Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 8/15 kur. 373-379
  • Kukunjuka Katika Upendo Wetu kwa Wanadamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukunjuka Katika Upendo Wetu kwa Wanadamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUUIGA MFANO WA MUNGU
  • KAZI YA LAZIMA YA KUUHUBIRI UFALME NA KUFANYA WANAFUNZI
  • Kwa Sababu Gani Kujali Yale Yanayowapata Watu Wengine?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Ukarimu Unaleta Thawabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Upendo—“Njia Bora Zaidi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Iweni Wanafunzi wa Kweli wa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 8/15 kur. 373-379

Kukunjuka Katika Upendo Wetu kwa Wanadamu

1. Kama ilivyoonyeshwa na Yesu Kristo, ni nini yanayotiwa ndani katika kuonyesha upendo kwa ukamili kwa wanadamu wenzetu?

JE! UPENDO wako kwa wanadamu wenzako unakunjuka? Je! wewe unafanya maendeleo katika kukamilisha upendo wako? Hii inatia ndani mengi zaidi ya kuwa mfadhili na mkarimu kwa watu wanaokupenda wewe. Yesu Kristo alisema hivi: “Maana mkiwapenda wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi [watu wenye sifa mbaya] huwapenda wale wawapendao. Nanyi mkiwatendea mema wale wawatendeao mema, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo. Na mkiwakopesha watu huku mkitumaini kupata kitu kwao, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi, ili warudishiwe vile vile. Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu.”​—Luka 6:32-35.

2. Yehova ameonyeshaje fadhili na upendo hata kwa wasioshukuru na waovu?

2 Fikiria namna Yehova Mungu amekuwa mfadhili kwa wasio na shukrani na waovu. Wanafaidika kutokana na mipango aliyoipanga kuwezesha uhai uwepo duniani. Yeye hawanyimi mambo yaliyo ya lazima kwao wapate kuwa hai​—hewa, mwanga wa jua na mvua. “Ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) “Yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”​—Mt. 5:45.

3. Matendo ya wakati uliopita ya Yehova yanafunua nini juu ya uwezo wake wa kukataa kutoa mwanga wa jua na mvua?

3 Yehova Mungu ni mfadhili na mkarimu kwa hiari. Kama Muumba, yeye anao usimamizi juu ya vitu vyote vilivyo vya lazima kwa uhai naye aweza kukataa asitoe zawadi zake kwa njia ya uteuzi. Hii ni wazi kutokana na matendo yake ya wakati uliopita. Wakati wa Musa aliwanyima Wamisri mwanga wa jua kwa siku tatu, lakini wakati uo huo akawapa Waisraeli mwanga. (Kut. 10:23) Karne nyingi kufuata hapo, Yehova alizuia mvua isinye wakati ambapo Waisraeli walikuwa wasioaminika kwake. Kupitia kwa nabii wake Amosi, aliwakumbusha hivi: “Tena nimeizuia mvua msiipate, ilipobaki miezi mitatu kabla ya mavuno; nami nimenyesha mvua juu ya mji mmoja, nikaizuia mvua isinye juu ya mji mwingine; sehemu moja ilipata mvua, na sehemu isiyopata mvua ilikauka.”​—Amosi 4:7.

4. (a) Kwa sababu gani Yehova Mungu hakuwanyima wasioshukuru na waovu mahitaji ya maisha? (b) Yehova amefanyaje mengi zaidi ya kutoa mahitaji kwa kuonyesha upendo?

4 Lakini kwa sababu gani Yehova Mungu hakuwanyima waovu mwanga wa jua na mvua na hali aweza kufanya hivyo? Kwa sababu gani amekuwa mfadhili na mwenye upendo hata kwa wale wasioshukuru kwa zawadi zake? Yeye amefanya hivi awape nafasi ya kugeuka, wachague kumtumikia yeye. Kwa kweli, hata amefanya mengi zaidi kuliko kuwaruhusu wapate mahitaji ya maisha. Aliwapangia wao na wanadamu wengine mpango wa kuwekwa huru na dhambi na mauti. Ilimgharimu yeye sana kufanya hivi, kumtoa dhabihu Mwanawe mzaliwa wa pekee. (Yohana 3:16) Biblia yasema, “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Rum. 5:8) Tendo hili la upendo liliweka msingi halali wa kukomboa wanadamu kutoka kwa utumwa kwa dhambi ambamo waliingia Adamu alipojipotezea uhai mkamilifu wa kibinadamu na watoto wake waliokuwa hawajazaliwa.

5. Taifa la kibinadamu ni mali ya nani, na kwa sababu gani?

5 Bei ya ukombozi ilikuwa uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Yesu Kristo. Kwa kuwa uhai wake ndio uliokuwa bei, Yesu anashiriki uenyeji wa taifa la kibinadamu na Yehova Mungu, Mwanzilishi wa mpango huo. Ndiyo sababu Maandiko yanazungumza juu ya Mungu na Kristo vile vile kama wakifanya ununuzi. Twasoma juu ya “kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe.” (Matendo 20:28) Na juu ya Yesu Kristo, Ufunuo 5:9 unatangaza hivi: “Ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa.” Kwamba si washiriki wa kundi la Mungu peke yao waliomo kati ya wale walionunuliwa yaonyeshwa wazi na 1 Timotheo 2:6, NW, ambapo Yesu anatajwa kama akijitoa kama “ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.” Je! upendo wako kwa wanadamu wenzako unaendelea kukunjuka kwa sababu unafahamu kwamba wanadamu wote ni mali ya Mungu hasa na ya Kristo?

6. Mungu anathaminije uhai?

6 Yehova Mungu anauona uhai kama kitu chenye thamani kubwa sana. Yeye hataki wale aliowanunua kwa damu yenye thamani nyingi ya Mwanawe watoweke. Ni mapenzi yake kwamba watu wa kila mahali, bila ya kujali hali yao katika maisha, wajifunze kweli, waukubali mpango wake na kupata uzima. (1 Tim. 2:1-4) “Hapendi mtu ye yote apotee,” ndivyo alivyoandika mtume Petro, “bali wote wafikilie toba.”​—2 Pet. 3:9.

KUUIGA MFANO WA MUNGU

7, 8. Twaweza kujiuliza nini tunapoangalia kama tunaionyesha nia ya Mungu juu ya wanadamu?

7 Katika ukamatano wako na wengine, je! wewe unaonyesha nia ya Mungu juu ya wanadamu? Yehova Mungu anachukia sana uovu, lakini anawapenda wanadamu kama mali yake naye anawatakia wao mema tu. Je! wewe unatendea watu kama mali ya Mungu, ukiwataka wazishiriki baraka alizoziweka akibani kwa wale wanaoziheshimu haki zake za uenyeji? Ikiwa tunayo maoni yale yale Mungu aliyo nayo juu ya wanadamu, kumepaswa kuwepo ushuhuda wa kwamba tunajitahidi kuwa wafadhili, wakarimu na wenye upendo.

8 Unapoendelea kulichunguza jambo hili, waweza kujiuliza hivi: Wakati ninapokuwa na uhuru wa kutumia wakati wangu, mali na uwezo, je! navitumia hivi kwa faida yangu peke yangu, jamaa yangu na rafiki zangu? Au, nafikiria ninayoweza kuwafanyia wengine walio maskini au wale wawezao kuwa wapweke, hata ikiwa utu wao haunivutii mimi sana? Je! nawafanya wengine wajisikie wanafurahiwa? Je! nina nia ya kujitoa niwatumikie wengine bila ya kutazamia nilipwe cho chote nao? Mimi natendaje wakati mtu fulani ambaye amekuwa mkali sana kwangu anapopatwa na taabu kubwa ya kimwili? Je! namhurumia? Je! najaribu kumsaidia mtu huyo? Je! ningeweza kuwa na nia ya kumsaidia yeye kwa kazi za nyumbani​—nikimpikia chakula, kwenda kumnunulia vitu, kufua nguo, kusafisha nyumba? Je! ningekuwa na nia ya kumkopesha fedha hata nikijua kwamba mapato yake ni madogo sana hata huenda asiweze kunilipa?​—Linganisha Kutoka 23:4, 5.

9. Kama ilivyoonyeshwa na Yesu Kristo katika Luka 14:12-14, twaweza kuwa na uhakika wa nini tunapouiga mfano wa Mungu wa ukarimu?

9 Wakati ambapo ukarimu wako, fadhili na upendo vinaonyeshwa zaidi kupita ilivyotazamiwa na kuwatia ndani maskini na vile vile wale ambao huenda hawakukutendea vema, wewe unamwiga Yehova Mungu. Wewe unakunjuka katika upendo wako kwa wanadamu wenzako. Unatenda kupatana na uhakika wa kwamba wao wamenunuliwa na Mungu na Kristo. Kwa hiyo, waweza kuwa na uhakika wa kwamba Mungu atakuthawabisha. Yesu Kristo alikazia hili, akisema hivi: “Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali [kama ilivyo kawaida]; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo. Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.”​—Luka 14:12-14.

10. Fadhili yaweza kuwa na matokeo gani mema juu ya mtu mwenye uadui?

10 Zaidi ya hayo, kuwatendea wale wanaoonyesha roho ya uadui kwa fadhili na upendo kwaweza kukawafanya waione haja ya kuutambua uenyeji wa Mungu juu yao. Angalia namna Warumi 12:20 inavyosema juu ya hili: “Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.” Kama vile moto unavyoyeyusha chuma, huenda fadhili yako ikailainisha nia yake ya ukali kwako, kumwaibisha, asikitike juu ya namna alivyokutendea na kumvuta abadili njia zake. Yaweza ikafungua macho yake akaona maana hasa ya Ukristo na kumharakisha aanze kuchukua hatua za kushiriki nawe katika ibada ya kweli.

11. Ni nini kinachoamua kama mtu anaonyesha upendo, ukarimu na fadhili kwa ukamili?

11 Bila shaka, kadiri ambavyo sisi kama watu mmoja mmoja twaweza kutendea wengine mema inawekewa mipaka na hali. Huenda ukawapo upungufu wa kimwili na/au wa mambo ya fedha. Kwa hiyo mtu ye yote asivunjike moyo ati kwa sababu hawezi akafanya mengi kama vile mwingine anavyoweza kufanya. Jambo linaloamua kama sisi tunaonyesha upendo kamili, ukarimu na fadhili siyo wingi. Ni shauri la kuwa na roho yenye nguvu ya ukarimu, fadhili na upendo, tukitumia uwezo wetu na mali kwa ukamili tuwe chanzo cha kutia moyo na baraka kwa wengine.

12. Je! daraka kubwa alilo nalo Mkristo ni kuangalia ulimwengu wa wanadamu waliofarikishwa na Mungu?

12 Kama Wakristo wajibu wetu wa kwanza ni kwa jamaa zetu na waamini wenzetu. Maandiko yanasema hivi: “Mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Tim. 5:8) “Na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Gal. 6:10) Kwa hiyo, basi, ingekuwa kosa kusahau washiriki wa jamaa na waamini wenzetu huku tukijaribu kusaidia wengine wa ulimwengu wa wanadamu. Matendo yetu kwa wale wanaohusiana nasi kwa njia ya kimwili na ya kiroho yamepaswa yawe ya kutokeza tunapoonyesha fadhili, upendo na kupendezwa kwingi na hali yao.

13. Ni wakati gani ambapo kunyima mtu mambo ya kimwili kungekuwa wonyesho wa upendo kwake?

13 Lakini, nyakati nyingine wonyesho wa ukarimu usingeweza kuwasaidia wanaoonyeshwa ukarimu wenyewe. Watu wengine, nyakati nyingine hata Wakristo wenzetu, wanajionyesha kuwa wazembe, wavivu na wasio na nia ya kukubali kufanya kazi hata wakati ambapo kazi wanazoweza kuzifanya zinapatikana. Kama wangepewa msaada wa mambo ya kimwili, wasingetiwa moyo wabadili maoni yao mabaya juu ya kazi. Kwa habari yao amri ya Biblia katika 2 Wathesalonike 3:10 ingetumika: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.” Pia, Wakristo wanakataa kwa haki kusaidia wale ambao wanatumia vitu wanavyopewa kwa matendo na tabia zinazokatazwa kwa kimungu. Kwa kweli kumnyima mtu mambo fulani kwaweza kuwa wonyesho wa upendo na kupendezwa naye sababu yake inapokuwa kukazia akilini mwake na moyoni haja ya kubadilika wala siyo kutumia vibaya mali ambazo wengine walijitahidi sana wazipate.

KAZI YA LAZIMA YA KUUHUBIRI UFALME NA KUFANYA WANAFUNZI

14. Kwa sababu gani kutoa msaada wa kiroho ni jambo la haraka hasa leo?

14 Ulio wa muhimu zaidi kuliko upaji wa mambo ya kimwili ndio msaada ambao Wakristo wanaweza kutoa kwa njia ya kiroho. Hili ni jambo la haraka hasa sasa​—linalohusu uzima au kifo. Namna gani hivyo? Unabii wa Biblia na mambo yanayoonekana kwa kuutimiza unahakikisha kwamba tangu mwaka wa 1914 C.E. kizazi kilichopo sasa kimo katika “wakati wa mwisho.” (Mt. 24:3-14, 32-34; Luka 21:25, 26; 2 Tim. 3:1-5; Ufu. 6:2-8)a Hii maana yake ni kwamba wale wote wasio watumishi wa Yehova Mungu kama wanafunzi waliojitoa wa Mwanawe wamo katika hatari ya kupoteza maisha zao.

