Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 11/93 kur. 3-6
  • Vijana—Fanyeni Moyo wa Yehova Ushangilie

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vijana—Fanyeni Moyo wa Yehova Ushangilie
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1993
  • Habari Zinazolingana
  • Tunawafurahia Vijana Wanaotembea Katika Njia ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Tia Moyo Ufuatiaji wa Miradi ya Kiroho
    Huduma Yetu ya Ufalme—1992
  • Watoto Wenye Furaha Katika Ulimwengu Wenye Upotoe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Je, Dini Yangu Ni Chaguo Langu au la Wazazi Wangu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1993
km 11/93 kur. 3-6

Vijana—Fanyeni Moyo wa Yehova Ushangilie

1 Mtu atumiapo nguvu na idili ya ujana kwa njia ifaayo, maisha yaweza kufurahisha kwelikweli. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako.” (Mhu. 11:9) Nyinyi vijana mwahitaji kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya matendo yenu.

2 Namna unavyoishi maisha yako hufanyiza tofauti si kwako tu bali pia kwa wazazi wako. Mithali 10:1 husema: “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.” Lakini la maana hata zaidi, namna unavyoishi maisha yako huathiri Muumba wako, Yehova Mungu. Ndiyo sababu Mithali 27:11 pia huwatia moyo vijana hivi: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Nyinyi vijana mwaweza kuufanyaje moyo wa Yehova ushangilie leo? Hilo laweza kufanywa katika njia kadhaa.

3 Kwa Kielelezo Kifaacho: Nyinyi vijana mnapatwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” zilizotabiriwa katika Neno la Mungu. (2 Tim. 3:1, NW) Huenda pia mkawa chini ya misongo kutoka kwa wanashule wenzenu wasioamini na hata kutoka kwa walimu ambao waweza kupuuza maoni yenu yenye msingi wa Biblia. Mathalani, mwalimu mmoja alionyesha nadharia ya mageuzi kuwa jambo hakika na Biblia kuwa ngano. Hata hivyo, mhubiri mmoja mchanga katika darasa hilo aliitetea Biblia kwa uaminifu-mshikamanifu. Kama tokeo, mafunzo kadhaa ya Biblia yalianzishwa. Baadhi ya wale waliopendezwa walianza kuhudhuria mikutano. Imani yenu nyinyi ndugu na dada wachanga hushutumu ulimwengu usiomcha Mungu na kuvutia kwenye kweli, wale wenye moyo wa kufuatia haki.—Linganisha Waebrania 11:7.

4 Je! waweza kuwatia moyo marika wako kutanikoni ili wasishindwe na yale yaliyo mabaya? Kwa kuweka kielelezo chema shuleni, nyumbani, na kutanikoni, waweza kuimarisha imani ya wahubiri wengine wachanga. (Rum. 1:12) Fanya moyo wa Yehova ushangilie kwa kuwekea wengine kielelezo.

5 Kwa Mavazi na Kujipamba: Dada mmoja mchanga alitaniwa na kudhihakiwa kwa sababu ya mavazi yake ya kiasi na alibandikwa jina “mtakatifu.” Hilo halikumtisha yeye ajipatanishe na viwango vya ulimwengu visivyo vya kimungu. Badala ya hilo, yeye alieleza kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kiwango cha juu cha Mashahidi ndicho alichoshikilia. Je! una uhodari wa jinsi hiyo? Au waruhusu ulimwengu wa Shetani ukufinyange katika njia yao ya kufikiri na mwenendo wao? Ni furaha kama nini kuona wengi wenu vijana mkitii mafundisho ya Yehova na kukataa staili zisizofaa, mitindo, mabingwa wapewao heshima ya kiibada, na mafundisho ya ulimwengu na watawala wao, roho waovu!—1 Tim. 4:1.

