“Wasifaji Wenye Shangwe” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1995
1 Tuna sababu ngapi za kuwa na shangwe? Labda wachache wetu wamejaribu kuziorodhesha zote. Licha ya kuishi katika ulimwengu wenye msukosuko na mashaka, tuna sababu nyingi sana za kuwa na shangwe. Kama ilivyotangazwa katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1995, “Wasifaji Wenye Shangwe” ndicho kichwa chenye kutia moyo cha mikusanyiko ya wilaya ya 1995.
2 Tunamsifu Yehova kwa sababu alitufunza kweli. (Isa. 54:13; Yn. 8:32) Sisi nasi, tunaishiriki kweli kwa shangwe pamoja na wote ambao wanatafuta usalama na furaha. (Eze. 9:4; Mdo. 20:35) Udugu wetu wa Kikristo pia hutuletea shangwe. Familia ya kiroho yenye upendo huleta uradhi na furaha. Hizi ni sababu chache za shangwe yetu ambayo hutusukuma kumsifu Yehova. Hotuba za mkusanyiko na maonyesho yatavuta uangalifu wetu kwenye sababu za ziada za Kimaandiko za kuwa na shangwe katika siku hizi za mwisho zenye taabu.
3 Mkusanyiko wa Siku Tatu: Je, umefanya mipango na mwajiri wako upate likizo ili uhudhurie siku zote tatu za mkusanyiko? Wazazi wa watoto wenye umri wa kwenda shule ambao watahudhuria mmoja wa mikusanyiko wakati ambao shule hazijafungwa, wanapaswa kujulisha walimu kwa staha kwamba watoto wao hawatakuwepo shuleni siku ya Ijumaa kwa ajili ya sehemu hii muhimu ya ibada yao ya kidini. Mkusanyiko ulio karibu nawe uko wapi? Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1995 iliorodhesha tarehe na mahali pa mikusanyiko katika eneo letu. Kufikia sasa mwandishi wenu wa kutaniko amewajulisha juu ya habari zinazohusu kutaniko lenu.
4 Programu itaanza Ijumaa saa 3:40 asubuhi na kumalizika Jumapili saa 9:50 hivi alasiri. Jumamosi na Jumapili, programu itaanza saa 3:30 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Ni wale tu walio na migawo hususa ya kazi watakaoruhusiwa kuingia mapema.
5 Je, Utahudhuria?: Twasihiwa kuhudhuria siku zote tatu za mkusanyiko. Kwa nini hivyo? Yehova anataka tuwe hapo. Leo imani yetu na afya ya kiroho viko chini ya ushambulizi mwingi. Paulo alishauri kuhusu ‘kutoacha kukusanyika pamoja’ wakati ambapo Wakristo katika Yudea walikuwa chini ya msongo mwingi. (Ebr. 3:12, 13; 10:25) Wafilipi walikuwa wakiishi “kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka.” Hata hivyo, wao walikuwa “kama mianga katika ulimwengu.” (Flp. 2:15) Kwa nini Wakristo hawa wa karne ya kwanza walikuwa tofauti? Kwa sababu walifuata kwa utii miongozo ya roho takatifu ambayo ilikuwa ikiwaongoza kukutana pamoja ili “kuhimizana katika upendo na kazi nzuri.”—Ebr. 10:24.
6 Ulimwengu unaweza kutuvuta kwa njia tofauti, ukifanya kuwa dhaifu tamaa yetu ya kukutana na ndugu zetu na kumsifu Yehova. Mwaka huu tunakaribishwa kujitiisha kwa roho ya Yehova na kufurahia siku zote tatu za mkusanyiko. Je, tumeazimia kuhudhuria pamoja na familia yetu nzima? Twahitaji kutia nguvu upendo wetu na imani kwa ukawaida. Yehova ameandaa mikusanyiko ya kila mwaka ili kutusaidia kuhusiana na hilo.
7 Nenda na Hazina Nyumbani: Unaweza kunufaikaje kikamili kutokana na mkusanyiko? Kwa neno moja jibu ni “umakini.” Hii si kazi rahisi katika jamii ya leo isiyotulia na yenye haraka. Vijana kakawana wanaweza kuona kuwa makini kukiwa jambo gumu, lakini ni tatizo tunalokabili sote tunapohudhuria mkusanyiko wa wilaya. Tutapata kuwa makini kukiwa rahisi zaidi tukipanga kimbele. Jiulize, ‘Ni nini kichwa cha mkusanyiko?’ Tafakari juu yacho! ‘Kwa nini ninaenda na nitafanya nini wakati wa hizo siku tatu? Je, jioni zangu zitajawa na tafrija, au nimepanga wakati wa kutosha kwa ajili ya pumziko na pitio la mambo makuu ya mkusanyiko?’
8 Makala ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Februari 1, 1984, “Je, Wewe Hutafakari au Huota tu Ndoto za Mchana?” ilitoa madokezo kadhaa juu ya jinsi ya kunufaika kikamili kutokana na mikutano kisha ikafikia mkataa huu: “Nidhamu ya akilini labda ndiyo jambo la muhimu kuliko yote.” Msemaji anapoanza, kwa kawaida tunakaza fikira, lakini labda kufikia nusu ya hotuba, tunaacha umakini wetu upepesuke. Twaweza kuzuiaje hili lisitokee?
9 Kuna umaana wa kurudia madokezo yaliyotolewa wakati uliopita kwa sababu yanafanya kazi. Ikiwa yawezekana kwa vyovyote, jaribu kupata pumziko la kutosha kila usiku. Hili si rahisi sikuzote kwa sababu huenda kusafiri kukahusika, na ikiwa unakaa katika makao ya kukodiwa, huenda usiende kulala mapema au kupumzika kama upumzikavyo nyumbani. Mipango mizuri kwa kawaida itakusaidia kupata pumziko linalohitajiwa.
10 Kunakili maandishi sahili kumethibitika kuwa msaada katika kuwa makini. Ukijaribu kuandika habari nyingi mno, huenda hoja za maana sana zikakosekana kabisa. Kama dokezo, nakili maandishi ukiwa na nia ya kutoa muhtasari wa programu kwa mwanafunzi wa Biblia au mtu asiyeweza kutoka kitandani. Hata ingawa huenda huna mtu fulani hususa akilini, utakuwa na kusudi la kunakili maandishi, na baada ya mkusanyiko unaweza kupata pindi za kutoa mambo makuu ya programu unapokuwa ukitoa ushahidi wa vivi-hivi kwa washiriki wa familia wasioamini. Kwa kunakili maandishi na kushiriki kile ulichosikia, hutasahau haraka habari hiyo. Kujieleza huongeza kadiri ya kudumisha habari.
11 Ingawa chakula hakitaandaliwa tena, bado kuna gharama kubwa zitakazohusishwa katika kukodi mahali pa mkusanyiko, ambazo mara nyingi hutia ndani gharama za ziada za mfumo wa sauti, fasihi na kadhalika. Gharama hizi hulipiwaje? Kupitia michango yetu ya hiari, iwe ni kwa pesa taslimu au kwa cheki au hawala ya fedha itakayolipwa “Mashahidi wa Yehova.” Hili ni kupatana na Zaburi 96:8 na 2 Mambo ya Nyakati 31:12.
12 Wasifaji Wenye Shangwe Humheshimu Yehova kwa Mwenendo wa Kimungu: Mwaka uliopita tulipata maelezo yenye kutia moyo kuhusu mwenendo wetu kutoka kwa wafanyakazi wa hoteli na wafanyakazi wa mahali pa mkusanyiko. Meneja mmoja wa hoteli alitaarifu hivi: “Ni furaha sikuzote kuwapatia Mashahidi mahali pa kukaa kwa sababu wao wana subira na ni wenye kushirikiana na hutunza watoto kwa uangalifu.”
13 Twatamani ripoti zote zilizopokewa zingekuwa sawa na hiyo, lakini kwa kusikitisha, sivyo ilivyo. Mwenyekiti mmoja wa mkusanyiko alionelea hivi: “Baada ya vipindi, wengi wa matineja hujikusanya kwa idadi kubwa katika sebule [ya hoteli] usiku mno, wakicheka kwa sauti kubwa na kupiga yowe. Hili husumbua wageni wengine . . . , ambao huonekana kuwa wamekasirika. Wachanga fulani hukimbia kwenye ujia, wakifunga milango kwa nguvu huku wakitembelea vyumba vya mmoja na mwingine na kuzungumza kwa sauti kubwa katika hivyo vyumba.”
14 Tatizo lingine ambalo limeendelea kwa miaka mingi ni idadi kubwa ya ndugu wanaotembea kwenye ujia na nje ya jumba vipindi vikiendelea. Katika mkusanyiko mmoja mwaka uliopita, taarifa fulani kutoka kwa mwanafunzi wa Biblia ilipatikana katika sanduku la mchango. Ilisomeka hivi: “Sijapata kushtuliwa na kushangazwa hivi kwa sababu ya kelele, shughuli, mazungumzo na kutenda kwa njia isiyofaa katika vijia vya nje ya jumba wakati hotuba zinapoendelea . . . Mimi bado si Shahidi, ni mmoja ambaye anajifunza na kujua hofu ya kimungu na staha.” Kwa hakika hakuna mmoja wetu angependa kuacha maoni ya kwamba hatuna uthamini kwa maandalizi ya Yehova.
15 Nyakati zote twapaswa kujiuliza: ‘Mimi namwakilisha nani, na kwa nini ninahudhuria mkusanyiko huu?’ Hali yetu ya kiroho na ujitoaji kimungu unaonyeshwa katika usemi wetu, mwenendo, na uthamini kwa maandalizi ya kiroho. (Yak. 3:13; 1 Pet. 2:2, 3, 12) Akina ndugu ambao wamevumilia miaka mingi ya uzuizi na marufuku mara nyingi wanaonekana wakiwa wenye umakini zaidi na wenye staha kwenye mikusanyiko, wakibaki vitini mwao, wakikazia fikira hotuba na maonyesho.
16 Kuvaa na Kujipamba Kwako Huonyesha Mengi Kukuhusu: Kwenye 1 Samweli 16:7, tunakumbushwa kwamba “wanadamu huitazama sura ya nje; bali BWANA huutazama moyo.” Hivyo, mara nyingi watu huamua jinsi tulivyo kwa msingi wa sura yetu. Kuvaa na kujipamba kwetu hutazamwa kwa ukaribu, hasa tunapohudhuria mkusanyiko kwa ajili ya ibada na maagizo katika maisha ya Kikristo. Ikiwa wewe ni kijana anayekwenda shuleni au ikiwa kazi yako ya kimwili yakufanya ushughulike kwa ukaribu na watu ambao hufuata mitindo ya kilimwengu, huenda likawa jambo gumu kufuata viwango vya Kikristo vya mavazi yenye kiasi.
17 Viwango vya kuvaa na kujipamba hutofautiana kotekote ulimwenguni. Wakristo wanatarajiwa kuvaa mavazi yenye kiasi yaliyo na mpangilio mzuri. Ni nani apaswaye kuamua hilo? Wazazi wanapaswa kuhakikisha kwamba watoto wao matineja hawavai kama vijana wa kilimwengu shuleni. Miongozo yenye faida imetolewa ili kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima katika jambo hili linalohitaji uangalifu. Twatia moyo pitio la makala ya Amkeni! (Kiingereza) Februari 8, 1987, yenye kichwa “Je, Mavazi Humaanisha Nini Kwako?” Ni nini kilichoonekana kwenye baadhi ya mikusanyiko yetu mwaka uliopita?
18 Baada ya mmoja wa “Hofu ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya, tulipokea maoni haya: “Akina ndugu na dada wameboresha mavazi yao, kujipamba na mwenendo kwenye mkusanyiko mwaka huu. . . . Hata hivyo, bado kuna hali na mazoea ambayo yanahitaji kuboreshwa zaidi.” Baada ya mkusanyiko mwingine iliripotiwa kwamba mavazi yasiyo na kiasi yalionekana wazi sana. Ripoti hiyo ilitaja kwamba mavazi ya watu fulani yaliudhi wengine. Baadhi ya watu wa nje waliokuwapo pia waliona mavazi yasiyo na kiasi. Mavazi ya watu fulani yalionyesha sehemu kubwa sana ya mwili na yalikuwa yenye kubana sana.
19 Wengi wa akina ndugu na dada huvaa mavazi yenye kiasi, yenye heshima wanapokuwa kwenye mahali pa mkusanyiko. Hata hivyo, baadaye, wakati wa mapumziko baadhi ya akina ndugu na dada, wakiwa bado wamevalia beji zao, walivalia “mavazi ya kimitindo yasiyofaa watu wa Mungu.” Wazee wakiona kwamba wengine wana mwelekeo wa kuvaa kwa njia hii wakati wa utendaji wa mapumziko, ingefaa kutoa shauri lenye fadhili lakini lenye uthabiti kabla ya mkusanyiko kwamba mavazi kama hayo hayafai, hasa tukiwa wajumbe wenye kuhudhuria mkusanyiko wa Kikristo. Tafadhali pitia na wanafunzi wako wa Biblia ambao watahudhuria mkusanyiko miongozo iliyoonyeshwa juu kuhusu mwenendo na mavazi.
20 Kamera na Vifaa vya Kurekodia: Inafaa kutoa kikumbusha chenye fadhili kuhusu kamera na vifaa vya kurekodia. Tafadhali kumbuka, ikiwa wapanga kutumia kamera, kamera ya video yenye kuchukulika, au aina yoyote ya kifaa cha kurekodia, onyesha ufikirio kwa wale wanaokuzunguka. Kutembea-tembea vipindi vinapoendelea au hata kurekodi kutoka kitini mwako kwaweza kukengeusha wengine. Hakuna vifaa vya kurekodia vya aina yoyote vipaswavyo kuunganishwa kwenye mifumo ya umeme au ya sauti, wala hakuna vifaa vipaswavyo kufunga vijia vya kupitia. Iwe utaamua kupiga picha au kurekodi sehemu za programu kwa kamera ya video yenye kuchukulika au chombo cha kurekodia kaseti ni jambo la kibinafsi. Picha na mirekodio yaweza kuleta kumbukumbu zipendwazo inapoonwa wakati ujao. Vifaa hivyo vyote vyapasa kutumiwa kwa kiasi, katika njia ambayo haikengeushi wengine au kukuzuia kupata manufaa zaidi kutokana na programu. Baada ya kurudi nyumbani, je, kutakuwa na wakati wa kupitia mirekodio hiyo? Utapata kwamba kunakili maandishi kutatosha.
21 Viti: Kwenye “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1994, je, uliona maendeleo kuhusiana na jambo la kuhifadhi viti? Maendeleo fulani yamefanywa, lakini bado twahitaji kuwa na utambuzi wa kikumbusha hiki: VITI VYAWEZA KUHIFADHIWA TU KWA WASHIRIKI WA KARIBU WA FAMILIA YAKO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Tuko huko tukiwa wageni wa Sosaiti. Kodi ya jumba imelipwa kwa michango ya hiari. Je, lingekuwa jambo lenye upendo na ufikirio kuhifadhi viti ambavyo hatuna uhakika kama vitakaliwa? Twasikitika kwamba haitawezekana kwetu kushughulikia maombi ya sehemu zilizotengwa vyumba kwa wenye matatizo ya kimazingira, kama vile mizio.
22 Kila mkusanyiko hufanya uandalizi kwa ajili ya wale wenye uhitaji wa pekee, kama vile wazee-wazee na wasiojiweza kimwili. Tafadhali hakikisha hukalii moja ya sehemu hizi ikiwa hustahili. Pia, uwe macho kusaidia wale wenye uhitaji wa pekee kupata kiti ikiwa hawaambatani na mtu fulani mwenye daraka la kuwatunza.
23 Kushughulikia Mahitaji Yako ya Chakula ya Mkusanyiko: Kama mjuavyo, kuanzia mikusanyiko ya wilaya ya 1995 na makusanyiko ya mzunguko ya Septemba 1995 na siku za kusanyiko la pekee, hakuna chakula kitakachoandaliwa. Kila mtu apaswa kuleta chakula na kinywaji chake mwenyewe. Nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1995 iliandaa habari ya kina kuhusu ni kwa nini rekebisho hili limefanywa na ikatoa madokezo mazuri ya jinsi kila mtu anavyoweza kushughulikia mahitaji yake mwenyewe ya chakula na kinywaji kwenye mkusanyiko. Ingekuwa vizuri kwa wote kupitia nyongeza hiyo wao wenyewe na pia pamoja na wanafunzi wao wa Biblia wanapojitayarisha kuhudhuria mkusanyiko. Ni jambo la maana kwamba wanafunzi wa Biblia wajulishwe kwamba wote wanaohudhuria wanapaswa kuja na chakula chao wenyewe na kinywaji kwenye mkusanyiko. Ikiwa mipango yoyote inafanywa kwa ajili ya chakula cha jioni kwa wale wanaosafiri kutoka mbali na wanalala kwenye mahali pa mkusanyiko habari hii itapelekwa na wanaoshughulikia mkusanyiko wa wilaya kwa makutaniko yanayohusika.
24 Ili kukazia tu hoja zenye kutokeza, mtataka kukumbuka vitu hivyo vilivyodokezwa kwa ajili ya pumziko la mchana: chakula cha mchana chepesi, sahili, na chenye lishe sawa na kile ambacho mara nyingi watu hubeba wanapokwenda kwenye kazi ya kimwili, kama vile mikate iliyowekwa nyama katikati, matunda yaliyokaushwa, njugu, chakula kilichookwa, na matunda ya karibuni. Vinywaji vyaweza kutia ndani kahawa, soda, maji ya matunda, au maji ya chupa, katika kiwekeo kisichovunjika au flaski. Ikiwa viwekeo vidogo ni vya lazima, vyakubalika ikiwa vitatoshea chini ya kiti chako. Hata hivyo, hakuna viwekeo vikubwa vya tafrija ya familia, au vinywaji vya alkoholi vipaswavyo kuletwa kwenye jengo la mkusanyiko. Kula chakula au vitafunaji wakati programu inaendelea kwapaswa kuepukwa. Hili lingeonyesha ukosefu wa staha kwa chakula cha kiroho kinachoandaliwa.
25 Tahadhari ya ziada ni kwamba hakuna upishi unapaswa kufanywa katika mahali pa mkusanyiko au katika vyumba vya hoteli isipokuwa kuna nafasi ndogo kwa kusudi la kupikia. Ni vema kufikiri kwa uzito uhakika wa kwamba wakati ulioruhusiwa kwa ajili ya pumziko la mchana umepangwa ili tuweze kushiriki kiburudisho chepesi na kufurahia ushirika wa kitheokrasi wa ndugu na dada zetu. Tukiwa watu wa Yehova, twatambua kwamba chakula cha kiroho kwenye mikusanyiko ni chenye umuhimu zaidi kikilinganishwa na vitu vya kimwili, na twapaswa kufanya mipango ifaavyo.
26 Mnamo Novemba 3, 1995, wa kwanza kati ya “Wasifaji Wenye Shangwe” Mikusanyiko ya Wilaya utaanza. Je, umekamilisha matayarisho yako, na je, uko tayari sasa ili kufurahia siku tatu za ushirika wenye furaha na mambo mazuri ya kiroho? Twasali kwa unyofu kwamba Yehova atabariki jitihada zako za kuhudhuria mkusanyiko wa mwaka huu pamoja na ndugu na dada zako tunapotafakari juu ya jinsi ya kuwa wasifaji wenye shangwe wa Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Vikumbusha vya Mkusanyiko wa Wilaya
Ubatizo: Wataka kubatizwa wapaswa kuwa vitini mwao katika mahali palipoteuliwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Imeonekana kwamba wengine huvaa mavazi ambayo hayana heshima na yasiyofaa hiyo pindi. Akina dada hasa watataka kuangalia kimbele ikiwa mavazi wanayopanga kuvaa yanabaki yakiwa yenye kiasi hata yanapolowa. Vazi la kuogelea lenye kiasi na taulo vyapasa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na msemaji, mwenyekiti wa kipindi atatoa maagizo mafupi na kisha atataja wimbo. Baada ya ubeti wa mwisho, wakaribishaji watawaongoza wataka kubatizwa hadi kwenye mahali pa uzamisho. Kwa kuwa ubatizo katika mfano wa wakfu wa mtu ni jambo la uhusiano wa karibu na la kibinafsi kati ya mtu huyo na Yehova, hakuna uandalizi wa ule uitwao eti ubatizo wa kishirika ambapo wataka kubatizwa wawili au zaidi hukumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
Kadi za Beji: Tafadhali vaa kadi ya beji ya 1995 kwenye mkusanyiko na unaposafiri kwenda na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hili hufanya iwezekane kwetu kutoa ushahidi mzuri tunaposafiri. Kadi na vifuko vya beji vyapasa kupatikana kupitia kutaniko, kwa kuwa havitapatikana mkusanyikoni. Kumbuka kubeba kadi yako ya wakati huu ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia. Washiriki wa familia ya Betheli na mapainia wapaswa kuwa na vitambulisho vyao.
Nyimbo: Nyimbo zifuatazo zimeteuliwa kwa ajili ya programu ya mwaka huu: 3, 33, 38, 42, 45, 57, 72, 85, 106, 107, 148, 152, 155, 181, 183, 191, 200, na 217. Watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia huenda wakataka kupanga vipindi vya mazoezi ili waweze kushiriki kikamili katika kuimba nyimbo zote wakati wa programu ya mkusanyiko.
Utumishi wa Kujitolea: Je, waweza kutenga kando wakati kwenye mkusanyiko ili usaidie katika mojapo ya idara? Kutumikia ndugu zetu, japo kwa saa chache tu, kwaweza kusaidia sana na kuleta kiasi kizuri cha uradhi. Ikiwa waweza kusaidia, tafadhali ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kuchangia vizuri kwa kufanya kazi chini ya mwelekezo wa mzazi au mtu mzima mwingine mwenye kuchukua mambo kwa uzito.
Maneno ya Tahadhari: Kwa kuwa macho kuelekea matatizo yawezayo kutokea, twaweza kuepuka magumu yasiyo ya lazima. Mara nyingi wezi na watu wengine walaghai huibia watu ambao wako mbali na mazingira ya kwao. Hakikisha gari lako limefungwa nyakati zote, na usiache kamwe garini chochote chenye kuonekana kiwezacho kumfanya mtu avunje ili kuiba. Wezi na wenye kuibia watu mifukoni hukazia fikira vikusanyiko vikubwa. Halingekuwa jambo la hekima kuacha vitu vyovyote vyenye thamani kitini mwako. Huwezi kuwa na hakika kwamba kila mtu anayekuzunguka ni Mkristo. Kwa nini utokeze majaribu? Ripoti zimepatikana za majaribio yaliyofanywa na watu fulani wa nje ili kudanganya watoto na kuwatorosha. JUA MAHALI WATOTO WAKO WALIPO NYAKATI ZOTE.
Uangalifu wapaswa kutolewa pia ili kuepuka kujaza kupita kiasi magari yaliyokodiwa na kutaniko kwa ajili ya safari ya mkusanyiko. Ni afadhali kutumia fedha zaidi kwa gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au vibaya hata zaidi kuweka akina ndugu katika hatari za aksidenti na upotezo uwezekanao wa uhai kwa sababu ya kujaza gari kupita kiasi au kumtia moyo dereva aendeshe kasi zaidi ili mfike mwisho wa safari mapema. (Rum. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Akina ndugu wenye daraka wanaosafiri kwenye magari hayo wanapaswa kujihisi huru kutoa shauri lenye upendo kuhusiana na jambo hili ikihitajika.