Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 10/15 kur. 4-7
  • Taabu ya Familia —Ishara ya Nyakati

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Taabu ya Familia —Ishara ya Nyakati
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pesa na Kazi
  • Vifungo vya Ndoa Vilivyodhoofika
  • Vijana Washambuliwa
  • Mizizi ya Taabu ya Familia
  • Familia Zinazositawi
  • Je, Kuna Siri ya Kupata Furaha ya Familia?
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Fuatia Amani ya Kimungu Katika Maisha ya Familia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Maisha ya Jamaa—Namna Unavyoweza Kufanikiwa
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Pata Wakati Ujao Wenye Kudumu Kwa Ajili Ya Familia Yako
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 10/15 kur. 4-7

Taabu ya Familia—Ishara ya Nyakati

TAABU ya familia—wengi huiona kuwa ishara ya kwamba kanuni za kimapokeo za ndoa na uzazi zimeacha kutumiwa siku hizi. Wengineo huiona kuwa tokeo la badiliko la kisiasa, kiuchumi, na kijamii. Wengine bado huiona kuwa hasara moja zaidi tu ya tekinolojia ya ki-siku-hizi. Kwa kweli yale matatizo ambayo familia hung’ang’ana nayo leo huelekezea jambo fulani lenye umaana mwingi zaidi. Ona maneno ya Biblia kwenye 2 Timotheo 3:1-4:

“Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.”

Je! maneno hayo hayaonyeshi chanzo hasa cha matatizo ya leo? Taabu ya familia ya leo kwa wazi ni tokeo la moja kwa moja la hali zilizotolewa unabii kwamba zingetukia wakati wa siku za mwisho wa ulimwengu huu. Na kuna uthibitisho wenye kusadikisha kwamba kipindi hiki cha taabu kilianza katika mwaka wa 1914.a Tangu wakati huo, uvutano wa yule kiumbe-roho mwenye uwezo upitao wa kibinadamu aitwaye Shetani Ibilisi umekuwa hasa wenye kudhuru.—Mathayo 4:8-10; 1 Yohana 5:19.

Akiwa amezuiwa katika ujirani wa dunia tangu 1914, Shetani ni “mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:7-12) Kwa kuwa Shetani ni adui thabiti wa Mungu “aliye asili ya jamaa [familia, New World Translation] zote duniani na mbinguni,” je, yashangaza kwamba dunia imekuwa mahali penye hatari kwa familia? (Waefeso 3:15, Habari Njema kwa Watu Wote) Shetani amekusudia kuigeuza ainabinadamu yote kutoka kwa Mungu. Angeweza kutimiza hilo katika njia gani bora kuliko kutumia matatizo ili kuzishambulia familia?

Mengi zaidi yanahitajiwa kuliko nadharia zenye ufasaha za wale waonwao kuwa wastadi ili kuzilinda familia kutokana na shambulio hilo lipitao uwezo wa kibinadamu. Hata hivyo, Biblia husema hivi juu ya Shetani: “Hatukosi kuzijua fikira [mbinu, NW] zake.” (2 Wakorintho 2:11) Kuna kadiri fulani ya ulinzi katika kuzijua baadhi ya njia hususa ambazo katika hizo yeye hufanya shambulio lake.

Pesa na Kazi

Mbano wa kiuchumi ni mmojawapo wa silaha za Shetani za kushambulia zenye nguvu. Hizi ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” NW, au kama vile Revised Standard Version hufasiri 2 Timotheo 3:1, “nyakati za mkazo.” Katika nchi zinazositawi, matatizo kama vile ukosefu wa kazi za kuajiriwa, mishahara ya chini, na upungufu wa mahitaji ya msingi husababishia familia magumu mengi. Hata hivyo, hata katika United States iliyo nchi yenye utajiri kwa kulinganisha, mibano ya kiuchumi ina matokeo mazito. Uchunguzi mmoja katika U.S. ulionyesha kwamba pesa ni kimojawapo visababishi vya mapambano ya familia. Kitabu Secrets of Strong Families hueleza kwamba “wakati, uangalifu, [na] nishati” vinavyotolewa ili kuyatimiza mahitaji ya kazi ya kilimwengu yaweza pia kuwa “adui mwenye hila” anayebomoa kifungo cha ndoa.

Hali zimelazimisha idadi kubwa za wanawake watafute kazi za kuajiriwa. Mwandikaji Vance Packard aripoti hivi: “Kwa sasa, angalau robo ya vitoto vichanga na watoto wanaoanza kutembea wa Amerika wenye umri ya miaka mitatu wana akina mama wenye kazi fulani ya kuajiriwa.” Kutosheleza mahitaji ya watoto wadogo ambayo karibu hayawezi kutoshelezwa pamoja na kufanya kazi ya kuajiriwa kwaweza kuwa jitihada ngumu, yenye kuchosha—kukiwa na matokeo yasiyofaa kwa wazazi na watoto pia. Packard aongeza kwamba kwa sababu ya upungufu wa maandalizi ya kutosha ya kuwatunza watoto katika United States, “mamilioni kadha ya watoto leo wanakosa kupewa utunzaji mzuri wa kutosha katika miaka yao ya mapema.”—Our Endangered Children.

Mahali pa kazi penyewe mara nyingi hudhoofisha upatano wa familia. Wafanya kazi wengi huvutwa kuwa na mahusiano ya kingono pamoja na wafanya kazi wenzao. Wengine bado huanza kuhusika katika ufuatiaji wa ufanisi na hudhabihu maisha yao ya familia ili kufanya maendeleo katika kazi-maisha yao. (Linganisha Mhubiri 4:4.) Mwanamume mmoja alijihusisha sana katika kazi yake akiwa mwakilishi wa uuzaji hivi kwamba mke wake alijieleza mwenyewe kuwa “kana kwamba ni mzazi aliye peke yake.”

Vifungo vya Ndoa Vilivyodhoofika

Mpango wa ndoa wenyewe umeshambuliwa pia. Chasema kitabu The Intimate Enviroment: “Katika wakati uliopita, tazamio lilikuwa kwamba wenzi wa ndoa wangekaa wakiwa wamefunga ndoa mpaka mwenzi mmoja alipofanya kosa zito dhidi ya ndoa—uzinzi, ukatili, kutojali kwa kupita kiasi. Sasa watu wengi huona kusudi la ndoa kuwa utimizo wa kibinafsi.” Naam, ndoa huonwa kuwa dawa ya kuponya ukosefu wa furaha, uchovu, au upweke—si kuwa kifungo pamoja na mtu mwingine chenye kudumu muda wote wa maisha. Jambo linalokaziwa sasa ni faida unayopata katika ndoa, si lile unaloichangia ndoa. (Tofautisha na Matendo 20:35.) “Badiliko hilo kuu katika thamani za ndoa” limedhoofisha sana vifungo vya ndoa. Wasipoweza kupata utimizo wa kibinafsi, wenzi wa ndoa mara nyingi huamua kutaliki kuwa suluhisho la haraka.

Watu katika “siku [hizi] za mwisho” hutajwa kiunabii katika Biblia kuwa “wenye namna ya ujitoaji kimungu lakini wakithibitika kuwa bandia kwa nguvu za huo.” (2 Timotheo 3:4, 5, NW) Wastadi wengi huhisi kwamba mzoroto wa dini umekuwa na sehemu fulani katika kudhoofisha ndoa. Katika kitabu chake The Case Against Divorce, Dakt. Diane Medved aliandika hivi: “Kulingana na dini nyingi, Mungu alisema kwamba ndoa ilipaswa kuwa ya kudumu. Usipokuwa na uhakika juu ya Mungu au usipomwamini Yeye, basi unafanya utakavyo.” Tokeo ni kwamba, ndoa inapokuwa na matatizo, wenzi wa ndoa hawajaribu kutafuta masuluhisho yafaayo. “Wao huikomesha ndoa.”

Vijana Washambuliwa

Watoto wanashambuliwa na mibano ya leo. Idadi kubwa mno ya watoto hupigwa kijeuri na kutendewa vibaya na wazazi wao kwa maneno au kingono. Kupitia talaka, mamilioni zaidi hunyimwa ule uvutano wenye upendo wa wazazi wawili, na maumivu ya talaka ya wazazi mara nyingi hudumu kwa muda wa maisha yote.

Vijana hukumbwa na mivutano yenye nguvu. Kijana Mwamerika wa wastani anapofikia umri wa miaka 14, anakuwa ameshuhudia mauaji 18,000 na namna nyinginezo nyingi za jeuri, ngono haramu, kuharibu mali ya watu kimakusudi, na uhalifu kwa kutazama televisheni tu. Muziki pia huwa na uvutano wenye nguvu juu ya vijana, na muziki mwingi hukosa adabu kwa njia ya kushtua, ukitaja ngono waziwazi, au hata una mambo ya kishetani. Shule hufundisha watoto nadharia kama vile mageuzi zinazoelekea kudhoofisha imani katika Mungu na Biblia. Mbano wa marika huwachochea wengi washiriki katika ngono ya kabla ya ndoa na utumizi mbaya wa vileo au dawa za kulevya.

Mizizi ya Taabu ya Familia

Kwa hiyo shambulio dhidi ya familia linatia ndani mambo mengi na laweza kusababisha uharibifu mwingi. Ni nini kiwezacho kusaidia familia ziokoke? Mshauri wa familia John Bradshaw adokeza hivi: “Kanuni zetu za uzazi hazijafanyiwa maendeleo kwa uzito katika miaka 150. . . . Ninaamini kwamba zile kanuni za zamani hazifanyi kazi tena.” Hata hivyo, suluhisho si kanuni nyingine zenye kufanyizwa na wanadamu. Yehova Mungu ndiye Mwanzilishi wa familia. Yeye ajua bora zaidi ya mtu mwingine yeyote umaana wa maisha ya familia katika furaha yetu ya kibinafsi na kile kinachohitajiwa ili kufanya familia iwe na furaha na yenye nguvu. Je! itushangaze kwamba Neno lake, Biblia huandaa suluhisho la taabu ya familia?

Biblia hueleza jinsi maisha ya familia yalivyopata kuharibika. Wenzi wa ndoa wa kwanza wa kibinadamu, Adamu na Hawa, waliwekwa katika mazingira ya bustani yenye kupendeza na kupewa daraka lenye kuthawabisha la kuigeuza dunia iwe paradiso ya tufeni pote. Mungu aliamuru kwamba Adamu awe kichwa cha familia. Hawa alihitaji kushirikiana na ukichwa wake akiwa “msaidizi,” au “kikamilisho.” Lakini Hawa aliasi mpango huo. Alijitwalia ukichwa wa mume wake na kutotii lile katazo moja la pekee ambalo Mungu alikuwa amewawekea. Adamu alijiuzulu ukichwa wake akaungana na mke wake katika uasi huo.—Mwanzo 1:26–3:6, NW.

Matokeo yenye uharibifu ya kugeuka huko kutoka mpango wa Mungu yalianza kuonekana mara hiyo. Wakiwa si safi wala bila hatia tena, Adamu na Hawa waliitikia wakiwa na haya na kujihisi wenye hatia. Adamu, ambaye mapema zaidi alikuwa amemtaja mke wake katika maneno ya kishairi yenye upendezi, sasa alimtaja kwa ubaridi kuwa ‘huyo mwanamke uliyenipa.’ Maneno hayo hasi yalikuwa ni mwanzo tu wa huzuni ya ndoa. Jitihada za Adamu za bure za kupata ukichwa wake tena zingetokeza katika yeye ‘kumtawala’ Hawa. Hawa, naye, angekuwa na “tamaa” kwa mume wake, yaelekea katika njia ya kupita kiasi au isiyosawazika.—Mwanzo 2:23; 3:7-16.

Haishangazi kwamba, ugomvi wa ndoa wa Adamu na Hawa ulikuwa na matokeo yenye kudhuru wazao wao. Mwana wao wa kwanza, Kaini, alikuwa mwuaji asiye na huruma. (Mwanzo 4:8) Lameki, mzao wa Kaini, aliongezea poromoko hilo la maisha ya familia kwa kuwa wa kwanza kurekodiwa katika kufunga ndoa ya wake zaidi ya mmoja. (Mwanzo 4:19) Hivyo Adamu na Hawa hawakupitisha tu urithi wa dhambi na kifo bali pia kigezo kibaya cha familia ambacho kimekuwa ndiyo hali ya jamii ya kibinadamu tangu wakati huo. Katika siku hizi za mwisho, ugomvi wa familia umefikia upeo usiofikiwa wakati mwingine wowote.

Familia Zinazositawi

Hata hivyo, si familia zote zinazoharibiwa na mibano ya leo. Kwa mfano, mume mmoja huishi pamoja na mke wake na binti zake wawili katika jumuiya ndogo katika United States. Ingawa majirani wao wengi wana tatizo la uwasiliano kati ya wazazi na wazao wao, yeye na mke wake hawana, wala hawahangaiki kwamba huenda binti zao wakajaribu dawa za kulevya au ngono. Jumatatu jioni, wakati vijana wengine wamekodolea macho yao televisheni, familia yao nzima huwa imekusanyika kuzunguka meza ya kulia chakula kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia. “Jumatatu usiku ni usiku wetu wa pekee kuwa pamoja na kuongea,” yeye aeleza. “Binti zetu huhisi huru kuongea na sisi waziwazi juu ya matatizo yao.”

Kwa upande mwingine, kuna mzazi aliye peke yake katika Jiji la New York ambaye pia hufurahia upatano wa familia usio wa kawaida pamoja na binti zake wawili. Siri yake ni nini? “Sisi hatufungui televisheni mpaka mwisho-juma,” yeye aeleza. “Tuna mazumgumzo ya kila siku ya andiko moja la Biblia. Pia tunaweka kando jioni moja kwa ajili ya mazungumzo ya Biblia ya familia.”

Familia zote mbili ni za Mashahidi wa Yehova. Zinafuata shauri kwa familia lililomo katika Biblia—na hilo hufanya kazi. Hata hivyo, si familia hizo pekee zinazofanya hivyo. Kuna mamia ya maelfu ya familia zilizo kama hizo zinazopata matokeo mazuri kwa kutumia kanuni za maisha ya familia zinazopatikana katika Kitabu hicho.b Kanuni hizo ni zipi hasa? Zinaweza kufaidije wewe na familia yako? Kwa kujibu tunakualika uchunguze makala zinazoanza kwenye ukurasa ufuatao.

[Maelezo ya Chini]

a Kupata uthibitisho wa zaidi kwamba siku za mwisho zilianza katika 1914, ona sura 18 ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society ya New York, Inc.

b Kupitia funzo la Biblia nyumbani bila malipo, Mashahidi wa Yehova hutoa msaada wa kibinafsi katika kutumia kanuni za Biblia katika familia. Unaweza kuwapata kwa kuandikia watangazaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Hali mbaya ya uchumi husababisha taabu nyingi kwa familia katika nchi zinazositawi

[Hisani]

U.S. Navy photo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kwa kutumia kanuni za Biblia, familia nyingi zinakinza mibano ya leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki