Panga Sasa Kuhudhuria “Wapendao Uhuru” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1991
1 Kwa kuona jinsi hali za ulimwengu zilivyo leo, haishangazi kwamba katika nchi nyingi watu hutamani uhuru mwingi zaidi kuliko ule wanao. Lakini uhuru wa kweli waweza kupatikana wapi? Yesu Kristo alisema: “Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yn. 8:31, 32) Uhuru huo si wa aina ile yenye mipaka ambao wanadamu hutumaini wanapokataa mtawala mmoja wa kisiasa au muundo wa serikali kwa kupendelea mwingine. Badala yake, hufikia kiini cha matatizo ya kibinadamu. Aliyokuwa akizungumzia Yesu ni uhuru kutokana na kifungo cha utumwa kwa dhambi. (Ona Yohana 8:24, 34-36.) Hivyo, mtu anapokuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo, matokeo ni badiliko dhahiri katika maisha yake, ukombozi.
2 MKUSANYIKO WA SIKU TATU: Mfululizo wa “Wapendao Uhuru” Mikusanyiko ya Wilaya ya 1991 utaanza Afrika Mashariki katika Novemba 1-3. Kipindi cha kufungua kitaanza saa 4:20 Ijumaa asubuhi, na mkusanyiko utamalizika saa 10 hivi Jumapili alasiri. Habari zilizoteuliwa kwa uangalifu zenye umaana kwa afya yetu ya kiroho zitatolewa katika kila pindi. Unamna-namna wa habari zitaonyesha jinsi uhuru uliotajwa katika Warumi 8:21 uwezavyo kuwa wetu. Habari zenye kuchochea zitakuzwa na kutolewa kwa hotuba, maonyesho, mahoji, na drama moja.
3 Lifanye liwe azimio lako kutokosa hata kipindi kimoja. Huenda hilo likataka kudhabihu mambo fulani ya kibinafsi na kufanya marekebisho katika ratiba yako. Huenda ikahitajiwa kabisa kufanya mipango ya pekee na mwajiri-kazi wako. Wengi hata huachilia manufaa za kifedha ili kuhudhuria vipindi vyote. Bila shaka Yehova atabariki wale wanaofanya jambo hilo kuwa jambo la sala ya moyo mweupe na ambao hutia jitihada yenye kuhisiwa moyoni ili wahudhurie.—Lk. 13:24.
4 WASILI MAPEMA: Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa jitihada zao za kuwa wenye kutegemeka na kufika kwa wakati. (Lk. 16:10) Hilo ni la maana pia wakati wa kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya. Wasili mapema kila siku, na uwe umeketi kabla ya programu kuanza. Hilo litataka kuruhusu wakati wa kutosha kutunza mambo yanayohitaji kuelekezewa fikira, kama vile kuegesha gari lako na kupata viti kwa ajili ya familia yako.
5 Kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya hutupa sisi fursa nzuri ya kufurahia ushirika mzuri. Lakini kutembelea marafiki mpaka usiku sana kwaweza kuzuia jitihada zetu za kufika kwa wakati siku itakayofuata. Wasiwasi mwingi na mtamauko unaweza kutokea kwa sababu ya kuanza tukiwa tumechelewa na kwa sababu hiyo kufanya haraka-haraka asubuhi. Ili kuzuia jambo hilo, ni jambo lenye mafaa kuweka wakati mzuri wa kwenda kulala. Kwa kushikamana na ratiba kwa uthabiti, yaelekea wote watapata pumziko zuri usiku na kuwa tayari kuanza mapema kesho yake. Hilo linawaepusha kufika wakati programu inapoendelea, jambo ambalo linakengeusha fikira na linaweza kuudhi wale ambao tayari wameketi. Kuwasili mapema kila siku kutakuruhusu kuwa na ushirika na ndugu na dada zako. Upendo wa Kikristo na kufikiriana, pamoja na heshima kwa Yehova na mambo ya kiroho anayoandaa, kwapasa kutusukume tufanye yote tuwezayo tuwasili kwa wakati.
