Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • fy sura 1 kur. 4-12
  • Je, Kuna Siri ya Kupata Furaha ya Familia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Kuna Siri ya Kupata Furaha ya Familia?
  • Siri ya Furaha ya Familia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • FAMILIA NI NINI?
  • FAMILIA YAKABILI MKAZO
  • SIRI YA KUPATA FURAHA YA FAMILIA
  • Fuatia Amani ya Kimungu Katika Maisha ya Familia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Furahia Maisha ya Familia
    Furahia Maisha ya Familia
  • Kuona Njia ya Kupata Furaha ya Jamaa
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Familia—Binadamu Wanaihitaji!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Siri ya Furaha ya Familia
fy sura 1 kur. 4-12
Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 4

SURA YA KWANZA

Je, Kuna Siri ya Kupata Furaha ya Familia?

Picha katika ukurasa wa 5

1. Kwa nini familia zilizo thabiti ni za maana katika jamii ya kibinadamu?

FAMILIA ndiyo shirika la kale zaidi duniani, nayo ina fungu la maana katika jamii ya kibinadamu. Muda wote wa historia, familia zilizo thabiti zimesaidia kufanyiza jamii imara. Familia ndiyo mpango bora zaidi ili kulea watoto wawe watu wazima.

2-5. (a) Fafanua usalama ambao mtoto huhisi katika familia yenye furaha. (b) Ni matatizo gani yanayoripotiwa katika familia fulani?

2 Familia yenye furaha ni mahali pa usalama na ulinzi. Ebu wazia kwa muda mfupi familia iliyo bora. Wakati wa mlo wao wa jioni, wazazi wenye kujali huketi pamoja na watoto wao na kuzungumza juu ya matukio ya hiyo siku. Watoto huongea-ongea kwa msisimko wanaposimulia baba na mama yao yale yaliyotendeka shuleni. Wakati wa starehe unaotumiwa wakiwa pamoja huburudisha kila mtu kwa ajili ya siku nyingine nje ya nyumbani.

3 Katika familia yenye furaha, mtoto hujua kwamba baba na mama yake watamtunza awapo mgonjwa, labda wakipokezana kukaa kando ya kitanda chake usiku kucha. Yeye ajua kwamba aweza kumwendea mama au baba yake akiwa na matatizo ya maisha yake ya ujana na kupata shauri na utegemezo. Ndiyo, mtoto huyo huhisi akiwa salama, haidhuru nje kumejaa taabu jinsi gani.

4 Watoto wanapokua, kwa kawaida wao huoa au huolewa na kuwa na familia yao wenyewe. “Mtu hung’amua jinsi alivyo na deni kwa wazazi wake anapokuwa na mtoto wake mwenyewe,” yasema mithali fulani ya Mashariki. Wakiwa na hisi yenye kina cha shukrani na upendo, watoto ambao wamekua hujaribu kufanya familia zao wenyewe ziwe zenye furaha, nao pia hutunza wazazi wao wenyewe ambao sasa wanazeeka, wanaofurahia kuwa pamoja na wajukuu.

5 Labda kufikia sasa wewe unafikiri hivi: ‘Mimi naipenda familia yangu, lakini si kama ile ambayo imetoka tu kufafanuliwa. Mwenzi wangu nami tuna ratiba zinazotofautiana na hatuonani mara nyingi. Mara nyingi sisi huongea kuhusu matatizo ya pesa.’ Au je, wasema, ‘Watoto na wajukuu wangu huishi katika mji mwingine, nami sipati kamwe kuwaona’? Ndiyo, kwa sababu ambazo mara nyingi hupita uwezo wa udhibiti wa wale wanaohusika, maisha mengi ya familia si bora. Bado, watu fulani huwa na maisha za familia zenye furaha. Jinsi gani? Je, kuna siri ya kupata furaha ya familia? Jibu ni ndiyo. Lakini kabla ya kuzungumza juu ya hiyo, twapaswa kujibu swali la maana.

FAMILIA NI NINI?

6. Ni familia za aina gani zitakazozungumziwa katika kitabu hiki?

6 Katika nchi za Magharibi, familia zilizo nyingi ni baba, mama, na watoto. Wazakuu (babu na nyanya) huenda wakaishi katika nyumba zao wenyewe kwa muda mrefu kadiri wawezavyo. Ingawa uwasiliano unaendelezwa pamoja na watu wa ukoo wa mbali zaidi, wajibu kuelekea hao ni mdogo. Kwa msingi, hiyo ndiyo familia tutakayozungumzia katika kitabu hiki. Hata hivyo, familia nyinginezo zimezidi kuwa jambo la kawaida katika miaka ya juzijuzi—familia yenye mzazi mmoja, familia ya kambo, na familia ambayo wazazi wayo hawaishi pamoja kwa sababu moja au nyingine.

7. Ni nini iliyo familia pana?

7 Jambo la kawaida katika tamaduni fulani ni ile familia iliyo pana. Katika mpango huu, ikiwezekana, wazakuu wanatunzwa kwa kawaida na watoto wao, na vifungo vya karibu na madaraka huenea hadi kwa watu wa ukoo wa mbali. Mathalani, washiriki wa familia huenda wakasaidia kutegemeza, kulea, na hata kulipia elimu ya wapwa wao wa kike, wapwa wao wa kiume, au watu wa ukoo wao wa mbali zaidi. Kanuni tutakazozungumzia katika kichapo hiki zinatumika pia katika familia zilizo pana.

FAMILIA YAKABILI MKAZO

8, 9. Ni matatizo gani katika nchi fulani yanayoonyesha kwamba familia inabadilika?

8 Kwa kuhuzunisha, leo familia inabadilika—si kwa njia bora. Kielelezo cha hilo kinaonwa katika India, ambako mke huenda akaishi na familia ya mume wake na kufanya kazi nyumbani akiwa chini ya mwelekezo wa wakwe zake. Lakini siku hizi, ni jambo la kawaida kwa wake Wahindi kutafuta kazi za kuajiriwa nje ya nyumbani. Hata hivyo inaonekana kwamba wangali wanatazamiwa kutimiza madaraka yao ya kidesturi nyumbani. Swali linalotokezwa katika nchi nyingi ni, Kwa kulinganishwa na washiriki wengine wa familia, mke aliye na kazi nje ya nyumbani apaswa atazamiwe kufanya kiasi gani cha kazi nyumbani?

9 Katika jamii za Mashariki, mahusiano imara ya familia zilizo pana ni ya kidesturi. Hata hivyo, chini ya uvutano wa mtindo wa maisha wa Magharibi wa kukazia haki za mtu binafsi na mkazo wa matatizo ya kiuchumi, familia iliyo pana ya kidesturi inadhoofika. Kwa hiyo, wengi huona utunzaji wa washiriki wa familia waliozeeka kuwa mzigo wenye kulemea badala ya kuwa wajibu au pendeleo. Wazazi fulani walio wazee-wazee hutendwa vibaya. Kwa kweli, kutenda vibaya na kupuuza waliozeeka kunapatikana katika nchi nyingi leo.

10, 11. Ni mambo gani ya hakika yanayoonyesha kwamba familia inabadilika katika nchi za Ulaya?

10 Talaka inazidi kuwa jambo la kawaida. Katika Hispania kiwango cha talaka kiliongezeka hadi ndoa 1 kati ya 8 kufikia mwanzo wa mwongo wa mwisho wa karne ya 20—ongezeko kubwa kutoka kiwango cha ndoa 1 kati ya 100 cha miaka 25 tu mbele ya hapo. Uingereza, yenye kuripotiwa kuwa na kiwango cha juu zaidi cha talaka katika Ulaya (ndoa 4 kati ya 10 zatazamiwa kutofaulu), imeona ongezeko la ghafula katika idadi ya familia zenye mzazi mmoja.

11 Wengi katika Ujerumani wanaonekana kuwa wakiiacha kabisa familia ya kidesturi. Katika miaka ya 1990 asilimia 35 ya familia zote za Kijerumani zilikuwa na mshiriki mmoja tu na asilimia 31 zilikuwa na washiriki wawili tu. Wafaransa pia wanaoa au wanaolewa mara chache zaidi, na wale wanaooa au wanaoolewa hutalikana mara nyingi zaidi na mapema zaidi kuliko ilivyokuwa kawaida ya hali. Wengi zaidi na zaidi hupendelea kuishi pamoja bila madaraka ya ndoa. Mielekeo inayofanana na hiyo inaonwa ulimwenguni pote.

