Tumia Uwezo wa Kufundisha Katika Huduma ya Nyumba kwa Nyumba
1 Yesu alijulikana kuwa mhubiri wa habari njema. (Luka 8:1) Lakini mara nyingi zaidi aliitwa na kutajwa kuwa mwalimu. (Mt. 8:19; 9:11) Masimulizi yaliyopuliziwa roho huripoti kwamba “makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake.”—Mt. 7:28; Mk. 6:6.
2 Vivyo hivyo, mitume walikuwa walimu. Kulingana na desturi ya Paulo, ‘aliwapa sababu watu kutokana na Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejezo, aliyokuwa akiwafundisha.’ (Mdo. 17:2, 3, NW) Sisi twaweza kufanya nini ili kufanyia maendeleo uwezo wetu wa kufundisha katika huduma ya nyumba kwa nyumba?
UWE MWENYE KUBADILIKANA
3 Tufanyapo ziara za nyumba kwa nyumba, twakuta watu wenye malezi na mapendezi yenye kutofautiana sana. Baadhi yao hudai kuwa wanaiamini Biblia, wengine hawadai hivyo. Lazima tupatanishe ujumbe wetu na mwenye nyumba mmoja mmoja. Yesu alifanya nini aliposema na mwanamume mmoja “mwana-sheria”? Mwanamume huyo alimuuliza Yesu: “Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?” Yesu aliuliza: “Imeandikwa nini katika torati? Wasomaje?” (Luka 10:25-28) Yeye alitambua kwamba mwanamume huyo alikuwa “mwana-sheria” na jibu lake lilikiri hivyo.
4 Paulo alipohubiri kwenye Areopago, alithamini kwamba alikuwa akisema na Watu wa Mataifa ambao walikuwa na maarifa kidogo sana ya Maandiko ya Kiebrania au ya Yesu Kristo au hawakuwa na maarifa hata kidogo. Hivyo alieleza mambo kulingana na hali hiyo. (Mdo. 17:22-34) Vivyo hivyo, lazima sisi tufikirie mtu tunayeongea naye. Tukiongea na kijana, yatupasa kueleza mambo kwa kiwango ambacho ataelewa. Tukiongea na msomaji wa Biblia, tunahitaji kujipatanisha na hali hiyo, kama vile Yesu alivyofanya na yule “mwana-sheria.” Kwa sababu kila mtu mmoja mmoja tusemaye naye ni tofauti, yaelekea kila utoaji tufanyao utatofautiana kidogo. Ni jambo gani jingine tuwezalo kufanya ili tuwe walimu wenye mafanikio katika huduma ya nyumba kwa nyumba?
WAPE WATU SABABU
5 Kuwapa watu sababu kwamaanisha kutoa ujumbe katika njia ya kwamba utamsaidia mwenye nyumba aelewe na kufikia uamuzi kama ule ule tuliofikia. Hilo lataka kueleza mambo kikamili, hivi kwamba si kwamba tu mwenye nyumba atasikiliza bali pia ataona kuwa utoaji wetu wapatana na akili. Sisi twaweza kuelezaje mambo kwa mafanikio?
6 Swali kwa nini lataka sababu. Kila mwenye nyumba ana haki kabisa ya kuuliza kwa nini tunamtembelea, kwa nini ujumbe wetu ni wenye uharaka sana hivyo, na kwa nini apaswa kuuamini. Kwa hiyo, jiulize maswali hayo wewe binafsi unapotayarisha kwa ajili ya huduma ya nyumba kwa nyumba.
7 Tukiisha kujua majibu ya maswali hayo, tutataka kueleza mambo hayo katika njia ya kwamba mwenye nyumba atapata uelewevu. Kumbuka, Paulo alitumia ‘marejezo’ kueleza Maandiko.—Mdo. 17:3, NW.
8 Vielezi na maswali yanayofaa husaidia sana. Huwafanya watu wafikiri juu ya kweli na husaidia kusitawisha uthamini wa moyoni. Tusomapo Maandiko, yape maneno makuu mkazo unaofaa. Hilo husaidia watu kufikiri juu ya yale yanayosomwa. Katika habari hii, kitabu Kiongozi cha Shule hutoa madokezo mengi hususa katika masomo ya 10, 15, 25, 31, na 34. Chukua wakati kufikiria madokezo hayo, na kuyatumia unaposhiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba.
9 Tukiwa na daraka la kufundisha watu mambo yote aliyotuamuru Yesu twapaswa kusukumwa tufikirie kwa uzito uhitaji wa Kuangalia daima kufundisha kwetu.’ (1 Tim. 4:16) Kujifunza jinsi ya kufundisha hutaka wakati na jitihada kwa upande wetu. Paulo alimwambia Timotheo kwamba wale ambao ‘hufanya kazi ngumu katika kunena na kufundisha’ ‘wanaonwa kuwa wastahiki heshima maradufu.’ (1 Tim. 5:17, NW) Usisite kuomba usaidizi wa wazee na wahubiri wengine wenye sifa za ustahili. Sali daima kwamba Yehova atatubariki tuendeleapo ‘kufanya bidii katika kufundisha.’—1 Tim. 4:13.