15. Ni kwa njia gani ambavyo hali ya watu leo inatofautiana na ile ya wale waliouawa wakati wa hukumu fulani za kimungu za hapo kwanza?

15 Kila mahali watu wana haja ya kujulishwa hatari hii. Hali yao ni tofauti na ile ya watu waliouawa wakati wa hukumu fulani za kimungu za hapo kwanza. Kwa mfano, hata kama Yehova Mungu asingaliwatumia Wababeli kufikiliza hukumu juu ya Yuda na Yerusalemu isiyoaminika mwishowe maelfu yaliyotoweka wakati huo yangalikufa tu. Kufa kwao hakukumaanisha kuharibiwa kabisa. Lakini hukumu itakayofikilizwa juu ya wale wanaokataa kumjua Mungu na kuzitii “habari njema” juu ya Yesu Kristo katika kizazi hiki ndiyo itakayokuwa ya kukata maneno. Biblia yatuambia hivi: ‘Wataadhibiwa kwa maangamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake.’ (2 The. 1:9) “Hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele.” (Mt. 25:46) Nao waokokaji wa uharibifu huo hawataendelea kuishi miaka michache tu kisha wafe. Sivyo, mbele yao wanalo tumaini la uzima wa milele, bila ya magonjwa, huzuni wala maumivu.​—Ufu. 7:14-17; 21:3-5.

16. Yehova Mungu alifanya nini kabla ya kuifikiliza hukumu yake juu ya Yuda na Yerusalemu isiyoaminika wakati wa Ezekieli?

16 Wakifikiria kilichomo hatarini, je! mashahidi wa Yehova wa Kikristo hawana sababu ya kujitahidi kama wawezavyo kuwafikia watu wakiwa na ujumbe wenye kuokoa uhai kutoka kwa Neno la Mungu? Kufanya kwao hivyo kungeonyesha heshima ifaayo kwa tamaa ya Mungu kwamba watu wote watubu na kuishi kupatana na maarifa yaliyo sahihi. Kabla Yehova Mungu hajawaruhusu Wababeli wauharibu Yerusalemu na kuiacha nchi ya Yuda ikiwa tupu aliagiza wapewe onyo. Aliifikiria miaka michache ya ziada ya maisha ambayo ingefurahiwa na wale waliolitii onyo kama kitu chenye thamani. Alitaka kuachilia wengi kama ambavyo ingaliwezekana wasipatwe na kifo kibaya sana kwa sababu ya vita au matokeo yake. Kwa hiyo alimpa nabii wake Ezekieli daraka kubwa sana, akisema hivi: “Nimekuweka kuwa mlinzi wa nyumba ya Israeli; basi, sikia neno hili litokalo katika kinywa changu, ukawape maonyo haya yatokayo kwangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; wewe usimpe maonyo, wala husemi na huyo mtu mbaya ili kumwonya, kusudi aache njia yake mbaya na kujiokoa [nafsi] yake; mtu yule mbaya atakufa katika uovu wake; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Lakini ukimwonya mtu mbaya, wala yeye hauachi ubaya wake, wala njia yake mbaya, atakufa katika uovu wake; bali wewe umejiokoa [nafsi] yako.”​—Eze. 3:17-19.

17. Agizo la Ezekieli limepaswa litusaidie tuthamini nini juu ya agizo letu la kuhubiri na kufanya wanafunzi?

17 Kwa kuwa wanadamu wamo katika hatari kubwa sana leo, je! tufikiri kwamba daraka letu kwa maisha za watu ni dogo kuliko la Ezekieli? Hata! Agizo la kuhubiri na kufanya wanafunzi lililotolewa na Yesu Kristo zaidi ya karne kumi na tisa zilizopita lilipaswa kuendelea kutumika “mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 28:19, 20, NW) Je! wewe unaliona daraka lako la kutimiza agizo hili?

18. Kwa sababu gani kusudi la Mungu la kuagiza onyo litangazwe halitashindwa kwa sababu ya kutokuaminika kwa watu mmoja mmoja?

18 Je! hii maana yake ni kwamba wewe kama mtu mmoja ukishindwa watu watatoweka milele? Sivyo, kwa maana kazi si ya mwanadamu bali ya Mungu. Yeye anafungua mioyo ya watu mmoja mmoja, nalo ni pendeleo kubwa kwetu kuwa ‘wafanya kazi pamoja naye.’ (Matendo 16:14; 1 Kor. 3:9) Ili atoe onyo, Yehova Mungu aweza kuyafanya ‘mawe yapige kelele.’ (Luka 19:40) Kwa hiyo ijapokuwa watu mmoja mmoja wanaweza wakashindwa, hakuna litakalozuia kusudi la Mungu lisitimizwe na kuwafikia watu kwa kadiri ambavyo anataka kabla ya uharibifu wa taratibu ya mambo iliyopo. Nao mashahidi wa Yehova wa Kikristo kama kundi hawatashindwa kulitangaza onyo. Upendo wao kwake na kwa wanadamu wenzao ni wenye nguvu sana kuweza kuwavuta wafanye yote wawezayo kusaidia watu waione njia ya wokovu kabla haijakuwa kuchelewa mno. Wao ni wenye nia ya kupanga mambo yao ya kipekee, hata kurekebisha hali, watimize hili. Sivyo, haitakuwa lazima mawe yapige kelele.

19. Kwa sababu gani wasioaminika hawatakuwa huru na hatia ya damu?

19 Lakini hii haitawaondoa watu mmoja mmoja wanaoshindwa kuonyesha upendo wa kweli na kupendezwa na wanadamu wenzao wasiwe na hatia ya damu. Kwa mfano, kama baba akimwachilia mtoto wake hata anaingia hatarini, yeye asingekuwa hana hatia hata mtu mwingine akimwokoa mtoto asife. Vivyo hivyo, mtu anayejidai kuwa mtumishi wa Yehova lakini anayeshindwa kutimiza wajibu wake kwa wengine asingekuwa hana hatia. Nia yake isiyo ya upendo na ya kutojali ingekuwa sawa na kuua. Asingeweza kujipa udhuru kwamba alihubiri kidogo, kwa maana Yehova Mungu angejua kadiri ya kutojali naye angefikiliza hukumu kwa sababu hiyo.​—Rum. 14:12.

20. Kwa sababu gani huu sio wakati wa kufanya utumishi wa kuonyesha tu? Toa mfano.

20 Huu sio wakati wa mtu ye yote kujaribu kusonga mbele akifanya utumishi wa kuonyesha tu au wa kujitia katika masumbufu ya maisha au mawazo ya shughuli hata asiwe na wakati wa kufikia watu. Kazi iliyo kubwa zaidi katika historia ya wanadamu ya kuokoa uhai inakaribia kikomo. Kwa hiyo, je! haifai tujinyime mambo fulani, mapendezi fulani? Je! hivyo sivyo watu wanavyofanya nyakati za msiba? Wao hawaachi wakati walio nao ndio uiongoze kazi yao ya kuokoa maisha bali wanaendelea kujitahidi wawezavyo maadamu kuna haja na wana nguvu za kutosha.

21. Ni maulizo gani yawezayo kuulizwa juu ya namna tunavyojisikia juu ya kuuhubiri Ufalme?

21 Je! hivyo ndivyo wewe unavyojisikia juu ya kazi ya lazima ya kuuhubiri Ufalme? Unapowafikia watu katika nyumba zao, je! moyo wako unakuvuta wewe uendelee kwa muda unaoweza kufanya hivyo, bila ya kuisahau haja ya pumziko na kuburudika na vile vile kutimiza wajibu mwingine wa Maandiko? Au, unatazamia kuacha na pengine kujitia katika namna fulani ya tafrija au mchezo? Je! unatumia nafasi kwa njia nzuri nyakati nyingine​—shuleni, kazini au mahali penginepo unapokuwa kila siku​—kusema na watu juu ya kweli? Je! wewe unapendezwa kweli na kupelekea watu wa jamaa na wengine unaowafahamu ujumbe wa Biblia? Je! u macho vile vile kufahamu inapofaa zaidi kuacha mwenendo mwema badala ya maneno utoe ushuhuda?

22. Ni nini yanayotiwa ndani katika kufanya wanafunzi?

22 Vile vile na ikumbukwe kwamba agizo ambalo Yesu Kristo alilitoa si shauri la kuhubiri tu au kutangaza kweli ya Mungu. Wamepaswa watu wafundishwe wawe wanafunzi wake. Je! wewe unajitahidi vya kutosha uwarudie wale wanaoonyesha kupendezwa na kujaribu kuanza funzo la nyumbani la Biblia nao? Imewapasa watu wajue, si yale tu Biblia inayoyasema, lakini vile vile namna ambavyo wanaweza kuishi kupatana nayo. Kwa kuwa mtume Paulo alikuwa amefanya yote aliyoweza kufundisha kweli, angeweza kusema hivi: “Mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu.” (Matendo 20:26, 27) Je! wewe unahakikisha kama Paulo kwamba kufundisha kwako hakuna makosa katika mambo yaliyo ya maana sana na kwamba wale unaowafundisha wanayaelewa kabisa matakwa ya Mungu? Bila shaka tusingetaka tushiriki makosa ya mtu kwa kuficha habari anazopaswa kuzijua.

23. Ukitumia 2 Wakorintho 3:2, 3, onyesha nia ambayo imempasa mtu awe nayo kwa wale wanaofundishwa na kwa matokeo mema ya kufundisha kunakofaa.

23 Vile vile, kupendezwa kwingi na wale tunaowafundisha na kuwapenda ni kwa maana. Mtume Paulo aliwaandikia Wakorintho juu yake mwenyewe na juu ya wafanya kazi wenzake hivi: “Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa [roho ya] Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama.” (2 Kor. 3:2, 3) Tunapokuwa na upendo mwingi sana na kupendezwa na wale tunaowafundisha, wale wanaofundishwa watakuwa kama “barua” zilizoandikwa mioyoni mwetu. Tunapoutegemea msaada wa roho ya Mungu na kufanya yote tuwezayo, watakaoitikia watakuwa kama barua za Kristo, zilizoandikwa na roho ya Mungu mioyoni. Ndiyo, matokeo ya roho ya Mungu mioyoni mwao yatawavuta waonyeshe utu wa Kikristo, ambao watazamaji wanaweza kuuona au ‘kuusoma.’ Je! Wewe unajitahidi kutokeza “barua” hizo kama ‘mfanya kazi pamoja’ na Mungu?

24. Kufikiri kwa uzito juu ya utendaji wetu kama watumishi wa Yehova kwaweza kuwa na matokeo gani kwetu?

24 Unapoufikiria utendaji wako kama mtumishi wa Yehova Mungu, bila shaka waweza kukumbuka mambo mengi ya kufurahisha. Kweli, huenda ukasema kama ingaliwezekana ungalifanya zaidi na huenda ukaona sehemu ambazo waweza kuziendeleza. Hata waweza kuchukizwa nyakati nyingi kwa sababu huwezi kabisa kuonyesha “barua” zo zote zilizo hai. Lakini ikiwa wewe umejitahidi kulitimiza agizo la Kikristo kuhubiri na kufundisha, waweza kuendelea kuwa na uhakika wa kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo wanapendezwa na utumishi wako wa kujitoa. Ni jambo la kawaida kuyaona madaraka yetu wazi zaidi sasa kuliko wakati tulipokuwa “watoto wachanga” wa kiroho. Ni vema. Ikiwa, kwa upande mwingine, wengine kati yetu wamekuwa wachoyo kidogo, imewapasa wafikiri kwa uzito juu ya kukunjuka kabisa katika kuonyesha fadhili, ukarimu na upendo kwa wanadamu wenzetu. Ee, siku ya kisasi cha kimungu na itukute tukiwa wenye kustahili ulinzi kwa maana tumetenda kupatana na upendo ambao Yehova Mungu na Yesu Kristo wanao kwa wanadamu!

​—Kutoka The Watchtower, Feb. 15, 1974.

[Maelezo ya Chini]

a Ili upate habari zaidi zenye kuhakikisha kipindi cha kuanzia mwaka wa 1914 C.E. na kuendelea kama “Siku za mwisho” za hii taratibu, tazama kitabu True Peace and Security​—From What Source?, kurasa 73-89.

[Picha katika ukurasa wa 377]

Kama vile Ezekieli alivyotoa onyo la Mungu kabla ya uharibifu wa Yerusalemu, ndivyo na wanafunzi wa Yesu walivyo na daraka la kuwaonya watu juu ya hatari kubwa zaidi iliyoko mbele ya wanadamu leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki