Lisifu Jina la Mungu Kikamili
1 Tunashangilia kama nini baraka nyingi za Yehova! Katika Afrika Mashahidi wakati wa mwaka huu wa utumishi, kumekuwako vilele vipya katika wahubiri, mapainia, na mafunzo ya Biblia. Pia kulikuwako hudhurio zuri la Ukumbusho la zaidi ya 44,800. Maelfu ya wahubiri wamehudhuria mikusanyiko ya wilaya, na sisi sote tumenufaika kutokana na chakula kingi cha kiroho kinachoandaliwa katika programu zetu nzuri za kusanyiko letu la mzunguko na za siku ya kusanyiko la pekee. Pia tumepokea baraka nyingine nyingi.
2 Tunaweza kuonyeshaje uthamini wetu kwa yote ambayo Yehova hufanya kwa ajili yetu? Twaweza kufanya hivyo kwa kulisifu jina la Mungu kikamili!—Zab. 145:21.
ENDELEA KULISIFU JINA LA MUNGU
3 Twaweza kulisifuje jina la Yehova kikamili wakati wa Agosti? Tutaendelea kuonyesha zile broshua za ukubwa wa gazeti. Kwa kujitayarisha kwa bidii yenye kuendelea na kuwa na broshua zilizoteuliwa kati ya hizo tuendapo katika utumishi wa shambani, tutakuwa tumetayarishwa tumsifu Yehova na labda tusaidie wengine wajifunzi jinsi wao pia wanavyoweza kumsifu.
4 Kichwa chetu cha Mazungumzo ni “Dini Inayompendeza Mungu.” Twaweza kutayarisha matangulizi yanayofaa yakitegemea habari iliyo kwenye kurasa 9-15 za kitabu Kutoa Sababu. Baadhi ya wenye nyumba watazungumza nawe kwa urahisi maoni yao juu ya dini. Ijapokuwa watu walio wengi wana dini, Mathayo 7:13, 14 huonyesha kwamba si dini zote zinazokubalika kwa Mungu. Inatumainisha kujua kwamba ibada ya kweli inaweza kupatikana. Biblia huonyesha kwenye Waefeso 4:5, 13 kwamba takwa moja ni umoja miongoni mwa waabudu. (Soma.) Mstari wa 13 huonyesha maana ya kuwa na maarifa sahihi ya Mwana wa Mungu. Hiyo yamtaka mtu apate kujua yale ambayo Biblia hufundisha juu ya Yesu na uhusiano wake na Mungu. Takwa jingine la dini ambayo humpendeza Mungu ni kwamba lazima mtu aishi kulingana na viwango vya hali ya juu vya adili vya Biblia kama inavyoonyeshwa kwenye Tito 1:16. (Soma. Toa mfano mmoja au miwili kama vile unyofu au adili bora.) Mwenye nyumba akionekana kuwa anapendezwa kikweli, toa broshua inayomfaa.
JITAYARISHE VIZURI
5 Kujitayarisha ni jambo muhimu ikiwa tutakuwa na mafanikio katika kufundisha wengine. Kwa nini usijitayarishe pamoja na washiriki wengine wa familia, pamoja na yule aliyekufundisha kweli, au pamoja na mtu mwingine katika kikundi chenu cha funzo la kitabu? Kwa kufanyia mazoezi utoaji wako, utajihisi ukiwa na uhakika zaidi na kudhihirisha usadikisho wa kibinafsi unaponena na watu katika eneo.
6 Utoaji wetu wapasa kuonyesha kupendezwa kwetu na watu. Mwenye nyumba akubalipo broshua, waweza kumwonyesha jinsi programu yetu ya funzo la Biblia hufanywa. Au waweza kuamua kwamba ingefaa zaidi kufanya hivyo wakati wa ziara ya kurudia.
7 Tufikiapo mwisho wa mwaka huu wa utumishi wenye matukio makubwa, ni jambo lenye kuleta shangwe kama nini kuwa wapokeaji wa baraka nyingi sana kutoka kwa Yehova! Sisi sote na tutumie mwezi huu unaobaki wa mwaka wa utumishi wa 1991 kulisifu jina la Yehova kikamili tutazamiapo kwa shauku kumtumikia Yehova milele katika ulimwengu wake mpya.