6 SIKILIZA KWA MAKINI: Kusikiliza kunamaanisha kuwa msikivu kweli kweli kwa akili na moyo wetu pia, kwa masikio yetu na uwezo wetu wa kuelewa. Tunahitaji kusikiliza na “kulisikia neno la BWANA, [Yehova, NW]” (Yer. 2:4) Kwenye Isaya 55:2 Yehova aliamuru Israeli: “Nisikilizeni kwa bidii [makini, NW].” Neno “makini” hufasiriwa kuwa “uangalifu uliokazwa au wa juhudi.” Ikiwa sisi ni wasikivu wakati wa mkusanyiko, ‘tutasikiliza na kuongezewa elimu’ tukiwa makini. (Mit. 1:5) Kusikiliza na kujifunza kwenye mkusanyiko wa wilaya mara nyingi hutaka jitihada na mkazo zaidi wa fikira kuliko itakiwavyo katika Jumba la Ufalme. Kwa nini? Tunaketi kwa vipindi virefu zaidi vya wakati, na kuna vikengeusha fikira vingi zaidi kwa sababu ya hesabu kubwa ya watu wanaohudhuria. Ikiwa sisi si waangalifu, tutajinyima na kukosa kupokea faida kamili za mlo mnono wa kiroho ulioandaliwa. (1 Pet. 2:2) Ni nini laweza kufanywa? Ni jambo la kupendeza sana kuona kwamba wajumbe wengi wa mkusanyiko wamekuza zoea lenye msaada la kuandika habari wakati wa programu. Ingawa baada ya wakati fulani baadhi ya hotuba kwenye mkusanyiko wa wilaya zitatokea katika vichapo, nyingine hazitatokea. Wote wanatiwa moyo kuwa na mradi wa kuandika mambo fulani wakati wa mkusanyiko wa wilaya kwa sababu hiyo ni njia nzuri ya kukaza fikira zako kwa yale yanayosemwa.
7 Mambo ya kuandikwa hayapasi kuwa mengi au yenye maelezo marefu. Kwa kawaida fungu la maneno machache linatosha kwa wazo kuu. Hata watoto wadogo watafaidika zaidi kutokana na hotuba na kusaidiwa kukaza fikira ikiwa wanapewa kitabu cha kuandikia na kalamu au penseli ili waweze kuandika mambo makuu ya msemaji na maandiko makuu au mawazo mapya ambayo huenda yakatolewa. Wazee huliona kuwa jambo la faida kuwa na mambo yaliyoandikwa kwa njia nadhifu kwa ajili ya kuongoza pitio lenye maana la programu ya mkusanyiko wakati wa Mkutano wa Utumishi unaofuata mkusanyiko wa wilaya. Pia, huenda wakataka kuunganisha nyingi za habari zilizotolewa kwenye mkusanyiko katika kazi yao ya kufundisha na kufanya uchungaji.
8 MUUNGANIKE KATIKA WIMBO NA SALA: Sehemu moja ya ibada yetu inatia ndani kumheshimu Yehova kwa kuimba sifa zake, kama vile Yesu na mitume wake walivyofanya. (Mk. 14:26) Maneno ya paulo katika 1 Wakorintho 14:15 kuhusu kuimba huonekana yakidokeza kwamba kuimba kulikuwa sehemu ya kawaida ya ibada ya Kikristo. (Ona pia Huduma ya Ufalme Yetu ya Februari 1991, ukurasa wa 3.) Mikusanyiko ya wilaya inatupa fursa isiyo na kifani tuunganike pamoja na maelfu ya ndugu na dada zetu katika kusifu Yehova kwa wimbo na sala. Hata hivyo, wengine wameonyesha ukosefu wa staha kwa sehemu hizi za maana sana za ibada yetu. Jinsi gani? Kwa kufika isivyolazima kwenye mkusanyiko wakati au baada ya wimbo na sala ya kufungua. Mwishoni mwa programu, wengine huacha viti vyao wakati wa wimbo au kabla ya sala. Katika pindi chache huenda kukawa na sababu nzuri za kufanya hivyo. Hata hivyo, je! heshima inayostahili na uthamini unaonyeshwa kwenye meza ya kiroho ya Yehova ikiwa wengine wanaacha fursa ya kuimba na kusali pamoja ili tu kwamba wafikie magari yao au wale mapema?—Mt. 6:33.
