Toa Magazeti Katika Kila Pindi
1 Tuna sababu nzuri ya kuthamini Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kuna magazeti gani mengine yaliyo na uvutio wa kimataifa kama hayo? Mwezi huu magazeti yatatolewa katika utendaji wetu wa kuhubiri, na jinsi matoleo ya Oktoba yalivyo na habari yenye nguvu! Kwa kawaida, sisi huangusha mengi ya magazeti yetu katika kazi ya nyumba kwa nyumba; hata hivyo, tutataka kuwa tayari pia kuyatoa kwenye kila pindi ifaayo.
2 Unapotoa “Mnara wa Mlinzi,” la Oktoba 1 huenda ukachochea kupendezwa katika makala “Ulimwengu Usio na Vita—Lini?” kwa kusema:
◼ “Watu wengi wanajiuliza ni kwa nini ulimwengu usio na vita yaonekana hauwezi kupatikana licha ya jitihada zote za wanadamu. Wewe wafikiri nini kuhusu taarifa hizi kwenye ukurasa wa 5 wa Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1? [Soma sentensi ya kwanza katika kila moja la mafungu mawili ya kwanza chini ya kichwa kidogo “Dini—Kizuizi Kikubwa,” na uruhusu itikio.] Bila shaka, hili halimaanishi kwamba kutakuwa na vita sikuzote. Ona ahadi ya Mungu hapa kwenye Isaya 9:6, 7.” Waweza kusoma andiko hili kutoka katika Biblia yako au kama lilivyonukuliwa katika makala ya Mnara wa Mlinzi. Eleza kifupi kwamba Mnara wa Mlinzi hutangaza Ufalme wa Yehova kuwa tumaini pekee la ulimwengu wenye amani, na umtie moyo mtu huyo afanye andikisho.
3 Unapotoa “Amkeni!” la Oktoba 22 unaweza kusema:
◼ “Waonaje swali lililo kwenye jalada la gazeti hili: ‘Kwa Nini Maisha Ni Mafupi Mno?’ [Ruhusu itikio.] Mfululizo huu wa makala huelekeza fikira kwa kile wanachosema wanasayansi wa kisasa na watu wengine kuhusu kuzeeka, kisha hukazia fikira juu ya kile ambacho Muumba wetu ameahidi kuhusu mataraja ya uhai udumuo milele. Ningependezwa kukuachia nakala hii ikiwa utataka kuisoma.”
4 Unapokuta watu wenye mwelekeo wa kidini, kwa nini usikazie makala moja kutoka “Mnara wa Mlinzi” la Oktoba 15? Utoaji huu waweza kutokeza itikio lifaalo:
◼ “Ningependa kupata maoni yako kuhusu swali hili: Je, inawezekana kumpenda Mungu na kwa wakati uleule kumhofu?” Ruhusu jibu, kisha usome maelezo ya andiko ya makala “Kwa Nini Umhofu Mungu wa Kweli Sasa?” (Mhu. 12:13) Tumia moja ya vielezi vilivyo kwenye ukurasa wa 427 wa kitabu Kutoa Sababu, na utoe andikisho.
5 Uhubiripo nyumba kwa nyumba, usipuuze maduka. Wale ambao kwa kawaida hutoa ushahidi madukani husema kuwa utendaji huu ni wenye kufurahisha na wenye matokeo. Ungeweza kujaribu utoaji sahili kama huu unapotoa “Amkeni!” la Oktoba 8:
◼ “Twajua kwamba wanabiashara hutamani kujua habari za karibuni zaidi kuhusu masuala yanayoathiri jumuiya yao. Nina hakika makala hizi zitakupendeza.” Kisha shiriki naye kifupi hoja moja kutoka ile makala “Familia za Mzazi Mmoja—Zaweza Kufanikiwa kwa Kadiri Gani?”
6 Ikiwa mtu unayemfikia ana shughuli nyingi kikweli, ungeweza kuonyesha magazeti na kusema:
◼ “Najua hukuwa ukitazamia mgeni leo, kwa hiyo nitasema kifupi. Ningependa kukupa fursa ya kusoma jambo lililo la maana.” Taja makala uliyoteua, na utoe magazeti.
7 Weka rekodi ya nyumba kwa nyumba yenye uangalifu, na uwarudie wote uliowaangushia magazeti. Hakikisha unafuatia ahadi zote za andikisho. Acheni tujitayarishe na kuwa macho kutoa magazeti yetu katika kila pindi ifaayo.