Tuna Utume
1 Yesu aliwaamuru mitume wake ‘kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi.’ (Mt. 28:19) Katika nchi 232 na vikundi vya visiwa duniani pote, zaidi ya wasifaji milioni tano wa Yehova Mungu ni ushuhuda ulio hai wa kutimizwa kwa amri ya Yesu. Lakini vipi sisi binafsi? Je, sisi huchukua kwa uzito ule utume wa kuhubiri?
2 Wajibu wa Kiadili: Utume ni “amri ya kufanya matendo yaliyoagizwa.” Tumeamriwa na Kristo tuhubiri. (Mdo. 10:42) Mtume Paulo alitambua kwamba jambo hili lilimbidisha, au kumwajibisha kiadili, kujulisha habari njema. (1 Kor. 9:16) Ili kutoa kielezi: Wazia kwamba wewe ni baharia kwenye mashua inayozama. Nahodha anakuamuru uonye abiria na kuwaelekeza kwenye mashua za kuokolea uhai. Je, utapuuza amri na kujali kujiokoa mwenyewe tu? Kwa hakika sivyo. Wengine wanakutegemea. Maisha zao zimo hatarini. Wewe unawajibika kiadili kufikiliza utume wako ili kuwasaidia.
3 Sisi tumeamriwa kimungu tutoe onyo. Hivi karibuni Yehova atakomesha mfumo huu wote wa mambo ulio mwovu. Tokeo la hatimaye la mamilioni ya watu halijulikani. Je, ingekuwa sawa kwetu kupuuza hatari ya wengine na kujali tu kujiokoa wenyewe? Bila shaka sivyo. Sisi twawajibika kiadili kusaidia kuokoa maisha za wengine.—1 Tim. 4:16.
4 Vielelezo vya Uaminifu vya Kufuata: Nabii Ezekieli alihisi uwajibikaji kutoa ujumbe wenye onyo kwa Waisraeli wasio waaminifu. Yehova alimwonya kwa mkazo juu ya matokeo ikiwa angeshindwa kufikiliza mgawo wake: “Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; wewe usimpe maonyo . . . , mtu yule mbaya atakufa katika uovu wake; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako.” (Eze. 3:18) Ezekieli alitimiza kwa uaminifu-mshikamanifu utume wake hata alipokabili upinzani mkali. Kwa hiyo, alishangilia wakati hukumu za Yehova zilipokuwa zikitekelezwa.
5 Karne kadhaa baadaye, mtume Paulo aliandika kuhusu daraka lake la kuhubiri. Yeye alijulisha: “Sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu.” Paulo alihubiri hadharani na nyumba hadi nyumba kwa sababu alitambua kwamba kushindwa kufanya hivyo kungemfanya awe na hatia ya damu mbele ya Mungu.—Mdo. 20:20, 26, 27.
6 Je, sisi tuna bidii ya Ezekieli? Twahisi kubidishwa kuhubiri kama alivyofanya Paulo? Utume wetu ni sawa na wao. Lazima tuendelee kutimiza daraka letu la kuonya wengine, ujapokuwa ubaridi wao, kutopendezwa, au upinzani. Maelfu zaidi bado wanaweza kuitikia ujumbe wa Ufalme na kujulisha: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zek. 8:23) Upendo wetu kwa Mungu na mwanadamu mwenzetu na utuhamasishe tusife moyo. Tuna utume wa kuhubiri!