Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 3/1 kur. 13-19
  • “Kondoo Wengine” na Chakula cha Jioni cha Bwana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kondoo Wengine” na Chakula cha Jioni cha Bwana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mabadiliko Katika Maoni
  • Sikukuu ya Kupitwa na Ukumbusho
  • Umaana wa Kuhudhuria Ukumbusho
  • Kuonyesha Hangaiko la Upendo kwa Wote
  • Uhitaji wa Kujichunguza Mwenyewe
  • Kusherehekea Katika Mwaka wa 1985
  • Kwa Nini Tunaadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • “Endeleeni Kufanya Hivi Kwa Kunikumbuka Mimi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • ‘Kufahamu Sisi Ni Nini Wakati wa Ukumbusho’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • ‘Fanyeni Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 3/1 kur. 13-19

“Kondoo Wengine” na Chakula cha Jioni cha Bwana

“[Yesu] ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya za ulimwengu mzima.”​—1 YOHANA 2:2, NW.

1. Ni matokeo gani mazuri yametokana na ‘kuhubiriwa kwa habari njema za ufalme’?

YESU alisema: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo, 24:14, NW) Wengine wa kizazi cha 1914 wangali hai kushuhudia kwamba Mashahidi wa Yehova wametimiza amri hiyo kwa uaminifu. Matokeo ni kwamba mamia ya maelfu ya watu wenye mioyo minyofu, ambao wamefunguliwa macho wakaona wazi hali za kushindwa za ulimwengu huu, wameitikia vizuri habari njema. Wamejiweka wakf kwa Yehova Mungu na kushikamana na Ufalme kwa utii, wakajulisha wakfu huo kwa ubatizo wa maji. Kulikuwa na watu 179,421 waliochukua mwendo huo wa hekima wakati wa mwaka wa 1984. Kwa kufanya hivyo, waliambia watu wenye jina la Mungu hivi: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”​—Zekaria 8:23

2. Ni jambo gani limeongoza wakati wa Yesu wa kukusanya “kondoo wengine” wake?

2 “Mkutano mkubwa” huo wa waabudu wanaoongezeka daima ni sehemu ya wale walioelezwa na Yesu kuwa “kondoo wengine” wake. (Ufunuo 7:9, 15; Yohana 10:16) Wana tumaini zuri sana la kuishi milele katika paradiso ya kidunia. (Zaburi 37:29) Yesu alitabiri kwamba angewakusanya pamoja wafuasi wake hao waaminifu baada ya kwanza kuelekeza fikira za uchungaji zisizogawanyika kwenye mkusanyo wa “kundi dogo” la watu wa mfano wa kondoo ambao kwao anapatanisha agano jipya. (Luka 12:32; Waebrania 9:15) Tukikumbuka mkusanyo huo wa jamii mbili za watu wa mfano wa kondoo kuwaingiza katika “kundi moja,” tunaweza kufahamu ni kwa sababu gani mtume Yohana alisema kwamba Yesu Kristo “ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya za ulimwengu mzima.”​—1 Yohana 2:1, 2, NW.

Mabadiliko Katika Maoni

3, 4. (a) Ni maoni gani yaliyobadilika ambayo wengi wamekuwa nayo juu ya kusherehekea Chakula cha Jioni cha Bwana? (b) Yesu alimaanisha nini kwa kusema, ‘Kwa maana mara mlapo na mnywapo’?

3 Wakusanyikaji wengi walio wapya wa “kondoo wengine” walikuwa wakisherehekea Misa au Ushirika, na wingi wa mara za sherehe hiyo hata namna ilivyofanywa iliongozwa na imani za tengenezo la kidini walilokuwa wakifuata. Lakini, sasa wamekuja kutambua kwamba Chakula cha Jioni cha Bwana kinapasa kusherehekewa mara moja tu kila mwaka. Kwa sababu gani iko hivyo? Sikukuu ya Kupitwa ya Kiyahudi ilisherehekewa mara moja tu kila mwaka, na Yesu alianzisha Ukumbusho usiku uo huo wa Kupitwa, Nisani 14. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake: “Endeleeni kufanya hivyo kwa kunikumbuka mimi. . . . Kwa maana mara mwulapo mkate huu na kunywa kikombe hiki, ninyi mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka afikapo.” (1 Wakorintho 11:24-26, NW) Kwa wazi Yesu alimaanisha kwamba wanafunzi wake wanapaswa kushika sherehe ya kifo chake Siku ya Kupitwa, ambayo ilikuja mara moja kwa mwaka. Basi, hiyo imesherehekewa “mara nyingi” wakati wa maisha ya kundi la Kikristo. Kwa kweli, tayari Ukumbusho umekwisha kusherehekewa mara 1,952.

4 Kuna tofauti nyingine ya maana katika maoni ambayo jamii ya “kondoo wengine” imekuja kuthamini. Badala ya kushiriki mkate na divai kama wengi kati yao walivyofanya zamani katika kanisa fulani, sasa wanakuta hali yao ikiwa ‘imerekebishwa upya’ kuwa ile ya watazamaji. Kwa sababu gani iko hivyo, na je! tuna Maandiko ya kuunga mkono utaratibu unaoruhusu kuwe na watazamaji na pia washiriki?​—2 Wakorintho 13:11, NW; 2 Timotheo 3:16, 17.

5. (a) Eleza hatua zile za msingi ambazo ni lazima mtu achukue ili afaidike kutokana na dhabihu ya Yesu. (b) Kwa sababu gani Mungu amechukua hatua kwa njia ya pekee kwa ajili ya wale wafuasi 144,000 wa Kristo Yesu?

5 Ili mtu ye yote afaidike kutokana na “dhabihu ya upatanisho” ya Kristo Yesu, kuna hatua fulani zinazohitaji kuchukuliwa, bila kujali kama mtu huyo ana tumaini la kupata uzima mbinguni au ana tumaini la kupata uzima katika Paradiso ya kidunia. Hatua hizo za msingi ni kama zifuatavyo: (1) kutwaa maarifa sahihi ya kujua Neno la Mungu (Warumi 10:13-15); (2) kuzoea imani (Waebrania 11:6); (3) toba (Mathayo 4:17); (4) uongofu (kugeuka) (Matendo 3:19); (5) wakfu (Luka 9:23); na (6) ubatizo (Mathayo 28:19). Ni baada ya hatua hizo kuchukuliwa Mungu anapotenda kwa njia ya pekee kuelekea mtu anayechagua awe mmoja wa wale 144,000, au “kundi dogo.” Kwa kusudi gani? Ili mtu huyo awe mwana wa kiroho wa Mungu akiwa na taraja la kuwa kuhani na mfalme pamoja na Kristo Yesu. (Ufunuo 20:4, 6) Kuna mabaki tu ya wana wa kiroho hao ambao sasa wako hai, nao ndio kwa kufaa wanaoshiriki mifano. Basi, hiyo inaeleza ni kwa sababu gani hesabu iliyo kubwa sana kati ya Mashahidi wa Yehova wanakuwa watazamaji wala si washiriki.

Sikukuu ya Kupitwa na Ukumbusho

6. Kwa sababu gani wengine wameshindania jambo la kwamba “kondoo wengine” wanapaswa kushiriki mifano, na hilo linatokeza ulizo gani?

6 Wengine wamedokeza kwamba hesabu kubwa inayoongezeka ya “kondoo wengine” wanapaswa kushiriki mifano. Wanawaza hivi: Kwa kuwa ‘torati ni kivuli cha mema yatakayokuwa,’ na kwa kuwa moja la matakwa ya Torati lilikuwa kushika sikukuu ya Kupitwa upande wa Waisraeli na pia wakaaji wageni waliotahiriwa, hiyo ingemaanisha kwamba jamii zote mbili za watu wa mfano wa kondoo zilizo katika “kundi moja” lililo chini ya “mchungaji mmoja” zinapaswa kushiriki mifano ya Ukumbusho. (Waebrania 10:1; Yohana 10:16; Hesabu 9:14) Jambo hilo linatokeza ulizo la maana: Je! sikukuu ya Kupitwa ilikuwa mfano wa kufananisha Ukumbusho?

7. Ni katika njia gani mbalimbali sikukuu ya Kupitwa ilikuwa “kivuli cha mema yatakayokuwa”?

7 Ni kweli kwamba bila shaka sehemu fulani za mwadhimisho wa Kupitwa katika Misri zilitimizwa katika Yesu. Paulo anafananisha Yesu na mwana-kondoo wa Kupitwa, akisema, “Kristo kupitwa kwetu ametolewa dhabihu.” (1 Wakorintho 5:7, NW) Kunyunyizwa kwa damu ya mwana-kondoo wa Kupitwa juu ya miimo na vizingiti vya milango kulimhakikishia ukombozi mzaliwa wa kwanza ndani ya nyumba ya Kiisraeli. Vivyo hivyo, ni kupitia unyunyizaji wa damu ya Kristo kwamba “kundi la mzaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa katika mbingu” linapokea ukombozi, au “kufunguliwa kwa njia ya ukombozi.” (Waebrania 12:23, 24; Waefeso 1:3, 7, NW) Zaidi ya hilo, hakuna hata mfupa mmoja wa mwana-kondoo wa Kupitwa uliopasa kuvunjwa, na jambo hilo pia lilipata utimizo katika Kristo Yesu. (Kutoka 12:46; Zaburi 34:20; Yohana 19:36) Kwa hiyo, ni kweli ikisemwa kwamba, katika mambo fulani, sikukuu ya Kupitwa ilikuwa moja ya sehemu nyingi zilizokuwa katika Torati ambazo zilikuwa “kivuli cha mema yatakayokuwa.” Sehemu zote hizo zilielekeza kwa Kristo Yesu, “Mwana-kondoo wa Mungu.”​—Yohana 1:29.

8-10. (a) Ni katika njia gani ya maana inayohusu damu sikukuu ya Kupitwa ilitofautiana na Ukumbusho? (b) Maagano yanayoshirikishwa na Ukumbusho yanakaziaje tofauti nyingine? (c) Jambo hilo linatuongoza tukate shauri namna gani?

8 Hata hivyo, sikukuu ya Kupitwa haikuwa kwa njia ya kabisa kabisa mfano wa kufananisha Chakula cha Jioni cha Bwana. Kwa sababu gani sivyo? Wakati siku ya Kupitwa ilipoanzishwa katika Misri, nyama ya mwana-kondoo aliyeokwa kwa moto ililiwa, lakini hakuna sehemu yo yote ya damu ya mwana-kondoo wa Kupitwa iliyoliwa. Lakini, tofauti na hivyo, wakati Yesu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake aliwaagiza waziwazi wale waliokuwapo wale nyama yake na kunywa damu yake, vitu hivyo vikiwa vimefananishwa na mkate na divai iliyokuwapo. (Kutoka 12:7, 8; Mathayo 26:27, 28) Katika jambo hilo la maana sana, yaani damu, sikukuu ya Kupitwa haikuwa mfano wa kufananisha Chakula cha Jioni cha Bwana.

9 Kuna jambo jingine lisilopasa kusahauliwa. Yesu alizungumza maagano mawili yanayohusiana pamoja na wanafunzi wake, “agano jipya” na ‘agano kwa ajili ya ufalme.’ (Luka 22:20, 28-30, NW) Maagano yote mawili yalihusu jambo la kwamba wenye kushiriki wangekuwa njiani wakielekea kushiriki kama makuhani na wafalme pamoja na Kristo Yesu. Lakini katika Israeli hakuna mkaaji mgeni aliyetahiriwa angeweza kamwe kuwa kuhani au mfalme. Katika jambo hilo, pia, tunaona tofauti kati ya karamu ya Kupitwa katika Israeli na Chakula cha Jioni cha Bwana.

