Ufunuo—Mafumbo Yafumbuliwa
1 Kitabu cha Ufunuo kimekuwa fumbo kwa muda mrefu. Kwa karne nyingi wanachuo wa Biblia walitafuta kufumbua siri zacho, ingawa kwa mafanikio madogo. Lakini habari iliyovuviwa kimungu katika Ufunuo haikukusudiwa iendelee kuwa siri milele. Hicho ni sehemu ya Neno la Mungu tunalohitaji kufahamu. (2 Tim. 3:16, 17) Kwa furaha, Mungu anafumbua Ufunuo huku unabii wacho mbalimbali wenye kusisimua ukitimizwa katika siku yetu. Kama vile Yehova alivyomtumia Yohana kuwasilisha njozi hizo kwa Wakristo wenzi, leo Yeye hutumia “mtumwa mwaminifu” ili kufunua maana ya unabii huo wenye kusisimua.—Mt. 24:45-47; Ufu. 1:1-3.
2 Toleo la Machi: Kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! kimeelimisha na kuwatia moyo sana watu wa Mungu. Lakini kwa nini kipendeze watu katika eneo lako? Ni kwa sababu kichapo hicho chenye kupendeza hushughulika na matukio ya kusisimua yanayotukia katika siku hizi za mwisho yanayoelezwa katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Je! watu wenye kufikiri hawapendezwi na wakati ujao kama ulivyofunuliwa na Mungu? Ingawa kitabu cha Biblia cha Ufunuo huonyesha hukumu za haki za Mungu, pia hicho hutoa ahadi za baraka nzuri ajabu za wakati ujao. (Ufu. 21:1-5) Kuelewa ujumbe wacho uliovuviwa hutusaidia kuelewa mahali tupo katika mkondo wa wakati na hukazia akilini mwetu umuhimu wa kufanya mapenzi ya Mungu.
3 Je! kitabu Upeo wa Ufunuo ni kigumu sana umma usikielewe? Kwa wazi, wengi hawakukiona kuwa kigumu sana kuelewa. Angalia machache tu ya maelezo mengi yaliyotolewa na wasomaji wa kitabu hicho. Mwanamume mmoja alisema: “Habari hii ni yenye nguvu. Lakini ni ya kupendeza. Mimi naipenda.” Mhubiri wa kanisa alisema: “Sijapata kamwe kuona wala kusoma kitabu kingine chenye kupendeza zaidi na cha kweli kuliko kitabu hiki!” Mtu mwingine aliyesoma kitabu hicho kwa muda usiozidi juma moja alisema: “Sasa nimepata kuelewa kabisa kweli. Ninataka kubadili maisha yangu yote.” Kwa wazi, wengi wanapata furaha wanaposoma kitabu cha Biblia cha Ufunuo na kukielewa kwa mara ya kwanza maishani mwao na kuanza kushika maneno yacho.
4 Pendekeza Upeo wa Ufunuo kwa
Wengine kwa Moyo Mweupe: Unapokuwa na mazungumzo ya Kimaandiko pamoja na wengine katika Machi, usisite kuwaonyesha wanaopendezwa kitabu Upeo wa Ufunuo. Watajie wale wanaotaka kukisoma kwamba wanaweza kutia alama sehemu za kitabu ambazo hawaelewi, na utakaporudi, utazungumza mambo hayo pamoja nao. Hiyo yaweza kuwa njia ya kujua kadiri ya kupendezwa kwao na uandae msingi wa kufanya rudio.
5 Zaidi ya kufanya utumishi wa nyumba kwa nyumba, wengi wamefanikiwa kukitoa kitabu Upeo wa Ufunuo kwa njia ya vivi hivi kwa watu wa ukoo, marafiki, na watu wanaofanya biashara nao. Taja jinsi umefaidika kibinafsi na kitabu hicho kutokana na vielezi vya waziwazi, chati zenye kusaidia, na misaada mingine mizuri ajabu ya kufundisha. Hilo laweza kuwatia moyo wengine wachunguze kitabu cha Ufunuo, ingawa huenda wakawa walihisi kuwa kinatia mambo mengi sana ndani kuweza kukielewa.
6 Jinsi tulivyopendelewa kuwa na maarifa ya matukio ya wakati ujao yakifunuliwa katika kitabu cha Ufunuo na kuelezwa kupitia mfereji wa Mungu leo! Tukiwa tumepewa maarifa hayo, tofauti na waandishi wa siku za Yesu na makasisi leo, acheni sisi tusikose kujulisha au kufumbua maana ya Neno la Mungu kwa wale watakaosikiliza. (Linganisha Luka 11:52.) Tufanyapo hivyo, inatumainiwa kwamba wengi zaidi wataitikia tumaini la uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu na kuungana nasi katika kufanya mapenzi ya Muumba wetu.—Ufu. 4:11.