Endelea Kutazama, Endelea Kusonga Mbele Pamoja na Yehova
“Neno langu, litokalo katika kinywa changu . . . litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isa. 55:11.
1. Tuna msingi gani wa kuwa na hakika kwamba Yehova atatimiza makusudi yake?
BILA shaka, sikuzote Yehova analetea makusudi yake matokeo mazuri. Neno lake, na pia historia ya wanadamu, inashuhudia Yehova amefanya hivyo nyakati zilizopita, likituhakikishia kuendelea kwake kupendezwa na kutimiza unabii wa Ufalme na ahadi iliyofanywa katika Edeni. Na lazima tuendelee kutazama mbele sikuzote kama Yehova afanyavyo. Unabii mwingi ambao haujatimizwa bado unatupa sababu nyingi zenye nguvu za kutazama mbele.
2. Tumegawiwa kazi gani ya maana sana, nasi tunao msaada wa nani katika kuitimiza?
2 Walakini, si kwamba tu tunataka kuendelea kutazama mbele pamoja na Yehova Mungu bali pia tunataka tuendelee kusonga mbele pamoja naye, kwa maana yeye ana kazi nyingi ya kufanywa na watumishi wake duniani. Sehemu ya kazi hiyo ni kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu ili watu waweze kujitambulisha kama wanauunga mkono au wanaupinga. (Mt. 24:14; 25:31-46) Kama vile Ufunuo 14:6, 7 unavyoonyesha, mzigo wa kazi hii ya kuhubiri hauko juu ya mabega ya watumishi wa Mungu wa kidunia peke yao; wanao msaada wa majeshi ya kimalaika, katika kuongoza mambo na pia katika kuyasimamia kwa werevu.
3. Tuna wajibu gani juu ya waamini wenzetu?
3 Tukiwa wafuasi wa kweli wa Kristo, walioagizwa kuendesha utendaji huu, lazima tuwe waaminifu na wa kweli mtu na mwenzake. Tunataka tuwe wenye msaada kama tunavyoweza mtu na mwenzake, kwa maana tuna wajibu mkubwa zaidi kuhudumiana kuliko kuhudumia wale walioko nje. “Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Gal. 6:10) Nani ajuaye tutapata nafasi inayofaa ya kufanya hivyo muda mrefu namna gani? Kwa hiyo na tufanyiane mema yote tunayoweza kabla hali mbaya sana za uchumi au mateso makali hayajazuia jitihada zetu. Halafu, nyakati zenye magumu zikitupata, tutakuwa na nia inayohitajiwa kuendelea kusaidiana na kutiana moyo. Kwa hiyo na tuwe wenye nia ya kuchukuliana udhaifu na makosa. Badala ya kuwa wenye kukasirika-kasirika kwa sababu ya mambo madogo madogo na kulalama, na tuwe wenye nia ya kutaabikia haki, kutaabikia amani katika kundi. Ndiyo, “ndugu, msinung’unikiane, msije mkahukumiwa,” vikali.—Yak. 5:9.
NI JAMBO GANI LILILOKO MBELE KARIBUNI SANA?
4, 5. (a) Ni mambo gani yaliyoko mbele yetu? (b) Tunaweza kuwa na uhakika wa nini juu ya “dhiki kubwa”?
4 Kati ya mambo yaliyoko mbele karibuni sana ni kufikilizwa kwa hukumu za Mungu juu ya ‘Babeli Mkuu,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. (Ufu. 17:15-18) Hii itaonyesha mwanzo wa “dhiki kubwa.” (Mt. 24:21) Wafuasi wa kweli wa nyayo za Yesu Kristo na wenzi wao wataiokoka. Halafu? Shetani na majeshi yake, wakijulikana kwa mfano wa Gogu wa Magogu, watashambulia watu wa Mungu, wakionea kijicho amani yao na ufanisi. Hiki kitakuwa kionyesho kwa majeshi ya kimbinguni yakiwa chini ya Yesu Kristo yaendee majeshi ya Ibilisi yanayoonekana kupigana nayo, hii ikionyesha mwanzo wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16) Pigano hilo litakuwa na vita ya ndugu na ndugu wakiuana, magonjwa ya kipuku (yenye kuambukia watu wengi sana), mawe ya mvua ya barafu, umeme, moto na kiberiti, mawimbi yenye nguvu ya bahari kuu na matetemeko ya dunia, yote yakiwa ya kushuhudia enzi kuu ya haki ya Yehova Mungu.—Ezek. 38:14-23.
5 Hata kutokee nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakomboa watu wake. Kwa hiyo maadamu tunamjua Yehova Mungu kwa kweli na kumtumikia bila choyo hatutakuwa na sababu ya kuogopa. Kama jamii tutaiokoka “dhiki kubwa,” tuwe msingi wa dunia mpya.
6. Kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba kipindi cha “dhiki kubwa” kitakuwa wakati wetu wa kufurahi, na hii ituhusuje hata sasa?
6 Jambo jingine tunaloweza kuwa na hakika nalo ni kwamba kipindi cha “dhiki kubwa,” siku ya Yehova, kitakuwa wakati wa kufurahi. Fikiria shukrani ambayo bila shaka Nuhu na jamaa yake walikuwa nayo kwa njia ya Yehova ya wokovu mvua ilipoanza kunya; fikiria furaha ambayo bila shaka Waisraeli waliona walipokuwa wanaokoka upande mwingine wa Bahari ya Shamu kisha wakaona Farao na jeshi lake wakimezwa katika bahari hiyo. Vita ya Mungu katika Har–Magedoni itakuwa kubwa ajabu zaidi kuliko matendo hayo makuu ya Yehova ya kuokoa yalivyokuwa. Kweli, “dhiki kubwa” itakuwa yenye kuogofya nayo itafuatana na magumu fulani. Lakini watumishi wa Mungu watasisimka kushuhudia kile ambacho wamekuwa wakitangaza na kutazamia kwa miaka mingi. Kitakuwa kitu cha kukumbuka kwa furaha na uradhi kweli kweli kwa wale watakaofufuliwa kwa wafu. Kufikiri kwenyewe juu ya jambo hili kumepaswa kuchochee bidii yetu kujulisha siku ya Yehova inayokaribia mbio mbio.
KUINGIA KATIKA DUNIA ILIYOSAFISHWA
7. (a) Wanadamu watabarikiwa kwa kuwa na wazazi wa namna gani? (b) Ni wanaume wa namna gani watakaowakilisha watawala wa kimbinguni, kwa matokeo gani?
7 Lo! itakuwa furaha namna gani kuingia katika dunia itakayosafishwa baada ya “dhiki kubwa” na kuona mwanzo wa utawala wa miaka elfu wa Kristo na bibi-arusi wake ambaye ni wanaume na wanawake 144,000 walionunuliwa duniani! Watakuwa wakielekeza fikira zao kwa wanadamu, wakiwa na kusudi la kukuza jamaa kubwa ya wana na mabinti wakamilifu. Lo! namna hawa watakavyokuwa wazazi wenye upendo! Wataanza kazi zao za wazazi wakiongozwa na upendo na huruma, watatoa uongozi na msaada unaohitajiwa ili waokokaji wa dhiki washinde udhaifu wao mbalimbali na kutokamilika. Halafu, baada ya Yesu Kristo kufufua wafu, bibi-arusi atafanya kazi pamoja naye kusaidia watakaofufuliwa waanze kuelekea kwenye ukamilifu. Hema ya Yehova Mungu itakuwa pamoja na wanadamu kupitia kwa yale ambayo Kristo na bibi-arusi wake watakuwa wakiwafanyia. (Ufu. 21:1-4) Watawakilishwa duniani na wanaume waaminifu wakiwa wakuu. (Zab. 45:16) Wakuu hawa hawatakuwa kama wanasiasa wapotovu wenye kujitafutia faida zao wenyewe ambao wametawala watu kwa karne nyingi. Bali, watakuwa kama wale ambao Musa aliambiwa achague: “Watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu.” (Kut. 18:21) Hawa watatoa usimamizi wenye upendo, pamoja na usalama na starehe kwa wote.—Isa. 32:1, 2.
8. Tunaweza kutazamia hali gani katika taratibu mpya ya Mungu, na kwa sababu gani?
8 Baada ya ulimwengu usiomwogopa Mungu kuharibiwa na baada ya Shetani na mashetani wake kutiwa katika shimo refu lisilopimika, hakutakuwa na uovu tena, hakutakuwa na dini ya uongo tena, hakutakuwa na matendo ya kishetani tena. ‘Hakuna atakayedhuru wala kuharibu katika mlima wa Mungu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua Yehova, kama vile maji yanavyoifunika bahari.’ (Isa. 11:9) Si kwamba tu kutakuwa na amani kati ya mataifa yote na makabila yote, bali pia kutakuwa na amani kati ya wanadamu na viumbe vingine vya dunia: “Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; . . . nami nitawalalisha salama salimini.” Wanadamu watatumia utawala wenye upendo; wanadamu hawataogopa wanyama, nao wanyama hawataogopa wanadamu kwa njia isiyofaa. Dunia yote itaonyesha utukufu wa Muumba wake, ambaye ndiye “Mungu wa amani,” na itaonyesha utukufu wa Yesu Kristo, ambaye ndiye “Mfalme wa amani.”—Hos. 2:18; Rum. 16:20; Isa. 9:6.
TUMAINI LA UFUFUO
9. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba wafu watafufuliwa?
9 Tunaweza pia kutazamia kufufuliwa kwa wafu tukiwa na uhakika kabisa. Kwa sababu gani? Kwa sababu Mungu ametupa ahadi nyingi juu ya jambo hilo, naye hawezi kusema uongo. (Tito 1:2) Zaidi ya hayo amewapa wanadamu wote uhakikisho kamili juu yake kwa maana alimfufua Yesu kwa wafu. (Matendo 17:31) Kuna uhakika mwingi sana kwamba kutakuwa na ufufuo hata Yehova anawahesabu wafu kama kwamba wako hai hasa, kama vile Yesu alivyowaambia Masadukayo wa siku zake wenye mashaka.—Mt. 22:31, 32.
10. Ni nini kitakachofufuliwa, na kutoka wapi?
10 Ni nini kitakachofufuliwa? Si mwili uliokufa, kwa maana umerudishwa mavumbini na pengine ulikwisha ingia katika vitu vingine vilivyo hai. Kama vile mtume Paulo anavyoonyesha: “Uipandayo haihuiki, isipokufa; nayo uipandayo, huupandi mwili ule utakaokuwa, ila chembe tupu,” naye “Mungu huipa mwili kama apendavyo.” (1 Kor. 15:35-38) Ndiyo, kitakachofufuliwa kutoka kaburini, Sheol au Hades si mwili wenye chembe zile zile, bali nafsi kama ilivyosemwa mapema kwa unabii juu ya Yesu: “Kwa sababu hutaachia Hadeze nafsi yangu.”—Zab. 16:10; Matendo 2:24-27, Swahili Congo Bible.
11. (a) Ufufuo wa kwanza ni nini? (b) Ni nani wanaoushiriki, na wakati gani?
11 Nafsi au mtu atakayefufuliwa atakuwa na mwili wa namna gani? Wale watakaoshiriki ufufuo wa kwanza watakuwa na mwili mtukufu, wa kimungu na usioharibika. Ufufuo wa kwanza ni wa kwanza kwa wakati, umuhimu na ubora, nao ni wa wafuasi wa nyayo za Kristo, waliotiwa mafuta, wale 144,000 walioonyeshwa wamesimama juu ya Mlima Sayuni. (Ufu. 20:4, 6; 14:1, 3) Kwa habari ya kufufuliwa kwa watiwa mafuta wanaolala wakati wa kuwapo kwa Bwana, tunasoma hivi: “Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.” (1 The. 4:16) Paulo anaendelea kusema hivi juu ya mabaki ya kikundi hiki wanaokufa baada ya ufufuo huo: “Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.” (1 The. 4:17; Ufu. 14:13) Kama inavyoonyeshwa katika 1 Wakorintho 15:51, 52, hii maana yake ni kwamba hawalali katika mauti, bali wanafufuliwa mara moja na kupewa uzima wa kimbinguni na kuunganishwa na Bwana Yesu Kristo katika mbingu zisizoonekana.
12. Ni nani wengine watakaofufuliwa, na ufufuo wa wengine kati yao unaweza kutazamiwa wakati gani?
12 Namna gani juu ya wanadamu wengine waliokufa? Mtume Paulo alihakikisha kwamba “kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” Vivyo hivyo, Yesu alisema kwa unabii kwamba “wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake” na kutoka. Tena, tunaambiwa kwamba “Mauti na Hadeze” vitatoa wafu wote waliomo ndani yavyo. Kati ya hawa atakuwamo mtenda mabaya mwenye huruma aliyetundikwa kando ya Yesu ambaye Yesu alimwambia hivi: “Kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29; Ufu. 20:13, Swahili Congo Bible; Luka 23:42, 43, NW) Kwa kuwa inaelekea wanaume waaminifu kuanzia kwa Habili mpaka kwa Yohana Mbatizaji watapewa mgawo wa kuwa wajumbe wa Ufalme huo, inaelekea watakuwa kati ya watakaofufuliwa kwanza. (Zab. 45:16) Wo wote kati ya wale ambao wametimiza matakwa ya Mungu ya kuokoka “dhiki kubwa” lakini ambao wamekufa au ambao bado huenda wakafa kabla ya tukio hilo bila shaka wao pia watafufuliwa mapema wakati wa utawala wa miaka elfu. Hili lingekuwa jambo la akili, kwa maana watu hao wangeweza kusaidia sana kuelimisha wasio haki wengi watakaofufuliwa.
13. Wanadamu waliokufa watafufuliwa wakiwa na hali gani?
13 Namna gani wale watakaofufuliwa waishi duniani? Watakuwa na miili ya namna gani? Watakuwa na sura gani? Bila shaka watafanana sana na walivyokuwa kabla hawajakufa ili waweze kujijua na kujulikana na wengine. (Yohana 11:39-44) Mtu mrefu hatarudi akiwa mtu mfupi, wala mtu mzee sana hatarudi akionekana kama kijana. Wanaume watakuwa wanaume, na wanawake, wanawake. Watakuwa na nyutu zao zile zile na kumbukumbu ile ile. Kama vile ilivyokuwa kwa waliofufuliwa zamani, ndivyo watakaofufuliwa watakavyokuwa na miili kamili isiyo na upungufu. Hawatarudi wakiwa na hali ya ugonjwa-ugonjwa iliyofanya wafe. Lakini hii haimaanishi kwamba watakuwa na miili mikamilifu, kwa maana hiyo isingepatana na nyutu zao zisizo kamilifu. Bali, watatokea wakiwa na miili isiyokamilika na miili yao itazidi kukaribia ukamilifu wakati wote wanapofanya maendeleo ya kiroho, wakishinda udhaifu wao mbali-mbali na kutokamilika kwao kwa kutii utawala wa Ufalme na kupokea faida zenye kulipia dhambi za dhabihu ya Yesu.
14, 15. (a) Kufufuliwa kwa wafu ni wonyesho wa nini kwa upande wa Mungu, kulingana na maneno ya nani? (b) Yesu ataonaje juu ya kufufua wafu?
14 Mpango wa ufufuo ni wonyesho wa upendo kwa upande wa Yehova Mungu, kama inavyoonekana kutokana na maneno ya Ayubu mwenye saburi na mwaminifu: “Mtu akikufa, ataishi tena? . . . Wewe utaita, nami nitakujibu, utakuwa na hamu kwa kazi ya mikono yako.” Ndiyo, Yehova Mungu ana hamu kwa wale waliomo Sheol au Hades, zaidi kwa wale waliohakikisha ukamilifu wao kwake wakiwa katika majaribu makali kama Ayubu.—Ayubu 14:14, 15, Swahili Congo Bible.
15 Na kwa kweli kufufuliwa kwa mamilioni yasiyohesabika kutamfurahisha sana Yesu Kristo pia. Linaloonyesha Yesu ni mwenye nia na anafurahia kufanyia wanadamu hivi ni itikio lake kwa mwenye ukoma aliyemjia wakati mmoja, akamwambia hivi kwa imani: “Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa.” Naye Yesu akamwambia nini? “Nataka; takasika. Na mara ukoma wake ukamwondoka.”—Luka 5:12, 13.
16. Kutazamia ufufuo kwa imani kunaweza kutusaidiaje hata sasa?
16 Kwa kweli ufufuo pia ni jambo la kutazamiwa nasi kwa hamu nyingi na furaha. Tukifanya hivyo kwa imani tunaweza kutiwa moyo kweli kweli na kujipatia baraka pamoja na wanadamu wenzetu hata sasa. Wapendwa wakifa, hatutapatwa na huzuni na masikitiko ya kupita kadiri ya wale wasio na tumaini. (1 The. 4:13, 14) Tutaweza kufariji wenye kuomboleza kwa unyofu. (2 Kor. 1:3, 4) Kwa kuwa tunalo tumaini la ufufuo, tunayo hakika ya kwamba hata wanadamu wakituua, hawawezi kutufuta katika kumbukumbu ya Mungu watuzuie tusifufuliwe kwa wafu. (Mt. 10:28) Hii inatutia nguvu tuendelee kuwa waaminifu kwa Yehova Mungu hata wanadamu wawe wanaweza kutufanyia nini.—Ufu. 2:10; 12:11.
17. Uwezekano wa kupoteza thawabu ya uzima umepaswa uwe na matokeo gani juu yetu?
17 Jambo jingine linalotuchochea tuwe waaminifu ni uhakika wa kwamba kunao uwezekano wa kupoteza thawabu ya uzima. (Linganisha 2 Timotheo 4:8.) Biblia inaonyesha wazi kwamba wazoeao dhambi kwa makusudi—wale ambao wanaitenda roho ya Mungu dhambi—hawatafufuliwa kwa wafu. (Mt. 12:31, 32; Ebr. 10:26, 27) Bila shaka hii imepaswa itutie moyo tufuate mfano wa mtume Paulo kwa kujitahidi tuendeleze uaminifu. Paulo alisema hivi kwa habari yake mwenyewe: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” (1 Kor. 9:27) Ndiyo, tusiisahau kamwe thawabu ya uzima na kukosa kujitahidi kwa kushikamana na Yehova Mungu kwa uaminifu.
ENDELEA KUTAZAMA, ENDELEA KUSONGA MBELE
18. Kwa kuwa tuko mbioni, imetupasa tujichukueje?
18 Kwa kweli tuna mengi ya kutazamia. Matumaini ni maangavu kweli kweli, si wakati ujao ulio karibu sana tu bali pia miaka elfu moja iliyoko mbele! Mwendo wetu umefananishwa na mbio na inaweza kusemwa kwamba tuko katika sehemu ya mwisho ya kumalizia mbio. Mbio inaleta maoni gani? Je! haileti maoni ya kwamba imempasa mtu ajitahidi sana na kujikaza afikie mradi ule wa kushinda mbio hiyo? Kwa kweli, lili hili ndilo tunaloombwa tufanye: “Na tuweke kando kila mzigo mzito [uwe ni kutafuta mali za kimwili au maelekeo yenye dhambi ya mwili], na dhambi ile ituzingayo kwa upesi [kupoteza imani]; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu [kwa kumkazia macho sana].”—Ebr. 12:1, 2.
19. Yesu aliwapa wafuasi wake shauri gani awasaidie waepuke kunaswa mtegoni na kupoteza thawabu?
19 Ndiyo, Yesu alituwekea mfano naye anatushauri ‘tuendelee kutafuta ufalme kwanza na haki yake.’ (Mt. 6:33) Yesu alionya pia juu ya wakati uu huu wa mwisho katika unabii wake mkuu: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; . . . Kesheni.”—Luka 21:34-36.
20. Nia yetu juu ya ulimwengu imepaswa iwe nini?
20 Kwa kweli mwendo wa hekima kwetu ni kukaza fikira juu ya kitu ambacho tunaishi kwa ajili yake. Tunajua kwamba hizi ndizo “siku za mwisho,” na kwa hiyo shauri la Paulo linatumika kwetu hata zaidi kuliko wakati alipolitoa mara ya kwanza: “Muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale . . . wautumiao ulimwengu [wawe] kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.” (1 Kor. 7:29-31) Sababu gani tutumie ulimwengu sana, tukiuacha uwe jambo tunaloshughulikia zaidi sana katika maisha zetu, kana kwamba haitupasi kukosa cho chote ulio nacho, na kufanya hivyo kwa kupoteza hali yetu ya kiroho? Badala yake, na tukumbuke kwamba ‘ulimwengu unapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.’ Hiyo ni ahadi nzuri sana kama nini! Je! tunaonyesha kwamba kweli sisi tunaiamini kwa kutenda kabisa kulingana na inavyosema, tukiweka maisha yetu yote juu ya uhusiano wetu na Mungu na kutoacha uhusiano mwingine wo wote au anasa iwe na ubora usioipasa?—1 Yohana 2:17.
21. Nia yetu imepaswa iwe nini juu ya kufurahia vitu vya kimwili sasa, na kwa sababu gani?
21 Kwa sababu gani tunaswe katika kutafuta mali za kimwili? Katika mmoja wa mifano yake, Yesu alituonya tusiwe na nia hiyo, akisema hivi: “Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.” (Luka 12:16-21) Zaidi ya hayo, je! Yesu hakuahidi kwamba tukiendelea kutafuta kwanza ufalme wa Mungu na haki yake Mungu atatupa mahitaji yetu ya kimwili? (Mt. 6:33) Wala haitupasi tuhangaikie isivyofaa vitu vya kimwili tutakavyokuwa navyo katika taratibu mpya ya mambo. Kama vitu hivyo vingalikuwa vya maana, Yehova angalikuwa ameviandika katika Neno lake. Tunajua kwamba vitu vya kimwili wala hata wingi wa anasa sio unaofurahisha watu leo. Watu wenye furaha zaidi duniani ni watu wa Yehova nao hasa wamo kati ya maskini kwa habari ya vitu ambavyo ulimwengu unathamini sana. Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika taratibu mpya ya mambo hatutakosa kitu cho chote cha kimwili. Na la maana zaidi ni kwamba tutakuwa na baraka nyingi sana za kiroho na urafiki bora wa waabudu wenzetu wa Mungu mmoja aliye wa kweli Yehova, na wote watakuwa wakionyesha matunda ya roho yake.—Zab. 133:1; Gal. 5:22, 23; 1 Tim. 6:17.
22. Sisi mmoja mmoja tunaweza kusonga mbele na Yehova kwa njia gani na katika pande gani?
22 Mpaka wakati huo tunazo nafasi nzuri za kuendelea kusonga mbele kwa kuzidisha uhusiano wetu na Yehova, kukuza upendo kwa wale tunaohusiana katika imani na kupatanisha maisha zetu zaidi na mapenzi ya Mungu. Funzo letu la kipekee na sala, kuhudhuria katika mikutano ya kundi na kutumia kwa bidii mambo tunayojifunza vinasaidia sana kutuletea maendeleo ya kiroho. Kwa kutumia mipango ya Yehova tuendelee kukua kiroho, si kwamba tu tutaendeleza imani yetu kuwa yenye nguvu bali pia tutachochewa kutumia vizuri nafasi zetu kusaidia wengine wawe na tumaini lililotolewa na Mungu na kuishi kupatana nalo. Maendeleo tunayofanya sasa yatatupa mwanzo mzuri katika kusitawisha nia inayohitajiwa kukua mpaka kufikia ukamilifu wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo na bibi-arusi wake. Kwa hiyo na tuendelee kusonga mbele.
23. Paulo alitoa uhakikisho gani katika Waebrania 6:10, 11, kwa sababu ya mambo gani ya hakika?
23 Yehova atatimiza mambo ambayo amekusudia na kuahidi. Neno lake halitamrudia bila matokeo. Hakuna shaka juu ya jambo hili. Kama vile mtume Paulo anavyotuhakikishia, Mungu si dhalimu na kwa hiyo hatasahau mambo yote ambayo ‘tulifanya kwa kupenda jina lake.’ Kwa hiyo na tuendelee kuonyesha “kupendezwa kule kule kwenye shauku, mpaka tumaini [letu] litakapotimizwa mwishowe.”—Ebr. 6:10, 11, New English Bible.
—Kutoka The Watchtower, Feb. 1, 1975.