“Watu wa Kuchukiwa na Mataifa Yote”
1 Miaka ya karibuni sisi sote tumefurahia kusikia juu ya ripoti zenye kusisimua juu ya baraka za kustaajabisha zinazofurahiwa na watu wa Yehova ulimwenguni pote. Kuhalalishwa kwa kazi katika Malawi baada ya miaka 26 ya mnyanyaso wenye ukatili kulitufanya tutoe machozi ya shangwe. Tulifarijika tuliposhuhudia kuanguka kwa Ukomunisti usiomcha Mungu katika Ulaya Mashariki ambao ulisababisha kuwekwa huru kwa maelfu ya ndugu kutoka nira ya mnyanyaso. Tulitazama kwa hangaiko la hamu wakati uhuru wetu wa ibada ulipopingwa katika Ugiriki; tulichangamshwa tulipopata ushindi uliovuma katika mahakama iliyo kuu zaidi katika Ulaya. Tumekuwa tukifurahishwa na ripoti kuhusu upanuzi mkubwa wa matawi ya Sosaiti ambao umefanya kutokezwa kwa wingi wa fasihi kwa ajili ya wenye kutafuta kweli. Tulistaajabu sana tulipojua kwamba zaidi ya watu 7,400 walibatizwa kwenye mkusanyiko katika Kiev, Ukraine. Ndiyo, maendeleo hayo makubwa yamezidisha uchangamfu wetu!
2 Ijapokuwa sababu yetu ya kuwa na shangwe ni kubwa, twapaswa kulinda dhidi ya kuwa na uchangamfu wa kupita kiasi. Mfululizo wa ripoti zenye upendeleo waweza kutufanya tuamue kwamba upinzani wa habari njema unaporomoka na kwamba watu wa Yehova wanapata ukubali ulimwenguni pote. Kufikiri huko kwaweza kudanganya. Ijapokuwa tumepata ushindi fulani fulani wa kuridhisha na kupata mafanikio fulani ya kupunguziwa vizuizi vya habari njema katika nchi fulani, hatupaswi kusahau kwamba kanuni yetu ya uhusiano na ulimwengu haibadiliki. Tukiwa wafuasi wa Yesu sisi “si wa ulimwengu.” Kwa hivyo, tuna uhakika wa kuwa “watu wa kuchukiwa na mataifa yote.” (Yoh. 15:19; Mt. 24:9) Kwa muda ambao mfumo huu wa mambo utakuwapo, hakuna jambo lolote litakalobadilisha kawaida ya kwamba “wote wapendao kuishi maisha ya utauwa [ujitoaji kimungu, NW] katika Kristo Yesu wataudhiwa.”—2 Tim. 3:12.
3 Historia yathibitisha ukweli wa onyo hilo. Ijapokuwa Yesu, Mwanzilishi wa Ukristo, alitoa ushahidi wa kustaajabisha mbele ya watawala wenye nguvu na raia wao, alitendwa vibaya kila siku na alikuwa katika hatari ya daima ya kuuawa. Hata ingawa wafuasi wake waliwasaidia wengi kuwa wanafunzi, wakashiriki kuandika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na kuonyesha karama za roho za kufanya miujiza, wao vilevile walichukiwa na kutendwa vibaya. Ujapokuwa mwenendo wao mwema na upendo kwa jirani, Wakristo wote walionwa na wengi kuwa “madhehebu” hafifu ‘iliyonenwa vibaya kila mahali.’ (Mdo. 28:22) Ijapokuwa kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote leo limekuwa likitumiwa na Yehova kwa njia ya ajabu kutimiza mapenzi yake, limekuwa likipingwa sana na kunenewa maovu na kila chombo cha mfumo huu wa mambo. Hakuna sababu ya kutazamia upinzani huo upungue.
4 Katika karne ya kwanza, Shetani alinyanyasa wanafunzi wa Yesu kwa njia mbalimbali. Wapinzani wenye chuki walisema uwongo mtupu uliowasingizia. (Mdo. 14:2) Kuliwa na matisho makali kwa kujaribu kuwaogofya. (Mdo. 4:17, 18) Umati wenye hasira ulijaribu kuwanyamazisha. (Mdo. 19:29-34) Walitiwa gerezani bila sababu ya haki. (Mdo. 12:4, 5) Wanyanyasi mara nyingi walitumia jeuri ya kimwili. (Mdo. 14:19) Katika visa fulani wasio na hatia waliuawa kimakusudi. (Mdo. 7:54-60) Mtume Paulo alivumilia karibu kila namna zote hizo za kutendwa vibaya. (2 Kor. 11:23-27) Wapinzani walikuwa na haraka ya kutafuta fursa yoyote ya kuingilia kazi ya kuhubiri na kutesa wafanyakazi waaminifu hao.
5 Leo Shetani anatumia mbinu hizohizo. Uwongo mtupu umesemwa, ukituonyesha kwa njia isiyo ya kweli kuwa farakano na kidhehebu kilichopotezwa njia. Katika nchi nyingine, mamlaka zimetangaza fasihi zetu kuwa zenye kuharibu umoja nao wamezipiga marufuku. Heshima yetu kwa utakato wa damu imedhihakiwa na kubishwa peupe. Katika miaka ya 1940, umati wenye ghasia ulishambulia ndugu zetu kwa sababu ya suala la bendera, wakawajeruhi, na kuharibu mali yao. Maelfu wamepelekwa gerezani kwa sababu ya suala la kutokuwamo. Katika nchi zenye utawala wa kiimla wameshtakiwa kwa uwongo kuwa wataka-mapinduzi, ikisababisha wengi kuumizwa vibaya na kuuawa katika magereza na kambi za mateso. Mbano huo umekuwa haupungui, ikionyesha wazi kwamba sisi ni watu wa kuchukiwa bila sababu ya haki.—Ona Wapiga Mbiu, sura 29.
6 Twaweza Kutazamia Nini Wakati Ujao? Ijapokuwa watu wa Yehova huenda wakapata ushindi wa mara kwa mara katika sehemu fulani ya dunia, hali kwa ujumla yabaki ileile. Ibilisi aendelea kuwa mwenye hasira kwa sababu ya kushushwa kwake katika 1914. Yeye ajua kuwa wakati wake ni mchache. Ghadhabu yake bila shaka itazidi kadiri dhiki kuu ikaribiapo. Yeye anajishughulisha kabisa na vita yake dhidi ya Mfalme mtawazwa, Kristo Yesu, naye ameazimia kupigana mpaka mwisho. Yeye na roho wake waovu wanaweza kuonyesha hasira yao kwa watu wa Yehova hapa duniani tu, “wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”—Ufu. 12:12, 17.
7 Hivyo, tutazamiapo wakati ujao, twahitaji kuwa na maoni ya uhalisi juu ya mambo ya kutarajia. Hakuna sababu ya kufikiri kwamba Ibilisi ataacha chuki yake au kukata tamaa. Chuki juu yetu ambayo ameingiza katika ulimwengu huu yaweza kulipuka wakati wowote na mahali popote. Katika nchi nyingi uhuru wetu wa kuhubiri umepatikana tu baada ya kuung’ang’ania kwa muda mrefu. Uhuru huo waweza kuwa wa muda mfupi, wenye kuendelezwa tu na mtawala wa sasa mwenye huruma au sheria isiyojulikana. Mapinduzi makubwa yaweza kutokea kwa ghafula, yakileta fujo nyingi na matendo mabaya juu ya haki za kibinadamu.
8 Usitawi na uhuru tunaofurahia sasa katika nchi kadhaa waweza kumalizika ghafula, ukifanya ndugu zetu watendwe vibaya sawasawa na wakati uliopita. Hatupaswi kujiruhusu tutiwe katika roho ya kutohangaikia au kutojali, tukifikiri kwamba maadui zetu wameshindwa. Chuki ya ulimwengu huu huenda isionyeshwe kikamili sikuzote, lakini hubaki yenye nguvu. Kila kitu katika Neno la Mungu huonyesha kwamba upinzani wa ulimwengu utazidi badala ya kupungua mwisho ukaribiapo. Kwa hiyo twapaswa kuwa macho, tukijionyesha kuwa wenye “busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua.” (Mt. 10:16) Twapaswa kutambua kwamba tutakuwa na ‘ushindani’ hadi mwisho, na uvumilivu ndio ufunguo wa kuokoka kwetu.—Yud. 3; Mt. 24:13.
9 Katika sehemu ya ulimwengu tunamoishi, kazi yaweza kufaulu bila kizuizi chochote kinachotambuliwa na wapinzani. Hilo laweza kutufanya tuwe wenye shaka juu ya kuwapo kwa hangaikio lolote kubwa. Hata hivyo, kuna uhitaji wa kuwa macho. Hali zaweza kubadilika haraka. Bila kutoa onyo, wapinzani wanaweza kutumia suala fulani na kulitumia dhidi yetu. Waasi-imani hutafuta daima sababu fulani ya kulalamika. Viongozi wa kidini wenye hasira ambao huhisi kutishwa na kazi yetu huenda wakatushutumu hadharani. Mipango yetu ya kujenga Jumba la Ufalme katika eneo letu huenda ikatokeza kwa ghafula mashindano yenye kukasirisha ujirani wote. Maneno yenye hamaki yanaweza kuonekana kwenye magazeti, yakitoa sifa isiyofaa juu yetu. Watu mashuhuri wa mahali petu huenda wakatusingizia kimakusudi, wakisababisha jirani zetu wawe wabaya sana tunapowatembelea. Hata wapendwa wetu katika nyumba zetu wenyewe huenda wakachukizwa nasi na kutunyanyasa. Kwa hiyo kuna uhitaji wa kuwa macho, tukitambua kwamba uadui wa ulimwengu ungalipo, nao waweza kutokea wakati wowote.
10 Hilo Lapaswa Kutuathirije? Yote hayo yafaa kuathiri kufikiri kwetu na mtazamo wetu wa wakati ujao. Kwa njia gani? Je! hilo lapaswa kutuhangaisha, na kufanya tuogope mambo ambayo huenda tukavumilia? Je! twapaswa kupunguza kazi yetu ya kuhubiri kwa sababu watu fulani katika jamuiya yetu huenda wakasumbuliwa nayo? Je! kuna sababu ya maana kuhisi tumechokozeka tunapotendewa maovu isivyo haki? Je ni jambo lisiloepukika kwamba kutendewa vikali kutatunyang’anya shangwe yetu ya kumtumikia Yehova? Je! kuna ukosefu wowote wa hakika kuhusu matokeo? La, kamwe! Kwa nini?
11 Hatupaswi kamwe kusahau uhakika wa kwamba habari tunayohubiri yatoka kwa Yehova, si kwetu. (Yer. 1:9) Sisi tuna wajibu wa kutii sihi hii: “Liitieni jina lake. Yatangazeni matendo yake kati ya mataifa . . . katika dunia yote.” (Isa. 12:4, 5) Amevumilia kutendwa vibaya kwa watu wake kwa kusudi mahususi, yaani, ‘ili jina lake litangazwe katika dunia yote.’ (Kut. 9:16) Twafanya kazi tuliyoamriwa na Yehova, naye ndiye atupaye uhodari wa kuongea kwa ujasiri. (Mdo. 4:29-31) Hii ndiyo kazi ya maana, ya kunufaisha na yenye uharaka zaidi ambayo yaweza kufanywa katika siku hizi za kumalizia za mfumo huu wa kale.
12 Ujuzi huu hutupa uhodari wa kuwa na msimamo thabiti kwa kupinga Shetani na ulimwengu huu moja kwa moja. (1 Pet. 5:8, 9) Kujua kwamba Yehova yu pamoja nasi hutufanya tuwe “hodari na moyo wa ushujaa,” tukiondoa sababu zozote za woga mbele ya wanyanyasi wetu. (Kum. 31:6; Ebr. 13:6) Huku sikuzote tukijaribu kuwa na busara, wenye kusababu vizuri, na wenye akili tunapotishwa na wapinzani, tutajulisha waziwazi kwamba tumeazimia “kumtii Mungu kuliko wanadamu” ibada yetu inapopingwa. (Mdo. 5:29) Kunapokuwa na fursa inayofaa ya kuongea ili kujitetea, tutafanya hivyo. (1 Pet. 3:15) Hata hivyo, hatutapoteza wakati wetu tukibishana na wapinzani wagumu wanaopendezwa na kutuharibia sifa. Badala ya kukasirika au kujaribu kulipiza kisasi wanapotutenda maovu au kutushtaki kiuwongo, sisi ‘twawaacha’ tu.—Mt. 15:14.
13 Uvumilivu wetu kupitia majaribu unampendeza Yehova. (1 Pet. 2:19) Ni lazima tulipie gharama gani kupata ukubali huo? Je! twapaswa kujiuzulu wenyewe tuache kutumikia kwa shangwe kwa sababu twachukiwa na twapingwa? Bila shaka la! Yehova aahidi kuthawabisha utii wetu kwa ‘furaha na amani.’ (Rum. 15:13) Kujapokuwa na kuteseka kwingi, Yesu aliendelea kuwa na furaha kwa sababu ya “furaha iliyowekwa mbele yake.” (Ebr. 12:2) Ndivyo ilivyo kwetu sisi. Kwa sababu zawadi ya uvumilivu wetu ni kubwa sana, twachochewa ‘kufurahi na kushangilia’ ijapokuwa twapatwa na majaribu makali. (Mt. 5:11, 12) Hata wakati wa dhiki, shangwe hii, yenyewe, ni sababu ya kusifu na kumheshimu Yehova kwa kutegemeza ujumbe wa Ufalme.
14 Je! kuna mashaka yoyote juu ya matokeo ya mwisho, yakitusababisha tuhangaike au tusitesite? La, tokeo la hitilafiano kati ya tengenezo la Yehova na ulimwengu wa Shetani liliamuliwa zamani sana. (1 Yoh. 2:15-17) Bila kujali wingi wa upinzani, Yehova atatupa ushindi. (Isa. 54:17; Rum. 8:31, 37) Hata ingawa twajaribiwa kabisa, hakuna kitakachotuzuia kupata zawadi. Hatuna sababu ya ‘kujisumbua kwa neno lolote,’ kwa sababu Yehova ametupa amani kwa kujibu dua zetu.—Flp. 4:6, 7.
15 Kwa hiyo twamshukuru Yehova kila wakati tusikiapo ripoti juu ya ndugu zetu wanaookolewa kutoka mnyanyaso au wanaopewa uhuru wa kuhubiri maeneo ambayo wamekuwa na kizuizi wakati uliopita. Twafurahi wakati hali zenye kubadilika zifunguapo fursa kwa maelfu ya watu wenye moyo mweupe wajue ujumbe wa Ufalme. Twafurahia kwelikweli Yehova anapochagua kutupa ushindi tunaposhughulika na wapinzani wenye chuki. Twajua kwamba atabariki na kusitawisha kazi yetu katika njia yoyote ile ihitajiwayo ili kukweza nyumba yake ya ibada ya kweli na kuwapa watu ‘wanaotamanika’ fursa ya kuingia.—Hag. 2:7; Isa. 2:2-4.
16 Kwa wakati uleule, twajua vema kwamba adui yetu, Shetani, ni mwenye nguvu sana, naye atatupinga sana mpaka mwisho. Mashambulio yake yaweza kuwa wazi na mabaya sana, au yaweza kuwa yenye ujanja na yenye kudanganya. Mnyanyaso waweza kutokea ghafula mahali ambapo pamekuwa na amani tupu wakati uliopita. Wapinzani waovu waweza kuwa wakali mno na wakatili katika jitihada za kutuumiza isivyo haki. Kwa wakati unaofaa itakuwa wazi kwa wote kwamba wao kwa kweli ‘wanapigana na Mungu,’ naye atawaharibu kabisa. (Mdo. 5:38, 39; 2 The. 1:6-9) Kwa sasa, kujapokuwa yale ambayo ni lazima tuvumilie, twaazimia kubaki tukiwa imara katika kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu na kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Sisi ndio watu wenye furaha zaidi duniani, tukijua kwamba ‘tukiiisha kukubaliwa tutaipokea taji ya uzima.’—Yak. 1:12.