9 Lazima tuwe waangalifu ili kwamba kwa kufuatia manufaa za kibinafsi, haturuhusu maelekeo ya kiulimwengu ya mimi kwanza au vitabia visivyo vya kimungu kama vile choyo na ubinafsi vizuie maendeleo yetu ya kiroho. Katika miaka ya majuzi, wengi wa ndugu na dada zetu katika nchi za Ulaya Mashariki waliweza hatimaye kufurahia uhuru wa kuimba na kusali. Kama vile wao walivyochangamkia kuweza kuimba na kusali wakiwa hesabu kubwa, acheni nasi tuonyeshe roho iyo hiyo ya uthamini kwa mambo matakatifu sasa na tusione kamwe fursa zetu za kuimba na kusali pamoja kwa njia ya vivi hivi.
10 ADABU ZETU ZA KIKRISTO: Adabu zetu za Kikristo na sura yetu kwenye mikusanyiko ya wilaya vimetuletea sifa njema tukiwa Mashahidi wa Yehova. Hii ni kwa sababu tunachukua ibada yetu kwa Yehova kwa uzito na kwa sababu hatuioni mikusanyiko yetu kuwa vikusanyiko vya kirafiki tu. Tunapokuja pamoja katika pindi hizo za pekee, tunapaswa kuendeleza heshima yetu ya Kikristo na kuwa na akili timamu ya kiroho kwa kujiendesha ifaavyo nyakati zote tukiwa wahudumu.—1 Kor. 10:31-33.
11 Ikiwa tunashindwa kufanya hivyo, tunaathiri furaha ya wengine, hata kuwakwaza wapya. Je! tunaitikia na kuonyesha uthamini hata kwa fadhili ndogo tunazoonyeshwa? Tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu wale wanaotuzunguka na kuonyesha heshima na ufikirio. Kila mtu apaswa atambue kwamba wakati programu inapoendelea, ni wakati wa kusikiliza, si kutembea huku na huko au kuzungumza.—Kum. 31:12.
12 Sehemu nyingine ambayo adabu zetu za Kikristo zaweza kumtukuza Yehova Mungu ni katika kushughulika na wale wanaotuandalia mahali pa kulala. Tunapaswa tuonyeshe uthamini na kufikiria wale wanaotualika, tuwe wenye adabu na si wenye kudai mno. (Gal. 6:10) Mashauri mazuri yametolewa kuhusu mwenendo ufaao kwenye mahali petu pa kulala. Wengi wameitikia vema na wanajitahidi kwa bidii kushirikiana kikamilifu na tunawatia wote moyo kuwa na uamuzi mzuri na utambuzi, na kuwa tayari ‘kufanya mambo yote kwa ajili ya Injili.’—1 Kor. 9:19-23.
13 Ni jambo linalostahili kufikiriwa kuacha mahali petu pa kulala katika hali nzuri, na safi. Usafi na ufikirio wapasa kuonyeshwa si kwa mavazi na mwenendo wetu tu bali pia kwa jinsi tutendeavyo mali ya wengine. Je! kuna sababu yoyote kwa nini chumba kilichokodishwa au kutolewa kwetu bure hakipaswi kuachwa kikiwa safi na nadhifu? Tabia yenye kukosa ufikirio huharibu sifa yetu njema. Kwenye mikusanyiko ya wilaya ijayo, sisi sote twapaswa kulifanya liwe azimio letu kujiendesha wenyewe ili ‘tuyapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’—Tit. 2:10.
14 KWA WAZAZI: Watoto wachanga na matineja wanaalikwa na wanatarajiwa kuhudhuria “Wapendao Uhuru” Mkusanyiko wa Wilaya. Uhuru ambao ulimwengu unatoa waweza kuongoza kwenye kifo chao cha kiroho, kama vile Adamu alivyopoteza uhuru uliopewa ainabinadamu pale mwanzoni. Tengenezo la Yehova lenye upendo limetuandalia sote kufikiri kwa usahihi kuhusu jambo hilo. Tunatiwa moyo kuona wachanga ambao wamejifunza kukaza fikira zaidi kwenye mikutano yote ya Kikristo na ambao wanapendezwa sana na programu ya mkusanyiko. (Zab. 148:12, 13) Lakini mengi yanategemea kielelezo na usimamizi wa wazazi. Wachanga wengi wamezoezwa vizuri sana kuandika habari. Ikiwa wewe ukiwa mzazi bado hujawafunza watoto wako kuandika habari, mbona usitumie wakati unaobaki kabla ya mkusanyiko wenu ufanye hivyo? Hata walio wachanga sana wanaweza kutiwa moyo waandike mitajo ya Maandiko na maneno ya msingi yanayohusiana wanayosikia yakisemwa na wasemaji. Wazazi fulani wanapanga kupitia habari kuu kutoka programu ya siku baada ya kurudi mahali pao pa kulala au wanaposafiri kwenda nyumbani.
15 Bila shaka, wazazi walio wengi wanathamini kwamba mbetuko wa asili wa watoto ni kucheza. Hawana maarifa maishani, nao hawajakomaa. Basi, wanapaswa kufundishwa wakati wa kusikiliza na jinsi ya kujiendesha wenyewe kwenye mikutano. Hili linataka usimamizi mzuri wa wazazi wao. Wazazi fulani wamelegea katika sehemu hii. Nyakati nyingine, ingawa huenda wazazi wakawa wanamwonyesha Yehova kicho kinachofaa wakati wa sala, watoto wao wanacheza na kukengeusha fikira za wengine. Wazazi wanapaswa kujua watoto wao wanafanya nini wakati wa sala. Pia, wao wanafanya nini wanapoondoka kwenye viti vyao wakati wa programu? Je! watoto wanaachwa bila usimamizi wakati na baada ya programu ya mkusanyiko?—Mit. 29:15.
16 Watoto fulani wametenda kwa njia isiyo ya adabu na yenye utundu na hata wamekosa kuwaheshimu ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao wamejaribu kuwarekebisha kwa njia ya fadhili. Utundu na mwenendo kama huo usiofaa Wakristo mara nyingi huwa tokeo la uendekevu na ukosefu wa nidhamu nyumbani. Bila shaka wafaa kurekebishwa. Wazazi wote Wakristo wapaswa kusimamia watoto wao kwa uangalifu nyakati zote wanapoendelea “kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Efe. 6:4, NW.
17 Ushirikiano wenu kamili unaombwa kwa habari ya kuhifadhi viti. Tafadhali kumbukeni kwamba VITI VINAWEZA KUHIFADHIWA KWA WASHIRIKI WA KARIBU WA JAMAA YAKO PEKE YAO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Tafadhali msiwawekee wengine viti. Nyakati fulani, viti vya ziada haviwekewi mtu fulani hasa. Hili ni jambo la kutoonyesha upendo na linawapotosha wakaribishaji na wengine wanaotafuta viti vilivyo wazi. Kupatana na shauri la Biblia, tunapaswa tujitahidi kuonyesha shauku ya kidugu na tushirikiane kikamili na mpango unaokubaliwa kwa ajili ya kuhifadhi viti. Hakuna yeyote aliye na haki ya viti vingi zaidi ya vile vinavyohitajiwa kwa ajili ya familia yake au kikundi cha gari.—2 Pet. 1:7.
18 Viti havipaswi kuhifadhiwa usiku kucha. Mahali pa mkusanyiko hapapaswi kufunguliwa kabla ya saa 1:00 asubuhi kwa yeyote isipokuwa wafanyakazi wa kujitolea walio kazini kabla ya wakati huo. Hakuna yeyote ya wafanyakazi hao atakayeruhusiwa kuhifadhi viti mpaka baada ya saa 1:00 asubuhi, wakati wengine wanaporuhusiwa kuingia jengo hilo. Wakaribishaji watakuwa katika mahali pao walipogawiwa kabla ya wakati huo ili kuelekeza yale yanayofanywa, ili kuepuka kukiuka maelekezo ya Sosaiti kuhusu uhifadhi wa viti. Tafadhali mshirikiane kikamili na wakaribishaji wanapotimiza migao yao kwa faida ya wote waliohudhuria.
19 Inadokezwa kwamba uamuzi mzuri ufanywe kwa habari ya kuleta vitu vya kibinafsi kwenye mahali pa mkusanyiko. Wakati uliopita, watu fulani wameleta mizigo mikubwa ambayo haiwezi kuwekwa chini ya viti. Hii iliwekwa kwenye vijia au juu ya viti. Jambo hili linafanya wengine wanyimwe viti, na hata linaweza kuvunja sheria za kuzima moto na za usalama. Tunahitaji kuonyesha ufikirio katika mambo hayo.
20 Kwa hakika, watu wa Yehova huthamini kuweza kukutana pamoja kwenye vifaa vizuri ili kunufaishwa na programu ya kiroho iliyotayarishwa. Tunathamini pia utumishi mwingi na usaidizi mwingine unaotolewa katika mikusanyiko hiyo. Kwa uangalifu mwingi na kwa gharama kubwa kwa Sosaiti, mipango hufanywa kwa ajili ya viti vya kutosha, kuweka mifumo ya sauti yenye gharama sana, kuendesha Idara ya Utumishi wa Chakula yenye mafanikio, na kushughulikia hesabu fulani ya mipango mingine na utumishi mbalimbali ambao hufanya kuhudhuria mikusanyiko kuwe jambo la kuonewa shangwe na lenye kuburudisha kiroho.
21 Gharama hizo hulipwa kwa michango yenu ya hiari katika kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote ya Sosaiti. Ukitaka kuandika hundi ya pesa, unaweza kuandika ilipwe Sosaiti katika nchi yenu. Kwa manufaa yenu, masanduku ya michango yenye maandishi yaliyo wazi yatawekwa kotekote katika vifaa vya mkusanyiko. Michango yote huthaminiwa sana sana, na Sosaiti yataka kuwashukuru kimbele kwa utegemezo wenu na ukarimu wenu wenye umoja wa masilahi ya Ufalme katika njia hii. Mtu mmoja alionyesha uthamini wake kwa jambo la kwamba kiasi cha mchango hakikudokezwa: ‘Linaonekana kuwa jambo la kuvutia kujua kwamba tunaachiwa uamuzi—mpaka kwenye kina chenyewe cha uthamini wetu. Hivyo ni kwa shukrani kwamba tunahisi tukiwa na moyo wa kutoa zaidi kuliko ilivyo kawaida.’ Tuna uhakika kwamba wote wakiwa mtu mmoja mmoja watasukumwa wahisi daraka lao kuhusiana na gharama hizo na watashirikiana kikamili kwa kushiriki kwa kadiri hali zao zinavyowaruhusu.—Lk. 6:38.
22 UWEPO KWENYE “WAPENDAO UHURU” MKUSANYIKO WA WILAYA! Kwa kuhudhuria “Wapendao Uhuru” Mkusanyiko wa Wilaya na kusikiliza programu kwa makini, tutaendeleza uthamini wetu kwa uhuru ujao kupitia Kristo na kwa utumizi mwema wa uhuru wa Kikristo. Fanya mipango yako sasa na uwepo wakati wa wimbo wa kufungua na uhudhurie vipindi vyote mpaka sala ya kumalizia Jumapili alasiri.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Vikumbusho vya Mkusanyiko wa Wilaya
MAHALI PA KULALA: Mipango kwa mwaka huu, kwa sehemu iliyo kubwa, itafuata kiolezo cha miaka iliyotangulia. Mikusanyiko iliyo mingi hutumia vyumba vya kulala au vifaa vilivyo mahali pa mkusanyiko ili wote wanaohudhuria wapate mahali pa kulala. Huenda kukawa na mahali pa kulala katika nyumba za watu binafsi. Hata hivyo, tafadhali kumbukeni kwamba, si jambo linalofaa wajumbe wachukue kivivi hivi tu ukaribishaji-wageni wa ndugu zao na kutazamia wawakaribishe siku za ziada ili waweze kuzuru sehemu fulani wakati wa likizo au kufanya mambo mengine kabla au baada ya mkusanyiko. Vyumba hivi ni kwa ajili ya wakati wa mkusanyiko tu. Wale wanaopata mahali kama hapo pa kulala wapaswa wahakikishe kwamba wao na watoto wao wanatenda kwa njia yenye staha kuelekea nyumba ya mkaribishaji wao na wasiharibu kitu chochote au kupekua-pekua mali au sehemu za faragha za nyumba hiyo. Wenye nyumba wakiwa na matatizo yoyote kuhusiana na jambo hili wanapaswa kujulisha Idara ya Mahali pa Kulala mara moja kwenye mkusanyiko, na ndugu waliopo watafurahi kusaidia. Mnaweza kupeleka fomu ya maombi ya mahali pa kulala iliyojazwa kupitia msawazishaji wa mkusanyiko katika kundi lenu.
UBATIZO: Wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa wajitahidi kuwa kwenye viti vyao katika sehemu iliyoonyeshwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Mavazi yenye kiasi na taulo yapasa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Akina dada hasa watataka kuchunguza kimbele waone kama mavazi wanayopanga kuvaa yanaonyesha uchi yanapolowa maji. (Ona Huduma ya Ufalme, Novemba 1987, ukurasa 3, fungu 6) Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na mnenaji, mwenyekiti wa kipindi hicho atawatolea wanaobatizwa maagizo mafupi kisha ataomba wimbo uimbwe. Mstari wa mwisho uanzapo, wakaribishaji watawaelekeza wenye kubatizwa kwenye mahali pa uzamisho au kwenye magari yatakayowapeleka hapo, huku wasikilizaji wale wengine wakimaliza kuimba wimbo. Kwa kuwa ubatizo kwa kufananisha kujiweka wakfu kwa mtu ni jambo la siri na la kibinafsi kati ya mtu na Yehova, hakuna uandalizi kwa ule unaoitwa eti ubatizo wa shirika ambao watu wawili au zaidi wanaotaka kubatizwa wanakumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
KITAMBULISHO CHA MAPAINIA: Mapainia wote wa kawaida na wa pekee, na waangalizi wasafirio pia watahitaji kuleta kadi yao ya Utambulisho na Mgawo kwenye mkusanyiko. Mapainia ambao watakuwa wamekuwa kwenye orodha kwa miezi sita tangu waanze upainia wakati wa mkusanyiko wa wilaya watakaouhudhuria wanaweza kupokea tikiti za chakula za mkusanyiko wakionyesha Kitambulisho chao kwenye mkusanyiko huu mmoja tu. Hivyo, tunza kadi hiyo kama vile ungetunza pesa. Huwezi kupata nyingine kwenye mkusanyiko. Vichapo vyovyote vitakavyotolewa kama zawadi au vingine kwa bei ya painia vitapatikana kwa mapainia katika chumba cha vitabu tu, kwa kuonyesha Kitambulisho chao. Wale walio katika utumishi wa Betheli wanaweza kupokea maandalizi yayo hayo kwa kuonyesha Kitambulisho chao cha Betheli.
UTUMISHI WA KUJITOLEA: Msaada wa kujitolea unahitajiwa ili mkusanyiko wa wilaya uendeshwe vizuri. Hata kama unaweza kufanya kazi kwa sehemu fulani tu ya mkusanyiko, utumishi wako utathaminiwa. Ikiwa unaweza kusaidia, tafadhali piga ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea unapowasili kwenye mkusanyiko. Watoto wa umri ulio chini ya miaka 16 waweza kuchangia pia kufanikiwa kwa mkusanyiko, wanatakwa wafanye kazi pamoja na mzazi au mtu mwingine mzima mwenye kujali daraka.
KADI ZA BEJI ZA SHAVU LA KOTI: Tafahali vaa kadi ya beji ya shavu la koti iliyotayarishwa kipekee kwenye mkusanyiko na pia unaposafiri kwenye na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hii inatuwezesha tutoe ushahidi mzuri tunaposafiri. Unapaswa upokee kadi ya beji ya shavu la koti kupitia kundi lako kwa sababu hazipatikani kwenye mkusanyiko.
TAHADHARI: Hata uwe unaegesha wapi, unapaswa ufunge gari lako wakati wote na usiache ndani kitu chochote kinachoonekana. Fungia mizigo yako yote nyuma ya gari, ikiwezekana. Pia, ujilinde dhidi ya wevi na wakwepuzi wa mifuko wanaovutiwa na mikusanyiko mikubwa. Hii inatia ndani kutoacha kitu chochote chenye thamani bila mtu wa kukitunza katika viti kwenye mikusanyiko. Tafadhali iweni waangalifu.