, lile “Agano Jipya.” Sababu ya kufanya hivyo ni nini? Je! kuna sababu yo yote inayofanya jina la Mungu listahili kutiwa katika sehemu hiyo ya mwisho ya Biblia?

[Maelezo ya Chini]

a Shughuli za kuchapwa kwa kitabu hicho ni za tarehe za karne fulani za baadaye, ingawa hivyo, zinalo jina la kimungu kwa maendelezo ya Jehova.

b Mwanzo 15:2; Kutoka 6:3; 15:3; 17:16; 23:17; 33:19; 34:23; Kumbukumbu la Torati 3:24. Pia Tyndale alitia jina la Mungu katika Ezekieli 18:23 na 36:23, katika tafsiri zake zilizoongezwa mwishoni mwa The New Testament, Antwerp, 1534.

[Blabu katika ukurasa wa 17]

Watafsiri wa Authorized Version walitunza jina la Mungu, Yehova, katika mistari minne tu, mahali kwingine wakatumia MUNGU na BWANA badala yalo

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Ikiwa kutumiwa kwa jina la Mungu ‘hakufai kabisa,’ mbona linaonekana mara karibu 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania ya awali?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

Kulionea Jina la Mungu Uadui?

Kwa sasa hakuna tafsiri ya Biblia inayotumiwa katika lugha ya Kiafrikaana (inayosemwa na watu wa Afrika Kusini wenye asili ya Kiholanzi) iliyo na jina la Mungu. Hilo ni jambo la kushangaza, kwa kuwa tafsiri nyingi za lugha za kikabila zinazosemwa katika nchi hiyo zinatumia sana jina hilo. Na tuone ilivyotokea.

Agosti 24, 1878, dai lenye nguvu lilifanywa kwenye mkutano wa Chama cha Waafrikaana wa Kweli (G.R.A) la kwamba Biblia itafsiriwe katika Kiafrikaana. Miaka sita baadaye, jambo hilo likatokezwa tena, na mwishowe uamuzi ukafanywa wa kuanza kuitafsiri Biblia kutoka lugha za awali. Kazi hiyo alikabidhiwa S. J. du Toit, Mkurugenzi wa Elimu katika Transvaal.

Barua ya maagizo aliyoandikiwa du Toit ilikuwa pamoja na mwongozo huu: “Jina la kipekee la Bwana, Yehova au Yahveˆ, limepasa liachwe bila kutafsiriwa [yaani, lisibadilishwe kwa kutumia Bwana wala Mungu] mwanzo mpaka mwisho.” S. J. du Toit alitafsiri vitabu saba vya Biblia katika Kiafrikaana, na jina Yehova likaonekana toka mwanzo mpaka mwisho.

Vichapo vingine pia vya Afrika Kusini, wakati mmoja vilikuwa na jina la Mungu. Kwa mfano, katika De Korte Catechismus (Katekisimu Fupi), cha J. A. Malherbe, 1919, maneno yafuatayo yalionekana: “Ni Jina gani la Mungu lililo kuu?” Jibu ni nini? “Yehova, linaloandikwa BWANA kwa herufi kubwa katika Biblia zetu. [Jina] hili hakupewa kamwe kiumbe ye yote.”

Katika Die Katkisasieboek (katekisimu iliyochapishwa na Federated Sunday School Commission ya Kanisa la Dutch Reformed katika Afrika Kusini) ulizo lifuatalo lilionekana: “Je, basi tusilitumie kamwe jina Yehova au BWANA? Ndivyo Wayahudi wanavyofanya . . . Hiyo siyo maana ya amri ile. . . . Tunaweza kutumia Jina lake, lakini tusilitumie bure kamwe.” Mpaka majuzi, chapa mpya-mpya za Die Halleluja (kitabu cha nyimbo) zilikuwa pia na jina Yehova katika nyimbo fulani fulani.

Ingawa hivyo, tafsiri ya du Toit haikupendwa na watu wengi, na mwaka wa 1961 Tume ya Tafsiri ya Biblia iliteuliwa kusimamia uchapishwaji wa Biblia ya Kiafrikaana. Tume hiyo ilikuwa na maongozi ya kuondoa jina la Yehova katika Biblia. Mwaka wa 1971 Chama cha Biblia cha Afrika Kusini kilichapisha “tafsiri ya muda” ya vitabu vichache vya Biblia katika Kiafrikaana. Ijapokuwa jina la Mungu lilitajwa katika utangulizi, halikutumiwa katika maandishi yenyewe ya tafsiri. Hali moja na hiyo, mwaka wa 1979 tafsiri mpya ya “Agano Jipya” na Zaburi ilitokea nayo vilevile haikutumia jina la Mungu.

Isitoshe, tangu mwaka wa 1970 kutajwa kwa jina Yehova kumeondolewa katika Die Halleluja. Na kuchapishwa kwa sita kwa chapa iliyosahihishwa ya Die Katkisasieboek, iliyochapishwa na Kanisa la Dutch Reformed katika Afrika Kusini, sasa kumeondoa pia jina hilo.

Kwa kweli, jitihada za kutaka kuondoa kabisa namna ya Yehova hazihusu vitabu tu. Kanisa la Dutch Reformed katika Paarl hapo zamani lilikuwa lina jiwe kuu la pembeni ambalo juu yalo yalichorwa maneno haya JEHOVAH JIREH (“Yehova Atatoa”). Picha ya kanisa hilo na jiwe kuu lake la pembeni ilionekana katika toleo la Oktoba 22, 1974 la gazeti Amkeni! katika lugha ya Kiafrikaana. Tangu wakati huo, jiwe kuu hilo la pembeni limebadilishwa na jingine lililo na maneno haya DIE HERE SAL VOORSIEN (“BWANA Atatoa”). Andiko na tarehe iliyo juu ya jiwe kuu la pembeni vimeachwa bila kubadilishwa, lakini lile jina Yehova limeondolewa.

Kwa sababu hiyo, Waafrikaana wengi leo hawalijui jina la Mungu. Washiriki wa kanisa wanaolijua wanaepa kulitumia. Baadhi yao hata wanalipinga, wakisema kwamba jina la Mungu ni BWANA na kulaumu Mashahidi wa Yehova kuwa ndio wametunga jina hilo Yehova.

[Picha]

Kanisa la Dutch Reformed katika Paarl, Afrika Kusini. Hapo awali, jina Yehova lilichongwa juu ya jiwe kuu la pembeni (upande wa juu kulia). Baadaye, likabadilishwa (upande wa juu kushoto)

[Picha katika ukurasa wa 18]

Jina la Mungu kwa namna ya Yohoua lilionekana mwaka wa 1278 katika kitabu kiitwacho Pugio fidei kama linavyoonwa katika hati hii (yenye tarehe ya mpaka karne ya 13 au 14) katika maktaba ya Ste. Geneviève, Paris, Ufaransa (ukurasa wa 162b)

[Picha katika ukurasa wa 19]

Katika tafsiri yake ya vitabu vya kwanza vitano vya Biblia, vilivyochapishwa mwaka wa 1530, William Tyndale alilitia jina la Mungu katika Kutoka 6:3. Katika taarifa ya kupeleka kwenye tafsiri, alieleza matumizi yake ya jina hilo

[Hisani]

(Picha imetolewa kwa ruhusa ya American Bible Society Library, New York)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki