Je! Twahitaji Biblia?
OKSANA, mwanamke mmoja mchanga kutoka Urusi, alifurahi sana alipoona Biblia ikitolewa na mwuza-vitabu mmoja wa barabarani katika Moskow. Mwandamani wake, John, aliyetoka nchi ambako Biblia zilipatikana kwa urahisi, alivutiwa na idili ya Oksana. “Mimi [John]—nikiwa mmoja asiyeamini kuwako kwa Mungu—nilitaka kumnunulia [Biblia hiyo],” yeye akiri. Ingawa Oksana alikataa mwanzoni, hatimaye alikubali zawadi hiyo ya John.
Kama vile Oksana, wengi wanatamani sana kuwa na Biblia. Ndivyo ilivyo hasa katika nchi ambako imezuiliwa kwa miaka mingi. Kwa kielelezo, watangazaji wa gazeti hili, wanajitahidi kuendelea kuutosheleza ule uhitaji mkubwa wa Biblia katika zile jamhuri zilizokuwa za Sovieti, na pia katika sehemu nyinginezo za ulimwengu. Kwa mara ya kwanza, watu wengi katika maeneo hayo wana nafasi ya kuichunguza Biblia ifaavyo—na wengi wanavutiwa na ujumbe wayo wenye nguvu.
Wahakiki na Wenye Kutilia Shaka
Kinyume cha hilo, hasa katika Ulaya Kaskazini, Biblia imeachwa kwenye rafu kukusanya vumbi tu. Wengine husema kwamba ni “Historia iliyokufa!” wakiongeza, “Iliandikiwa enzi nyingineyo. Haimhusu mwanadamu wa kisasa hata kidogo.” Hata makasisi mashuhuri wametoa taarifa hadharani zinazoiondolea Biblia sifa. Askofu mkuu Mwanglikana Desmond Tutu aripotiwa katika The Star, gazeti la habari la Afrika Kusini, akiwa amesema hivi: “Kuna sehemu za Biblia ambazo hazina thamani ya kudumu.” Taarifa hizo zimewasababisha wengi watake kujua wanapaswa kuiamini Biblia kwa kadiri gani hasa.
Uhitaji wa Mwongozo
Ni lazima wahakiki na waamini vilevile wakubali kwamba, ulimwengu unahitaji masuluhisho yafanyayo kazi, zaidi ya wakati mwingine wowote. “Mwanadamu asipojifunza haraka namna ya kudhibiti kadiri badiliko linavyotokea katika shughuli zake binafsi pamoja na zile za jamii yote ya watu,” akaandika Alvin Tofller katika kitabu chake Future Shock, “tutapatwa na maangamizo . . . makuu.” Onyo hilo lilitolewa miaka zaidi ya 20 iliyopita. Maangamizo ambayo Tofllar alisema juu yayo yaonekana kuwa yakitukia wakati uu huu.
Karne hii ikaribiapo mwisho wayo, maendeleo ya kitekinolojia na falsafa za kibinadamu zimeshindwa kutokeza uthabiti wa ulimwengu. Mahali pa matumaini ya hivi karibuni ya ule utaratibu wa ulimwengu mpya pamechukuliwa na hali ya kufadhaika, na maisha ya wengi yameshushwa hali kuwa shindano la kila siku la kubaki hai.
Takwimu huonyesha kwamba tofauti ya kiuchumi iliyo kati ya matajiri na maskini imekuwa shimo kubwa mno. Uchunguzi wa hivi karibuni waonyesha kwamba asilimia 82.7 ya utajiri wa ulimwengu ni mali ya asilimia 20 tu ya wakaaji wao. Je! ni ajabu kwamba vita, njaa kuu, magonjwa, ghasia, na michafuko vimo kwa wingi katika nchi nyingi? Mbano wa kukabiliana na hali ya maisha inayozidi kuwa mbaya unasababisha mkazo mkubwa juu ya hisiamoyo za watu. Likiwa tokeo, hata ile sehemu ya msingi kabisa ya jamii, yaani familia, inaharibika.
Ingawa wengi, kama vile Tofller, hudokeza kwamba ni daraka la mwanadamu “kujitahidi kutafuta njia mpya kabisa za kupata uthabiti na usalama,” uthitibisho waonyesha kwamba wanadamu hawana uwezo wa kujiandalia masuluhisho yao wenyewe.
Njia Iliyo ya Pekee
Biblia Takatifu, ambayo ilianza kuandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita, haikubadilika muda wa karne ambazo zimepita. Kanuni zayo hazibadiliki. Kwa kielelezo, maneno ya Yeremia 10:23 yameonyeshwa kuwa ya kweli leo zaidi ya wakati mwingine wowote kabla ya hapo: “Ee BWANA [Yehova, NW], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Ikiwa wanadamu hawawezi kuelekeza mwendo wao, ni nani awezaye? Biblia huonyesha Chanzo pekee cha kweli cha mwelekezo: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—Isaya 48:17.
Kupitia kurasa za Biblia, Yehova Mungu hutufundisha tujisaidie wenyewe. Zimejaa shauri linalotuonyesha njia tupaswayo kutembea. Shauri layo lafaa leo kama lilivyofaa siku liliyoandikwa. Makala ifuatayo itachunguza jinsi Biblia inavyofaa enzi yetu ya kisasa. Katika habari mbalimbali, kutoka afya hadi utajiri, maisha ya familia, na mwenendo wa kibinafsi, utaweza kuona kwamba Biblia kwa kweli ni mwamba wa uthabiti katika udongo wa ulimwengu wa leo usio thabiti.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Biblia ni nanga ya uthabiti katika ulimwengu wa leo wenye msukosuko