Sura 19
Wakati Ujuzi Juu ya Mungu Unapoijaa Dunia
1, 2. Uumbaji wa Yehova ulikujaje kuharibiwa?
TUSEME msanii fulani mashuhuri amemaliza tu uchoraji wa picha bora sana. Yeye huiona kwa kufaa kuwa nzuri sana—kitu cha ustadi! Lakini wakati wa usiku mshindani fulani mwenye wivu anaiharibu. Kwa kueleweka, hilo humletea huyo msanii uchungu mwingi. Ana hamu kama nini ya kumwona mhalifu huyo akifungwa gerezani! Na unaweza kuwazia jinsi msanii huyo anavyotamani sana kuona ubuni wake ukirudishwa kwenye uzuri wao wa awali.
2 Kama vile msanii huyu, Yehova aliumba kitu cha ustadi katika kuitayarisha dunia na kuweka wanadamu juu yayo. Baada ya kuumba mwanamume na mwanamke, yeye alitangaza kazi yake yote ya kidunia kuwa ‘njema sana.’ (Mwanzo 1:31) Adamu na Hawa walikuwa watoto wa Mungu mwenyewe, naye aliwapenda. Aliwatakia wakati ujao mtukufu na wenye furaha. Ni kweli, Shetani aliwaongoza kwenye uasi, lakini uumbaji mzuri ajabu wa Mungu haukuharibiwa kwa njia isiyorekebika.—Mwanzo 3:23, 24; 6:11, 12.
3. “Uhai ulio kwelikweli” ni nini?
3 Mungu ameazimia kurekebisha mambo. Anataka sana kutuona tukiishi kwa njia aliyokusudia awali. Kuwako kwetu kwa muda mfupi na kwa taabu si “uhai ulio kwelikweli,” kwani ni wa hali ya chini zaidi ya ule ambao Yehova amekusudia. “Uhai ulio kwelikweli” ambao Mungu anatutakia ni “uhai udumuo milele” chini ya hali kamilifu.—1 Timotheo 6:12, 19, NW.
4, 5. (a) Tumaini la Paradiso litatimizwaje? (b) Sababu gani tufikirie tumaini letu la wakati ujao?
4 Ujuzi juu ya Mungu huleta daraka mbele ya Yehova. (Yakobo 4:17) Lakini fikiria baraka utakazofurahia ukitumia ujuzi huo na kufikilia uhai udumuo milele. Katika Neno lake, Biblia, Yehova Mungu amechora kwa rangi picha nzuri ya jinsi uhai utakavyokuwa katika dunia iliyo Paradiso ambayo iko karibu sana. Bila shaka, tukiwa watu wa Yehova sisi hatumtumikii Mungu kwa sababu tu ya kutamani thawabu. Twamtumikia Mungu kwa sababu twampenda. (Marko 12:29, 30) Zaidi ya hayo, sisi hatuchumi uhai kwa kumtumikia Yehova. Uhai udumuo milele ni zawadi itokayo kwa Mungu. (Warumi 6:23) Sisi tutanufaika tukitafakari juu ya uhai huo kwa sababu tumaini la Paradiso latukumbusha Yehova kuwa Mungu wa aina gani—“mthawabishaji [mwenye upendo] wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6, NW) Tumaini linalowaka kwa uangavu akilini na mioyoni mwetu litatuwezesha kuvumilia magumu katika ulimwengu wa Shetani.—Yeremia 23:20.
5 Acheni sasa tukazie fikira tumaini lenye msingi wa Biblia la uhai udumuo milele katika Paradiso ya kidunia ya wakati ujao. Uhai utakuwaje wakati ujuzi juu ya Mungu unapoijaa dunia?
BAADA YA HAR–MAGEDONI—DUNIA ILIYO PARADISO
6. Har–Magedoni ni nini, nayo itamaanisha nini kwa wanadamu?
6 Kama ilivyoonyeshwa mapema, karibuni Yehova Mungu atauharibu mfumo mwovu wa mambo uliopo. Ulimwengu unaelekea kwa kasi kwenye kile ambacho Biblia huita Har–Magedoni, au Armagedoni. Huenda neno hilo likawafanya watu wengine wafikiri juu ya uharibifu wa kinyukilia wenye kusababishwa na mataifa yanayopigana, lakini Har–Magedoni si ya aina hiyo. Kama vile Ufunuo 16:14-16 linavyoonyesha, Har–Magedoni ni “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Ni vita inayohusisha “wafalme wa ulimwengu wote,” au mataifa. Karibuni Mwana wa Yehova Mungu, Mfalme aliyewekwa rasmi, ataanza pigano hilo. Tokeo la hilo ni hakika kabisa. Wote wanaopinga Ufalme wa Mungu na ambao ni sehemu ya mfumo mwovu wa Shetani wataangamizwa. Ni wale tu walio waaminifu-washikamanifu kwa Yehova watakaookoka.—Ufunuo 7:9, 14; 19:11-21.
7. Shetani na roho waovu wake watakuwa wapi wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, na hilo litanufaishaje wanadamu?
7 Ebu wazia kwamba wewe umeokoka msiba huo mkubwa. Uhai ungekuwaje duniani katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa? (2 Petro 3:13) Hatuhitaji kukisia, kwani Biblia hutuambia, na yale inayosema ni yenye kusisimua. Twajifunza kwamba utendaji wa Shetani na roho waovu wake utakomeshwa, wakiwa wamefungiwa katika abiso ya kutotenda wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo. Viumbe hao waovu, wenye nia mbovu, hawatakuwa tena wakiotea-otea, wakisababisha taabu na kujaribu kutuchochea kufanya matendo yenye kukosa uaminifu dhidi ya Mungu. Ni kitulizo kama nini!—Ufunuo 20:1-3.
8, 9. Katika ulimwengu mpya, itakuwaje kwa taabu, maradhi, na kuzeeka?
8 Baada ya wakati fulani, namna zote za ugonjwa zitatoweka. (Isaya 33:24) Wakati huo walemavu watasimama, kutembea, kukimbia, na kucheza wakiwa na miguu yenye afya, iliyo na nguvu. Baada ya kuishi miaka mingi katika ulimwengu ulio kimya, viziwi watasikia sauti za shangwe zinazowazunguka. Vipofu watakata pumzi kwa kicho waanzapo kuuona ulimwengu wa rangi nzuri ajabu na maumbo. (Isaya 35:5, 6) Hatimaye, wataona nyuso za wapendwa wao! Labda wakati huo uwezo wao wa kuona utazuiwa kwa muda tu na machozi ya shangwe.
9 Ebu fikiria! Hakuna miwani tena, hakuna tena mikongojo na fimbo za kutembelea, hakuna madawa, hakuna kliniki za kutibu meno wala hospitali! Maradhi ya kihisiamoyo na mshuko wa moyo hayatawanyang’anya watu furaha tena. Hakuna utoto utakaokumbwa na maradhi. Madhara ya kuzeeka yataondolewa. (Ayubu 33:25) Tutakuwa wenye afya na wenye nguvu zaidi. Kila asubuhi tutaamka kutoka usingizi wa usiku tukiwa na nishati zaidi, tukiwa na nguvu nyingi na wenye hamu kwa ajili ya siku mpya ya uhai wenye nguvu, utendaji, na kazi yenye kuridhisha.
10. Waokokaji wa Har–Magedoni watafanya mgawo upi wa kazi?
10 Kutakuwa na kazi nyingi yenye kufurahisha ya kufanywa na waokokaji wa Har–Magedoni. Wao wataigeuza dunia kuwa paradiso. Masalio yoyote ya mfumo mchafu wa kale yataondolewa mbali. Mashamba na bustani yatatokea mahali pa mitaa michafu na bara lililoharibiwa. Wote watafurahia nyumba zenye ustarehe na zenye kupendeza. (Isaya 65:21) Kadiri wakati upitapo, zile sehemu za dunia zilizo za kiparadiso zitapanuka na kuungana mpaka dunia yote inapofikia kiwango cha uzuri kilichowekwa na Muumba huko nyuma katika bustani ya Edeni. Itaridhisha kama nini kushiriki katika kazi hiyo ya kurudisha hali ya kwanza!
11. Ni uhusiano gani wa wakati ujao utakaokuwako kati ya wanadamu na mazingira ya dunia na wanyama?
11 Yote hayo yatafanywa chini ya mwongozo wa kimungu hivi kwamba mazingira hayatadhuriwa. Wanadamu watakuwa na amani pamoja na wanyama. Badala ya kuwachinja bila huruma, wanadamu watakuwa tena na usimamizi wenye daraka juu ya dunia, wakiwatunza vizuri. Ebu ona akilini mbwa-mwitu na wana-kondoo, simba na ndama, wakila pamoja—na wanyama wa nyumbani wana usalama kabisa. Hata mtoto mdogo hatakuwa na kitu cha kuhofu kutoka hayawani-mwitu, wala utulivu wa ulimwengu huo mpya hautavurugwa na watu wakatili, walio wakali sana. (Isaya 11:6-8) Huo utakuwa ulimwengu mpya wenye amani kama nini!
WANADAMU WAGEUZWA
12. Isaya 11:9 linatimizwaje leo, nalo litatimizwaje katika Paradiso?
12 Isaya 11:9 latuambia ni kwa sababu gani madhara hayatafanywa katika dunia yote. Lasema hivi: “Dunia itajawa na kumjua [“ujuzi juu ya Yehova,” NW] BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Hilo lahusu watu kwa sababu wanyama hawawezi kutwaa “ujuzi juu ya Yehova” (NW) na kufanya mabadiliko, kwa kuwa wanaongozwa na silika. Lakini ujuzi juu ya Muumba wetu hubadili watu kwelikweli. Bila shaka tayari wewe mwenyewe umefanya mabadiliko kutokana na kutumia ujuzi juu ya Mungu maishani mwako. Mamilioni wamefanya hivyo. Kwa hiyo, unabii huu umeanza kutimizwa tayari katika wale wanaomtumikia Yehova. Hata hivyo, huo unaelekeza pia kwenye wakati ambapo watu ulimwenguni pote watakapoacha mazoea yoyote ya kinyama au yaliyo jeuri na kuwa wenye amani milele.
13. Ni programu gani ya elimu itakayokuwako duniani?
13 Utakuwa wakati mtukufu kama nini ujuzi juu ya Mungu unapoijaa dunia! Kutakuwa na programu ya elimu yenye kuenea chini ya mwelekezo wa Mfalme Yesu Kristo na watawala wenzake 144,000. “Hati-kunjo” mpya zitatumiwa wakati huo. Yaelekea hizo ni maagizo ya Mungu yaliyoandikwa yatakayotumiwa yakiwa msingi wa kuelimisha wakazi wa dunia. (Ufunuo 20:12) Wanadamu watajifunza amani, si vita. Silaha zote zinazoleta uharibifu zitatoweka milele. (Zaburi 46:9) Wakazi wa ulimwengu mpya watafundishwa kutendea wanadamu wenzao kwa upendo, staha, na adhama.
14. Ulimwengu utakuwaje tofauti wakati wanadamu ni familia moja yenye kuunganika?
14 Wanadamu watakuwa familia moja yenye kuunganika. Hakutakuwa na vizuizi kwa muungamano na udugu. (Zaburi 133:1-3) Hakuna nyumba ya yeyote itakayohitaji kufungwa kwa kufuli ili kuzuia wezi. Amani itatawala katika kila moyo, katika kila nyumba, katika kila sehemu ya dunia.—Mika 4:4.
UFUFUO WENYE SHANGWE
15. Ni vikundi vipi viwili vitakavyofufuliwa duniani?
15 Katika Mileani hiyo, ufufuo utatendeka. Wale waliotenda dhambi kimakusudi dhidi ya roho takatifu, au kani ya utendaji ya Mungu, kwa kutenda kinyume cha udhihirisho au mwelekezo wayo bila kutubu hawatafufuliwa. (Mathayo 23:15, 33; Waebrania 6:4-6) Bila shaka Mungu ataamua ni nani waliotenda dhambi kwa njia hiyo. Lakini vikundi viwili tofauti vitafufuliwa—“waadilifu na wasio waadilifu.” (Matendo 24:15, NW) Kwa kuwa kutakuwa utaratibu mzuri, ni jambo linalofaa kukata maneno kwamba wa kwanza watakaokaribishwa kwenye uhai tena duniani watakuwa waadilifu, wale waliomtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu.—Waebrania 11:35-39.
16. (a) Ni nani watakaokuwa miongoni mwa “waadilifu” watakaofufuliwa duniani? (b) Ni waaminifu wapi wa nyakati za kale unaotaka kukutana nao hasa, na kwa sababu gani?
16 Badala ya kusikia habari juu ya vita, misiba, na kifo, watumishi wa Yehova watapokea ripoti nzuri ajabu juu ya ufufuo. Itasisimua wee kupata kujua juu ya kurudi kwa wanaume na wanawake waaminifu kama vile Abeli, Henoko, Noa, Abrahamu, Sara, Ayubu, Musa, Rahabu, Ruthu, Daudi, Eliya, na Esta. Wao watatoa habari hakika za kihistoria zenye kuchochea kama nini wanapoeleza mambo ya kindani juu ya masimulizi mengi ya Biblia! Bila shaka wao na wale waadilifu ambao wamekufa katika nyakati za majuzi zaidi watakuwa na hamu vivyo hivyo kupata kujua juu ya mwisho wa mfumo wa Shetani na jinsi Yehova alivyotakasa jina lake takatifu na kutetea enzi kuu yake.
17. Waaminifu watatoa msaada gani kwa wengine wanaofufuliwa?
17 Waaminifu hao watakuwa wenye kusaidia kama nini katika hatua ifuatayo ya ufufuo, wakati maelfu ya mamilioni ya “wasio waadilifu” wanapoachiliwa kutoka katika vifungo vya kifo! Wanadamu walio wengi hawakuwa na nafasi kamwe ya kumjua Yehova. Shetani alikuwa ‘akipofusha akili zao.’ (2 Wakorintho 4:4) Lakini kazi ya Ibilisi itaangamizwa. Wasio waadilifu watarudi kwenye dunia nzuri na yenye amani. Wao watakaribishwa na watu waliopangwa vizuri kitengenezo ili kuwafundisha juu ya Yehova na Mwana wake anayetawala, Yesu Kristo. Maelfu ya mamilioni ya wale wanaofufuliwa wanapopata kumjua na kumpenda Muumba wao, ujuzi juu ya Yehova utaijaa dunia kwa njia isiyo na kifani.
18. Unafikiri utahisije unapowakaribisha wapendwa wanaofufuliwa?
18 Ufufuo utaleta shangwe iliyoje mioyoni mwetu! Ni nani ambaye hajateseka kwa sababu ya adui wetu kifo? Kwa kweli, ni nani ambaye hajahisi kuvunjika moyo kabisa wakati ugonjwa, uzee, aksidenti, au ujeuri ulipoondoa uhai wa mpendwa na kuvunja kifungo fulani cha upendo au urafiki? Basi, ebu wazia ile shangwe ya watu wengi kuungana pamoja tena katika Paradiso. Akina mama na akina baba, wana na mabinti, marafiki na watu wa ukoo, watakimbiliana ili kukumbatiana, wakicheka na kulia kwa shangwe.
UKAMILIFU HATIMAYE!
19. Ni muujiza gani utakaotendeka wakati wa Mileani?
19 Muda wote wa Mileani, muujiza mzuri ajabu utakuwa ukitendeka. Kwa wanadamu, itakuwa labda ndiyo sehemu yenye kusisimua zaidi ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Yehova atamwelekeza Mwana wake atumie manufaa za dhabihu ya fidia kwa kila mwanamume na mwanamke mwaminifu na mtiifu. Kupitia njia hiyo, dhambi yote itaondolewa na wanadamu watainuliwa kwenye ukamilifu.—1 Yohana 2:2; Ufunuo 21:1-4.
20. (a) Kuwa mkamilifu kutamaanisha nini? (b) Waokokaji wa Har–Magedoni na wale wanaofufuliwa wataanza kuwa hai katika maana kamili kabisa wakati gani?
20 Ukamilifu! Huo utamaanisha nini? Utamaanisha kurudi kwenye ule uhai ambao Adamu na Hawa walifurahia kabla hawajatenda dhambi dhidi ya Yehova Mungu. Wanadamu watafikia viwango vya Mungu kikamili—kwa njia zote zinazoweza kuwaziwa—kimwili, kiakili, kihisiamoyo, kiadili, kiroho. Lakini je, wakati huo watu wote watafanana sawasawa? La, hasha! Uumbaji mbalimbali wa Yehova—miti, maua, wanyama—unatufundisha kwamba yeye anapenda unamna-namna. Wanadamu wakamilifu watakuwa na nyutu na stadi tofauti-tofauti. Kila mmoja atafurahia uhai kama vile Mungu alivyokusudia uwe. Ufunuo 20:5 (NW) husema hivi: “Mabaki ya wafu hayakuja kwenye uhai mpaka miaka elfu ilipokuwa imekwisha.” Kama vile umati mkubwa wa waokokaji wa Har–Magedoni, wale wanaofufuliwa watakuwa hai katika maana kamili kabisa wanapofikia ukamilifu usio na dhambi.
21. (a) Ni nini kitakachotukia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo? (b) Ni nini kitakachompata Shetani na wote wanaomuunga mkono?
21 Wanadamu wakamilifu watakabili jaribu moja la mwisho. Mwishoni mwa Mileani, Shetani na roho waovu wake wataachiliwa kutoka katika abiso kwa muda mfupi nao wataruhusiwa kufanya jitihada ya mwisho ya kugeuza watu kutoka kwa Yehova. Wengine watatanguliza tamaa mbaya mbele ya upendo kwa Mungu, lakini uasi huo utafupizwa. Yehova atawaangamiza watu hawa wenye ubinafsi pamoja na Shetani na roho waovu wake. Ndipo wakosaji wote watakapotoweka milele.—Ufunuo 20:7-10.
UTAFANYA NINI?
22. Unatazamia kufanya nini katika Paradiso?
22 Umilele utaendelea mbele ya wale wampendao Yehova Mungu na kuishi katika dunia iliyo Paradiso. Hatuwezi kuwazia hata kidogo shangwe yao, na wewe pia waweza kushiriki katika hiyo. Muziki, usanii, ufundi—matimizo mbalimbali ya wanadamu wakamilifu yatapita zile kazi bora zaidi za wastadi waliokuwa mashuhuri zaidi katika ulimwengu wa kale! Kwa vyovyote vile, wanadamu watakuwa wakamilifu na watakuwa na wakati usio na kikomo mbele yao. Ebu wazia yale utakayoweza kufanya ukiwa mwanadamu mkamilifu. Fikiria, pia, yale ambayo wewe na wanadamu wenzako mtajifunza juu ya uumbaji wa Yehova—kuanzia yale maelfu ya mamilioni ya galaksi zinazoenea ulimwengu wote mzima hadi zile chembe zilizo ndogo zaidi kuliko atomi ndogo sana. Mambo yote yanayotimizwa na wanadamu yataufurahisha zaidi moyo wa Baba wetu wa kimbingu mwenye upendo, Yehova.—Zaburi 150:1-6.
23. Sababu gani uhai katika Paradiso hautakuwa wenye kuchosha kamwe?
23 Uhai hautakuwa wenye kuchosha wakati huo. Utazidi kuwa wenye kupendeza, kadiri wakati upitavyo. Waona, ujuzi juu ya Mungu hauna mwisho. (Warumi 11:33) Muda wote wa umilele, sikuzote kutakuwa na zaidi ya kujifunza na mambo mapya ya kuchunguza. (Mhubiri 3:11) Na uendeleapo kujifunza juu ya Yehova Mungu, utafuliza kuishi—si kwa miaka michache tu bali milele!—Zaburi 22:26.
24, 25. Sababu gani unapaswa kuishi sasa kwa kupatana na ujuzi juu ya Mungu?
24 Je, wakati ujao wenye kufurahisha kwenye dunia iliyo paradiso haustahili jitihada au dhabihu yoyote utoayo? Bila shaka unastahili! Basi, Yehova amekutolea ufunguo wa wakati ujao huo mzuri sana. Ufunguo huo ni ujuzi juu ya Mungu. Je, utautumia?
25 Ikiwa wampenda Yehova, utapata furaha katika kufanya mapenzi yake. (1 Yohana 5:3) Unapofuatia mwendo huo, utapata baraka zilizoje! Ukitumia ujuzi juu ya Mungu, huo unaweza kukuletea maisha yenye furaha zaidi hata katika ulimwengu huu wenye taabu. Na thawabu za wakati ujao ni nyingi sana, kwani huo ni ujuzi uongozao kwenye uhai udumuo milele! Sasa ndio wakati ufaao wa wewe kutenda. Azimia kuishi kwa kupatana na ujuzi juu ya Mungu. Onyesha upendo wako kwa Yehova. Heshimu jina lake takatifu na umthibitishe Shetani kuwa mwongo. Kisha, Yehova Mungu, aliye Chanzo cha hekima na ujuzi wa kweli, atashangilia juu yako katika moyo wake ulio mkuu na wenye upendo. (Yeremia 31:3; Sefania 3:17) Naye atakupenda milele!
TAHINI UJUZI WAKO
“Uhai ulio kwelikweli” ni nini?
Baada ya Har–Magedoni, ni nini kitakachotendeka duniani?
Ni nani watakaofufuliwa duniani?
Wanadamu watakuwaje wakamilifu nao watajaribiwaje mara ya mwisho?
Tumaini lako ni nini kuhusu Paradiso?
[Picha katika ukurasa wa 188, 189]
Je, watumaini kuishi katika Paradiso, wakati ujuzi juu ya Mungu unapoijaa dunia?