Si Wachuuzi wa Neno la Mungu
“TULIKUWA tukiuza huduma yetu ili kupata pesa.” Hayo ni maneno ya mmoja aliyekuwa “mhudumu wa sala za simu” aliyehojiwa katika ripoti ya uchunguzi wa waevanjeli wa televisheni wa Amerika mwisho-mwisho wa 1991.
Programu hiyo ilikazia huduma tatu za uenezaji evanjeli kupitia televisheni katika United States. Ilifunua kwamba watu walipunjwa kwa kupokonywa makumi ya mamilioni ya dola kila mwaka na huduma hizo tatu tu. “Huduma” moja ilisimuliwa kuwa “kiwanda cha shughuli ya upaji chenye usitawi wa kiwango cha juu.” Zote zilikuwa zimehusika katika upunjaji mwingi. Je! hilo lakushangaza?
Dini Inachunguzwa kwa Uangalifu
Si waevanjeli wa televisheni tu bali hata dini za kawaida, zisizopendelea upande wowote zinachunguzwa kwa uangalifu na serikali, mashirika ya upelelezi ya kibinafsi, na watu kwa ujumla. Katika visa fulani hisa za kanisa, masilahi ya kisiasa zinazotegemezwa kifedha na dini, na maisha ya anasa ya makasisi wenye kulipwa mishahara ya juu yametokeza maswali juu ya ufaaji wa hilo.
Baadhi ya viongozi wa kidini hulinganaje na ule usimulizi ufaao wa huduma ya Kikristo uliotolewa na mtume Paulo karibu miaka 2,000 iliyopita? Aliandika hivi: “Sisi si kama walio wengi, walighoshio [wachuuzi wa, NW] neno la Mungu; bali kama kwa weupe wa moyo, kama kutoka kwa Mungu, mbele za Mungu, twanena katika Kristo.” (2 Wakorintho 2:17) Ni nani wafaao ufafanuzi huo leo?
Ili usaidiwe kukadiria mambo, acheni tutazame kwa ukaribu zaidi jinsi huduma ya Kikristo ya Paulo na wenzake ilivyotegemezwa kifedha. Ilikuwa tofauti katika njia gani na huduma nyinginezo za siku yake?
Wahubiri Wasafirio wa Karne ya Kwanza
Akiwa mhubiri mwenye kusafiri, Paulo hakuwa wa pekee. Katika siku hiyo wengi walisafiri ili kueneza maoni yao juu ya dini na falsafa. Mwandishi wa Biblia Luka asema juu ya “Wayahudi kadhaa wenye kupunga pepo wabaya, walisafiri huko na huko.” (Matendo 19:13, Habari Njema kwa Watu Wote) Yesu Kristo alipowashutumu Mafarisayo, aliongeza hivi: “Mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu.” (Mathayo 23:15) Yesu mwenyewe alikuwa mhudumu mwenye kusafiri. Aliwazoeza mitume na wanafunzi wake wamwige kwa kuhubiri si katika Yudea na Samaria peke yake bali “mfikio wa mbali zaidi wa dunia.”—Matendo 1:8, NW.
Katika safari zao, wafuasi wa Yesu walikutana na wahubiri wasio-Wayahudi. Katika Athene, Paulo aligongana na wanafalsafa Waepikureo na Wastoiko. (Matendo 17:18) Kotekote katika Milki ya Roma, Wasiniki walijaribu kuwavuta watu kwa hotuba za peupe. Wafuasi wa Isisi na Serapisi walieneza uvutano wao juu ya wanawake na watumwa wakiwa na ahadi za kuwa na usawa wa kidini na wa kijamii na wanaume huru. Madhehebu ya uzazi ya Mashariki yaliandaa chanzo cha dini nyingi za kifumbo za Kigiriki na Kiroma. Ahadi ya kufunikiwa dhambi na tamaa ya kushiriki siri za kimungu iliwavutia wafuasi kwa vile viabudiwa bandia Demeta, Dionisio, na Sibele.
Gharama Zililipwaje?
Hata hivyo, kusafiri kuligharimu pesa nyingi. Zaidi ya nauli za mizigo, ada, na nauli za kusafiri kwa meli, wasafiri walihitaji chakula, mahali pa kukaa, kuni, nguo, na utunzaji wa afya. Wahubiri, walimu, wanafalsafa, na wanadini za kifumbo walitosheleza mahitaji yao katika njia tano kuu. (1) Walifundisha ili kupata mishahara; (2) walifanya kazi za kuajiriwa wakifanya kazi za utumishi na ufundi mbalimbali; (3) walikubali ukaribishaji-wageni na upaji wa hiari; (4) walijishikamanisha na wafadhili matajiri, mara nyingi wakiwa wafunzi; na (5) waliomba-omba. Akijitayarisha mwenyewe kwa ajili ya majibu makali, Diogenes, Msiniki mmoja aliyekuwa mwombaji maarufu aliomba msaada hata kutoka kwa sanamu zisizo na uhai.