12. Watoto hutesekaje kwa sababu ya mabadiliko katika familia ya kisasa?

12 Namna gani watoto? Katika Marekani na nchi nyinginezo nyingi, wengi zaidi na zaidi wanazaliwa nje ya ndoa, wengine wanazaliwa na matineja vijana. Wasichana wengi matineja wana watoto kadhaa kutoka kwa baba tofauti-tofauti. Ripoti kutoka kotekote ulimwenguni husimulia juu ya mamilioni ya watoto wasio na makao wanaozurura ovyo barabarani; wengi wanaponyoka nyumba ambako wanatendwa vibaya au wanafukuzwa na familia ambazo haziwezi kuwategemeza tena.

13. Ni matatizo gani yenye kuenea kotekote yanayoinyang’anya familia furaha?

13 Ndiyo, familia imo katika hali ya hatari. Kwa kuongezea yale ambayo yametajwa tayari, uasi wa kitineja, kutendwa vibaya kwa watoto, ujeuri wa wenzi wa ndoa, uraibu wa alkoholi, na matatizo mengine yenye uharibifu hunyang’anya familia nyingi furaha. Kwa idadi kubwa ya watoto na watu wazima, familia si mahali pa usalama hata kidogo.

14. (a) Kulingana na watu fulani, ni nini vilivyo visababishi vya hali ya hatari ya familia? (b) Mwanasheria mmoja wa karne ya kwanza aliufafanuaje ulimwengu wa leo, na utimizo wa maneno yake umekuwa na uvutano gani juu ya maisha ya familia?

14 Kwa nini familia imo katika hali ya hatari? Watu fulani hulaumu kule kuingia kwa wanawake katika kazi ya kuajiriwa kuwa sababu ya hali ya hatari ya familia ya siku ya leo. Wengine huelekeza kwenye poromoko la kiadili la leo. Na sababu nyinginezo hutajwa. Karibu miaka elfu mbili iliyopita, mwanasheria maarufu alitabiri kwamba misongo mingi ingekumba familia, alipoandika hivi: “Siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Je, yeyote angetilia shaka kutimizwa kwa maneno haya leo? Katika ulimwengu wenye hali kama hizi, je, inashangaza kwamba familia nyingi zimo katika hali ya hatari?

SIRI YA KUPATA FURAHA YA FAMILIA

15-17. Katika kitabu hiki, ni mamlaka gani itakayoelekezewa kuwa yenye siri ya kupata furaha ya familia?

15 Shauri juu ya jinsi ya kupata furaha katika familia hutolewa kutoka pande zote. Katika Magharibi, ugavi wenye kuendelea wa vitabu na magazeti ya kujisaidia mwenyewe hutoa shauri. Tatizo ni kwamba washauri wa kibinadamu hupingana, na shauri linalofaa leo huenda likaonwa kuwa halifai kesho.

16 Ni wapi basi, tuwezako kutafuta mwongozo wa familia wenye kutegemeka? Basi je, wewe ungeendea kitabu kilichokamilishwa miaka ipatayo 1,900 iliyopita? Au ungehisi kwamba kitabu cha jinsi hiyo lazima kiwe hakifai hali ya kisasa hata kidogo? Ukweli ni, siri ya kweli ya kupata furaha ya familia inapatikana katika chanzo cha jinsi hiyo hasa.

17 Chanzo hicho ni Biblia. Kulingana na uthibitisho wote, hiyo ilipuliziwa na Mungu mwenyewe. Katika Biblia twapata taarifa ifuatayo: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16) Katika kichapo hiki sisi tutakutia moyo ufikirie jinsi Biblia iwezavyo kukusaidia ‘unyooshe mambo’ unaposhughulika na mikazo na misongo inayokabili familia leo.

18. Kwa nini ni jambo linalofaa kuikubali Biblia kuwa mamlaka katika kutoa mashauri katika ndoa?

18 Ikiwa una mwelekeo wa kupuuza uwezekano wa kwamba Biblia yaweza kusaidia kufanya familia ziwe na furaha, fikiria hili: Yule aliyepulizia Biblia ndiye Mwanzilishi wa mpango wa ndoa. (Mwanzo 2:18-25) Biblia husema kwamba jina lake ni Yehova. (Zaburi 83:18) Yeye ndiye Muumba na ‘Baba, ambaye kwake kila familia hupata jina layo.’ (Waefeso 3:14, 15) Yehova ametazama maisha ya familia tangu mwanzo wa wanadamu. Yeye ajua matatizo yawezayo kutokea naye ametoa shauri ili kuyasuluhisha. Muda wote wa historia, wale waliotumia kanuni za Biblia kwa moyo mweupe katika familia zao walipata furaha kubwa zaidi.

