Je, Unalitumia Neno la Mungu Sawasawa?
1 Yesu Kristo alikuwa mfundishaji mkubwa kupita wote aliyepata kuishi duniani. Alisema kwa njia iliyogusa mioyo ya watu, akachochea hisia-moyo zao, na kuwahamasisha wafanye matendo mema. (Mt. 7:28, 29) Sikuzote yeye alitumia Neno la Mungu kuwa msingi wa ufundishaji wake. (Luka 24:44, 45) Alimpa Yehova Mungu sifa kwa yote aliyojua na aliyoweza kufundisha. (Yn. 7:16) Yesu aliwekea wafuasi wake kielelezo bora kwa kulitumia Neno la Mungu sawasawa.—2 Tim. 2:15, NW.
2 Mtume Paulo pia alikuwa kielelezo chenye kutokeza kwa kulitumia Neno la Mungu kwa matokeo. Yeye hakuwasomea wengine Maandiko tu; alieleza na kusababu aliyosoma, akitoa ithibati kutoka Neno la Mungu kwamba Yesu ndiye aliyekuwa Kristo. (Mdo. 17:2-4) Hali kadhalika, mwanafunzi mwenye ufasaha Apolo “alikuwa hodari katika maandiko,” naye aliyatumia sawasawa katika kufanya utoaji wenye nguvu wa ile kweli.—Mdo. 18:24, 28.
3 Kuwa Mfundishaji wa Neno la Mungu: Wapiga-mbiu wa Ufalme wa siku ya kisasa wamefurahia mafanikio bora zaidi katika kufundisha watu wenye mioyo ya haki kwa kurejezea na kusababu kutokana na Biblia. Katika kisa kimoja, ndugu aliweza kutumia Ezekieli 18:4 pamoja na maandiko yaliyohusiana kusababu na pasta na washiriki wake watatu wa parokia juu ya matokeo yasiyoepukika ya waovu na waadilifu. Likiwa tokeo, washiriki fulani wa kanisa walianza kujifunza, na mmoja wao hatimaye aliikubali kweli. Katika kisa kingine, dada aliombwa amweleze mume mwenye kupinga wa mwanamke anayependezwa kwa nini Mashahidi wa Yehova hawaadhimishi Krismasi na siku za kuzaliwa. Alipokuwa akisoma majibu ya Kimaandiko moja kwa moja kutoka kitabu Kutoa Sababu, mwanamume huyo alikubaliana na hilo. Mke wake alipendezwa sana na kukubali kwake hivi kwamba akasema: “Tutakuja kwenye mikutano yenu.” Na yule mume akakubali!
4 Tumia Msaada Upatikanao: Huduma ya Ufalme Yetu na programu ya Mkutano wa Utumishi hutoa mwelekezo unaofaa wa kutusaidia jinsi ya kulitumia Neno la Mungu. Watangazaji wengi wameonyesha uthamini kwa utoaji mbalimbali uliodokezwa ambao unachapishwa na kutolewa maonyesho kwa manufaa yetu na ambao umethibitika kuwa wa wakati unaofaa na wenye matokeo. Kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kina mawazo mengi sana juu ya jinsi ya kueleza sawasawa masomo ya msingi zaidi ya 70 yanayosimuliwa katika Neno la Mungu. Kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele huandaa muhtasari sahihi wa mafundisho yote ya msingi ya Biblia ambayo walio wapya wanahitaji kuelewa. Masomo 24 na 25 katika kitabu Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huonyesha jinsi wafundishaji wenye stadi hutoa utangulizi vizuri, kusoma na kutumia maandiko. Twapaswa kutumia vizuri msaada huu wote unaopatikana kwetu.
5 Tunapolitumia Neno la Mungu sawasawa, tutaona kwamba “li hai, tena lina nguvu, . . . tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo” ya wale ambao twahubiria. (Ebr. 4:12) Mafanikio tunayofurahia kwa kulitumia, yatatuchochea tuseme kweli kwa ujasiri mkubwa zaidi!—Mdo. 4:31.