10 Basi jambo hilo linatuongoza tukate shauri namna gani? Jambo la kwamba mkaaji mgeni aliyetahiriwa alikula mkate usiotiwa chachu, mimea michungu, na mwana-kondoo wa Kupitwa halithibitishi kwamba leo wale wa “kondoo wengine” wa Bwana wanaokuwapo penye Ukumbusho wanapaswa kushiriki mkate na divai.

Umaana wa Kuhudhuria Ukumbusho

11. Ni kwa sababu gani za maana “kondoo wengine” wanapaswa kuhudhuria Ukumbusho?

11 Lakini, je! hilo linaonyesha kwamba si jambo la maana kwa wale wa jamii ya “kondoo wengine” kuwapo kwenye sherehe ya Ukumbusho? Sivyo hata kidogo! Hiyo ni pindi ya wafuasi wote wa Yesu walio mfano wa kondoo kumkumbuka Yesu katika maana ya pekee sana. Katika pindi hiyo “kondoo wengine” wanakumbuka kwamba tayari wamefaidika kwa sababu ya imani yao katika damu ya Kristo iliyomwagwa mpaka wakafikia kadiri ya kwamba sasa wanaonwa na Yehova kuwa “wamefua mavazi yao marefu na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Hiyo ndiyo sababu wanaweza kutoa “utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake” Mungu. (Ufunuo 7:14, 15, NW) Wanaweza pia kukumbuka kwamba ni lazima waendelee ‘kutafuta Yehova, uadilifu, na upole’ kwa tumaini la kuachiliwa wakati wa “siku ya hasira ya Yehova,” na baada ya hapo wawe na furaha ya kufikia ukamilifu wa kibinadamu. Mwishowe wanaweza kutangazwa na Yehova kuwa waadilifu hasa, na jambo hilo litatokea baada ya Yesu kupokeza Ufalme kwa Baba yake.​—Sefania 2:2, 3, NW; 1 Wakorintho 15:24; Ufunuo 20:5.

12. Ni faida gani zinazotokana na kusikiliza hotuba ya Ukumbusho?

12 Sababu nyingine ya maana ya kuhudhuria ni kwamba kweli zinazozungumzwa wakati wa hotuba ya Ukumbusho ni kati ya ‘mambo yenye kina kirefu ya Mungu,’ ‘chakula kigumu kilicho cha watu waliokomaa,’ wala si maziwa tu ya “fundisho la msingi.” (1 Wakorintho 2:10; Waebrania 5:13–6:1, NW) Hotuba ya Maandiko itaongeza kina cha kuthamini upendo ambao Yehova alionyesha kwa kuanzisha mpango huo wa Ufalme ulio mzuri sana ili kubariki jamaa ya kibinadamu. Pia ni nafasi ya ‘kukaza macho zaidi kwenye Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ Upendo ambao Yesu alionyesha kwa ajili yetu, hata mateso yaliyompata, haupasi kamwe kuchukuliwa kuwa jambo la kikawaida tu. (Waebrania 12:2, 3, NW) Zaidi ya hilo, sisi sote tunaweza kukubali kwamba mengi ya mawazo yenye thamani kubwa ambayo Yesu alizungumza pamoja na mitume wake wakati wa kuanzisha Ukumbusho​—mawazo yanayohusu umoja, upendo, na kutukuzwa kwa jina la Yehova​—yanaweza kushirikiwa na “kondoo wengine” na pia “kundi dogo.”

Kuonyesha Hangaiko la Upendo kwa Wote

13. Kwa sababu gani ni jambo la maana kupitishia wahudhuriaji wote mifano?

13 Ni jambo la maana kwamba kila mtu aliye kwenye Chakula cha Jioni cha Bwana akumbushwe juu ya utaratibu ulioanzishwa na Yesu. Kupitisha kwa uhalisi mkate na divai kutoka mtu mmoja kwenda kwa mwingine kunasaidia kuongeza kina cha uthamini wa mambo matakatifu ambayo yanakuwa yametoka tu kuzungumzwa jioni hiyo. Pia kunawezesha kila mmoja aingie katika maandishi kuonyesha tumaini lake la uzima ni nini​—la kimbingu au la kidunia.a Kufuata utaratibu unaofaa kunaingiza kundi katika upatani wa jambo linalofanywa duniani pote jioni hiyo.​—1 Wakorintho 14:40.

14. Wazee wanaweza kuonyeshaje hangaiko lenye upendo kwa kila mmoja wa wapakwa mafuta aliye mgonjwa usiku wa Ukumbusho?

14 Tuseme mmoja wa wapakwa mafuta katika kundi ni mgonjwa na hawezi kuhudhuria Ukumbusho. Sasa iwe namna gani? Kila jitihada inapasa kufanywa ili mmoja wa wazee ampelekee Mkristo huyo mgonjwa mifano kisha, ikifaa, mzee huyo anaweza kutoa maelezo machache yanayofaa kabla ya kumtolea mifano na kumaliza kwa sala inayofaa. Mgonjwa huyo atajisikia ametiwa moyo kama nini! Matendo hayo ya hangaikio lenye upendo yanaendeleza roho ya upendo ndani ya kundi. (Ona pia ukurasa wa 23.)—Zaburi 133:1.

15. Eleza njia nyingine ambazo kwazo heshima inaweza kuonyeshwa juu ya Chakula cha Jioni cha Bwana.

15 Maulizo mengine ya kupendeza yametokezwa juu ya utaratibu na namna ya mifano inayopasa kutumiwa kwenye Ukumbusho. Majibu kwa maulizo hayo yatapatikana ukurasa wa 17 chini ya “Kuheshimu Chakula cha Jioni cha Bwana.” Wazee wenye madaraka wangefaa kufuata kwa uangalifu mambo ambayo yamepangwa humo.

16, 17. (a) Ni ulizo gani ambalo wengine wameuliza juu ya kushiriki Ukumbusho, na ni nani peke yake anayeweza kutoa jibu? (b) Mungu anawatoleaje ushuhuda wenye kusadikisha wale waliozaliwa kwa roho yake?

16 Kuna wengine wanaodhikishwa na mashaka juu ya kama wanastahili kushiriki mifano. Ulizo hilo linatokea nyakati nyingine katika majuma yale yanayotangulia sherehe ya Chakula cha Jioni cha Bwana. Mara nyingi maulizo hayo yanatokezwa na wengine ambao wameshirikiana majuzi na Mashahidi wa Yehova. Je! wewe umekuwa na mashaka ya namna hii yakipita katika akili yako? Unaweza kuamuaje mwendo unaofaa kufuata?

Uhitaji wa Kujichunguza Mwenyewe

17 Paulo alipendekeza hivi kuhusu Chakula cha Jioni cha Bwana: “Kwanza acheni mtu ajikubali mwenyewe baada ya uchunguzi mwingi, na hivyo acheni ale kati ya mkate na kunywa kati ya kikombe.” (1 Wakorintho 11:28, 29, NW) Je! umeona kwamba Paulo anasema wewe ndiwe unayepaswa ‘kujikubali mwenyewe baada ya uchunguzi mwingi’? Bila shaka, si vibaya kusema juu ya jambo zito kama hilo pamoja na Mkristo aliyekomaa, lakini ni lazima wewe peke yako uamue uhusiano wako wa kibinafsi pamoja na Yehova na Mwana wake. Mungu haachi ye yote wa wale 144,000 akiwa na shaka. Tunahakikishiwa hivi: “Ile roho yenyewe hushuhudia pamoja na roho yetu kwamba sisi tu watoto wa Mungu.” Ni roho ya Mungu inayoamsha ndani ya moyo wa mshiriki ye yote wa mwili wa Kristo usadiki wa kwamba yeye ni mmoja wa wana wa kiroho wa Mungu. Mchaguliwa huyo anajua hivyo na si lazima aulize mwingine katika kundi ili athibitishiwe.​—Warumi 8:15, 16, NW.

18. Ni mambo gani ya kihistoria juu ya “kondoo wengine” tunayopaswa kujua?

18 Historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova inaonyesha kwamba tangu mwaka wa 1931 fikira zaidi zilianza kuwekwa juu ya “kondoo wengine” kupitia ujumbe wa Ufalme. Halafu Mei 31, 1935, wakati ilipotolewa hotuba “Umati Mkubwa,”b “mkutano mkubwa” ambao Yohana aliona katika njozi ulitambulishwa wazi kuwa unahusiana na “kondoo wengine.” Mkazo huo mpya ulionyesha nini? Kwa uhakika mkusanyo wa “kundi dogo” ulikuwa ukikaribia kumalizika na wakati ulikuwa umefika Yesu ageuze fikira zake kwenye mkusanyo wa “kondoo wengine” kupitia usimamizi wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”​—Mathayo 24:45-47.

19. Ni uchunguzi gani wa kibinafsi unaoweza kufaa wale walio wapya zaidi ambao wamedai kuwa wapakwa mafuta?

19 Kwa kuyafikiria yaliyotangulia, tunawaambia wote wale ambao wameanza kushirikiana hivi majuzi na watu wa Yehova na ambao huenda wakawa wamedai kuwa mmoja wa jamii ya wapakwa mafuta, kwamba: Chunguza kwa uangalifu uone una uhusiano gani na Yehova. Jiulize mwenyewe, Je! tumaini la kimbingu ninalodai kuwa nalo linaelekea kidogo kuwa ni wazo lililosalia kutokana na fundisho la makanisa nililokuwa nalo kwamba wanakanisa wote wanaenda mbinguni? Je! kwa njia yo yote tumaini langu linakamatana na tamaa fulani ya kichoyo au misisimuko tu ya moyoni? Paulo alisema: “Mungu hawezi kusema uongo.” (Waebrania 6:18) Wala roho takatifu ya kulelea wana haiwezi kusema uongo. Basi, mtu ye yote aliyezaliwa kikweli kwa roho ya Mungu haendelei kusumbuliwa na mashaka bali anaweza kushuhudia kwa dhamiri njema kabisa kwamba yeye ni mmoja wa wana wa Mungu.

Kusherehekea Katika Mwaka wa 1985

20. Ukumbusho una maana gani kwa Mashahidi wa Yehova?

20 Bila shaka, Chakula cha Jioni cha Bwana ndiyo sherehe iliyo kubwa zaidi mwakani kwa Wakristo wote wa kweli. Hakuna pindi nyingine iliyo kama hiyo katika umaana, kusudi au utaratibu. Kwa hiyo, dunia itakapokuwa ikizunguka katika mhimili wake, ikifanya jua liendelee kushuka chini kwenye upeo wa macho sehemu zote za dunia, kila kundi la Mashahidi wa Yehova, kubwa na hata dogo, na kila kikundi kilicho peke yake watakutana pamoja kwa kutii amri ya Bwana Mkubwa.

21. Ni nia na matazamio gani ambayo Ukumbusho katika mwaka wa 1985 unapasa kutokeza katika mioyo ya watu wa Mungu?

21 Basi wanafunzi wote walio wa mfano wa kondoo wanafurahi sana kwa sababu ya taraja la kushiriki pamoja katika sherehe nyingine ya Ukumbusho. Pindi ya mwaka huu na iwe wakati wa kitiamoyo chenye kujenga watumishi wote wa Yehova. Na iingize ndani yao sana roho ile ile ya uhakika kama ya Kielelezo chao, Yesu Kristo, aliyesema: “Jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”​—Yohana 16:33.​—Kutoka w2/15/85

[Maelezo ya Chini]

a Katika kundi moja kubwa kumekuwa na zoea la kwamba wenye kupitisha mifano wanasimama mwisho wa kila mstari wa viti kisha wanawatolea ishara za mwili wale walioketi mstarini. Mtu ye yote anayetaka kushiriki amekuwa akipaswa kutolea mpitishaji ishara ya kwamba anataka kufanya hivyo. Lakini, kama ilivyoonyeshwa juu, jambo hilo halingefaa kufanywa.

b Hotuba hiyo ilitolewa huko Washington, D.C., na J. F. Rutherford, aliyekuwa wakati huo msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti.

Wewe Unaweza Kukumbuka​—

◻ Kwa sababu gani sikukuu ya Kupitwa haikuwa mfano wa kufananisha Ukumbusho?

◻ Ni hatua gani sita ambazo ni lazima zichukuliwe kabla ya kufaidika kutokana na dhabihu ya Yesu?

◻ Kwa sababu gani ni jambo la maana sana wewe uhudhurie Ukumbusho?

◻ Kwa sababu gani ni jambo lenye faida kujichunguza mwenyewe kabla ya Ukumbusho?

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Kuheshimu Chakula cha Jioni cha Bwana

Mifano Itakayotumiwa

Mkate usiotiwa chachu: Mkate, kama matzoth wa Kiyahudi usiotiwa dawa, ambao umetengenezwa kwa unga wa ngano na maji tu unaweza kutumiwa. Msitumie matzoth ambayo imetengenezwa kwa vichanganyiko kama chumvi, sukari, vimea vya pombe, mayai au vitunguu. Mnaweza kujitengenezea wenyewe mkate usiotiwa chachu mkitumia maelezo yanayofuata: Changanya kikombe kimoja na nusu cha unga wa ngano (ikiwa hauwezi kupatikana, tumia unga wa mchele, mahindi au nafaka nyingine) pamoja na kikombe kimoja cha maji, kwa njia hiyo ukitengeneza mkando wenye majimaji. Halafu tandaza mkando uwe mwembamba sana. Uweke juu ya kikaangio kisha uuchome-chome vitundu vidogo-vidogo kwa uma. Uoke katika joko la kuokea (au kikaangio) mpaka uwe mkavu na mgumu kuweza kuvunjika.

Divai: Tumieni divai isiyoongezewa cho chote kama Chianti, Burgundy, au claret. Epukeni divai zinazonywewa mara baada ya chakula ambazo zimeongezewa nguvu au zikarekebishwa kwa kutiwa brandy, kama vile sherry, port au muscatel. Msitumie divai iliyoongezewa vikolezo au ladha za mimea fulani, kama vile Dubonnet na divai nyingine za kuamsha hamu ya kula chakula. Divai iliyotengenezewa nyumbani inaweza pia kutumiwa ikiwa haikutiwa utamu, haikutiwa kikolezo wala kutiwa nguvu kwa kuongezewa kitu kingine.

Matayarisho ya Jumba la Ufalme

Meza ya mifano: Funikeni meza kwa kitambaa safi cha mezani kisha kuwe na sahani na bilauri za divai za kiasi kinachotosha ili zipitishwe kwa wakati unaofaa. Mkate unaweza kuvunjwa na divai imiminwe kabla ya mkutano. Yesu hakuanzisha kanuni yo yote ya kidesturi kuhusu jambo hilo. Hali zikidai iwe hivyo, funikeni mifano kwa kitambaa safi ili kuilinda na wadudu.

Wapitishaji: Toeni maagizo mapema kuhusu utaratibu utakaofuatwa ili kuepuka ukawizaji wo wote au mvurugo katika kupitishia wahudhuriaji wote mifano, kutia ndani msemaji na wapitishaji.

Wakaribishaji: Wakaribishaji wanaotosha wawepo muda mwingi kabla ya mwanzo wa mkutano ili wote waweze kukaribishwa wafikapo na kupewa kiti.

Mapambo ya maua: Hayo yanaweza kufanywa, lakini yasizidi kiasi, tena yawe ya kiasi cha kupendeza.

Utaratibu wa Mkutano

Wakati wa sherehe: Ingawa hotuba inaweza kuanza mapema zaidi, mifano haipasi kupitishwa mpaka baada ya jua kushuka. Inapasa iamuliwe kulingana na mahali penu ni wakati gani jua linaposhuka siku ya Aprili 4.

Hotuba ya Ukumbusho: Msemaji anapaswa kutayarisha vizuri ili aweze kutoa habari yake bila kupita wakati aliopewa. Inapasa kutolewa waziwazi kisha iwe ya kuwatia moyo wote waliopo.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ukumbusho unaongeza kina cha kupenda Yehova na Mwana wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki