Uwe Mwenye Nafsi Yote Katika Huduma ya Shambani
Sehemu ya 2: Kusitawisha Shauku
1 Ni rahisi kuwa wenye shauku juu ya utendaji fulani tunapoufurahia. Kwa kawaida ni kweli pia kwamba mtu hufurahia kufanya jambo ambalo amejitayarishia. Hakika hiyo ni kweli katika kutimiza kikamili huduma yetu.—2 Tim. 4:5.
KUJITAYARISHA NI KWA MUHIMU
2 Shauku yetu katika huduma ya shambani inahusiana moja kwa moja na jambo la kwamba tumejitayarisha vizuri kadiri gani na twatoka kwenda katika utumishi wa shambani mara nyingi kadiri gani. Kwa mfano, ikiwa mtu tumpataye katika huduma ya nyumba kwa nyumba ajitambulisha kuwa Mwislamu, tungeweza kusema nini? Mhubiri aliyejitayarisha vizuri angeweza kujibu: “Hilo lapendeza. Sijapata kuongea na Waislamu wengi. Lakini nimesoma jambo fulani kuhusu mafundisho yenu katika kitabu hiki cha mafundisho. [Fungua kwenye ukurasa 23 wa kitabu Kutoa Sababu.] Kinasema kwamba nyinyi mnaamini kwamba Yesu alikuwa nabii lakini kwamba Muhamadi alikuwa ndiye nabii wa mwisho na aliye wa maana zaidi ya wote. Sivyo? [Ruhusu jibu.] Je! mwaamini pia kwamba Musa alikuwa nabii wa kweli? [Ruhusu jibu, yaelekea litakuwa ndiyo.] Je! naweza kukuonyesha katika Maandiko Matakatifu aliyojifunza Musa kutoka kwa Mungu kuhusu jina binafsi la Mungu?” Halafu usome Kutoka 6:3. Kwa njia hiyo, huenda ukaanzisha mazungumzo yenye kupendeza.
3 Ni vigumu kwa wengi wetu kukumbuka nambari hususa za kurasa. Lakini kwa utayarishaji na mazoezi kidogo, twaweza kutumia ile sehemu inayoitwa “Vizuia-Mazungumzo” karibu na mwanzo wa kitabu Kutoa Sababu. Katika sehemu hiyo zimetiwa ndani kurasa kadhaa za habari ili kutusaidia kujibu watu wanaojitambulisha na dini mahususi.
4 Pia kitabu Kutoa Sababu kina kisehemu kizuri juu ya matangulizi. Kwa nini usitayarishe matangulizi yako yafanane na hayo? Huenda tukahitaji kupatanisha utoaji wetu na hali. Mwishoni mwa habari zilizo nyingi katika kitabu Kutoa Sababu, mna kisehemu “Mtu akisema,” kikiandaa habari iliyo wazi katika kujibu maswali au vipingamizi hususa vinavyohusiana na habari. Hata hivyo habari zote hizo nzuri, ni zenye thamani kwa kadiri tu tunazitumia katika utayarishaji wetu.
JINSI YA KUTAYARISHA
5 Uwe chonjo kwa habari ya vichapo vyovyote ambavyo vitazungumzwa kwenye Mkutano wa Utumishi na uwe navyo ili kuvirejezea wakati wa mazungumzo au maonyesho. Kwa njia hiyo, unaweza kunufaika kikamili zaidi kutokana na matayarisho ya wengine.
6 Inanufaisha kutumia wakati fulani kutayarisha kwa ajili ya utumishi. Hakikisha umepata fasihi utakayohitaji. Tumia dakika chache kufikiria Kichwa cha Mazungumzo. Pitia maandiko yaliyotumiwa, na kuchunguza upate mambo hususa ya kuzungumzia katika fasihi ambayo itatumiwa. Kufanya hivyo pamoja mkiwa familia kunaweza kusaidia.
7 Mwe na vipindi vya mazoezi. Mwaweza kufanya mazoezi nyakati mbalimbali—baada ya Funzo la Kitabu la Kundi, kwenye vikusanyiko vya kirafiki, mkiwa vikundi-vikundi, kati ya milango. Kufanya utoaji na kuzungumza na kufanya maonyesho ya jinsi ya kushughulikia vipingamizi kwaweza kuwa jambo lenye kufurahisha na kuandaa pindi nzuri za kunoa stadi zetu.
8 Utayarishaji wa bidii yenye kuendelea utajenga shauku yetu kwa ajili ya huduma hivi kwamba tutakuwa wafanyakazi stadi na kuvuna uradhi wenye shangwe.—Yn. 2:17.