6 Kwa Chaguo la Vitumbuizo na Tafrija: Wazazi wahitaji kukumbuka umaana wa kusaidia watoto wao wachague kwa hekima aina ya vitumbuizo na tafrija zifaazo. Ndugu mmoja aliisifu familia njema ambayo alikuja kuipenda sana. Wakiwa wenye kufuatilia mambo ya kiroho, wazazi waliandaa mwongozo uliotumiwa pia katika tafrija ya familia. Ndugu huyo alionelea hivi: ‘Mimi huvutiwa kwamba wao hufanya mambo pamoja. Si kwamba wazazi husaidia watoto wajitayarishe kwa ajili ya utumishi tu, bali unapokuwa wakati wa tafrija, wao hufurahia kwenda kupanda milima, kuzuru majumba ya kuhifadhi vitu vya kale, au kukaa tu nyumbani na kucheza au kufanya kazi katika miradi. Jinsi wanavyopendana na kupenda wengine hufanya uhisi mwenye uhakika kwamba watatembea katika kweli wakati ujao, haidhuru ni nini kitakachotukia.’

7 Bila shaka, kuna nyakati ambapo haiwezekani kwa familia nzima kushiriki katika tafrija na vitumbuizo. Nyinyi vijana mwahitaji kufahamu hilo na ule uzito wa kuchagua jinsi mtakavyotumia sehemu fulani ya wakati wenu wa starehe. Shetani ameazimia kudanganya watu wengi kadiri awezavyo. Vijana na wale wasio na ujuzi ni rahisi kudanganywa hasa na matendo yake ya hila na ushawishi wenye kudanganya. (2 Kor. 11:3; Efe. 6:11) Kwa hiyo leo, Shetani hutumia njia mbalimbali ili kukufanya ukengeushwe na ufuatilie kwa ubinafsi maisha ya kutafuta anasa na ya ukosefu wa adili.

8 Televisheni ni kishawishi kikuu kinachochochea mtindo-maisha wenye kufuatia mali na ukosefu wa adili. Kwa kawaida sinema na vidio huonyesha jeuri na ngono ya waziwazi. Muziki upendwao umekuja kuwa wenye kupotoka na wenye uchafu zaidi. Vishawishi vya Shetani vyaweza kuonekana kuwa bila dhara, lakini vimenasa maelfu ya vijana Wakristo kuwa na fikira na mwenendo usiofaa. Ili kukinza misongo hiyo, ni lazima ufuatilie uadilifu kwa bidii. (2 Tim. 2:22) Ikiwa marekebisho yahitajiwa katika kufikiri au mwenendo wako kuhusu vitumbuizo na tafrija, hayo yaweza kufanywaje? Mtunga-zaburi atoa jibu: “Kwa moyo wangu wote nimekutafuta. Usiniache nipotee mbali na maagizo yako.”—Zab. 119:10.

9 Kupa michezo na mabingwa wa vitumbuizo heshima ya kiibada ni jambo la kawaida. Kumhofu Yehova kutakusaidia usiwape wanadamu wasio wakamilifu heshima ya kiibada. Hata ukosefu wa adili katika ngono hupewa heshima ya kiibada na wengi leo. Waweza kulinda dhidi ya mwelekeo huo kwa kuepuka vitabu vya umalaya na muziki uliopotoka. Kuhusu muziki, toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1993 lilionelea hivi: “Muziki ni zawadi ya kimungu. Lakini kwa vijana wengi, unakuwa kishughulishaji akili kisichofaa. . . . Fanya shabaha yako iwe kuweka muziki mahali panapoufaa na kuacha utendaji wa Yehova uwe hangaiko lako kuu. Uwe mteuzi na mwangalifu juu ya muziki unaochagua. Hivyo utaweza kutumia vizuri—wala si vibaya—zawadi hiyo ya kimungu.”

10 Sitawisha chuki kamili kwa yaliyo mabaya. (Zab. 97:10) Unaposhawishwa kufanya yaliyo mabaya, fikiria jinsi Yehova aonavyo jambo hilo, na ufikirie matokeo: mimba zisizotakwa, magonjwa yenye kuenezwa kingono, kuvunjika kihisiamoyo, kukosa kujistahi, na kupoteza mapendeleo kutanikoni. Epuka kutazama maonyesho ya televisheni, sinema, vidio, nyimbo, au mazungumzo yanayoutia moyo uovu. Epuka kushirikiana na wale ambao Biblia huita “wapumbavu.” (Mit. 13:19) Uwe mteuzi; chagua kuwa na ushirika wa karibu na wale kutanikoni wanaompenda Yehova na viwango vyake vyenye uadilifu.

11 Ndiyo, vijana ambao kwa kweli wataka kufanya moyo wa Yehova ushangilie watatii shauri jema lipatikanalo kwenye Waefeso 5:15, 16: “Angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.” Ni nini kitakusaidia ‘kuangalia sana’ maendeleo yako katika siku hizi za mwisho?

12 Kushughulikia Mahitaji ya Kiroho: Kwenye Mathayo 5:3, (NW) Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” Wewe pia waweza kuwa mwenye furaha kwa kutambua uhitaji wako wa kiroho. Kujazia uhitaji huo hutia ndani ushiriki wenye bidii katika kuhubiri habari njema, kwa kuwa hilo hujenga imani yetu katika mambo tujifunzayo.—Rum. 10:17.

13 Kutokana na ono lako kibinafsi wajua kwamba haiwi rahisi sikuzote kushiriki kwa kawaida katika huduma. Sehemu kubwa ya hilo yaweza kusababishwa na kukosa uhakika. Hivyo, jitihada yenye nguvu yahitajiwa upande wako. Kwa kushiriki katika huduma kwa kawaida, utaendeleza stadi zako za kutoa ushahidi na kujenga uhakika katika uwezo wako wa kuhubiri.

14 Fanya mipango uhubiri pamoja na wahubiri wenye ujuzi zaidi kutanikoni, kama vile mapainia wa kawaida na wazee. Sikiliza kwa uangalifu utoaji wao mbalimbali na jinsi washughulikiavyo vipingamizi mlangoni. Tumia vizuri kitabu Kutoa Sababu na madokezo yaliyotolewa katika Huduma ya Ufalme Yetu. Kabla ya muda mrefu kupita utapata shangwe nyingi hata zaidi kutoka kwa huduma kwa sababu watoa yote uliyo nayo kwa Yehova.—Mdo. 20:35.

15 Vijana fulani wameweza kutumia kwa faida fursa ili kutoa ushahidi shuleni na wamefanikiwa sana katika kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kijana mmoja Mkristo asema: “Wakati wa vipindi visivyo vya masomo shuleni, nilikuwa na fursa nyingi za kutoa ushahidi, hasa nyakati za sikukuu. Nilipoacha vichapo vya Biblia juu ya dawati langu mahali ambapo wengine wangeweza kuviona, wanafunzi wengi wenye kupendezwa walinijia.” Hatimaye, idadi fulani ya wanafunzi na hata mwalimu alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kwa kweli, mwalimu huyo alifanya maendeleo kufikia hatua ya kuwa Shahidi aliyejiweka wakfu. Yehova hushangilia sana wakati waabudu vijana kama wewe waleteapo sifa jina lake.

16 Njia nyingine ya kutosheleza uhitaji wako wa kiroho ni kupitia funzo la kibinafsi. Ili kufanya moyo wa Yehova ushangilie, ni lazima tupate ujuzi juu yake, makusudi yake, na matakwa yake kwetu. Je! wewe huweka wakati kando kwa ajili ya funzo la kibinafsi? Je! wewe hujifunza kwa kawaida, kama vile ambavyo wewe huchukua wakati kula kwa kawaida? (Yn. 17:3) Je! una ratiba ya kibinafsi ya kusoma Biblia kwa kuongezea kujaribu kufuatana na ratiba ya kusoma Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Je! wewe hutayarisha vema kwa ajili ya mikutano yote? Je! wewe husoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa kawaida? Hasa je, wewe huchukua wakati kusoma kila makala katika mfululizo wa “Vijana Huuliza . . . ” ukisoma kila andiko kwa uangalifu? Usisahau kitabu ambacho Sosaiti imebuni hasa kwa ajili ya mahitaji yako ya kiroho, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Vijana Wakristo na wazazi wao ulimwenguni pote wameandika kusema jinsi ambavyo kitabu hicho kimewasaidia kumkaribia Yehova zaidi.

17 Usomapo Biblia na misaada ya kitheokrasi ya kujifunzia Biblia, hiyo yakuambia juu ya Yehova, kufikiri kwake, na makusudi yake. Fikiria jinsi ambavyo habari hii ingekuwa yenye msaada kwako. Husianisha yale usomayo na yale uliyotangulia kusoma. Kutafakari kwahusika. Kutafakari huruhusu habari hiyo ifike ndani ya moyo na ikuchochee.—Zab. 77:12.