19-21. Ni maono gani ya kisasa yaonyeshayo nguvu za Biblia za kusuluhisha matatizo ya ndoa?

19 Kwa kielelezo, mke fulani wa nyumbani katika Indonesia alikuwa mcheza kamari wa kupindukia. Kwa miaka kadhaa yeye alipuuza watoto wake watatu na alibishana na mume wake kwa kawaida. Kisha akaanza kujifunza Biblia. Polepole mwanamke huyo akaja kuamini yale ambayo Biblia ilisema. Alipotumia shauri layo, alikuwa mke bora. Jitihada zake, zenye kutegemea kanuni za Biblia, zilileta furaha kwa familia yake nzima.

20 Mke wa nyumbani katika Hispania asema hivi: “Tulikuwa tumeoana mwaka mmoja tu tulipoanza kuwa na matatizo mazito.” Yeye na mume wake hawakushiriki pamoja mambo mengi, nao hawakuongea sana isipokuwa wakati walipokuwa wakibishana. Wajapokuwa na binti mchanga, waliamua kupata mtengano wa kisheria. Lakini, kabla ya hilo kutendeka, wao walitiwa moyo waiendee Biblia. Walilichunguza shauri layo kuhusu wanaume na wanawake ambao wameoana nao wakaanza kulitumia. Muda si muda, waliweza kuwasiliana kwa amani, na familia yao ndogo ikaunganika kwa furaha.

21 Biblia husaidia pia watu wenye umri mkubwa. Mathalani, fikiria ono la mume na mke fulani Wajapani. Mume alikuwa mwenye kukasirika upesi na mjeuri nyakati nyingine. Mwanzoni, mabinti wa mume na mke hao walianza kujifunza Biblia, ujapokuwa upinzani wa wazazi wao. Kisha, mume akajiunga na mabinti wake, lakini mke akaendelea kupinga. Hata hivyo, miaka ilipopita, yeye aliona matokeo mazuri ya kanuni za Biblia juu ya familia yake. Mabinti wake walimtunza vizuri, na mume wake akawa mpole sana. Mabadiliko hayo yalimsukuma mwanamke huyo aiendee Biblia mwenyewe, nayo ikawa na tokeo lilo hilo zuri juu yake. Bibi huyo mzee-mzee akarudia-rudia kusema: “Tulikuja kuwa mume na mke kwelikweli.”

22, 23. Biblia husaidiaje watu wa malezi yote ya kitaifa wapate furaha katika maisha yao ya familia?

22 Watu hao mmoja-mmoja wamo miongoni mwa wale wengi sana ambao wamejifunza siri ya kupata furaha ya familia. Wamekubali shauri la Biblia na kulitumia. Ni kweli, wanaishi katika ulimwengu uleule mjeuri, usio na adili, uliokazwa kiuchumi kama wengineo wote. Zaidi ya hayo, wao si wakamilifu, lakini wanapata furaha katika kujaribu kufanya mapenzi ya Mwanzilishi wa mpango wa familia. Kama vile Biblia isemavyo, Yehova Mungu ‘ndiye akufundishaye ili upate faida, akuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.’—Isaya 48:17.

23 Ingawa Biblia ilikamilishwa karibu miaka elfu mbili iliyopita, shauri layo kwa kweli lafaa hali ya kisasa. Zaidi, iliandikwa kwa ajili ya watu wote. Biblia si kitabu cha Kiamerika wala cha Magharibi. Yehova “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu,” na Yeye ajua umbile la wanadamu kila mahali. (Matendo 17:26) Kanuni za Biblia hufanya kazi kwa kila mtu. Ukizitumia, wewe pia utakuja kujua siri ya kupata furaha ya familia.

JE, UNAWEZA KUYAJIBU MASWALI HAYA?

Familia inapatwa na nini leo?—2 Timotheo 3:1-4.

Ni nani aliyeanzisha mpango wa familia?—Waefeso 3:14, 15.

Ni nini iliyo siri ya kupata furaha ya familia?—Isaya 48:17.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki