Waangalizi Wanaoongoza—Mwangalizi wa Utumishi
1 Mwangalizi wa utumishi anapendezwa sana na kila kitu kinachohusiana na maendeleo ya kazi ya kueneza evanjeli katika eneo la kutaniko. Hivyo, yeye hutimiza fungu muhimu katika kutusaidia kutimiza daraka letu la kuhubiri habari njema. Akiwa mweneza-evanjeli mwenye bidii, yeye huongoza katika kupanga mambo yote yanayohusiana na utumishi. Akiwa mwalimu mwenye uwezo, yeye husaidia wahubiri mmoja-mmoja waboreshe matokeo yao katika huduma.—Efe. 4:11, 12.
2 Mzee huyo husimamia moja kwa moja kazi ya watumishi wa huduma waliogawiwa kushughulikia fasihi, magazeti, na maeneo. Yeye ndiye mwenye wajibu wa kuhakikisha kwamba kuna ugavi wa kutosha wa fasihi, magazeti, na fomu za utumishi za matumizi zapatikana kila mwezi. Mara moja kwa mwaka yeye hupitia faili ya maeneo kuona kama maeneo yote yamehubiriwa kikamili, naye hugawia ndugu wanaostahili watembelee maeneo fulani ya kibiashara au maeneo mengine ikiwa lazima.
3 Mwangalizi wa utumishi ana daraka la kusimamia sehemu mbalimbali za mahubiri, kutia ndani za kibiashara, barabarani, na kutoa ushahidi kwa njia ya simu. Yuko chonjo kupanga mipango inayotumika ya kukutana ya utumishi katika juma, kutia ndani siku za likizo. Yeye huonyesha kupendezwa kikweli na utendaji wa funzo la Biblia. Yeye hutafuta njia za kutoa msaada wa kiroho kwa wale wanaokuwa wasio wa kawaida au wasiotenda katika huduma. Yeye anahangaikia kazi ya mapainia, na husimamia programu ya Mapainia Wasaidia Wengine.
4 Akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, mwangalizi wa utumishi hupendekeza marekebisho yoyote yanayohitajika katika vikundi vya Funzo la Kitabu la Kutaniko. Anapotembelea kikundi chenu, hakikisha unahudhuria na kushiriki naye katika utumishi wa shambani.
5 Wote kutanikoni wapaswa kushirikiana kwa hiari na mwelekezo unaotolewa na mwangalizi wa utumishi. Kufanya hivyo kutatusaidia kuwa na matokeo zaidi katika kazi ya kufanya wanafunzi na tutapata shangwe nyingi zaidi katika huduma yetu.