18 Twashangilia kuwaona vijana wanaotambua uhitaji wao wa kiroho wakihudhuria mikutano ya kutaniko. Nyinyi vijana Wakristo mwaweza kuwatia moyo wengine kwa kutoa maelezo yenye maana kwa kawaida wakati wa mikutano. Fanya uwe mradi wako kutoa angalau jibu moja kwenye kila mkutano. Sitawisha uhusiano mwingi mchangamfu na watu wa kila rika kutanikoni kwa kushiriki katika ushirika wenye kujenga kabla na baada ya mikutano. (Ebr. 10:24, 25) Ndugu mmoja mchanga alisema kwamba wazazi wake walimtia moyo kuzungumza na angalau ndugu au dada mmoja mwenye umri mkubwa zaidi kwenye kila mkutano. Leo yeye huthamini ujuzi ambao amepata kwa kushirikiana na washiriki wa kutaniko wenye umri mkubwa zaidi.

19 Fuatia Miradi ya Kiroho: Yasikitisha kwamba maisha za vijana wengi yakosa kusudi na mwelekezo. Hata hivyo, je, si yapendeza kupata hisia inayotokana na kuweka miradi ya kitheokrasi na kisha kuitimiza kwa mafanikio? Miradi hiyo, ifuatiwayo kwa nuru ya elimu ya kimungu, itakuwa yenye kutosheleza binafsi sasa na hatimaye itaongoza kwenye wokovu wa milele.—Mhu. 12:1, 13.

20 Unapoweka miradi, fanya hilo liwe jambo la sala. Zungumza na wazazi wako na wazee. Jichunguze mwenyewe na uwezo wako mbalimbali, na uweke miradi ifaayo kulingana na yale unayoweza kutimiza na si kwa kulinganishwa na mtu mwingine. Kila mtu ni tofauti kitabia—kimwili, kiakili, kihisiamoyo, na kiroho. Kwa hiyo, usitazamie kutimiza kila kitu ambacho mtu mwingine atimiza.

21 Ni nini baadhi ya miradi ambayo waweza kufikilia? Ikiwa wewe si mhubiri bado au hujabatizwa bado, kwa nini usifanye hiyo iwe miradi yako? Ikiwa wewe ni mhubiri, ungeweza kufanya mradi wa kutoa kiwango fulani cha wakati katika huduma kila juma. Jitahidi kuwa mwalimu mwenye uwezo kwenye ziara za kurudia, na ufanye uwe mradi kuongoza funzo la Biblia. Ikiwa wewe ni kijana aliyebatizwa uliye shuleni, kwa nini usifanye uwe mradi wako kufanya upainia msaidizi wakati wa miezi ya likizo? Kuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Kor. 15:58, NW.

22 Msaada Kutoka kwa Wazazi Ni Muhimu: Vijana kutanikoni hawapaswi kuhisi kwamba wako peke yao katika jitihada zao za kupata uhai. Yehova, kupitia tengenezo lake, ameandaa mashauri ili yawasaidie vijana hao katika maamuzi mengi ya kila siku na kushinda vipingamizi maishani. Bila shaka, wazazi waliojiweka wakfu wana daraka la msingi la kusaidia watoto wao kufanya maamuzi yafaayo. Kwenye 1 Wakorintho 11:3, Biblia humweka mume kuwa kichwa cha nyumba. Kwa hiyo, katika nyumba ya Kikristo, baba huchukua uongozi katika kufundisha watoto amri za Mungu, huku mke akifanya kazi pamoja naye kwa ukaribu. (Efe. 6:4) Hilo hufanywa kupitia mazoezi yenye kudhamiria yaanzayo utotoni. Kwa kuwa ubongo wa mtoto hukua mara tatu kwa ukubwa wakati wa mwaka wa kwanza wa maisha, wazazi hawapaswi kuona uwezo wa kujifunza wa kitoto kuwa mdogo kuliko vile ulivyo. (2 Tim. 3:15) Watoto wakuapo, wazazi wahitaji kuwafundisha kwa kuendelea wampende Yehova na kusitawisha uhusiano mwema naye.

23 Mahali bora zaidi pa kuanzia, ni kielelezo chema cha kimzazi. Hilo litafanya mengi katika kusaidia watoto wako kiroho kuliko kusema nao mambo mengi juu ya yale wapaswayo au wasiyopaswa kufanya. Kuweka kielelezo kifaacho cha kimzazi kungeweza kutia ndani kuonyesha matunda ya roho nyumbani, kuelekea mke wako na kuelekea watoto wako. (Gal. 5:22, 23) Wengi wamejionea wenyewe kwamba roho ya Mungu ni uvutano wenye nguvu kwa ajili ya mema. Hiyo yaweza kukusaidia kufinyanga akili na mioyo ya watoto wako.

24 Wazazi pia wahitaji kuweka kielelezo chema katika mazoea ya funzo la kibinafsi, kuhudhuria mikutano, na ushirika wa kawaida katika huduma ya shambani. Ikiwa wewe husema kwa idili juu ya kweli nyumbani, huchukua uongozi wenye idili katika huduma, na una maoni yafaayo juu ya funzo la kibinafsi, watoto wako watatiwa moyo kupendezwa kikweli na mambo ya kiroho.

25 Litayarishwapo kwa uangalifu, funzo la Biblia la familia la kawaida na lenye maana laweza kuwa lenye kupendeza na kufurahisha, wakati wa kuwa pamoja mkiwa familia kwa njia itoayo uhakikishio. Chukua wakati kufikia moyo wa watoto wako. (Mit. 23:15) Ingawa familia nyingi hutumia pindi hii ili kutayarisha kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, kufikiria uhitaji hususa wa familia mara kwa mara kwaweza kutia moyo. Kuuliza maswali ya maoni na kusikiliza majibu ya kila mshiriki wa familia kutaelimisha na pia kuburudisha. Kuongoza funzo linufaishalo kila mshiriki wa familia ni ugumu halisi kwa kila kichwa cha familia. Lakini inathawabisha kama nini wote wanapokua kiroho! Kwa kushirikisha kila mmoja, roho ya furaha itaenea.

26 Mazoezi yako yenye upendo na ya ustadi sasa ni muhimu kwa ajili ya kuokoa maisha za watoto wako. (Mit. 22:6) Hilo likiwa akilini, ni rahisi kuelewa kwamba huu waweza kuwa ufundishaji wa maana zaidi ambao utapata kuutoa. Usifikiri kamwe kwamba uko peke yako katika kazi hii ya pekee na yenye maana. Jifunze kumtegemea Yehova kabisa ili kupata mwongozo katika kushughulikia madaraka ya familia yako. Si hayo tu. Kuna wengine wanaoweza kutoa msaada pia.

27 Yale Ambayo Wengine Waweza Kufanya Ili Kusaidia: Wazee waweza kuwatia ndani vijana, pamoja na wazazi wao, katika kusafisha Jumba la Ufalme. Tia moyo watoto kwenye mikutano ya kutaniko. Wazee na watumishi wa huduma waliogawiwa sehemu za Mkutano wa Utumishi wapaswa wawe macho kuona mikono ya watoto iliyoinuliwa kunapokuwa na sehemu za ushiriki wa wasikilizaji. Tafuteni fursa za kutumia vijana walio vielelezo vyema katika maonyesho wakiwa na wazazi wao. Vijana fulani waweza kuhojiwa na kutoa maelezo mafupi.

28 Usichukue jitihada zao kivivi-hivi. Vijana wamethibitika kuwa wa maana sana kutanikoni. Kwa mwenendo wao mwema, wengi ‘wameyapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu.’ (Tit. 2:6-10) Tambua uhitaji wa kupongeza vijana wanaoshiriki hata katika njia ndogo. Hilo huwatia moyo kutayarisha na kuwa na tamaa ya kufanya hivyo tena wakati ujao. Kupendezwa huko hakuwezi kukaziwa kupita kiasi; ni kwenye thamani sana. Je! wewe ukiwa mzee au mtumishi wa huduma umewafikia mara ngapi washirika wachanga zaidi wa kutaniko ili kuwapongeza kwa ajili ya hotuba au wonyesho katika mkutano?

29 Mapainia, mwaweza kufanya nini ili kusaidia? Kwa nini msipitie ratiba yenu kuona jinsi ya kutia ndani watoto wa shule katika mipango yenu ya alasiri na miisho-juma? Je! wewe husema kwa njia ifaayo juu ya chaguo lako la utumishi wa wakati wote? Je! waonyesha kwa sura yako kwamba wewe hupata shangwe katika huduma yako? Je! wewe huipendekezea wengine, hasa vijana? Unapofanya kazi mlango kwa mlango, je, mazungumzo yako ni yenye kujenga na yenye kufaa? Ikiwa ndivyo, basi ukiwa painia wewe pia washiriki katika utendaji huu wa kuzoeza ulio wa maana sana.

30 Wote kutanikoni wapaswa wajue vyema kazi hii ya maana ya kuwazoeza vijana. Je! waweza kufanya mipango hususa kufanya kazi katika huduma ya shambani pamoja nao? Je! waweza kufanya mazoezi ya utoaji pamoja nao katika kujitayarisha kwa ajili ya kazi ya mlango kwa mlango? Je! wewe uko macho kuona fursa za kutia moyo utendaji wa kiroho wa wakati ujao mnapofanya kazi pamoja katika huduma? Kila mhubiri apaswa kutambua kwamba hata maneno machache yaweza kuchochea fikira zifaazo kuelekea miradi ya kiroho ya maisha yote, kwa manufaa ya milele ya kijana huyo.

31 Vijana Waweza Kujisaidia: Vijana, twatia moyo kila mmoja wenu kuendelea kutii mafundisho ya Yehova na kukataa yale yanayotolewa na ulimwengu. Endelea kujitahini mwenyewe kwa kuchunguza mwenendo wako na hisia za ndani. Mtazamo wako ni nini kumwelekea Yehova na yale ambayo akutazamia ufanye katika maisha ya kila siku? Je! waendelea kupiga vita vikali dhidi ya uvutano wa mawazo ya Shetani? (1 Tim. 6:12) Kwa kuwa wanadamu, na hasa vijana, hutamani kiasili kupata kibali cha marika wao, je, wewe hujipata umeshawishwa kufuata umati katika kufanya yale yaliyo mabaya? (Kut. 23:2) Mtume Paulo alielewa kulikuwa na msongo mkubwa wa kujipatanisha na njia za ulimwengu.—Rum. 7:21-23.

32 Ujasiri hutakwa ili kukinza uvutano wa ulimwengu, kuchukua mwendo tofauti na ule wa marika wa ulimwengu, na kutii mafundisho ya Mungu. Watu wa kale walifanya hivyo kwa mafanikio mengi. Fikiria ujasiri wa Noa. Yeye aliushutumu ulimwengu mzima kupitia imani yake na kwa kuendelea kuwa tofauti na watenda mabaya wa wakati wake. (Ebr. 11:7) Piga vita vikali kwa sababu hivyo vyastahili. Usiige wale walio dhaifu, wasio na ujasiri, wenye hofu wanaofuata umati wa Shetani. Kinyume cha hilo, tafuta ushirika wa wale wanaopata upendeleo machoni pa Yehova. (Flp. 3:17) Uwe na washirika watakaotembea nawe kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu. (Flp. 1:27) Kumbuka kwamba kuna njia moja tu iongozayo kwenye uhai wa milele.—Mt. 7:13, 14.

33 Ikiwa sisi hupata shangwe kuona vijana wakileta sifa na staha kwa Mungu wetu, ni lazima hilo liwe lamletea yeye shangwe kama nini! Hakuna shaka kwamba Yehova hufurahi kuona vijana wakishiriki kikamili katika kupiga mbiu ya makusudi yake matukufu. Wao ni “urithi” kutoka kwake, na awatakia yale yaliyo bora tu. (Zab. 127:3-5; 128:3-6) Akionyesha kupendezwa kwa Baba yake, Kristo Yesu alipata shangwe nyingi katika kushirikiana na watoto wadogo, na alitumia wakati kuwatia moyo katika ibada yao kwa Yehova. Yeye aliwaonyesha shauku nyororo. (Mk. 9:36, 37; 10:13-16) Je! sisi huwaona vijana wetu katika njia hiyohiyo ambayo Yehova na Kristo Yesu huwaona? Je! vijana katika makutaniko yetu wajua jinsi Yehova na malaika waonavyo uaminifu-mshikamanifu wao na kielelezo chema? Wao wapaswa kupongezwa na kutiwa moyo wamfurahishe Yehova kwa kufikia miradi ya kiroho. Vijana, fuatieni miradi itakayowaletea baraka nyingi sasa na wakati ujao.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki