Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 5/8 kur. 22-23
  • Kujiua—Kuna Ufufuo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujiua—Kuna Ufufuo?
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wanatheolojia Wapinga Tumaini la Ufufuo
  • Asiye Haki Kufufuliwa
  • Nafasi Yenye Rehema
  • Maoni ya Kufaa, ya Kimaandiko Juu ya Uhai
  • Kujiua—Pigo la Vijana
    Amkeni!—1998
  • Tatizo la Ulimwenguni Pote
    Amkeni!—2001
  • Kwa Nini Watu Hukata Tamaa ya Kuishi?
    Amkeni!—2001
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 5/8 kur. 22-23

Maoni ya Biblia

Kujiua—Kuna Ufufuo?

HABARI za msiba juu ya kujiua sio mwisho wa jambo katika maisha ya watu wa ukoo na rafiki; ndio mwanzo—wa jambo lenye mchanganyiko wa hisia za kujisikitikia na kasirani, huzuni na hatia. Na hutokeza swali: Je! twaweza kuwa na tumaini kwa ajili ya rafiki yetu aliyejiua?a

Ijapokuwa kifo cha kujiletea hakiwezi kutetewa kamwe, si cha haki kamwe, mtume Paulo alitoa tumaini la kupendeza sana hata kwa wengine wasio haki. Ni kama alivyoambia mahakama ya sheria ya Kirumi: “Nina tumaini kwa Mungu . . . ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 24:15.

Hata hivyo, wanatheolojia wengi wamekataa kwa muda mrefu dokezo lolote kwamba ufufuo wa wasio haki waweza kutoa tumaini kwa wale wanaojiua. Kwa nini?

Wanatheolojia Wapinga Tumaini la Ufufuo

William Tyndale alitambulisha sehemu ya tatizo hilo katika dibaji ya Biblia yake ya karne ya 16: “Kwa kutia nafsi zilizoondoka katika mbingu, moto wa mateso, au toharani unazimaliza zile hoja ambazo Kristo na Paulo wathibitishia ufufuo.” Ndiyo, karne nyingi zilizopita, wanakanisa walianzisha wazo lisilo la Kibiblia: nafsi zisizoweza kufa zinazouacha mwili wakati wa kifo na kwenda moja kwa moja mbinguni, toharani, Limbo, au kwenye moto wa mateso. Wazo hilo lilipingana na fundisho la Biblia lililo wazi la ufufuo wa wakati ujao. Ni kama mhudumu Mbaptisti Charles Andrews alivyouliza: “Ikiwa nafsi tayari ina raha mbinguni (au tayari kwa haki inachomeka katika moto wa mateso,) kuna haja gani ya jambo jingine?” Yeye aliongeza hivi: “Kupingana huku kwa kindani kumeendelea kuathiri Wakristo katika karne zote.”

Tokeo moja la theolojia hiyo yenye kosa lilikuwa kwamba “tangu wakati wa Augustino [354-430 W.K.], kanisa limelaani kujiua kuwa ni dhambi,” asema Arthur Droge katika Bible Review, Desemba 1989, “dhambi isiyoweza kukomboleka, kama vile kuasi imani na uzinzi.”

Ile hukumu kali ya ‘kutoweza kukomboleka,’ au kwenda kwenye moto wa mateso bila tumaini, ilifikisha hoja ya kuwa hukumu hutolewa wakati wa kifo kwenye upeo wayo usio na uthibitisho. Lakubali hivi National Catholic Reporter: “Wawili wa madaktari wakubwa zaidi wa kanisa walilaani kujiua—Augustino akakuita ‘uovu wenye kuchukiza na wa kulaaniwa’ na Aquinas akionyesha kulikuwa dhambi [isiyosameheka] ya kufisha iliyotendwa Mungu na jumuiya—lakini si wanakanisa wote wamekubali.”

Kwa furaha, sisi twaweza kuepuka “kupingana huku kwa kindani” kwa kukubali kweli mbili za Biblia zinazopatana. Kwanza, “nafsi inayofanya zambi itakufa.” (Ezekieli 18:4, ZSB) Pili, tumaini halisi kwa nafsi zilizokufa (watu) ni kuishi tena kupitia “ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Basi, kwa kufaa tutazamie nini kwa watu wanaojiua?

