Wewe Unaweza Kuhamisha Milima!
INARIPOTIWA kwamba Mei 29, 1953 ulikuwa ndio wakati wa kwanza mwanadamu kusimama juu ya kilele cha mlima ulioinuka juu zaidi ya mingine yote ulimwenguni—Mlima Everest, meta 8,848 juu ya usawa wa bahari. Kwa kutegemezwa na wanaume zaidi ya 450, Edmund Hillary wa New Zealand na Tenzing Norgay, mmoja wa Washerpa wa kabila la Kinepali lenye wapandaji hodari, walifaulu kushinda hatari za barafu yenye kutelezesha, theluji yenye kuziba mwono wa macho, na ukosefu wa oksijeni ili wafikie sehemu ya juu ya mradi wao wenye kimo cha kilometa 8.8.
Hakika kupanda kileleta cha milima yenye kuinuka juu sana ni uhodari mkubwa. Hata hivyo hakuwezi kulinganishwa na jambo ambalo Yesu alieleza wanafunzi wake: “Mimi naambia nyinyi kwa uzito, kama imani yenu ingekuwa ya ukubwa wa mbegu ya haradali nyinyi mngeweza kusema kwa mlima huu, ‘Hama kutoka hapa kwenda pale’, nao ungehama; hakuna jambo lingekuwa lisilowezekana kwa nyinyi.” Ebu wazia, si kupanda mlima bali kuuhamisha!—Mathayo 17:20, The Jerusalem Bible.
Ni jambo gani lililoharakisha Yesu kusema hivyo kwa wanafunzi wake? Ni muda mfupi tu uliokuwa umepita tangu wao washindwe kuponya mvulana mwenye roho mwovu. Yesu alikazia sababu ya kushindwa kwao: Walihitaji imani nyingi zaidi. (Mathayo 17:14-20) Yeye alilinganisha imani na mbegu ya haradali, kitu ambacho wao walifahamu vizuri. Ingawa mbegu ya haradali ni miongoni mwa zile zilizo “ndogo kuliko mbegu zote,” baada ya miezi michache ya ukuzi ingekuwa mmea ulio kama mti. (Mathayo 13:31, 32) Hivyo, Yesu alikuwa akikazia uwezo mkubwa ambao imani kidogo ingeweza kuwa nao ikisitawishwa na kulishwa ifaavyo—mambo yenye kuonekana kama yasiyowezekana yangewezekana.
Lakini baada ya kukuza imani kama hiyo, ni milima ya aina gani ambayo wanafunzi wa Yesu wangeweza kuhamisha? Sawa na vile mlima halisi unavyoweza kuonekana mkubwa mno, vipingamizi vilivyo kama mlima vinaweza kuzuia maendeleo yetu katika utumishi wa Yehova. Huenda “milima” hiyo ikawa ni nini na ni jinsi gani sisi tunaweza ‘kuihamisha’?
Mtume Paulo ni kielelezo cha Mkristo aliyekabili vipingamizi vingi. Kwenye 2 Wakorintho 6:4-10 na 2 Wakorintho 11:23-28, unaweza kusoma kwamba alikosa mahitaji ya maisha, akapata mapigo, akafungwa gerezani, akavunjikiwa meli, na kupatwa na maafa mengine mengi. Zaidi ya mambo hayo, ulikuwako “mwiba katika mwili” kwa njia ya kitamathali, yawezekana ukiwa ni tatizo fulani kuhusu mwono wa macho yake. (2 Wakorintho 12:7; Matendo 14:5) Iliwezekanaje yeye kupita juu ya vizuizi hivyo vilivyo kama milima na kufaulu kufanya mapenzi ya Mungu kwake? “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” Paulo akaandika. Ilikuwa hivyo “ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu.” (Wafilipi 4:13; 2 Wakorintho 4:7) Hivyo, Paulo alikuwa na itibari kamili kabisa kwamba Yehova ana uwezo wa kumwimarisha kama ngome wakati wa uhitaji mkubwa zaidi. Yeye alikuwa na imani.
Kuhamisha Milima Leo
Je! tamaa yako wewe ni kuongeza utumishi wako kwa Yehova? Kama mamia ya maelfu ambao wamejiunga na hesabu zinazoongezeka za wahubiri wa wakati wote (mapainia), wewe pia huenda ukahisi uharaka wa nyakati hizi na huenda ukafikiria kwa uzito kupanua huduma yako. Hata hivyo, je! kipingamizi fulani kinachoonekana kuwa kisichopitika kinasimama mbele yako kama mlima mkubwa? Ikiwa ndivyo, je! wewe unaweza kuhamisha milima? Maelfu wamefanya hivyo katika jitihada zao za kuongeza utumishi wao kwa Yehova. Haya ni machache tu ya mambo waliyojionea.
Dada mmoja kijana ambaye angehitimu shule akiwa wa mbele zaidi katika darasa lake alitamani kupainia, lakini mlima wake ulikuwa ukosefu wa kazi ya kuajiriwa. Yeye anasimulia hivi:
“Kufikiri kwangu mwenyewe kwa mwelekeo hasi na mashaka yangu juu ya kupainia kukawa kipingamizi nilichopaswa kushinda. Kwa kuwa nilihangaikia sana kupata kazi kabla sijaanza kupainia, mimi nilikuwa sitii itibari na uhakika wangu kamili katika Yehova na uwezo wake wa kuandalia wale wanaotanguliza kwanza ibada yake. Niliendelea kufikiri hivi, ‘Kwanza nitatafuta kazi, na hapo ndipo nitajaza ombi langu la upainia.’ Mimi sikuwa nikipainia; kwa kweli nilikuwa nikipoteza wakati wenye thamani kubwa. Hata hivyo, mmoja wa wazee wa kundi alinionyesha kwamba kadiri ambavyo ningezidi kungojea kuanza kupainia, ndivyo kazi za wakati wote zingezidi kuvutia, kwa maana mimi sikuwa na jambo lolote la kunizuia nisizikubali.”
Yeye alifanya nini? “Mimi nilisali kwa uendelevu kumwomba Yehova roho takatifu yake ili iongoze na kuelekeza vitendo na kufikiri kwangu.” Dada huyu alifanya upainia msaidizi baada ya kuhitimu, halafu akaingia huduma ya painia wa kawaida. Muda mfupi baada ya hapo, alipata kazi ya kimwili inayofaa ambayo ilimpa nafasi ya kupangia ratiba yake ya upainia.
Mzee mmoja, ambaye mke wake alikuwa katika utumishi wa painia na aliyekuwa na watoto wawili wa kulea, alihisi kwamba alipaswa kufanya mengi kuliko kutegemeza jamaa yake kifedha tu. Kwa watazamaji fulani, mastakimu zenye kumzuia utumishi wa painia zilionekana kuwa zisizopitika, na bado yeye alitamani kupanua huduma yake. Ni nini kilichopasa kubadilishwa?
“Nafikiri kipingamizi kikubwa zaidi nilichopaswa kushinda kilikuwa mimi mwenyewe hasa,” yeye anasema. “Huduma ya shambani ni kitu ambacho sikuzote mimi nilifurahia, na kwa kuongea pamoja na wale walio katika huduma ya wakati wote na kuona baraka zao, niliona kwamba roho nzuri sana waliyoonyesha iliambukiza wengine. Ningeweza kujiona mwenyewe nikiwa katika huduma ya wakati wote siku moja. Tatizo la kufikiri kwangu lilikuwa kwamba kupainia kulikuwa jambo ambalo mimi nililifikiria tu. Lakini sikuwa nimejiwekea kamwe tarehe niliyopenda kutimiza mradi huo.
Baada ya ufikirio wenye sala, ndugu huyo alianza kujitahidia mradi wake wa utumishi wa wakati wote. Aliendea msimamizi wake kazini, akaeleza madhumuni yake, na kuomba aruhusiwe kufanya kazi saa chache zaidi kila juma. Kwa habari ya sera ya kampuni, ratiba ya namna aliyotaka ilikuwa haijaruhusiwa wakati wowote.
Yeye anaendelea kusema: “Msimamizi wangu alimaliza maongezi kwa kusema kwamba ilielekea zaidi kuwa nisingepokea ratiba niliyokuwa nikiomba. Mimi nilikuwa na uhakika kabisa kwamba kama uamuzi ungekuwa wake peke yake, jibu lingekuwa hapana. Kwa hiyo kibali kingeweza kupatikana kwa utegemezo wa Yehova tu. Juma moja na nusu baadaye, kibali cha ratiba yangu mpya kilipatikana kutoka kwa wakurugenzi. Baada ya kumtolea asante msimamizi wangu, nikaenda nje kwenye gari langu, nikaliendesha mwendo mfupi, nikaliegesha kando ya barabara, na kusema asante na shukrani kwa Yehova. Ndiyo, mradi wangu wa utumishi wa wakati wote ungeweza kuwa uhalisi.”
Dada mmoja aliyeolewa ‘alihamishaje’ mlima wake? Yeye anasimulia hivi: “Mimi nina watoto wanne na mume asiyeitikadi. Nilipoanza kufikiria kupainia, nilikuwa na vipingamizi vya kutosha. Kwanza, kwa muda fulani mume wangu alikosa kazi ya kuajiriwa, kwa maana kazi yake ilikuwa ya majira kwa majira, nami nilikuwa nikifanya kazi ya nusu-siku ili kusaidia gharama. Kwa hiyo nikajisemea kwamba mimi singeweza kupainia kwa sababu ya mastakimu zangu, hata ingawa nilikuwa na tamaa hiyo. Hata hivyo, hapa ndipo nilipolazimika kurekebisha kufikiri kwangu. Niling’amua kwamba kama ningeendelea kufikiri kwamba singeweza, singetia kamwe jitihada ya kujaribu. Swali lile jingine la maana nililopaswa kujibu lilikuwa, Nitapata wapi imara ya kupainia? Nilipata jibu kwenye Wafilipi 4:13. Si kwamba nilisali tu kwa Yehova juu ya jambo hilo bali nilianza pia kumtegemea yeye zaidi na zaidi. Nilichukua pia hatua zenye mafaa kuelekea kufikia mradi wangu kwa kupanga ratiba njema na nikajiandikisha kuwa painia msaidizi. Kadiri wakati ulivyopita, Yehova aliendelea kunifungulia njia ya kuingia utumishi wa painia. Mume wangu aliweza kurudi kazini, nami nikaweza kufanya kazi yangu ya nusu-siku iwe ya siku moja tu kwa juma. Muda si muda, nikawa painia wa kawaida.”
Zaidi ya hilo, pendeleo la kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia lilimfungukia, na huo ukathibitika kuwa msaada mkubwa katika huduma yake. “Nataka tu kuambia mtu yeyote anayefikiria kupainia asali kwa Yehova na kuweka jambo lile mikononi mwake,” anasema dada huyo. “Halafu tia jitihada inayohitajiwa, naye atakubariki kwa kujaribu.”—Zaburi 37:5.
Je! mambo hayo yaliyoonwa hayakusaidii wewe kuona jinsi imani ikifanyiwa mazoezi inavyoweza kusaidia Mkristo ashinde vipingamizi vilivyo kama milima? Hivyo, ikiwa ni tamaa yako kupainia, chunguza mastakimu zako. Ongea na wengine wanaopainia, na ujifunze kutokana na mambo waliyojionea. Chukua hatua zenye mafaa kuelekea kufikia mradi wako. Na juu ya yote, sali kwa Yehova juu ya tamaa yako; halafu mtegemee abariki jitihada zako. Ndiyo, wewe pia unaweza kuhamisha milima!