Endeleeni Kusema: “Njoo!”
1 Ni uandalizi wa ajabu kama nini ambao Yehova amefanya kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu! Kwa ajili ya huo tuna msingi wa mambo yote yanayohitajiwa ili kufanya watu wawe na furaha kwelikweli. (Yn. 3:16) Hata hivyo, kwa kusikitisha, ni wachache sana ambao wamepata kujua na kuiamini kweli hii kwa uthabiti. Ingawa hivyo, kwa sababu ya hangaikio lake lenye upendo kwa ainabinadamu, Yehova amepanga kufanya habari njema hizi zijulikane na watu kila mahali. Kupitia Mwana wake Yesu Kristo, ametoa fursa kwa wote wapate furaha na tumaini la uhai wa milele.—Yn. 17:3.
2 Kwa maelfu ya miaka, utambulisho wa Yule ambaye angefidia ainabinadamu kutoka dhambi na kifo haukujulikana. Ilikuwa ‘siri takatifu’ hadi Kristo Yesu akaja na “kuufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili.” (Rum. 16:25; 2 Tim. 1:10) Wafuasi wa Yesu walipiga mbiu ya habari njema hizi katika karne ya kwanza; sasa sisi tunaoishi nyakati za ki-siku-hizi tuna pendeleo tukufu la kutangaza habari njema hizohizo. Tunapohubiri ujumbe wa Ufalme, tunaushiriki na Yehova Mungu, Yesu Kristo, na ndugu za Kristo, wanaoalika watu wa kila namna ya maisha kwa kusema: “Njoo! . . . [uyatwae] maji ya uzima bure.”—Ufu. 22:17.
3 Bila shaka, si kila mtu atakayesikiliza habari njema hizi. Ni wachache sana husikiliza kwa uangalifu. Wengine huwakataa kijeuri watumishi wa Mungu, ambao huwaalika wanufaike kutokana na maji ya kweli yenye uhai. Ingawa hivyo, tukiwa na nguvu kutoka kwa Yehova, twavumilia katika kazi hii. Twajua kuwa kupenda kwetu kusema kweli na kusaidia yeyote atakayesikia kwampendeza Yehova na huleta baraka.
4 Katika huduma yetu ya Machi, tutatia moyo watafutaji kweli wasome kitabu Upeo wa Ufunuo na waonee shangwe tumaini linachotoa. Watapata baraka nyingi kwa kufanya hivyo. Iwayo yote, kitabu cha Ufunuo chahusu wakati ujao—wakati ujao wao na wetu. Baadhi ya walio sasa watumishi waliojiweka wakfu kwa Yehova kwanza walipendezwa na kweli baada ya kusoma masimulizi ya kitabu cha Ufunuo katika kimojapo vichapo vya Sosaiti. Sisi wenyewe tukiwa tumejifunza kitabu Upeo wa Ufunuo kwa kina kirefu, twaweza kuonyesha umuhimu wacho kwa wale wenye mioyo minyoofu walio na njaa ya kweli. Tunapopata watu wa aina hiyo katika huduma yetu, tutajitahidi kuonyesha jambo moja au mawili makuu kutoka kitabu Upeo wa Ufunuo ili kuwaonyesha thamani yacho. Miongoni mwa mambo mengine, twaweza kugusia masimulizi ya unabii mbalimbali wa Biblia ambao umekuwa ukitimizwa katika karne hii ya 20, kama wale waendeshaji-farasi wanne wenye kutokeza wanaoelezwa katika sura ya sita ya Ufunuo.
5 Ni jambo linalofaa zaidi kwetu kuongea juu ya maandalizi ya upendo ya Yehova kwa ainabinadamu tunapojitayarisha kuadhimisha ukumbusho wa kifo cha Yesu Aprili 6. Watu wachague kusikiliza au la, twavumilia katika mgawo wetu tuliopewa na Mungu kutoa mwaliko wenye kuchochea kwa yeyote anayetaka: “Njoo! . . . [uyatwae] maji ya uzima bure.”