Twahitaji Kutaniko
1 Wana wa Kora wakati mmoja walionyesha uthamini wao kwa kutaniko la Yehova kwa njia hii: “Siku moja Hekaluni mwako, ni bora kuliko siku elfu mahali pengine.” (Zab. 84:10, HNWW) Kwao, ulimwengu haukuwa na chochote cha kutoa kwa kulinganishwa. Ikiwa wahisi hivyo, wapaswa kufanya kutaniko kuwa kitovu cha maisha yako.
2 Tangu mwanzo walo, kutaniko la Kikristo limedhihirisha kwamba lina baraka za Yehova. (Mdo. 16:4, 5) Hakuna mmoja wetu anayepaswa kuona kutaniko kwa njia ya vivi-hivi au kuhisi kwamba ni njia tu ya kutuleta pamoja kimwili. Kutaniko ndipo mahali pa kupata kitia-moyo na nguvu kwa Mashahidi wa Yehova katika kila jumuiya. Hilo huandaa ushirika uliounganishwa ili tuweze kufundishwa na Yehova na kupangwa kwa ajili ya utendaji wa Ufalme.—Isa. 2:2.
3 Kutaniko la Kikristo ndilo njia ya msingi ya kutufundisha kweli. (1 Tim. 3:15) Ni lazima wafuasi wa Yesu “wawe kitu kimoja”—kwa umoja na Mungu, na Kristo, na mmoja na mwenzake. (Yn. 17:20, 21, HNWW; linganisha Isaya 54:13.) Hata twende wapi ulimwenguni, ndugu zetu wanaamini mafundisho na kanuni za Biblia na wanajiendesha kwa kupatana nazo.
4 Tunazoezwa na kutayarishwa kutimiza mgawo wetu wa kufanya wanafunzi. Kila mwezi, Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na Huduma ya Ufalme Yetu hutoa habari yenye msaada ya kutusaidia kuanzisha mazungumzo ya Kimaandiko. Mikutano imepangwa kutuonyesha jinsi ya kupata na kukuza upendezi. Ongezeko tunaloona ulimwenguni pote lathibitisha kwamba tuna msaada wa kimbingu katika kazi hii.—Mt. 28:18-20.
5 Kupitia kutaniko, tunapokea kitia-moyo cha kila siku ‘kutuhimiza katika upendo na kazi nzuri.’ (Ebr. 10:24, 25) Tunatiwa nguvu kuvumilia majaribu kwa uaminifu. Waangalizi wenye upendo hutusaidia kushughulika na misongo na mahangaiko. (Mhu. 4:9-12) Tunapewa shauri linalohitajika tunapokuwa katika hatari ya kwenda kando. Ni tengenezo gani jingine ambalo huandaa utunzi wenye upendo kama huo?—1 The. 5:14.
6 Ni mapenzi ya Yehova kwamba tubaki karibu na tengenezo lake ili kuhifadhi umoja wetu. (Yn. 10:16) Njia moja ambayo kutaniko hutusaidia kudumisha uwasiliano na jamii ya mtumwa mwaminifu ni kwa kutuma waangalizi wasafirio kwa ajili ya kututia moyo. Kuitikia kwetu mwelekezo wenye upendo hutuvuta katika ukaribu ambao hutusaidia kuendelea kuwa wenye nguvu kiroho.
7 Kutaniko ni la muhimu sana ikiwa tutaendelea kubaki tukiwa watu wa kiroho. Lingekuwa jambo lisilowezekana kumtumikia Yehova kwa kukubalika tukiwa mbali nalo. Basi, acheni tubaki karibu na kile ambacho Yehova ameandaa. Na tufanye kazi kwa kupatana na malengo yalo na kutumia kwa unyofu shauri tunalopata hapo. Ni katika njia hii tu kwamba tunaweza kuonyesha jinsi kutaniko lilivyo la maana kwetu.—Zab. 27:4.