Utamwambia Nini Mhindu?
1 Labda kama ujuavyo, kuna Wahindu wengi wanaoishi katika nchi mbalimbali, kutia ndani sehemu fulani katika eneo letu. Hilo lamaanisha kwamba mwishowe huenda ukakutana na Mhindu unapokuwa hudumani. Ukimkuta, utamhubiriaje?
2 Kumbuka Mambo Haya: Wamishonari ambao wamehubiria Wahindu kwa mafanikio husema kwamba si lazima ujifunze kwa kina kirefu kuhusu Uhindu ili utoe ushahidi wenye matokeo. Utoaji sahili, wenye busara wa ile kweli mara nyingi huleta itikio lifaalo. Omba uongee na kichwa cha nyumba hiyo kwanza. Ukikubaliwa, itakuwa rahisi kutoa ushahidi kwa washiriki wengine wa familia. Mwanzoni epuka kudokeza kwamba unaleta ujumbe bora kuliko ule ambao mwenye nyumba anaamini au kwamba wataka kuzungumza kuhusu Mungu wa pekee wa kweli au maandishi matakatifu ya kale zaidi. Kwa kuwa Wahindu wengi huiona Biblia kuwa kitabu cha Wazungu, unaweza kupunguza ubaguzi kwa kueleza kwamba hakichochei ukoloni au ubora wa jamii moja kuliko nyingine.
3 Tumia Vifaa Vifaavyo: Broshua mbili zimetayarishwa hasa kwa ajili ya Wahindu. Why Should We Worship God in Love and Truth? imechapishwa kwa Kigujarati na Kipunjabi. Our Problems—Who Will Help Us Solve Them? imechapishwa kwa lugha nyingine 11 za Kihindi. Zote mbili zapatikana katika Kiingereza. Broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” na Je! Kweli Mungu Anatujali? pia zimethibitika kuwa zenye matokeo tunapotolea ushahidi wale walio na malezi ya Kihindu. Broshua Anataka na kitabu Ujuzi vyaweza kutumiwa kwa mafanikio kuongoza mafunzo ya Biblia.
4 Weka Msingi Wenye Maeleano: Si vigumu kupata mambo yenye kueleana na Wahindu. Wao huamini kwamba tunaishi wakati ambapo uovu umefikia kilele chake na kwamba Mungu ataondolea ulimwengu huu matatizo kupitia msiba mkubwa utakaofuatwa na enzi ya kweli. Unaweza kuona jinsi itikadi hizo zinavyoweza kuhusianishwa kwa urahisi na mafundisho ya Biblia kuhusu siku za mwisho, dhiki kubwa, na ulimwengu mpya unaokuja. Kwa kuwa Wahindu wengi huona maisha kuwa yamejaa matatizo ambayo hayana utatuzi, wao hupendezwa na habari zinazohusu maisha ya familia, uhalifu, usalama, na linalotukia mtu anapokufa. Huu hapa ni utoaji aina mbili unaoweza kutumia.
5 Huu huenda ukamvutia mtu mwenye familia:
◼ “Ninawatembelea watu ambao wanahangaika kuhusu hali ya maisha ya familia katika nchi nyingi leo. Ni nini ambacho wafikiri kitasaidia kufanya familia ziwe pamoja? [Ruhusu jibu.] Watu fulani wanajua kile ambacho maandiko ya Hindu husema juu ya familia, lakini hawajapata fursa ya kulinganisha kile ambacho Biblia husema kuhusu habari hiyo. Ningependa kushiriki pamoja nawe wazo hili lililo kwenye Wakolosai 3:12-14.” Baada ya kusoma andiko, mwonyeshe mwenye nyumba sura ya 15 ya kitabu Ujuzi na useme: “Ningefurahi kutumia wakati mchache tusome sura hii pamoja.”
6 Huenda kijana akakubali huu:
◼ “Bila shaka wewe wamwamini Mungu. Unafikiri kusudi la Mungu kwetu ni nini?” Ruhusu jibu. Kisha soma Mwanzo 1:28 na useme: “Mahali pengi duniani kuna idadi ya watu wengi kupita kiasi ambao wamekumbwa na matatizo. Je, wafikiri Muumba angekuwa tayari kutusaidia kutatua matatizo yetu?” Baada ya kusikia jibu lake, geukia kichapo kifaacho.
7 Furahia Matokeo Mazuri: Mwanamume Mhindu mwenye umri wa miaka 22 alimfikia dada mmoja aliyekuwa akitoa ushahidi sokoni na kumwomba funzo la Biblia. Alimweleza dada huyo kwamba miaka minane iliyopita alipata kusikia mazungumzo ya Biblia kati yake na mama yake. Ijapokuwa alikuwa amevutiwa na majibu ya Biblia yenye kusaidia kwa matatizo ya binadamu, mama yake hakupendezwa na yeye alikuwa amejiona kuwa mchanga mno asiweze kufuatia kweli akiwa peke yake. Sasa akiwa mtu mzima, alitaka kujifunza zaidi. Mwanamume huyo mchanga hakupoteza wakati. Kwa siku 23 tu, alimaliza kujifunza kitabu Ujuzi, na miezi minne tu baada ya kukutana na dada huyo sokoni, aliomba abatizwe!
8 Ndugu mmoja alianzisha funzo na mwanamume Mhindu aliyekutana naye kwenye garimoshi. Mwanamume huyo alikuwa na matatizo katika ndoa yake. Pia alikuwa na tatizo la ulevi. Mwanamume huyo alikubali Shahidi amtembelee na kushiriki ushauri wa Biblia kwa maisha ya familia. Mafundisho ya adili ya Biblia yalimvutia, naye akakubali kujifunza Biblia. Yeye na familia yake wakaanza kuhudhuria mikutano pamoja. Baadaye waliwaambia marafiki na watu wa jamaa kweli hiyo. Kufikia sasa, sita kati ya watu hao wamekubali kweli!
9 Mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Hilo latia ndani wanaume na wanawake wanaodai kuwa wa dini isiyo ya Kikristo, kama vile dini ya Hindu. Kama kuna Wahindu katika eneo lako, kwa nini usiwatembelee na kutumia baadhi ya madokezo yaliyotolewa katika makala hii?