Asiye Haki Kufufuliwa

Yesu alimwambia mhalifu mmoja aliyehukumiwa kifo hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” Mwanamume huyo hakuwa mwenye haki—alikuwa mvunja sheria wala si mtu aliyejiua kwa kuvurugika akili. (Luka 23:39-43, ZSB) Yeye hakuwa na tumaini la kwenda mbinguni akatawale pamoja na Yesu. Kwa hiyo Paradiso ambayo mwizi huyo angeweza kutumaini arudie uhai ingekuwa dunia yenye kupendeza chini ya utawala wa Ufalme wa Yehova Mungu.—Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:1-4.

Mungu atamfufua mhalifu huyo kwa kusudi gani? Ili Yeye aweze kumhesabia bila huruma dhambi zake za wakati uliopita? Hata-a, kwa maana Warumi 6:7, 23 yasema: “Yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi,” na “mshahara wa dhambi ni mauti.” Ijapokuwa dhambi zake za wakati uliopita hazitahesabiwa kwake, bado yeye atahitaji ukombozi ili umwinue kufikia ukamilifu.

Kwa hiyo, mwanatheolojia Albert Barnes alikosea na kupotosha alipodai hivi: “Wale ambao wamefanya uovu watafufuliwa wahukumiwe, au kulaaniwa. Hilo litakuwa kusudi la kuwafufua; hilo ndilo lengo pekee.” Lo! jinsi hilo lilivyo jambo lisilomstahili Mungu wa haki na upendo! Badala yake, ufufuo kwenye uhai juu ya dunia paradiso utampa huyo aliyekuwa mhalifu (na wengine wasio haki) nafasi bora ya kuhukumiwa kwa yale watakayofanya baada ya ufufuo wao.—1 Yohana 4:8-10.

Nafasi Yenye Rehema

Kwa hiyo, rafiki waliopigwa bumbuazi wa mtu aliyejiua waweza kufarijika kujua kwamba ‘Yehova awahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.’ (Zaburi 103:10-14) Ni Mungu pekee anayeweza kuelewa kuhusika kwa ugonjwa wa akili, mkazo mkali sana, hata kasoro za jeni (chembe za tabia), katika “msiba wa kujiua,” ambao, National Observer lilionelea, “si tabia ya maishani mwote [bali] mara nyingi ni jambo la dakika chache au saa chache.”—Ona Mhubiri 7:7.

Ni kweli, mtu anayejiua hujinyima mwenyewe nafasi ya kutubu kujiua. Lakini ni nani anayeweza kusema kama mtu aliyechochewa ajiue angaliweza kubadilika moyo kama jaribio hilo lililotokeza kifo lingeshindwa? Kwa kweli, wauaji fulani wabaya wamebadilika na kupata msamaha wa Mungu wakati wa maisha yao.—2 Wafalme 21:16; 2 Mambo ya Nyakati 33:12, 13.

Kwa hivyo, kwa kuwa Yehova alilipa “fidia ya wengi,” ana haki ya kupanua rehema yake, hata kwa baadhi ya wenye kujiua, kwa kuwafufua na kuwapa nafasi yenye thamani ya ‘kutubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao.’—Mathayo 20:28; Matendo 26:20.

Maoni ya Kufaa, ya Kimaandiko Juu ya Uhai

Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu, wala si kitu cha kutumiwa vibaya au mtu kujikomeshea. (Yakobo 1:17) Kwa hiyo, Maandiko yatutia moyo tujione, si kama nafsi zisizoweza kufa, bali kama viumbe vyenye thamani vya Mungu yule atupendaye, ambaye huhazini kuwa kwetu hai, na ambaye hutazamia kwa shangwe wakati wa ufufuo.—Ayubu 14:14, 15.

Upendo huimarisha utambuzi wetu kwamba kujiua—mtu ajapoepuka mizigo yake mwenyewe—huongezea matatizo zaidi tu wapendwa wanaoachwa. Kwa habari ya yule aliyejiua kwa kukosa uamuzi mzuri, sisi binadamu hatuwezi kuhukumu kama atafufuliwa au la. Yeye alikuwa wa kulaumika kadiri gani? Mungu peke yake ndiye ‘hutafuta-tafuta mioyo yote, na mawazo yote ya fikira.’ (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Lakini twaweza kuwa na hakika kwamba ‘Mhukumu wa ulimwengu wote atatenda lililo la upendo, haki, na la kufaa!’—Mwanzo 18:25.

[Maelezo ya Chini]

a Makala hii imekusudiwa kwa ajili ya walioachwa na wale waliojiua. Kwa ajili ya mazungumzo kamili zaidi ya habari ya kujiua, ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Agosti 1, 1983, kurasa 3-11 na Amkeni! (Kiingereza), Agosti 8, 1981, kurasa 5-12.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]

Kollektie Rijksmuseum Kröller-Müller, Otterlo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki