Fundisha Wengine ili Wajinufaishe
1 Yehova anataka watu wote wajinufaishe. (Isa. 48:17) Yeye anajua kile ambacho hutuletea furaha ya kweli. Anatamani sana wanadamu waepuke afa na kufurahia uhai kwa kuzingatia amri zake. Sisi twajinufaisha zaidi kwa kuishi maisha zetu kulingana na njia ya Mungu. (Zab. 34:8) Twaweza kufundishaje wengine wafanye vivyo hivyo?
2 Watu Wanataka Nini? Ni nini ambacho huhangaisha wenye nyumba mahali unapoishi? Je, si usalama wa makao yao, kifungo imara cha ndoa yao, wakati ujao wa watoto wao, na mambo kama hayo? Wanapokuwa na matatizo, wao huenda wapi ili kupata msaada? Huenda wakajitegemea wenyewe, wakitegemea programu za kutoa ushauri, au wakategemea mwongozo wa wengine. Katika kufanya hivyo, wengi wameachwa wakiwa wametatizika kwa sababu ya mawazo yasiyopatana na yasiyotumika ya jinsi ya kujinufaisha. Lazima tuwasadikishie kwamba kile ambacho Neno la Mungu huandaa kiwe mwongozo ni bora zaidi. (Zab. 119:98) Twaweza kufanya hivi kwa kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kuongeza ubora wa maisha zao hata sasa wakifanya bidii kujifunza Biblia na kutumia yale inayosema.—2 Tim. 3:16, 17.
3 Maisha ya Familia Yaliyoboreshwa: Si watu wengi hutambua ifaavyo jinsi ambavyo shauri lililopuliziwa kwenye Waefeso 5:22–6:4 hufanya kazi katika kutatua matatizo ya familia. Ilikuwa hivyo kuhusu wenzi wa ndoa, ambao baada ya miaka kumi ya ndoa yao, waliamua kwamba wangetengana. Hata hivyo, mke alianza kujifunza Biblia, naye alifundishwa kanuni za Kimaandiko kuhusu maisha ya ndoa. Upesi mume akagundua mabadiliko aliyokuwa akifanya alipotumia kanuni za Biblia, naye akaanza kujifunza pia. Mume huyo baadaye alisema: “Sasa tumepata msingi wa maisha ya ndoa yenye furaha kikweli.”
4 Kusudi Halisi Maishani: Kijana mmoja mwenye uraibu wa dawa za kulevya alipotafuta msaada kutoka kwa Mashahidi, alifundishwa kwamba Yehova humjali kibinafsi. Alisema hivi: ‘Nilipata kujua kwamba Muumba ana kusudi kwa mwanadamu na huwapa wale wenye kibali chake uhai udumuo milele. Huwezi kuamini jinsi nilivyofurahi kuhusu jambo hilo. Leo nafurahia afya nzuri, amani ya akili, na uhusiano wa karibu na Mungu.’
5 Kila mtu aweza kunufaika na msaada wenye kutumika upatikanao katika Neno la Mungu. Kwa kuutumia ukiwa mwongozo wake, twahakikisha kwamba njia ya Yehova ni bora zaidi ya njia za ulimwengu. (Zab. 116:12) Ni pendeleo letu kuwapelekea wengine ujumbe huu, tukiwafundisha ili wajinufaishe. Tufanyapo hivyo, tutaona matokeo mengi mazuri.