Kutoa Utangulizi wa Kitabu Mankind’s Search for God
1 Wengi leo huhisi kwamba kupendelea kwao dini fulani ni jambo la kibinafsi. Hivyo, inaweza kuwa vigumu kuzungumza na majirani wetu kuhusu habari hiyo. Lakini sasa tuna kitabu Mankind’s Search for God, ambacho kimethibitika kuwa chenye msaada wa thamani katika kuwahubiria watu wa dini mbalimbali.
2 Wewe utasema nini ili uamshe kupendezwa kwa mwenye nyumba aweze kusoma kitabu hicho? Ni mambo gani au ni sehemu gani utakazokazia ambazo zitawavutia wale wanaodai kuwa Wakristo? wale wenye itikadi zisizo za Kikristo? au wale wasio na imani? Madokezo yafuatayo yatatusaidia tuwe tayari kuonyesha majirani wetu uhitaji wa ‘kumtafuta Yehova’ na ‘kumwita maadamu yu karibu.’ (Isa. 55:6) Madokezo haya yanaweza kufanywa yafae hali za kwenu.
3 Kwa Nini Tuchunguze Yale Tutakayosema?: Kwa kuwa wengi wanadai kuwa wametosheka na dini zao na hawataki kuzibadili, huenda tukahitaji kutunga utangulizi wetu ili kumsaidia mwenye nyumba achunguze kwa akili iliyofunguka yale tunayosema.
4 Baada ya salamu inayofaa, ungeweza kusema:
◼ “Katika kuzungumza kwetu na majirani wetu, tunapata kwamba watu wengi wametosheka na dini zao na hawataki kuzibadili. Lakini ikiwa watu wangechukua wakati kuchunguza itikadi za wengine, je! unafikiri hilo lingeongoza kwenye kuelewana zaidi na kupunguza chuki ulimwenguni? [Ruhusu itikio la mwenye nyumba.] Ona yale ambayo Biblia husema kuhusu wale wanaompenda Mungu na jinsi wanavyopaswa kuhisi juu ya wengine.” Baada ya kusoma Matendo 17:26, 27, vuta fikira kwenye mafungu 15 na 16 katika ukurasa wa 10 wa kitabu Mankind’s Search for God.
5 Wengi wamepata kwamba kufungua kitabu hicho kwenye sura fulani inayozungumzia dini ya mwenye nyumba kutavuta fikira zake. Ona jinsi hilo linavyoweza kufanywa.
6 Baada ya kujijulisha mwenyewe, huenda ukasema:
◼ “Kukiwa na dini nyingi sana leo, je! umepata kujiuliza jinsi tunavyoweza kutambua kama dini yetu inakubaliwa na Mungu?” Baada ya mwenye nyumba kujibu, elekeza fikira zake kwenye kisanduku kwenye ukurasa wa 377 wa kitabu Mankind’s Search for God, kinachoonyesha njia kumi za kutambua dini ya kweli, ukikazia hasa jambo la 7. Uliza mwenye nyumba kama anakubali kwamba mtu anayejizoeza dini ya kweli apaswa ahisi hivyo kuhusu watu wa jamii na mataifa mengineyo. Ikiwa wakati unaruhusu, angalieni maandiko matatu yaliyoonyeshwa. Halafu malizia kwa kusema kwamba zile sababu nyingine tisa zilizotolewa zina utegemezo uo huo wa Kimaandiko.
7 Mambo Mengine ya Kusaidia: Faharisi ya habari inayotia mengi ndani iliyo kwenye mwisho wa kitabu hicho yaweza pia kutumiwa. Kwa mfano, namna gani ikiwa watu wengi katika eneo wanahisi kwamba dini zote ni njia tofauti tu zinazoongoza kwa Mungu? Basi tazama chini ya kichwa “Dini” mahali ambapo kuna kichwa kidogo “‘dini zote sawa’: 12.” Hilo laonyesha jinsi faharisi iwezavyo kutusaidia kupata mambo ya kuzungumzia. Tunapozungumza na wale wasioamini kuwako kwa Mungu, tunaweza kuwaonyesha fungu la 1 na 2 kwenye ukurasa 329, linalozungumzia kutokuamini kwa ki-siku-hizi. Huenda “Maswali [matano] Yanayotaka Jibu” kwenye kurasa 17-18 yakawapendeza hasa wale walio na shaka kama Biblia hufundisha yale ambayo dini nyingi huhubiri.
8 Kwa kutumia viunganishi vyenye matokeo ili kutoa utangulizi wa kitabu Mankind’s Search for God, huenda tukaweza kusaidia watu tunaozungumza nao wamtafute-tafute Mungu mmoja wa kweli, Yehova.