Sura 3
Mungu wa Kweli Ni Nani?
1. Sababu gani wengi hukubaliana na maneno ya ufunguzi ya Biblia?
UTAZAMAPO angani katika usiku usio na mawingu, je, wewe hustaajabu kuona nyota nyingi sana? Unaelezaje kuwako kwazo? Na namna gani vile viumbe vyenye uhai vilivyo duniani—maua yenye rangi, ndege wenye nyimbo zao za kupendeza, nyangumi wenye nguvu wanaoruka baharini? Orodha ni ndefu. Vyote hivi visingaliweza kutokea kwa bahati-nasibu tu. Si ajabu kwamba watu wengi hukubaliana na maneno ya ufunguzi ya Biblia: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi [“dunia,” NW]”!—Mwanzo 1:1.
2. Biblia husema nini juu ya Mungu, nayo hututia moyo tufanye nini?
2 Wanadamu wamegawanyika sana juu ya swali kumhusu Mungu. Wengine hufikiri kwamba Mungu ni kani isiyo na utu. Mamilioni huabudu wazazi wa kale waliokufa, wakiamini kwamba Mungu yu mbali sana asiweze kufikiwa. Lakini Biblia hufunua kwamba Mungu wa kweli ni mtu halisi ambaye huonyesha upendezi mchangamfu kwetu tukiwa watu mmoja-mmoja. Ndiyo sababu inatutia moyo ‘tumtafute Mungu,’ ikisema: “Hawi mbali na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.
3. Sababu gani haiwezekani kufanya sanamu ya Mungu?
3 Mungu anaonekanaje? Wachache kati ya watumishi wake wameona maono ya kuwapo kwake kwa utukufu. Katika nyakati hizo yeye amejifananisha akiwa ameketi juu ya kiti cha ufalme, huku mwangaza wenye kutisha ukitanda kutoka kwake. Hata hivyo, wale walioona maono hayo hawakueleza kamwe juu ya uso dhahiri. (Danieli 7:9, 10; Ufunuo 4:2, 3) Hiyo ni kwa sababu “Mungu ni Roho”; yeye hana mwili wenye nyama. (Yohana 4:24) Kwa kweli, haiwezekani hata kidogo kufanyiza sanamu inayofanana kabisa na Muumba wetu, kwani “hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote.” (Yohana 1:18; Kutoka 33:20) Hata hivyo, Biblia hutufundisha mengi juu ya Mungu.
MUNGU WA KWELI ANA JINA
4. Ni nini baadhi ya majina ya cheo yenye kujaa maana yanayotumiwa kumhusu Mungu katika Biblia?
4 Katika Biblia, Mungu wa kweli hutambulishwa na misemo kama vile “Mungu Mweza Yote,” “Aliye Juu Zaidi,” “Muumba Mtukufu,” “Mfunzi Mtukufu,” “Bwana Mwenye Enzi Kuu,” na “Mfalme wa umilele.” (Mwanzo 17:1, NW; Zaburi 50:14, NW; Mhubiri 12:1, NW; Isaya 30:20, NW; Matendo 4:24, NW; 1 Timotheo 1:17, NW) Kutafakari juu ya majina hayo ya cheo kwaweza kutusaidia tukue katika ujuzi juu ya Mungu.
5. Jina la Mungu ni nini, nalo huonekana mara nyingi kadiri gani katika Maandiko ya Kiebrania?
5 Hata hivyo, Mungu ana jina lisilo na kifani ambalo huonekana karibu mara 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania pekee—mara nyingi zaidi kuliko lolote kati ya majina yake ya cheo. Miaka 1,900 hivi iliyopita, Wayahudi waliacha kulitamka jina la kimungu kwa sababu za kishirikina. Kiebrania cha Biblia kiliandikwa bila vokali. Kwa hiyo, hakuna njia yoyote ya kuwa sahihi juu ya jinsi Musa, Daudi, au wengine wa nyakati za kale walivyotamka zile konsonanti nne (יהוה) zifanyizazo jina la kimungu. Wasomi fulani hudokeza kwamba huenda ikawa jina la Mungu lilitamkwa “Yahweh,” lakini hawawezi kuwa na hakika. Tamko la Kiswahili “Yehova” limetumiwa kwa karne nyingi, na jina lililo sawa na hili katika lugha nyingi linakubaliwa na wengi leo.—Ona Kutoka 6:3 na Isaya 26:4 katika Union Version ya Kiswahili.
SABABU KWA NINI ULITUMIE JINA LA MUNGU
6. Zaburi 83:18 husema nini juu ya Yehova, na sababu gani tulitumie jina lake?
6 Jina la Mungu lisilo na kifani, Yehova, humtofautisha na miungu mingine. Hiyo ndiyo sababu jina hilo huonekana mara nyingi sana katika Biblia, hasa katika maandishi yayo ya Kiebrania. Watafsiri wengi hukosa kulitumia jina la kimungu, lakini Zaburi 83:18 husema hivi kwa wazi: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Kwa hiyo yafaa kwetu kulitumia jina la kibinafsi la Mungu tunapoongea juu yake.
7. Maana ya jina Yehova hutufundisha nini juu ya Mungu?
7 Jina Yehova ni namna ya kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha ‘kuwa.’ Hivyo, jina la Mungu lamaanisha “Yeye Husababisha Kuwe.” Kwa njia hiyo Yehova Mungu hujitambulisha kuwa Mkusudiaji Mkubwa. Sikuzote yeye husababisha makusudi yake yawe uhalisi. Ni Mungu wa kweli pekee awezaye kuwa na jina hilo kwa haki, kwani wanadamu hawawezi kamwe kuwa na hakika kwamba mipango yao itafanikiwa. (Yakobo 4:13, 14) Yehova pekee ndiye aweza kusema: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu . . . litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.
8. Yehova alitangaza kusudi jipi kupitia Musa?
8 Kila mmoja wa wale wazee wa ukoo Waebrania Abrahamu, Isaka, na Yakobo ‘waliliitia jina la Yehova,’ lakini hawakujua umaana kamili wa jina hilo la kimungu. (Mwanzo 21:33; 26:25; 32:9; Kutoka 6:3) Baadaye Yehova alipofunua kusudi lake la kukomboa wazao wao, Waisraeli, kutoka utumwani katika Misri na kuwapa “nchi ijaayo maziwa na asali,” huenda hilo lilionekana kuwa jambo lisilowezekana. (Kutoka 3:17) Hata hivyo, Mungu alikazia umaana udumuo milele wa jina lake kwa kumwambia nabii wake Musa hivi: “Waambie wana wa Israeli maneno haya, BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.”—Kutoka 3:15.
9. Farao alimwonaje Yehova?
9 Musa alimwomba Farao, mfalme wa Misri, awaruhusu Waisraeli waende kumwabudu Yehova jangwani. Lakini Farao, ambaye mwenyewe alionwa kuwa mungu na ambaye aliabudu miungu mingine ya Kimisri, akajibu hivi: “BWANA [“Yehova,” NW] ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui BWANA [“Yehova,” NW], wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.”—Kutoka 5:1, 2.
10. Katika Misri ya kale, Yehova alichukua hatua gani ili kutimiza kusudi lake lililowahusu Waisraeli?
10 Kisha Yehova akachukua hatua zaidi ili kutimiza kusudi lake, akitenda kwa kupatana na maana ya jina lake. Alileta mapigo kumi juu ya Wamisri wa kale. Pigo la mwisho liliua wazaliwa wote wa kwanza wa Misri, kutia ndani mwana wa Farao mwenye kiburi. Ndipo Wamisri wakataka sana Israeli waende zao. Hata hivyo, Wamisri fulani walivutiwa sana na nguvu za Yehova hivi kwamba wakajiunga na Waisraeli katika kuondoka Misri.—Kutoka 12:35-38.
11. Yehova alifanya muujiza upi kwenye Bahari Nyekundu, na adui zake walilazimika kukiri nini?
11 Farao mshupavu pamoja na jeshi lake, lenye mamia ya magari-vita, wakafuatia kukamata tena watumwa wake. Wamisri walipokaribia, Mungu aligawanya Bahari Nyekundu kimuujiza ili Waisraeli waweze kuvuka juu ya nchi kavu. Wale wenye kufuatia walipoingia bonde kavu la bahari, Yehova “akayaondoa magurudumu ya magari yao, hata yakaenda kwa uzito.” Wanavita Wamisri wakalia: “Na tukimbie mbele ya Israeli; kwa kuwa BWANA [“Yehova,” NW] anawapigania, kinyume cha Wamisri.” Lakini ikawa kuchelewa mno. Zile kuta kubwa mno za maji ziliporomoka nazo “[zi]kafunikiza magari na wapanda farasi, hata jeshi lote la Farao.” (Kutoka 14:22-25, 28) Hivyo ndivyo Yehova alijifanyia jina kubwa, na tukio hilo halikusahauliwa hadi siku hii.—Yoshua 2:9-11.
12, 13. (a) Jina la Mungu lina maana gani kwetu leo? (b) Watu wanahitaji kujifunza nini kwa uharaka, na sababu gani?
12 Jina ambalo Mungu amejifanyia lina maana sana kwetu leo. Jina lake, Yehova, ni uthibitisho kwamba yote yale ambayo amekusudia atayasababisha yatimie. Hilo latia ndani kutimiza kusudi lake la kwanza kwamba dunia yetu iwe paradiso. (Mwanzo 1:28; 2:8) Ili kutimiza hilo, Mungu ataangamiza wapinzani wote wa enzi kuu yake leo, kwani yeye amesema hivi: “Watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Ezekieli 38:23, NW) Ndipo Mungu atatimiza ahadi yake ya kuwakomboa waabudu wake ili waingie ndani ya ulimwengu mpya wa uadilifu.—2 Petro 3:13.
13 Wote wanaotaka upendeleo wa Mungu lazima wajifunze kuliitia jina lake kwa imani. Biblia huahidi hivi: “Kila atakayeliitia Jina la Bwana [“Yehova,” NW] ataokoka.” (Warumi 10:13) Ndiyo, jina Yehova limejaa maana sana. Kumwitia Yehova kuwa Mungu na Mkombozi wako kwaweza kukuongoza kwenye furaha isiyo na mwisho.
SIFA ZA MUNGU WA KWELI
14. Biblia hukazia sifa zipi za msingi za Mungu?
14 Funzo juu ya kukombolewa kwa Israeli kutoka Misri lakazia sifa nne za msingi ambazo Mungu anazo kwa usawaziko mkamilifu. Kushughulika kwake na Farao kulifunua nguvu zake zenye kutisha. (Kutoka 9:16) Njia yenye ustadi ambayo Mungu alishughulika na hali hiyo ngumu sana ilionyesha hekima yake isiyo na kifani. (Warumi 11:33) Yeye alifunua haki yake kwa kutekeleza adhabu juu ya wapinzani washupavu na waonevu wa watu wake. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Sifa ya Mungu iliyo kuu kuliko zote ni upendo. Yehova alionyesha upendo wenye kutokeza kwa kutimiza ahadi yake kuhusu wazao wa Abrahamu. (Kumbukumbu la Torati 7:8) Alionyesha upendo pia kwa kuruhusu Wamisri wengine waache miungu bandia na kunufaika sana kwa kuchukua msimamo wao kwa ajili ya Mungu pekee wa kweli.
15, 16. Mungu ameonyesha upendo kwa njia zipi?
15 Usomapo Biblia, utaona kwamba upendo ni sifa kuu ya Mungu, naye huuonyesha kwa njia nyingi. Kwa mfano, ni kutokana na upendo kwamba yeye akawa Muumba na kushiriki shangwe ya uhai kwa mara ya kwanza pamoja na viumbe vya roho. Mamia ya mamilioni ya hao malaika humpenda Mungu na kumsifu. (Ayubu 38:4, 7; Danieli 7:10) Mungu alionyesha upendo pia kwa kuumba dunia na kuitayarisha kwa ajili ya kuwapo kwa binadamu kwenye furaha.—Mwanzo 1:1, 26-28; Zaburi 115:16.
16 Tunanufaika na upendo wa Mungu kwa njia zilizo nyingi mno kutaja. Kwanza, kwa upendo Mungu amefanya miili yetu kwa njia nzuri ajabu hivi kwamba tunaweza kufurahia uhai. (Zaburi 139:14) Upendo wake unaonyeshwa kwa njia ya kwamba yeye huandaa “mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, aki[tu]shibisha mioyo [yetu] chakula na furaha.” (Matendo 14:17) Mungu hata “huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mathayo 5:45) Upendo humsukuma Muumba wetu pia atusaidie tupate ujuzi juu ya Mungu na kumtumikia kwa furaha tukiwa waabudu wake. Kwelikweli, “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Lakini utu wake unatia ndani mengi zaidi.
“MUNGU MWINGI WA HURUMA, MWENYE FADHILI”
17. Twajifunza nini juu ya Mungu kwenye Kutoka 34:6, 7?
17 Baada ya Waisraeli kuvuka Bahari Nyekundu, wao walihitaji bado kumjua Mungu vizuri zaidi. Musa alihisi uhitaji huo akasali hivi: “Ikiwa nimepata neema [“upendeleo,” NW] mbele zako, unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate neema [“upendeleo,” NW] mbele zako.” (Kutoka 33:13) Musa alipata kumjua Mungu vizuri zaidi aliposikia tangazo hili la Mungu mwenyewe: “BWANA [“Yehova,” NW], BWANA [“Yehova,” NW], Mungu mwingi wa huruma [“rehema,” NW], mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” (Kutoka 34:6, 7) Mungu husawazisha upendo wake na hukumu, hawakingi wale watendao dhambi kimakusudi wasipatwe na matokeo ya makosa yao.
18. Yehova amethibitikaje kuwa mwenye rehema?
18 Kama vile Musa alivyojifunza, Yehova huonyesha rehema. Mtu mwenye rehema husikitikia wale wanaoteseka na hujaribu kuwaletea kitulizo. Hivyo Mungu amehurumia wanadamu kwa kutoa uandalizi kwa ajili ya kitulizo cha kudumu watoke katika hali ya kuteseka, ugonjwa, na kifo. (Ufunuo 21:3-5) Huenda waabudu wa Mungu wakapatwa na misiba kwa sababu ya hali zilizomo katika ulimwengu huu mwovu, au huenda wasitende kwa hekima na hivyo wapatwe na taabu. Lakini wakigeuka wamwelekee Yehova kwa unyenyekevu ili kupata msaada, yeye atawafariji na kuwasaidia. Sababu gani? Kwa sababu yeye huwaonyesha waabudu wake ufikirio mwororo kwa rehema.—Zaburi 86:15; 1 Petro 5:6, 7.
19. Sababu gani tunaweza kusema kwamba Mungu ni mwenye fadhili?
19 Watu wengi wenye mamlaka hutendea wengine bila huruma. Tofauti na hilo, Yehova ni mwenye fadhili kama nini kuelekea watumishi wake wanyenyekevu! Ingawa yeye ni mamlaka iliyo juu zaidi kuliko zote katika ulimwengu wote mzima, yeye huwaonyesha wanadamu wote fadhili yenye kutokeza kwa njia ya ujumla. (Zaburi 8:3, 4; Luka 6:35) Yehova ni mwenye fadhili pia kwa watu mmoja-mmoja, akiitikia sihi zao mahususi za kupata upendeleo. (Kutoka 22:26, 27; Luka 18:13, 14) Bila shaka, Mungu hana wajibu wa kumwonyesha mtu yeyote upendeleo au rehema. (Kutoka 33:19) Kwa hiyo, tunahitaji kudhihirisha uthamini wenye kina kwa ajili ya rehema na fadhili ya Mungu.—Zaburi 145:1, 8.
SI MWEPESI WA HASIRA, HANA UPENDELEO, NA NI MWADILIFU
20. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova si mwepesi wa hasira na pia hana upendeleo?
20 Yehova si mwepesi wa hasira. Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba yeye hachukui hatua, kwani alifanya hivyo kwa kuharibu Farao mshupavu pamoja na jeshi lake katika Bahari Nyekundu. Yehova hana upendeleo. Kwa hiyo, Waisraeli, watu wake wenye kupendelewa, walipoteza upendeleo wake hatimaye kwa sababu ya kuendelea kwao kutenda makosa. Mungu hukubali watu kutoka mataifa yote kuwa waabudu wake, lakini ni wale tu wanaojipatanisha na njia zake za uadilifu.—Matendo 10:34, 35.
21. (a) Ufunuo 15:2-4 hutufundisha nini juu ya Mungu? (b) Ni nini kitakachoifanya iwe rahisi zaidi kwetu kufanya yale ambayo Mungu husema ni sawa?
21 Kitabu cha Biblia, Ufunuo, chakazia umaana wa kujifunza juu ya “amri za [Mungu] za uadilifu.” (NW) Chatuambia kwamba viumbe vya kimbingu huimba hivi: “Ni makuu, na ya ajabu, matendo yako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi; ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa. Ni nani asiyekucha, Ee Bwana, na kulitukuza jina lako? kwa kuwa wewe peke yako u Mtakatifu; kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa kuwa matendo yako ya haki [“amri zako za uadilifu,” NW] yamekwisha kufunuliwa.” (Ufunuo 15:2-4) Tunaonyesha hofu ifaayo kwa Yehova, au staha nyingi kwake, kwa kujipatanisha na yale anayosema ni sawa. Hilo hurahisishwa zaidi kwa kujikumbusha juu ya hekima na upendo wa Mungu. Amri zake zote ni kwa faida yetu.—Isaya 48:17, 18.
‘YEHOVA MUNGU WETU NDIYE MMOJA’
22. Sababu gani wale ambao hukubali Biblia hawaabudu Utatu?
22 Wamisri wa kale waliabudu miungu mingi, lakini Yehova ni “Mungu mwenye kutoza ujitoaji usiohusisha wengine.” (Kutoka 20:5, NW) Musa aliwakumbusha Waisraeli kwamba ‘BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wetu, BWANA [“Yehova,” NW] ndiye mmoja.’ (Kumbukumbu la Torati 6:4) Yesu Kristo alirudia kusema maneno hayo. (Marko 12:28, 29) Kwa hiyo, wale wanaoikubali Biblia kuwa Neno la Mungu hawaabudu Utatu wenye watu watatu au miungu mitatu katika mmoja. Kwa kweli, neno “Utatu” hata halionekani katika Biblia. Mungu wa kweli ni Mtu mmoja, aliye mbali na Yesu Kristo. (Yohana 14:28; 1 Wakorintho 15:28) Roho takatifu ya Mungu si mtu. Ni kani ya utendaji ya Yehova, inayotumiwa na Mweza Yote ili kutimiza makusudi yake.—Mwanzo 1:2; Matendo 2:1-4, 32, 33; 2 Petro 1:20, 21.
23. (a) Upendo wako kwa Mungu utaongezekaje? (b) Yesu alisema nini juu ya kumpenda Mungu, na tunahitaji kujifunza nini juu ya Kristo?
23 Ufikiriapo jinsi Yehova alivyo wa ajabu, je, hukubali kwamba yeye astahili ibada yako? Ujifunzapo Neno lake, Biblia, wewe utapata kumjua vizuri zaidi na utajifunza yale ambayo yeye anataka kutoka kwako kwa hali njema na furaha yako ya milele. (Mathayo 5:3, 6) Kwa kuongezea, upendo wako kwa Mungu utaongezeka. Hilo linafaa, kwani Yesu alisema hivi: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Kwa wazi, Yesu alikuwa na upendo huo kwa Mungu. Lakini Biblia hufunua nini juu ya Yesu Kristo? Daraka lake ni nini katika kusudi la Yehova?
Tahini Ujuzi Wako
Jina la Mungu ni nini, nalo hutumiwa mara nyingi kadiri gani katika Maandiko ya Kiebrania?
• Sababu gani ulitumie jina la Mungu?
• Ni sifa zipi za Yehova Mungu ambazo hasa hukuvutia wewe?
[Picha katika ukurasa wa 29]
Wewe wamjua vizuri kadiri gani Muumba wa vitu vyote?