Kuadhimisha Kifo Kitoacho Tumaini la Uhai wa Milele
1 Baada ya jua kushuka Aprili 6, 1993, tutaadhimisha kifo cha Wakili Mkuu wa uhai. (Mdo. 3:15) Naam, inafaa sana kukumbuka maisha na kifo cha Yesu Kristo. Tumaini letu la kuishi milele lategemea damu ya Yesu iliyomwagwa.
2 Ukumbusho hukazia umaana wa kifo cha Yesu katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Kusudi hilo latia ndani kuandaa dhabihu kamilifu ya kibinadamu inayohitajiwa kufidia wazao wa Adamu, ikiwezesha mabilioni yajizoeze imani na kuishi milele katika dunia paradiso.—Yn. 3:16.
3 Wote wapendao kweli na uhai wanatazamia sana kuadhimisha Chakula cha Bwana cha Jioni kwa kutii amri ya Yesu. (Lk. 22:19) Sisi mmoja mmoja twaweza kufanya nini ili kuonyesha uthamini wetu kwa uandalizi wa dhabihu ya fidia ya Kristo? Kwa kutambua umaana wa mwadhimisho huu, ni muhimu kupanga mambo vizuri. Wewe wafanya matayarisho gani kwa ajili ya tukio hili la pekee?
4 Kujitayarisha mapema Kwahitajiwa: Bila shaka, tutahakikisha kwamba kila mshiriki wa familia yupo. Twapaswa kujitayarisha kiakili kwa kusoma na kutafakari juu ya mafungu ya Biblia yaliyoandikwa kwenye 1993 Calendar kwa ajili ya Aprili 1-6. Itafaa kutia ndani habari juu ya umaana wa Ukumbusho katika funzo la Biblia letu la binafsi na familia kabla ya tu Aprili 6. Panga kufika mapema na ubaki kwa muda fulani baada ya mwadhimisho wa Ukumbusho ili kuwakaribisha wapya ambao huenda wakawa wanahudhuria kwa mara ya kwanza.
5 Katika majuma ya kabla ya Ukumbusho, waalike watu wote wenye kupendezwa unaowajua kwenye mwadhimisho huu. Vikaratasi vya mwaliko vimetiwa ndani ya upakizi wa kila mwaka wa fomu. Unapovitumia, kumbuka kuwajulisha watu wanaopendezwa mahali na wakati wa mwadhimisho wa mahali penu. Tayarisha orodha ya wale unaofikiria kualika. Je! wote wanaotaka kuhudhuria wana usafiri? Ikiwa sivyo, unaweza kufanya nini kuwasaidia? Ikiwa una nafasi ya ziada katika gari lako au unaweza kusaidia mtu kwa namna nyingine kwa nini usiwaulize wazee kama kuna mtu anayehitaji msaada?
6 Kwa sababu huu ni mwadhimisho wa maana zaidi wa mwaka na hudhurio kubwa linatazamiwa, wazee watahitaji kufanya matayarisho ya mapema. (1 Kor. 14:40) Juma moja hivi kabla ya Aprili 6, wazee watapanga kufanya mkutano wa pekee pamoja na ndugu watakaowasaidia wakati wa mwadhimisho, wakihakikisha wameelewa mpangilio wa kuketi na jinsi mifano yapasa kupitishwa. Ikiwa umepewa mgawo wa kusaidia katika pindi ya mwadhimisho ukiwa mkaribishaji au mwenye kupitisha, hakikisha umefuata sana maagizo ya wazee kuhusu mambo hayo. Kwa kuangalia vikumbusho katika sanduku lililopo ukurasa wa 7, wazee waweza kuhakikisha kwamba mipango yote kwa ajili ya wakaribishaji, wapitishaji, mifano, na msemaji imeshughulikiwa mapema vya kutosha.
7 Ni wachache tu wa ndugu za Yesu wanaobaki duniani leo, na katika wakati ujao usio mbali, mwadhimisho wa Chakula cha Bwana cha Jioni utafikia ukamilisho wake. (1 Kor. 11:25, 26) Maadamu tuna pendeleo la kufanya hivyo, na tuendelee kuadhimisha kifo kitoacho tumaini la uhai wa milele.