Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 11/15 kur. 510-514
  • “Bwana Awe na Roho Unayoonyesha”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Bwana Awe na Roho Unayoonyesha”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “ROHO” YA KUNDI
  • KUOKOA ROHO YA KUNDI
  • KUNDI LA KWANZA LA KIKRISTO NI KIELELEZO CHA LEO
  • WAANGALIZI WANYENYEKEVU, WENYE UPENDO
  • ROHO ILIYOONYESHWA NA WENGINE
  • KUJENGA WAABUDU WENZETU
  • Akila na Prisila—Wenzi Walio Kielelezo Chema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Ni Roho Ya Aina Gani Unayoonyesha?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Wakristo Wanahitajiana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Akila
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 11/15 kur. 510-514

“Bwana Awe na Roho Unayoonyesha”

“Bwana awe na roho unayoonyesha. Fadhili zake zisizostahilika ziwe pamoja na ninyi.”​—2 Tim. 4:22, NW.

1, 2. Roho aliyo nayo mtu inaweza kusemwa kwamba ni nini? Tafadhali toa mifano ya Maandiko. (Flm. 25)

KILA mtu ana roho fulani. Yaani, ana nia fulani, maelekeo au nguvu inayomwongoza afanye mambo. Kwa hiyo, si ajabu kwamba mara nyingi watu wanajulikana walivyo kwa sababu ya kusudi linaloongoza maneno na matendo yao.

2 Maandiko Matakatifu yanataja sifa za watu fulani zilizowaongoza kufanya mambo. Kwa mfano: Musa, nabii wa Yehova Mungu, anaelezwa kwamba alikuwa “mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hes. 12:3) Abigaili, ambaye mwishowe akawa mke wa Daudi Mfalme wa Israeli, alikuwa “mwenye akili njema.”​—1 Sam. 25:3, 39.

3. (a) Kwa sababu gani inawapasa Wakristo wawe na roho njema? (b) Paulo alitaka nini kuhusu roho ya Timotheo?

3 Wakristo wa kweli wameuvaa “utu mpya” na inawapasa wawe na roho njema. Ingawaje, wamejivika nguvu zenye kuongoza matendo yao, kama upendo, huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole na ustahimilivu. Wanasitawisha na kuonyesha matunda ya roho ya Mungu, yaani, upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole na kujiweza. (Gal. 5:22, 23; Efe. 4:20-24; Kol. 3:9-14) Bila shaka, inapasa watu wawe na nia nzuri katika kundi la Kikristo, kwa maana mtume Paulo alimwandikia Timotheo mfanya kazi mwenzake akasema: “Bwana awe na roho unayoonyesha. Fadhili zake zisizostahilika ziwe pamoja na ninyi.” (2 Tim. 4:22, tafsiri ya Kiingereza ya New World) Paulo alitaka Mungu amtumie Bwana Yesu Kristo kuikubali nguvu iliyoongoza mtendo ya Timotheo.

“ROHO” YA KUNDI

4. (a) Je! kundi lina roho? (b) Basi linatakiwa liwe na roho ya namna gani?

4 Kila mtu ana roho fulani anayoonyesha, na kundi zima la watu wa Mungu lina roho fulani pia. Mtu mwenye kuchunguza sana mambo ataiona nguvu hiyo ikifanya kazi katika akili na mioyo yao, na labda nguvu hiyo itatokeza roho ya urafiki, upendo, utulivu na amani, au juhudi na shauku. Bila shaka, huenda wakawa na roho yenye matokeo mabaya. Lakini inakuwa baraka kubwa wanapokuwa na roho njema! Ni wazi kwamba mtume Paulo alitaka makundi yaonyeshe roho hiyo. Aliandikia kundi la Wakristo waliokuwa mjini Filipi, akasema: “Fadhili zisizostahilika za Bwana Yesu Kristo ziwe pamoja na roho mnayoonyesha.” (Flp. 4:23, tafsiri ya Kiingereza ya New World) Mtume alisema ayo hayo alipowaandikia Wakristo Wagalatia.​—Gal. 6:18.

5. Roho nzuri sana ya kundi inaweza kuwa na mambo gani?

5 Je! wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Ikiwa wewe ni mmoja wao, kundi unaloshirikiana nalo lina roho ya namna gani? Huenda likawa lina roho nzuri sana, Huenda kundi likawa linaitikia sana mashauri linalopewa kutokana na Maandiko. Tena, huenda likawa lina roho ya upendo, uchangamfu, mapatano na ukaribishaji. Huenda washiriki wa kundi wakawa ni watu wa kiroho sana katika maoni yao. Ikiwa ndivyo walivyo, ‘fadhili zisizostahilika za Bwana Yesu Kristo ziko pamoja na roho mnayoonyesha.’​—Flm. 25.