Paulo alijua juu ya wahubiri fulani waliodai kuwa wahudumu Wakristo lakini, kama vile wanafalsafa Wagiriki wengine, wao walifanya urafiki na matajiri na waliwanyang’anya maskini. Alikaripia kundi katika Korintho, akisema: “Mnamvumilia hata mtu . . . mwenye kuwanyonya, mwenye kuwakandamiza [anayenyang’anya mlicho nacho, NW].” (2 Wakorintho 11:20, HNWW) Yesu Kristo hakunyang’anya kamwe chochote, wala Paulo na wafanyakazi wenzake. Lakini waevanjeli wenye pupa Wakorintho walikuwa “mitume wa uongo, watendao kazi kwa hila,” na wahudumu wa Shetani.—2 Wakorintho 11:13-15.
Maagizo ya Yesu kwa wanafunzi wake yalipinga kufundisha ili kupata mshahara. “Mmepata bure, toeni bure,” akashauri. (Mathayo 10:8) Ingawa kuomba-omba kulikuwa jambo la kawaida, kulidharauliwa siku hizo. Katika kimoja cha vielezi vyake, Yesu aonyesha mtumishi mmoja akisema, “Kuomba, naona haya.” (Luka 16:3) Kwa hiyo, hatupati kamwe katika masimulizi ya Biblia wanafunzi waaminifu wa Yesu wakiomba-omba pesa au vifaa. Waliishi kwa ile kanuni: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi asile chakula.”—2 Wathesalonike 3:10.
Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake watunze mahitaji yao katika njia mbili. Kwanza, kama vile Paulo alivyosema, wangeweza ‘kupata riziki kutokana na habari njema.’ Kwa jinsi gani? Kwa kukubali ukaribishaji-wageni unaotolewa kwa kupenda. (1 Wakorintho 9:14, HNWW; Luka 10:7) Pili, wangeweza kujiandalia wenyewe kimwili.—Luka 22:36.
Kanuni Zilizotumiwa na Paulo
Paulo alitumiaje kanuni hizo ambazo zimetangulia kutajwa? Kwa habari ya safari ya pili ya mishonari ya mtume huyo, Luka aliandika hivi: “Tukang’oa nanga kutoka Troa, tukafika Samothrake kwa tanga moja, na siku ya pili tukafika Neapoli; na kutoka hapo tukafika Filipi, mji wa Makedonia, mji ulio mkuu katika jimbo lile, mahali walipohamia Warumi; tukawa katika mji huu, tukikaa siku kadha wa kadha.” Wao wenyewe walishughulikia kusafiri kote, chakula, na mahali pa kukaa kulikohitajiwa.—Matendo 16:11, 12.
Hatimaye, mwanamke mmoja aitwaye Lidia alikubali “maneno yaliyonenwa na Paulo. Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake, akatusihi akisema, Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana [Yehova, NW] ingieni nyumbani mwangu mkakae, Akatushurutisha.” (Matendo 16:13-15) Labda angalau kwa sehemu kwa sababu ya ukaribishaji-wageni wa Lidia, Paulo angeweza kuwaandikia waamini wenzake katika Filipi hivi: “Namshukuru Mungu wangu kila niwakumbukapo, sikuzote kila niwaombeapo ninyi nyote nikisema sala zangu kwa furaha, kwa sababu ya ushirika wenu katika kuieneza Injili, tangu siku ile ya kwanza hata leo hivi.”—Wafilipi 1:3-5.
Luka ataja visa vingi vya watu wakiwakaribisha wafanyakazi Wakristo hao wenye kusafiri. (Matendo 16:33, 34; 17:7; 21:7, 8, 16; 28:2, 7, 10, 14) Katika barua zake zenye kupuliziwa, Paulo alithamini na kutoa shukrani kwa ajili ya ukaribishaji-wageni na zawadi ambazo alikuwa amepokea. (Warumi 16:23; 2 Wakorintho 11:9; Wagalatia 4:13, 14; Wafilipi 4:15-18) Hata hivyo, wala yeye wala wenzake hawakutoa kidokezo kwamba walipaswa wapewe zawadi au utegemezo wa kifedha. Mashahidi wa Yehova wanaweza kusema kwamba mtazamo huo mzuri huonwa bado miongoni mwa waangalizi wasafirio.
Hakutegemea Ukaribishaji-Wageni
Paulo hakutegemea ukaribishaji-wageni. Alikuwa amejifunza ufundi uliohitaji kazi ngumu na muda wa saa nyingi lakini ambao ulichuma mshahara wa chini. Wakati mtume huyo alipowasili Korintho akiwa mishonari, “a[li]mwona Myahudi mmoja, jina lake Akila, . . . na Prisila mkewe. . . . naye akafikilia kwao; na kwa kuwa kazi yao ya ufundi ilikuwa moja, akakaa kwao, wakafanya kazi pamoja, kwa maana walikuwa mafundi wa kushona hema.”—Matendo 18:1-3.
Baadaye, katika Efeso, Paulo alikuwa bado akifanya kazi kwa bidii. (Linganisha Matendo 20:34; 1 Wakorintho 4:11, 12.) Huenda ikawa alikuwa na ustadi maalumu wa kufanya kazi na cilicium, yale manyoya ya mbuzi, yasiyo laini, ya kutengenezea hema yaliyotoka eneo la nyumbani kwake. Twaweza kuwazia Paulo akiwa ameketi kwenye stuli, akiwa ameinama juu ya benchi yake ya kufanyia kazi, akikata na kushona hadi usiku wa manane. Kwa kuwa hakukuwa kelele nyingi ka-tika kiwanda cha kazi, ikifanya iwe rahisi kusema huku kazi ikiendelea kufanywa, huenda ikawa Paulo alikuwa na nafasi ya kutoa ushahidi kwa mwenye kiwanda hicho, waajiriwa wake, watumwa, wanunuzi, na marafiki wa mwenye kiwanda hicho.—Linganisha 1 Wathesalonike 2:9.
Mishonari Paulo alikataa kufanya huduma yake iwe biashara au kwa njia yoyote kufanya ionekane kana kwamba alikuwa akijifaidi kutokana na Neno la Mungu. Aliwaambia Wathesalonike hivi: “Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo kutufuata [kutuiga, NW]; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu; wala hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote. Si kwamba hatuna amri, lakini makusudi tufanye nafsi zetu kuwa kielelezo kwenu, mtufuate [mtuige, NW].”—2 Wathesalonike 3:7-9.
Wenye Kuiga wa Karne ya Ishirini
Hadi siku ya leo Mashahidi wa Yehova hufuata mfano mzuri wa Paulo. Wazee na watumishi wa huduma hawapokei mshahara wala malipo kutoka kwa makundi wanayotumikia. Badala ya hiyo wao huandalia familia zao kama mtu mwingineye yote, wengi wao wakifanya kazi za kuajiriwa. Wahudumu mapainia wa wakati wote hujiandalia wenyewe pia, wengi wakifanya kazi ya kutosha ili kutosheleza mahitaji ya msingi. Kila mwaka Mashahidi wengine husafiri kwa gharama yao wenyewe ili kuhubiri katika maeneo ya mbali yasiyofikiwa sana na habari njema. Familia za huko zikiwaalika washiriki milo au mahali pa kukaa, wao huthamini hayo lakini hawatumii vibaya ukaribishaji-wageni huo.
Kuhubiri na kufundisha kote kunakofanywa na Mashahidi wa Yehova ni kwa hiari, na wao hawatozi kamwe kwa ajili ya huduma yao. Hata hivyo, upaji wa kiasi kwa kazi yao ya kuhubiri ulimwenguni pote hukubaliwa na hupelekwa kwenye Watch Tower Society kwa kusudi hilo. (Mathayo 24:14) Huduma ya Mashahidi si ya kibiashara hata kidogo. Kama vile Paulo kila mmoja wao aweza kusema kikweli: “Niliihubiri kwenu Habari Njema ya Mungu bila kudai mshahara.” (2 Wakorintho 11:7, HNWW) Mashahidi wa Yehova si “wachuuzi wa Neno la Mungu.”
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
JINSI WENGINE WANAVYOTOA UPAJI KWA AJILI YA KAZI YA KUHUBIRI-UFALME
◻ MICHANGO KWA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE: Wengi huweka kando au hupangia kiasi cha fedha ambazo wanatia katika masanduku ya michango yaliyo na kibandiko hiki: “Michango kwa Kazi ya Sosaiti ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.” Kila mwezi, makundi hupeleka kiasi hicho ama kwenye makao makuu ya ulimwengu huko Brooklyn, New York, ama kwenye ofisi ya tawi iliyo karibu zaidi.
◻ ZAWADI: Upaji wa hiari wa pesa unaweza kupelekwa moja kwa moja kwenye Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201, au kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti iliyo karibu. Vito au mali nyingine zenye thamani zinaweza kutolewa pia. Barua fupi yenye kutaarifu kwamba hiyo ni zawadi ya moja kwa moja inapasa iambatane na michango hiyo.
◻ MPANGO WA UPAJI WENYE MASHARTI: Pesa zinaweza kupewa kwa Watch Tower Society zikishikiliwa zikiwa amana hadi kifo cha mpaji, kukiwa na uandalizi wa kwamba kukitokea kisa cha uhitaji wa kibinafsi, zitarudishwa kwa mpaji.
◻ BIMA: Watch Tower Society inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mpango wa bima ya maisha au katika mpango wa kustaafu kazi/malipo ya uzeeni. Sosaiti inapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
◻ AKIBA ZA BENKI: Akiba za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja mmoja zinaweza kuwekwa zikiwa amana kwa ajili ya au kuweza kulipwa wakati wa kifo kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki ya hapo. Sosaiti inapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
◻ HISA NA DHAMANA: Hisa na dhamana zinaweza kupewa kwa Watch Tower Society ama zikiwa zawadi ya moja kwa moja ama zikiwa chini ya mpango ambapo mapato yanaendelea kulipwa kwa mpaji.
◻ MASHAMBA NA NYUMBA: Mashamba na nyumba zinazoweza kuuzwa zinaweza kupewa kwa Watch Tower Society ama kwa kutoa zawadi ya moja kwa moja ama kwa kuweka shamba au nyumba ya maisha kwa ajili ya mpaji, ambaye aweza kuendelea kuishi huko muda wa maisha yake. Mtu anapaswa kuarifu Sosaiti kabla ya kuipa Sosaiti hati yoyote ya mashamba na nyumba.
◻ WASIA NA AMANA: Mali au pesa zinaweza kupangiwa kuwa urithi wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania kwa njia ya wasia wenye kutekelezwa kisheria, au Sosaiti inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Amana inayofaidi tengenezo la kidini inaweza kuandaa faida fulani za kodi. Nakala ya wasia au mkataba wa amana inapasa kupelekwa kwa Sosaiti.
Kwa habari zaidi kuhusu mambo ya jinsi hiyo, andikia International Bible Students Association, P. O. Box 47788, Nairobi, Kenya, au tumia anwani ifaayo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa 2.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
ALITAKA KUSAIDIA
TIFFANI mwenye miaka kumi na mmoja ni msichana wa shule katika Baton Rouge, Louisiana, U.S.A. Hivi karibuni, Shahidi wa Yehova
huyo mchanga aliandika insha yenye kichwa “Elimu Katika Amerika.” Likiwa tokeo, wazazi wake Mashahidi walipokea barua hii kutoka kwa mwalimu mkuu wa shule:
“Katika juma la Elimu ya Amerika, insha moja yenye kutokeza ya kila darasa husomwa kwenye simu ya ndani inayounganisha madarasa. Nilifurahia kusoma insha ya Tiffani asubuhi ya leo. Yeye kwa kweli ni mwanamke mchanga wa ajabu. Yeye ni mtulivu, mwenye kujiamini, aliye na kipawa, na mwenye madaha. Nimepata kuona mara haba sana mwanafunzi wa darasa la sita akiwa na sifa nyingi hivyo. Tiffani ni faida kwa shule yetu.”
Tiffani alijishindia mahali pa kwanza katika shindano hilo la insha. Baadaye aliandikia Watch Tower Society na kusema hivi: “Labda nilishinda shindano hilo kwa sababu tu ya kile kichapo Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. . . . Nilitumia zile sura juu ya elimu. . . . Asanteni sana kwa kuchapisha kitabu hicho chenye thamani na chenye kuchochea. Nilijishindia dola saba kwa insha yangu yenye kushinda. Ninachanga dola hizo 7 na nyingine 13, ikiwa jumla ya dola 20 kwa kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. . . . Ninapokuwa mkubwa, natumaini pia kujitolea kwa ajili ya utumishi wa Betheli.”
[Picha katika ukurasa wa 26]
Nyakati nyingine, Paulo alipata riziki yake kwa kutengeneza mahema