Yanufaisha Kama Nini Kukumbuka Yale Ambayo Yehova Amefanya!
1 Mwandikaji aliyepuliziwa wa Zaburi 48 alisihi wale walio katika Israeli ‘watembee katika Sayuni kwa kuizunguka, wahesabu minara yake, wayafikiri majumba yake, wapate kuambia kizazi kitakachokuja.’ Wakisukumwa na upendo kwa Yehova, wangependezwa sana na kila jambo la kitovu hicho cha kidunia cha utawala wa kitheokrasi. Mambo hayo yangekuwa yenye thamani kama nini kwa sababu hilo lilikuwa jiji ambalo Yehova alikuwa ameliweka jina lake mwenyewe! Wangeongea juu yalo, na hasa walipaswa wawe na uhakika kwamba wazao wao walisikia kuhusu mambo yote waliyohazini mioyoni mwao wenyewe.—Zab. 48:12, 13.
2 Sasa twaishi katika wakati ambao utawala wa kitheokrasi wa Mesiya wa Yehova umewekewa kitovu si katika Sayuni wa kidunia tena bali katika Yerusalemu wa kimbingu. (Ebr. 12:22) Ufalme wa Yehova mikononi mwa Yesu Kristo umekuwa ukitawala tangu 1914. (Ufu. 12:10) Utendaji wao ni wenye upendezi mkuu kwetu. Pia twapendezwa sana na njia ambayo Yehova ameongoza watumishi wake duniani ili waweze kutimiza mapenzi yake wakiwa wawakilishi waonekanao wa Ufalme huo. Mambo yenye kusisimua kuhusu hilo yameonyeshwa wazi katika kitabu chetu kipya Mashahidi wa Yehova—Wapiga Mbiu ya Ufalme wa Mungu. Tulifurahi kama nini kukipokea kwenye “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wetu wa Wilaya wa karibuni!
3 Kufikia Septemba 1, kitabu hicho kilikuwa tayari kimetolewa katika lugha 20, na utafsiri ulikuwa unaendelea ili kujazia mahitaji ya wale wanaoongea kwa ndimi nyinginezo 13. Je! nyumba yako imepata nakala? Je! mnakisoma? Je! mnaongea juu ya mambo mnayojifunza kutokana nacho?
4 Baada ya kuzitazama picha na kusoma maelezo mafupi ya habari, kama ilivyopendekezwa kwenye mkusanyiko, ndugu na dada wengi upesi waingia kwenye kiini cha ya habari yenyewe. Maelezo yao yalikuwa nini? Hapa pana machache tu.
5 Dada mmoja aliandika: “Hicho ndicho kitabu pekee ambacho nimepata kupokea ambacho nina hamu sana ya kukimaliza ili nikisome tena. Niko kwenye sura ya 25 sasa. Kadiri nizidivyo kusoma, ndivyo machozi yazidivyo kuja na moyo wangu unajawa na upendo kwa Yehova. Kitabu hicho ni chenye kutia-moyo sana na kuimarisha imani.”
6 Ndugu ambaye amekuwa akimtumikia Yehova kwa miaka zaidi ya 40 alisema: “Sikuwa nimeona kimbele jinsi kitabu hiki kingekuwa chenye kuvuta fikira sana hivi. Nilikawia usiku na kuamka mapema nikamaliza kukisoma kwa majuma mawili. Kwa kweli ni kimojapo vitabu vyenye kuchochea zaidi ambacho nimewahi kusoma. Hicho ni kipeo cha utafiti lakini pia kipeo cha kitia moyo.”
7 Programu ya Kawaida ya Kusoma: Watu kadhaa ambao walikisoma kitabu chote kwa haraka wameazimia kukisoma tena lakini wakati huu kwa mwendo taratibu kidogo.
8 Ikiwa kuna mshiriki zaidi ya mmoja katika nyumba yako aliye katika kweli, huenda ukataka kutumia sehemu za kitabu hicho kwa ajili ya funzo lenu la familia. Familia kadhaa zilianza kufanya hivyo siku chache tu baada ya kupokea nakala katika mkusanyiko. Hili halimaanishi kwamba mambo mengine, kama vile utayarishaji wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, yapasa kupuuzwa. Lakini waweza kuona kuna manufaa kutumia dakika nyinginezo 15 au 20 za kusoma na kuzungumza habari iliyo kwenye kitabu Wapiga Mbiu.
9 Familia fulani zasoma kurasa mbili au tatu—labda kwenye kichwa kidogo kimoja au viwili—kila jioni kabla ya kuondoka kwenye chakula cha jioni. Wakiwa mmoja-mmoja huenda wakawa tayari wamesoma sehemu kubwa ya kitabu, lakini wananufaika kutokana na mwendo wa taratibu kidogo pamoja na fursa ya kuzungumzia habari hiyo. Baadhi ya wale wanaofanya hivyo wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa miaka mingi. Wanaposoma, kumbukumbu nyingi zenye kupendeza zachochewa. Mioyo yao huchangamka wanapozungumza pamoja juu ya ushiriki wao wenyewe katika matukio yale wanayosoma.
10 Kwa sababu ya hali zilizo nyumbani kwako, huenda ukajipata unasoma peke yako. Dada mmoja aliyeandikia Sosaiti alisema: “Nimekuwa nikikisoma kitabu hicho kidogo kidogo kila usiku kabla ya kwenda kitandani. Kitabu hiki kinaniongezea uthamini wa kina kirefu na upendo kwa ile kweli, nami nahisi nikiwa karibu zaidi na Yehova na mwenye shukrani sana kwamba nimo sehemu ya tengenezo lake. Nafurahia kwelikweli kila ukurasa ninaosoma.”
11 Ijapokuwa kitabu ni kikubwa, sehemu moja-moja si kubwa. Sehemu ya kwanza ni ya haraka lakini yenye matukio ya kusisimua kutoka siku za Abeli mpaka mwaka 1992—katika kurasa 108 tu. Sehemu nyingine zaanzia kurasa 13 hadi 150. Kila ya sehemu hizi imegawanywa katika sura kadhaa. Badala ya kuharakisha kuzipitia, chukua sehemu moja, sura moja, au kichwa kidogo hatua kwa hatua; ifurahie; na ufaidike nayo.
12 Chukua Wakati Kufikiria Juu ya Yale Unayosoma: Kusudi lako litakuwa nini unaposoma? Kumaliza kurasa tu—kukamilisha kitabu—hakupaswi kuwa lengo lako. Kitabu Wapiga Mbiu kina rekodi ya urithi wako wa kiroho. Wapaswa kuijua vema. Chukua wakati ufikirie maana halisi ya unayosoma. Unapopitia utendaji wa mashahidi wa Yehova wa kale, fikiria jinsi unavyoweza kuiga imani yao. (Ebr. 12:1, 2) Unaposoma juu ya kusitawishwa kwa uasi-imani mkuu, angalia kipekee mitego ambayo iliwanasa wale ambao waligeuka, ili ulinde hali yako mwenyewe ya kiroho. Na unapopitia historia yetu ya ki-siku hizi, angalia sifa za kiroho za wale waliotumiwa na Mungu, jinsi walivyoonyesha kwamba kufanya mapenzi ya Mungu kulikuwa jambo la maana zaidi maishani mwao, jinsi walivyoitikia hali mbalimbali—baadhi yazo zikiwa ngumu sana—ambazo Mungu aliruhusu.—Ebr. 13:7.
13 Utaona ikiimarisha imani kuchunguza mambo yanayoonyesha jinsi Yehova ameongoza watu wake kwenye uelewevu wa wazi juu ya kweli ya Biblia ambayo twafurahia sasa. Uthamini wako kwa mpango unaoonekana ambao Yehova anatumia utakua unapofahamu vyema ukuzi wa tengenezo. Bila shaka utasisimuka unaposoma jinsi, kwa utimizo wa unabii, habari njema zimefika kwenye sehemu ya mbali zaidi ya dunia. Moyo wako utachangamshwa na mambo yaliyoonwa ya waaminifu katika sehemu zote za ulimwengu ambao wamefanya kazi kwa bidii kupiga mbiu ya Ufalme. Utaimarishwa kushughulika na majaribu ya binafsi unaposoma yale ambayo ndugu na dada waaminifu wamevumilia tayari kwa sababu ya upendo wao kwa Yehova.
14 Baada ya kusoma kisehemu cha habari hiyo, chukua wakati mzungumze pamoja juu ya thamani yacho na kupitia habari zote. Ikiwa una watoto wadogo, wahusishe waeleze picha na wakuambie wanayojua kuhusu watu walioonyeshwa. Hata kama unasoma peke yako, jitahidi kushiriki na wengine yale unayojifunza. Ikifaa, tumia habari katika ziara za kurudia na unapoongoza mafunzo ya Biblia nyumbani. Kwa kukirudia kitakazika akilini na moyoni mwako, na kunufaisha wengine pia.
15 Pendezwa Hata na Mambo Madogomadogo: Vipindi unavyojitolea kusoma kitabu Wapiga Mbiu vyapaswa kufurahisha na kunufaisha.
16 Je! ungependa familia yako itembelee makao makuu ya Mashahidi wa Yehova? Kurasa 208-9 zaonyesha vifaa vilivyotumiwa na Sosaiti karne moja iliyopita katika eneo la Pittsburgh. Kurasa 216-17 zakujulisha majengo yaliyotumiwa baadaye katika Brooklyn. Picha zilizo kwenye kurasa 352-6 zaweza kukusaidia kuona makao makuu leo. Sura 26 na 27 zimejaa habari kuhusu kazi inayofanywa Betheli, na kurasa 295-8 zatoa habari zaidi kuhusu maisha ya Betheli.
17 Wengi wetu hatuwezi kutembelea makao yaliyo mengi ya Sosaiti. Kurasa 357-401 za kitabu Wapiga Mbiu zakupeleka katika utalii wa ulimwengu. Hakuna haja ya kufanya haraka. Tumia wakati kidogo katika kila nchi na uifurahie. Tumia ramani ya ulimwengu iliyoko kwenye kurasa 415-17 kupata kila mahali. Soma maelezo yanayoambatana na picha ya kila tawi. Kupitia fahirisi waweza pia kupata habari nyingine zenye kusisimua za kila nchi. Tumia fursa hii upate kujua washiriki wa familia yako ya kiroho katika nchi nyinginezo.
18 Watu wanapokuwa pamoja kijamii, wao hucheza michezo wakati mwingine ambayo yahusisha ujuzi wa mambo hakika ya kawaida. Je! haingefaa zaidi kupata kujua tarehe za kufikiriwa na matukio katika historia ya kisasa ya watu wa Yehova? Utapata mambo mengi ya jinsi hiyo yameorodheshwa kwenye kurasa 718-23 katika kitabu Wapiga Mbiu. Orodha hiyo yaandaa mawazo ya msingi; waweza kuiongezea mambo madogomadogo yanayopatikana katika kitabu chote. Yatumie kwa ajili ya pitio. Walio wachanga katika familia labda watayakariri upesi. Wengine wetu tulio wakubwa huenda tukafanya polepole kidogo. Lakini hayo ni mambo madogomadogo ya historia ya kitheokrasi ambayo sisi sote twaweza kunufaika kutokana na kuyajua. Baada ya kujifunza tarehe na mambo ya msingi ya hakika, jenga kwenye msingi huo. Ona ni habari zipi unazoweza kukumbuka kuhusu kila tukio. Kisha ongea juu ya sehemu ambayo kila tukio ilikuwa nayo katika kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu. Kisha, zungumza jinsi limeathiri maisha yako mwenyewe na jinsi wewe unavyofaana na yale ambayo Yehova anafanya.
19 Ona Fursa Zinazopatikana Kwako: Unaposoma na kuzungumzia Mashahidi wa Yehova—Wapiga Mbiu ya Ufalme wa Mungu, utapata maoni yako yakifunguka kuhusu utimizo mtukufu wa Isaya 60:22. Kitabu hicho kwenye ukurasa 519 chasema hivi: “Utimizo wa ahadi kwamba ‘mdogo angekuwa elfu’ umetimia kikweli, tena kwa wingi! Katika kila mojawapo nchi 50 na zaidi, ambako hakukuwa hata na ‘mdogo’—ambako hakukuwa na Mashahidi wa Yehova wowote huko nyuma katika 1919, ambako hawakuwa wamehubiri hata kidogo—leo kuna wasifaji wa Yehova zaidi ya elfu moja. Katika baadhi ya nchi hizo, sasa kuna makumi ya maelfu, naam, hata zaidi ya mia moja elfu, ya Mashahidi wa Yehova ambao ni wapiga mbiu ya Ufalme wa Mungu wenye bidii! Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wamekuwa ‘taifa hodari’—wengi katika idadi wakiwa kutaniko lililounganika la tufeni kuliko idadi ya watu wote ya mojawapo mataifa huru ya ulimwengu angalau 80.”
20 Kazi hiyo ya ongezeko la Ufalme haijakoma hata kidogo. Kinyume cha hivyo, Yehova amezidisha mwendo wayo kwa kiwango kisicho na kifani. Wewe utaishiriki kwa kadiri gani? Je! unatambua fursa zote zilizo wazi kwako? Unapojifunza yale ambayo wengine wanafanya, moyo wako mwenyewe na usukumwe ujitoe ili kushiriki kikamili kazi hiyo tukufu ambayo Mungu wetu mwenye upendo anaielekeza kupitia Yesu Kristo katika siku yetu.