KUOKOA ROHO YA KUNDI

6. Ni hali gani isiyofaa iliyokuwa ikiachiliwa katika kundi la Korintho?

6 Inapasa roho njema hiyo iendelee kuwapo. Ubora wa kuhifadhi roho ya kundi ulikaziwa katika mji wa kale wa Korintho, Mtume Paulo alijulishwa kwamba uasherati ulikuwa ukiachiliwa kati ya Wakristo wa mji huo, “zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye.”​—1 Kor. 5:1.

7, 8. Kulingana na anayosema Paulo, kwa sababu gani ilikuwa lazima kumtenga Mkorintho huyo mwasherati?

7 Waangalizi wa kundi hilo hawakuwa wamemfukuza mtu huyo, lakini Paulo aliwahimiza “kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe [au, “uharibiwe,” New World]” Iliwapasa kumwondoa katika kundi la Kikristo aingie katika ulimwengu unaotawalwa na Shetani Ibilisi, unaongojea uharibifu. (1 Yohana 5:19) Kwa sababu gani iliwapasa kuchukua hatua hiyo? Ni kama vile Paulo alivyosema, “ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu” Kristo.​—1 Kor. 5:3-5.

8 Mtu huyo alipaswa kutengwa na ushirika ili “roho” au hali ya kiroho ya kundi iliyotegemea Neno la Mungu iokolewe. Ama sivyo, ‘chachu kidogo ingelichachusha donge zima,’ yaani, maongozi yenye kupotoa hali ya kiroho yangeenea katika kundi lote, naye Yehova angelikatilia mbali kundi hilo. Leo pia ni jambo la maana kuokoa roho ya kundi inayotegemea Neno lililoongozwa na Yehova.​—1 Kor. 5:6.

KUNDI LA KWANZA LA KIKRISTO NI KIELELEZO CHA LEO

9. Makundi ya karne ya kwanza kwa ujumla yalionyesha roho gani?

9 Ni kweli kwamba iliwapasa wazee wa makundi ya karne ya kwanza kukesha kiroho ili “roho iokolewe.” Ni wazi kwamba matatizo yalitokea nyakati nyingine. Hata hivyo, kwa ujumla roho ya makundi ya kwanza ya Kikristo ilikuwa na uchangamfu mwingi sana, upendo na kufikiriana kwingi sana. Yesu Kristo alikuwa amesema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Walionyesha upendo huo nyakati zote. Kwa mfano, mtume Yohana alimwita Gayo, mwabudu mwenzake, “mpenzi, nimpendaye katika kweli.”​—3 Yohana 1.

10. Mitume walikuwa na uhusiano wa namna gani pamoja na waamini wenzao?

10 Mitume walikuwa wakifanya kazi pamoja na ndugu na dada zao katika imani, wala hawakuwapigia makelele. Hawakuwa wakiwatolea amri kali-kali. Bali, wanaume hao waliisihi mioyo ya waamini wenzao. Basi ilifaa washiriki wa Kikristo wakaitwa “ndugu,” “wapenzi” na “washirika. . . katika fadhili zisizostahilika.” (Flp. 1:7, New World; 4:8; 1 Pet. 4:12; 1 Yohana 4:1) Hali hiyo ya upendo ilikuwako kwa sababu walitaka sana kuona warithi wenzao wa uzima wakiwa na hali njema ya kiroho.​—Yak. 2:5; 1 Pet. 3:7.

WAANGALIZI WANYENYEKEVU, WENYE UPENDO

11. Wewe unaweza kusema mtume Paulo aliwaonaje ndugu na dada zake wa kiroho? (1 The. 27)

11 Hali ya kupendana na kuheshimiana iliyoenea katika makundi ya karne ya kwanza ilionyesha kwamba Wakristo mmoja mmoja walikuwa na sifa hizo. Kwa mfano mchukue mwangalizi mwenye kusafiri, Paulo. Moyo wake ulikuwa ‘umekunjuka’ ili kuwapenda sana waamini wenzake katika Korintho. (2 Kor. 6:11-13) Tena, moyo wake ulijawa na kupenda ndugu na dada zake wa kiroho kila mahali. Si ajabu kwamba kila siku alipata kwa wingi “maangalizi ya makanisa yote”!​—2 Kor. 11:28.

12, 13. (a) Paulo alikuwa na roho gani alipowaonya wazee Wakristo katika Efeso? (b) Wazee wa Efeso walionaje Paulo alipowaaga?

12 Je! Paulo alikuwa mwenye kiburi, akapiga ubwana juu ya waabudu wengine wa Yehova? Hasha! Kwa mfano, hakukemea wazee Wakristo katika Efeso wala hakutumia mamlaka kuwafanyia madai alipokuwa akiwaonya. Aliwasihi kwa upendo. Waangalizi hao walijua kwamba mtume alisema kweli aliponena hivi: “Mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi.” (Matendo 2018, 19, 31) Lo! mzee mnyofu na mnyenyekevu namna gani! Bwana wake alimtazamia aonyeshe roho hiyo, maana Yesu Kristo alisema: “Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu.”​—Mt. 20:25-27.

13 Sasa, wafikirie tafadhali waangalizi hao wa Efeso. Je! walikuwa wenye uadui, wakajitenga wawe peke yao? Hasha! Sivyo Neno la Mungu linavyoonyesha. Wakati Paulo alipokuwa karibu kuwaaga katika Mileto, tunaambiwa kwamba ilikuwa hivi: “Akapiga magoti, akaomba pamoja nao wote. Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu, wakihuzunika zaidi kwa sababu ya neno lile alilosema, ya kwamba hawatamwona uso tena.” (Matendo 20:36-38) Wasingalifanya hivyo kama wasingalikuwa wanyenyekevu. Bila shaka, ‘Bwana alikuwa pamoja na roho waliyoonyesha.’

ROHO ILIYOONYESHWA NA WENGINE

14. Lidia alionyesha sifa gani ya pekee?

14 Lakini namna gani juu ya washiriki wengine wa kundi la kwanza la Kikristo? Wakristo leo wanapaswa kufuata mfano bora wa roho njema ambayo Maandiko yanaonyesha washirika wa kundi hilo walikuwa nayo. Kwa mfano, Lidia na nyumba yake, waliokuwa wakaaji wa Filipi, walikuwa kati ya watu wa kwanza walioukubali Ukristo katika Ulaya. Lidia alizikubali habari njema zilizohubiriwa na Paulo, akabatizwa, na mara baada ya hapo akaonyesha sifa za ukaribishaji. Alisema, “Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani mwangu mkakae.” Luka, msafiri mwenzi wa Paulo, aliandika akasema, “Akatushurutisha.” (Matendo 16:11-15) Labda ukaribishaji wa Lidia ni jambo mojawapo lililomfanya mtume awaambie baadaye Wakristo Wafilipi: “Namshukuru Mungu wangu kila niwakumbukapo . . . kwa sababu ya ushirika wenu katika kuieneza Injili, tangu siku ile ya kwanza hata leo hivi.” (Flp. 1:3-5) Naam, ‘Bwana alikuwa pamoja na roho iliyoonyeshwa’ na Wafilipi hao kutia na Lidia mwaminifu.

15-17. (a) Kwa sababu gani Akila na Prisila waliweza ‘kumweleza Apolo njia ya Mungu kwa usahihi zaidi’? (b) Inawezaje kusemwa kwamba Bwana alikuwa pamoja na roho iliyoonyeshwa na Akila na Prisila?

15 Akila Myahudi na Prisila mkewe walikuwa na roho njema pia. Walifukuzwa Rumi wakati Mfalme Klaudio alipoagiza Wayahudi waondolewe (mwaka 50 W.K.), basi wakawa wakaaji wa Korintho. Miezi kadha baadaye, mtume Paulo alifika huko wakampokea nyumbani kwao. Wote watatu walishirikiana kutengeneza hema. Bila shaka, Akila na Prisila walimsaidia mtume kulijenga kundi jipya la Korintho.​—Matendo 18:1-11.

16 Wakati Paulo aliposafiri baharini kwenda Shamu mwaka 52 W.K., Akila na Prisila walifuatana naye mpaka Efeso. Mume na mke huyo waliruhusu nyumba yao huko iwe ikitumiwa na kundi kama mahali pa kukutania. Huko huko Efeso, Akila na Prisila walipata pia pendeleo la ‘kumweleza Apolo njia ya Mungu kwa usahihi zaidi.’ (Matendo 18:18-26; 1 Kor. 16:8, 19) Waliweza kumfundisha hivyo kwa sababu walilifahamu sana Neno la Mungu na mapenzi yake.

17 Wakati mtume Paulo alipoandikia Wakristo Warumi karibu na mwaka 56 W.K., Akila na Prisila walikuwa wamekwisha rudi Rumi. Kwa mara nyingine waliruhusu nyumba yao huko itumiwe kama mahali pa mikutano ya Kikristo. Paulo aliwasalimu kwa kuwaita “watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia.” (Rum. 16:3-5) Wakati fulani, Akila na Prisila walikuwa wamehatirisha maisha yao kwa ajili ya Paulo. Muda mfupi kabla Paulo hajauawa kwa sababu ya imani karibu na mwaka 65 W.K., alimtuma Timotheo akamsalimie watu hao wazuri waliooana, waliokuwa wakiishi Efeso wakati huo. Wakati huo Akila na Prisila walikuwa wamekwisha kuwa Wakristo miaka mingi na bado ‘Bwana alikuwa pamoja na roho waliyoonyesha.’​—1 Tim. 1:3; 2 Tim. 4:19, 22.

18. Gayo, rafiki ya mtume Yohana, alikuwa mtu wa namna gani?

18 Karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K. mtume mzee, Yohana, aliandikia Gayo mwamini mwenzake barua yake ya tatu iliyoongozwa na Mungu. Mtume alimpenda Mkristo huyo mwema Gayo alikuwa ‘akienda katika kweli,’ na wengine walikuwa ‘wameshuhudia upendo wake mbele ya kanisa.’ Yohana alijua kwamba Gayo alikuwa mwanamume mkaribishaji na mwenye upendo.​—Yohana 1-8.

19. Kwa sababu gani tunasema bila shaka kwamba Bwana hakuwa pamoja na roho aliyoonyesha Diotrete?

19 Lakini kulikuwa na tofauti kubwa sana kati ya Gayo na mtu fulani aliyeitwa Diotrefe! Yohana alisema: “Naliliandikia kanisa neno, lakini Diotrefe, apendaye kuwa wa kwanza kati yao, hatukubali. Kwa hiyo, nikija, nitayakumbuka matendo yake atendayo, atoavyo upuzi juu yetu kwa maneno maovu; wala hatoshwi na hayo, ila yeye mwenyewe hawakaribishi hao ndugu, na wale watakao kuwakaribisha, huwazuia, na kuwatoa katika kanisa.” (3 Yohana 9, 10) Hakika Bwana hakuwa pamoja na roho aliyoonyesha Diotrefe.

20. Makundi ya kwanza ya Kikristo yalikuwa na watu wengi wa namna gani?

20 Mara kwa mara, mtu wa namna ya Diotrefe angeweza kutokea. Lakini makundi ya wakati huo yalikuwa na Wakristo wengi waaminifu, wenye nguvu za kiroho. Naam, yalikuwa na watu wenye upendo na wakaribishaji, kama Lidia na Gayo. Yalikuwa na watu kama Akila na Prisila, waliokuwa na ufahamu mwingi wa kiroho na nia ya kuruhusu nyumba zao zitumiwe kama mahali pa mikutano ya kundi. Hakika ‘Bwana alikuwa pamoja na roho waliyoonyesha watu hao.’ Ni mtu gani ampendaye Mungu leo asiyetaka kuwa kama wao?

KUJENGA WAABUDU WENZETU

21, 22. (a) Kwa sababu gani wazee Wakristo wa leo wanapaswa watake sana kuona roho ya makundi wanayotumikia? (b) Mwangalizi anaweza kujiuliza maulizo gani juu ya kundi analotumikia?

21 Kama tulivyoona, mtume Paulo aliihangaikia roho ya kundi la Korintho. Tena, alisema alitumaini kwamba ‘Bwana Yesu Kristo angekuwa pamoja na roho iliyoonyeshwa’ na makundi na watu mmoja mmoja. (1 Kor. 5:1-5; Gal. 6:18; Flp. 4:23; 2 Tim. 4:22; Flm. 25) Vivyo hivyo, Yesu Kristo aliyetukuzwa aliihangaikia roho iliyoonyeshwa na makundi yale saba yaliyoandikiwa barua katika Ufunuo. (Ufu. sura 2, 3) Kwa hiyo, inawapasa wazee Wakristo wa leo watake sana kuona roho inayoonyeshwa na makundi wanayotumikia.

22 Kwa kuwa mwangalizi ni mwanamume aliyewekwa na roho takatifu “kulilisha kanisa lake Mungu,” inampasa aijue hali ya kundi. (1 Pet. 5:2; Matendo 20:28; linganisha Mithali 27:23.) Inafaa ajiulize hivi: Ndugu na dada katika kundi wana furaha kweli? (Zab. 128:1) Je! nyuso zao zinaonyesha wanamtumikia Yehova wakiwa na ‘furaha ya moyo’? (Kum. 28:45-47) Je! wanahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida? (Ebr. 10:24, 25) Je! wanajifunza Biblia peke yao wanapokuwa nyumbani? (Yos. 1:7, 8) Kweli waamini hao wenzetu ni “wazima katika imani”? (Tito 2:2) Wanathamini sana mambo ya kiroho? (Zab. 27:4) Wanaonekana wakiuthamini sana uhusiano wao na Yehova Mungu na kutaka kumsifu kikweli?​—⁠Zab. 9:1, 2.

23. Ili wazee ‘walihubiri neno.’ lazima wafanye nini?

23 Tukichunguza mambo kwa unyofu huenda tukaona kwamba kuna uhitaji wa kusitawisha hali bora ya kiroho kundini. Tunaweza kufanya hivyo tunapokuwa jukwaani hasa. Mwangalizi Timotheo alilazimika kupambana na watu fulani kundini ‘waliokuwa na mashindano ya maneno,’ ‘wasiokuwa na nia inayofaa’ juu ya kweli. (2 Tim. 2:14, 23-25, tafsiri ya New World) Wangeleta “majira yenye matata” kundini kwa sababu ya kuwa humo. Kwa hiyo ilimpasa Timotheo ‘alihubiri neno’ la Mungu lisiloghoshiwa, si hekima ya kibinadamu. (2 Tim. 4:1, 2, tafsiri ya New World; linganisha 1 Wakorintho 2:1-5.) Vivyo hivyo, ili wazee leo wafaidi makundi kiroho, inawapasa ‘walihubiri neno,’ maelezo yao yategemee Biblia, wawe jukwaani au wawe katika mazungumzo ya faraghani.

24, 25. (a) Wazee wanaweza kutembelea waamini wenzao nyumbani kwao wakiwa na kusudi gani? (b) Je! kupatana na Maandiko wazee wanaweza kusali kwa ajili ya waabudu wale wengine wa Yehova?

24 Njia nyingine ya kujenga waamini wenzetu kiroho ni kuwatembelea nyumbani kwao. Yesu Kristo alifanya hivyo, akitaka kusaidia watu kiroho. (Luka 7:36-50; 19:1-27) Naye mtume Yohana alitaka kutembelea Gayo na wengine apate kuongea nao uso kwa uso juu ya mambo ya kiroho.​—2 Yohana 1, 12; 3 Yohana 1, 13, 14.

25 Wazee wa siku hizi wanaweza kutembelea waamini wenzao nyumbani kwao kwa sababu ya upendo wa Kikristo. Hawafanyi hivyo wakawachunguze, bali wakawasaidie kiroho na kuwatia moyo. Tena, inafaa waangalizi wataje ndugu na dada zao Wakristo katika sala. Inapendeza kuona kwamba, nabii Samweli aliwaambia Waisraeli hivi: “Walakini mimi, hasha! nisimtende [Yehova] dhambi kwa kuacha kuwaombea ninyi.” (1 Sam. 12:20, 23) Vilevile, mtume Paulo aliwekea waangalizi mfano mwema wa kusali kwa ajili ya wenzao wanaomwabudu Yehova.​—1 The. 1:1, 2; 2 Tim. 1:1-4; Flm. 4.

26. Inampasa mtu afanye nini ili Bwana awe pamoja na roho yake?

26 Kundi la watu wa Mungu litakuwa na roho njema yenye furaha wakisali kila mtu kwa ajili ya mwenzake. Tena, roho njema itadumu waangalizi Wakristo wakilichunga “kundi” kwa upendo. (Flp. 2:19, 20; 1 Pet. 5:1-4) Ni kweli kwamba ‘Bwana anaweza kuwa pamoja na roho unayoonyesha,’ lakini ili iwe hivyo, wewe mwenyewe unatakiwa ufanye jambo fulani lililo wazi. Inakupasa ulishike sana Neno la Mungu, umpendeze Yehova kabisa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki