Je! Wewe Unaweza Kufanya Upainia Msaidizi?
1 Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wajitoe kwa hiari katika huduma, na akawahakikishia kwamba kufuata njia hiyo kungewaletea furaha na baraka nyingi za kiroho. (Mt. 10:8b; Mdo. 20:35) Aprili iliyopita watu 1,994 walijionea wenyewe shangwe za utendaji ulioongezeka wakiwa mapainia wasaidizi. Je! wewe unaweza kushiriki katika mibaraka hiyo mwaka huu kwa kujiandikisha kuwa painia msaidizi wakati wa Machi ama Aprili ama labda miezi yote miwili?—Zab. 34:8.
2 Kuchunguza Hali Zako: Unapofikiria maono yaliyotajwa chini, jiulize: ‘Je! hali yangu yafanana na mojawapo mifano hii? Ninaweza kufanyaje marekebisho yanayohitajika ili niweze kufanya upainia msaidizi?’
3 Dada mmoja aliweza kufanya upainia msaidizi hata ingawa ana watoto watano na hufanya kazi ya kimwili. Yeye alithawabishwaje? Mume na watoto wake walimpa utegemezo bora sana, na kama tokeo la mfano mzuri wa dada huyo, mume wake alisukumwa kuwa mhubiri asiyebatizwa mwezi uliofuata.
4 Katika kundi moja wazee na watumishi wa huduma wote walitumika wakiwa mapainia wasaidizi wakati wa mwezi mmoja. Wengi wao walikuwa na kazi za kimwili, lakini walijishughulisha sana na utendaji wa kiroho miisho-juma. Uongozi mwema waliotoa katika kuhubiri na kupanga utumishi wa shambani ulifaidi kundi zima. Wahubiri 73 kati ya 77 walishiriki katika aina fulani ya utumishi wa upainia wakati wa mwezi huo.
5 Msichana wa shule wa miaka 15 alitumia likizo yake ya majuma mawili wakati wa masika kushiriki katika utumishi wa upainia msaidizi naye asema hivi: “Mimi ninaweza kuona tofauti kweli kweli, hasa maendeleo katika mazungumzo. Niliweza kuwa na mazungumzo mengi zaidi na watu mlangoni.”
6 Wale ambao wamestaafu kutoka kazi za kimwili huwa mara nyingi na fursa nzuri za kufuatia faida za Ufalme. Baada ya kifo cha mume wake, dada wa miaka 84 aliandika: “Watoto wangu wote walikuwa wamekua, wakafunga ndoa na kuwa na familia. Wao hawakuacha kunitunza, lakini ziara zao hazikuweza kushinda hisia za kufiwa na za upweke. Ndipo mmoja wa wazee katika kundi letu akadokeza kuwa nijaribu upainia msaidizi. Nilisitasita lakini hatimaye nikaamua kuujaribu. Ni shangwe iliyoje! Nilihisi kwamba Yehova alikuwa ameniruhusu kuishi kufikia umri huu ili niweze kuonja upainia msaidizi. Tangu wakati huo nimekuwa painia msaidizi kila mwezi.”
7 Ndugu mmoja ambaye huuza maliasili alirekebisha ratiba yake ya kuonyesha nyumba ili awe na wakati wa utumishi wa upainia. Wengine pia wamerekebisha kazi zao ili wapate nafasi ya utendaji huo ulioongezeka.
8 Fanya Mipango Yako Sasa: Kwa nini usifanye mipango inayofaa sasa ili ufanye upainia msaidizi katika Machi na Aprili? Ili kufanikiwa, kupanga kwa uangalifu kunahitajika. Hilo ni wazi kutokana na maono ya wale walioweza kufanya upainia msaidizi hata ingawa walikuwa na madaraka ya familia, kazi za kimwili za wakati wote, na wajibu mwingine wa Kimaandiko. Zungumza na wengine ambao wamefanikiwa kupainia ili ufaidike na maono yao. Pia, mfikie Yehova kwa sala, ukiomba msaada wake.—Isa. 40:29-31; Yak. 1:5.
9 Bila shaka yoyote, wale wanaopanga mambo yao ili kutumika wakiwa mapainia wasaidizi hupata shangwe nyingi. Ikiwa tayari haumo katika utumishi wa wakati wote, je! ungeweza kufurahia pendeleo hilo? Ukijitahidi kupanua pendeleo lako la kushiriki habari njema na wengine, bila shaka Yehova atakumwagia baraka tele.—Mal. 3:10.